Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

Maoni ya Biblia

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

KWA miaka mingi watu wameamini kwamba wafu wanaweza kuwaongoza walio hai. Hadithi moja ya kale iliyoandikwa na mshairi Mgiriki Homer kuhusu Odysseus, ambaye pia anaitwa Ulysses inaunga mkono wazo hilo. Shujaa huyo anayesimuliwa na Homer alitaka kujua jinsi angerudi kwenye kisiwa cha nyumbani cha Ithaca, kwa hiyo, akaenda kwenye ulimwengu wa wafu kutafuta ushauri wa mbashiri aliyekuwa amekufa.

Wakitamani kupata majibu ya maswali yenye kutatanisha kutoka kwa wafu, watu wengi wamewaendea wale wanaowasiliana na pepo, wamelala katika makaburi ya babu zao, au kufanya matambiko. Je, kweli inawezekana kupata mwongozo kutoka kwa wafu?

Zoea Lililoenea Sana

Dini nyingi kubwa hufundisha kwamba inawezekana kuwasiliana na wafu. Kitabu Encyclopedia of Religion kinasema kwamba “ufundi au zoea la kuinua na kuwasiliana na nafsi za wafu, ni aina fulani ya uaguzi.” Kisha kinaongeza kusema kwamba zoea hilo “limeenea sana.” Kitabu New Catholic Encyclopedia kinathibitisha jambo hilo kwa kusema kwamba “ufundi au zoea la kuinua na kuwasiliana na nafsi za wafu, katika njia mbalimbali, limeenea ulimwenguni pote.” Hivyo haishangazi kwamba baadhi ya wafuasi wa dini nyingi wamejaribu kupata habari kutoka kwa ulimwengu wa roho!

Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema kwamba ingawa zoea hilo la kuwasiliana na wafu “lilishutumiwa vikali na Kanisa, maandishi mengi yanaonyesha kwamba zoea hilo liliendelezwa katika Enzi za Kati na katika kile Kipindi cha Mwamko.” Biblia inasema nini kuhusu mambo hayo?

Je, Unapaswa Kuuliza Habari Kutoka kwa Wafu?

Katika nyakati za kale, Yehova Mungu aliwaamuru hivi watu wake: “Asipatikane ndani yako . . . yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu.” (Kumbukumbu la Torati 18:9-13) Kwa nini Yehova alitoa amri hiyo? Ikiwa ingewezekana kwa walio hai kuwasiliana na wafu, je, halingekuwa jambo lenye upendo kwa Mungu wetu kuruhusu jambo hilo? Lakini kwa kweli, haiwezekani kuwasiliana na wafu. Tunajuaje hilo?

Maandiko yanafundisha tena na tena kwamba wafu hawana fahamu. Ona kile Mhubiri 9:5 inasema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” Zaburi 146:3, 4 inasema: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” Na pia nabii Isaya alisema kwamba wafu ‘hawajiwezi katika kifo.’—Isaya 26:14.

Hata hivyo, watu wengi wanaamini kwamba kwa kutumia njia mbalimbali za kuwasiliana na pepo wameweza kuwasiliana na wapendwa wao waliokufa. Kwa kuwa kuna masimulizi mengi kama hayo, inaonekana kwamba wengi wamezungumza na mtu fulani aliye katika ulimwengu wa roho. Lakini kama maandiko yaliyotajwa hapo juu yanavyoonyesha, watu hao hawakuzungumza na wafu. Hivyo basi, walizungumza na nani?

Wanazungumza na Nani?

Biblia inasema kwamba wana wa roho wa Mungu walimwasi Muumba wao na hivyo wakawa roho waovu. (Mwanzo 6:1-5; Yuda 6, 7) Roho hao waovu huendeleza wazo la kwamba wanadamu huendelea kuishi baada ya kufa. Ili kuendeleza uwongo, huo wanajifanya kuwa watu waliokufa na kuzungumza na watu walio hai kutoka kwenye ulimwengu wa roho.

Biblia inaeleza kwamba baada ya Mfalme Sauli wa Israeli kukataliwa na Yehova kwa sababu ya kutomtii, Sauli alijaribu kumtumia mwanamke aliyewasiliana na pepo ili azungumze na nabii Samweli aliyekuwa amekufa. Sauli alipokea ujumbe kutoka katika ulimwengu wa roho, lakini ujumbe huo haukutoka kwa Samweli. Kwa kweli, Samweli alikuwa amekataa kumwona mfalme huyo, na aliwapinga wale waliokuwa wakiwasiliana na pepo. Kwa hiyo, Sauli alipokea habari kutoka kwa roho mwovu ambaye alijifanya kuwa Samweli.—1 Samweli 28:3-20.

Roho waovu ni adui za Mungu, na ni hatari kuwasiliana nao. Kwa sababu hiyo, Maandiko yanaamuru hivi: “Msiwaendee wenye kuwasiliana na pepo, wala msitafute shauri la wajuzi wa kubashiri matukio, ili kutiwa unajisi nao.” (Mambo ya Walawi 19:31) “Yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu,” inaonya Kumbukumbu la Torati 18:11, 12, “ni chukizo kwa Yehova.” Kwa kweli, moja kati ya mambo yaliyomfanya Mfalme Sauli akose uaminifu na hivyo auawe na Yehova ni “kuuliza [habari] kutoka kwa mwenye kuwasiliana na pepo.”—1 Mambo ya Nyakati 10:13, 14.

Hivyo basi, unapokabili maswali au maamuzi yenye kutatanisha, utamgeukia nani ili upate mwongozo bora? Maandiko yanamtaja Yehova Mungu kuwa “Mfundishaji Mkuu.” Wewe na wapendwa wako mkisoma Neno lake, Biblia, na kufuata mafundisho yake, itakuwa ni kana kwamba ‘masikio yenu yanasikia neno nyuma yenu likisema: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”’ (Isaya 30:20, 21) Ingawa leo Wakristo hawatarajii kusikia sauti ya Mungu wa kweli moja kwa moja, yeye anaweza kuwaongoza kupitia Biblia. Naam, ni kana kwamba Yehova mwenyewe anasema: ‘Niruhusu nikuongoze.’

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Mungu anamwonaje mtu anayejaribu kuwasiliana na wafu?—Kumbukumbu la Torati 18:9-13.

● Je, wafu wanaweza kuwapa walio hai ujuzi wowote? Kwa nini unajibu hivyo?—Mhubiri 9:5.

● Tunaweza kumgeukia nani tukiwa na uhakika wa kupata mwongozo? —Isaya 30:20, 21.