Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipata Upendo na Amani ya Kweli

Nilipata Upendo na Amani ya Kweli

Nilipata Upendo na Amani ya Kweli

Limesimuliwa na Egidio Nahakbria

Nilipokuwa mchanga nilijihisi mpweke na pia nilihisi kuwa sipendwi. Lakini sasa ninahisi kuwa ninapendwa na nina amani ya kweli ya akili. Ni nini kilichobadili hisia zangu? Acheni niwaeleze.

NILIZALIWA mwaka wa 1976 katika nyumba yenye sakafu ya udongo kwenye milima ya Timor Mashariki, ambayo wakati huo ilikuwa sehemu ya Indonesia. Nilikuwa wa nane katika familia maskini ya watoto kumi. Kwa kuwa wazazi wangu hawangeweza kutulisha sisi sote, walibaki na ndugu yangu pacha na wakamwomba binamu yangu anitunze.

Mnamo Desemba 1975, kabla tu sijazaliwa, Indonesia ilivamia Timor Mashariki na jambo hilo lilianzisha mapigano ya waasi dhidi ya serikali ambayo yaliendelea kwa zaidi ya miaka 20. Kwa hiyo, kumbukumbu zangu za maisha ya utotoni ni za vita na kuteseka. Ninakumbuka vizuri jinsi wanajeshi walivyovamia kijiji chetu na hivyo watu wakalazimika kukimbia. Mimi na binamu yangu tulitembea hadi kwenye milima iliyokuwa mbali ambako maelfu ya Watimori walikuwa wamekimbilia.

Hata hivyo, wanajeshi waligundua mahali tulipokuwa tumejificha na punde si punde wakaanza kutuvurumishia mabomu. Bado ninakumbuka hofu, vifo, na uharibifu uliofuata. Hatimaye, tuliporudi kwenye kijiji chetu, niliishi kwa hofu. Wengi wa majirani wetu walitoweka ghafla au kuuawa, nami nilihofia kwamba huenda hata mimi nikauawa.

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, binamu yangu aliugua na akafa, kwa hiyo wazazi wangu walinipeleka nikaishi na nyanya yangu. Alikuwa mjane, aliyechoshwa na maisha na aliniona kuwa mzigo. Alinifanyisha kazi kama mtumwa. Siku moja nilipokuwa mgonjwa sana hivi kwamba singeweza kufanya kazi, alinipiga vibaya na akaniacha nife. Mmoja wa binamu zangu alinipeleka nikaishi na familia yake.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilianza shule. Punde baadaye, mke wa binamu yangu aliugua na binamu akashuka moyo sana. Kwa kuwa sikutaka kuwaongezea mzigo, nilitoroka na kujiunga na kundi la wanajeshi wa Indonesia lililokuwa likiishi msituni. Niliwasaidia kuosha nguo, kupika, na kusafisha kambi yao. Walinitendea kwa fadhili, nami nikajihisi kuwa ninathaminiwa. Lakini baada ya miezi kadhaa, watu wangu wa ukoo walijua nilipokuwa, nao wakawashurutisha wanajeshi hao wanirudishe nyumbani.

Mwanaharakati wa Kisiasa

Baada ya kumaliza shule ya sekondari, nilihamia Dili, mji mkuu wa Timor Mashariki na kujiunga na chuo kikuu. Nilipokuwa huko, nilikutana na vijana wengi waliokuwa na malezi kama yangu. Tuliamini kwamba harakati za kisiasa ndizo tu zingesaidia taifa letu kupata uhuru na kuleta mabadiliko katika jamii. Kikundi chetu cha wanafunzi kilipanga maandamano ya kisiasa ambayo hatimaye yaligeuka na kutokeza ghasia. Wengi kati ya marafiki wangu walijeruhiwa. Wengine wao waliuawa.

Wakati Timor Mashariki ilipopata uhuru mwaka wa 2002, nchi hiyo ilikuwa imeharibiwa kabisa, makumi ya maelfu ya watu walikufa, na mamia ya maelfu hawakuwa na makao. Nilitumaini kwamba hali zingekuwa nzuri. Lakini ukosefu wa kazi, umaskini, na misukosuko ya kisiasa iliendelea kuongezeka.

Mwelekeo Mpya

Wakati huo, nilikuwa nikiishi na watu wa ukoo, kutia ndani kijana aliyeitwa Andre, ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu nilishikilia sana dini ya Ukatoliki sikufurahi kwamba mtu wangu wa ukoo alishirikiana na dini nyingine. Lakini nilitaka kuijua Biblia na mara kwa mara nilisoma Biblia ya Andre iliyokuwa katika chumba chake cha kulala. Mambo niliyosoma yalinichochea nitake kujua mengi zaidi.

Katika mwaka wa 2004, Andre alinipatia mwaliko wa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu, nami nikakubali kwenda. Kwa sababu sikusoma vizuri mwaliko huo, nilifika saa mbili kabla ya mkutano huo kuanza. Mashahidi wenyeji na wale waliotoka nchi nyingine walipowasili, walinisalimu kwa uchangamfu na kunikaribisha vizuri. Nilifurahi sana. Wakati wa hotuba ya Ukumbusho, niliandika maandiko yaliyotajwa na baadaye nikayalinganisha na Biblia yangu ya Kikatoliki ili nithibitishe ikiwa mambo ambayo msemaji alisema yalikuwa sahihi. Bila shaka yalikuwa sahihi!

Juma lililofuata, nilihudhuria Misa katika kanisa letu. Kwa sababu baadhi yetu tulichelewa, kasisi aliokota ubao na akatufukuza nje ya kanisa kwa hasira. Tulipokuwa tumesimama nje, kasisi huyo alimaliza Misa yake kwa kuwaambia wahudhuriaji, “Amani ya Yesu iwe pamoja nanyi.” Mwanamke mmoja jasiri alimwambia hivi, “Unawezaje kuongea kuhusu amani wakati wewe umetoka tu kuwafukuza watu wale kanisani?” Kasisi huyo hakujibu. Niliondoka na sikurudi tena katika kanisa hilo.

Muda mfupi baada ya hapo, nilianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Mashahidi pamoja na Andre. Jambo hilo liliwashtua watu wetu wa ukoo nao wakaanza kutupinga. Nyanya ya Andre alituonya hivi: “Nitachimba shimo na kuwazika ninyi wavulana ikiwa hamtaacha kujifunza na watu wa dini hiyo mpya.” Hata hivyo, hatukuogopeshwa na vitisho vyake. Tuliazimia kufanya maendeleo ya kiroho.

Nafanya Mabadiliko

Kadiri nilivyojifunza Biblia ndivyo nilivyoanza kuhisi kwamba hapo awali sikujua upendo ni nini. Sikuwa na huruma na ilikuwa vigumu kwangu kuwaamini watu wengine na kwa sababu hiyo kila wakati nilikuwa tayari kujitetea. Hata hivyo, Mashahidi walinijali kikweli. Nilipokuwa mgonjwa sana na watu wangu wa ukoo wakanipuuza, Mashahidi walinitembelea na kunisaidia. Upendo wao haukuwa wa “maneno matupu,” bali ulikuwa “upendo wa kweli na wa vitendo.”—1 Yohana 3:18, Biblia Habari Njema.

Ingawa nilikuwa na sura na utu wenye kutisha, Mashahidi walinitendea kwa “hisia-mwenzi” na “upendo wa kindugu.” (1 Petro 3:8) Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nikaanza kuhisi kwamba ninapendwa. Nilianza kuwa mpole, na nikaanza kumpenda Mungu na wanadamu wenzangu. Kwa hiyo, mnamo Desemba 2004, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Andre alibatizwa muda mfupi baadaye.

Baraka Licha ya Matatizo

Baada ya kubatizwa, nilikuwa na hamu ya kuwasaidia watu wengine ambao hawakujua upendo wa kweli na haki. Kwa sababu hiyo, nikaanza kushiriki katika huduma ya Kikristo ya wakati wote, au upainia, kama inavyojulikana na Mashahidi wa Yehova. Iliburudisha zaidi kuwaambia wengine ujumbe wa Biblia wenye kujenga kuliko kushiriki katika maandamano ya kisiasa na kuzusha ghasia. Hatimaye, nilikuwa nikiwasaidia watu kikweli!

Katika mwaka wa 2006, misukosuko ya kisiasa na ya vikundi tofauti-tofauti ilizuka tena nchini Timor Mashariki. Vikundi vilipigana kwa sababu ya mizozo ya muda mrefu. Jiji la Dili lilishambuliwa mara kadhaa, na watu ambao kiasili walitoka upande wa mashariki wa nchi hiyo waliamua kukimbia ili wasiuawe. Mimi na Mashahidi wengine, tulikimbilia mji wa Baucau, mji mkubwa ulioko kilomita 120 hivi mashariki ya Dili. Hata ingawa hali yetu ilikuwa ngumu, tulibarikiwa kuanzisha kutaniko jipya—kutaniko la kwanza nje ya Dili.

Miaka mitatu baadaye, katika mwaka wa 2009, nilipata mwaliko wa kuhudhuria shule ya pekee ya wahudumu wa Kikristo wa wakati wote, huko Jakarta, Indonesia. Mashahidi wa Jakarta walinikaribisha nyumbani kwao na mioyoni mwao. Upendo wao wa kweli ulinivutia sana. Nilijihisi nikiwa sehemu ya “ushirika . . . wa akina ndugu” wa ulimwenguni pote, “familia” ya kimataifa ambayo ilinijali kikweli.—1 Petro 2:17.

Hatimaye Napata Amani!

Baada ya kumaliza shule hiyo, nilirudi Baucau, ambako ninaishi hadi leo. Ninafurahia kuwasaidia wengine kiroho katika eneo hili, kama tu nilivyosaidiwa. Kwa mfano, katika kijiji kimoja nje ya Baucau, mimi na Mashahidi wengine tunafundisha watu 20 hivi Biblia, kutia ndani watu wengi wenye umri mkubwa ambao hawajui kusoma na kuandika. Kikundi hicho chote kinahudhuria mikutano ya kila juma, na watatu kati yao wamejiunga nasi katika “familia” ya kiroho wakiwa washiriki waliobatizwa wa kutaniko la Kikristo.

Miaka kadhaa iliyopita, nilikutana na Felizarda, msichana mchangamfu aliyekubali kujifunza kweli za Biblia, akafanya maendeleo haraka, na kubatizwa. Tulioana mwaka wa 2011. Pia ninafurahi kusema kwamba Andre, mtu wangu wa ukoo, anatumika katika ofisi ya Mashahidi wa Yehova ya Timor Mashariki. Hata watu wengi wa ukoo wangu, kutia ndani nyanya ya Andre, ambaye wakati mmoja alitisha kwamba atatuzika, sasa wanaheshimu imani yangu.

Zamani nilikuwa na hasira na nilijihisi kuwa sipendwi wala siwezi kupendwa. Lakini ninamshukuru Yehova kwamba hatimaye nimepata upendo na amani ya kweli!

[Picha katika ukurasa wa 19]

Egidio akiwa mwanaharakati wa kisiasa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Egidio na Felizarda wakiwa na washiriki wa Kutaniko la Baucau, Timor Mashariki