Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Programu kwa Ajili ya Wagonjwa Mahututi—Lengo Ni Nini? (Julai 2011) Nikiwa mfanyakazi wa huduma za jamii, nilizoezwa kuwatunza wagonjwa mahututi na ninaweza kuthibitisha kwamba mambo mliyosema katika Amkeni! la Julai 2011 ni ya kweli. Vituo vya afya ambavyo vina vifaa vinavyohitajika ili kuwatunza wagonjwa mahututi ni vya lazima katika ulimwengu tunamoishi. Ninasubiri kwa hamu wakati ambapo serikali ya Mungu itakuja, na hakuna mtu atakayesema “Mimi ni mgonjwa,” na Mungu atafuta machozi kutoka katika macho yetu.—Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4.

M. R., Italia

Sikufurahi kwamba mlitaja “nepi za watu wazima” katika makala hiyo. Maneno hayo yanamshushia heshima mtu yeyote ambaye analazimika kuvaa vitambaa hivyo. Hakuna mfuko wowote unaotumiwa kupakia vitu hivyo unaotumia maneno hayo.

Jina limebanwa, Marekani

“Amkeni!” lajibu: Asante kwa kutujulisha jambo hilo. Tunamhurumia mtu yeyote anayekabiliana na matatizo makubwa ya afya, na hatungetaka kumwumiza mtu zaidi kwa kutumia maneno ambayo huenda wengine wakayaona kuwa yenye kushusha heshima. Tunaomba msamaha kwa wasomaji wetu ambao waliudhika kwa sababu ya jambo hilo.

Vijana Huuliza . . . Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano? (Julai 2011) Asanteni kwa makala hiyo. Nina umri wa miaka 26. Nilikuwa ninataka kufungua akaunti katika kituo cha mawasiliano, si kwa sababu nilitaka kuwa na marafiki wengi zaidi, lakini kwa sababu watu wengi walikuwa wakinitia moyo nifanye hivyo. Makala hiyo ilinisaidia sana. Unaweza kupata marafiki wengi bila kufungua akaunti katika kituo cha mawasiliano.

M. P., Filipino

Nilitazamia makala hiyo ichambue sana vituo vya mawasiliano. Lakini makala hiyo ilizungumzia mambo kwa usawaziko. Ilizungumzia faida na madhara yake na ikatoa ushauri kuhusu jinsi tunavyoweza kujilinda kutokana na hatari za vituo vya mawasiliano. Ilikazia akilini mwangu umuhimu wa kuwa mwangalifu ninapopachika habari za kibinafsi katika Intaneti.

C. W., Marekani

Siri ya Kufanikiwa kwa Familia (Oktoba 2009) Toleo hilo la pekee limeisaidia sana familia yetu. Nilifurahia hasa masanduku yaliyokuwa na kichwa “Jaribu kufanya hivi” ambayo yalikuwa katika makala zote saba za mfululizo huo. Tayari familia yetu imetumia madokezo hayo hususa yaliyotolewa.

H. H., Korea

Mazungumzo ya Familia Asanteni sana kwa makala hiyo ya kila mwezi. Binti yetu mwenye umri wa miaka sita hufurahia sehemu yenye kichwa Watoto Watafute Picha naye hupenda ile sehemu ya kupaka rangi picha. Makala hizo hukazia daraka la wazazi la kuwazoeza watoto wao tangu wanapokuwa na umri mchanga. Kazi mnayofanya kwa ajili ya watoto inathaminiwa sana.

M. P., Poland