Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Kitabu Cha Unabii Sahihi, Sehemu Ya 3

Biblia Kitabu Cha Unabii Sahihi, Sehemu Ya 3

Biblia Kitabu Cha Unabii Sahihi, Sehemu Ya 3

“Tumempata Masihi”

Katika mfululizo huu wa makala nane, gazeti la “Amkeni!” litazungumzia jambo la pekee kuhusu Biblia—unabii wake, au utabiri. Makala hizi zitakusaidia kujibu maswali haya: Je, unabii wa Biblia ulibuniwa na wanadamu werevu? Au kuna mambo yanayoonyesha kwamba uliongozwa na roho ya Mungu? Tunakukaribisha uchunguze uthibitisho.

KARNE nyingi kabla ya Yesu kuzaliwa, manabii Waebrania walitabiri kuhusu kuja kwa Masihi, neno ambalo katika Kiebrania linamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Manabii hao walitoa habari hususa kuhusu maisha ya Masihi—kutia ndani nasaba yake—mahali na wakati ambapo angetokea, na mambo ambayo yangempata.

Wakristo katika karne ya kwanza W.K. waliamini kwamba unabii huo mbalimbali ulitimizwa na Yesu. Walihisi kama mwanafunzi Andrea ambaye alimwambia hivi ndugu yake Simoni: “Tumempata Masihi.” (Yohana 1:40, 41) Je, mkataa huo ulikuwa sahihi? Ingawa kuna unabii mwingi kumhusu Masihi, acheni tuchunguze baadhi tu ya unabii huo na katika kila kisa tutachunguza uthibitisho uliopo.

Unabii wa 1: “Atachukua wadhifa wa mfalme Daudi.”—Isaya 9:7, “Biblia Habari Njema.”

Utimizo: Injili ya Mathayo inaanza kwa maneno haya: “Kitabu cha historia ya Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Abrahamu.” Kisha Mathayo anafuata nasaba ya Yesu kupitia Daudi, kama anavyofanya pia Luka, mwandikaji wa Injili.—Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-38.

Historia inafunua nini?

● Maandishi ya mwanahistoria Myahudi Yosefu yanaonyesha kwamba rekodi za ukoo za familia za Kiyahudi zilipatikana katika hifadhi za rekodi za umma. Rekodi hizo ziliharibiwa katika mwaka wa 70 W.K. wakati ambapo Yerusalemu liliharibiwa. Lakini kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu, dai la kwamba Yesu alikuwa wa uzao wa Daudi lilikuwa limezungumziwa sana. (Mathayo 9:27; 20:30; 21:9) Endapo dai hilo lilikuwa la uwongo, mtu yeyote angelipinga au hata kulikanusha. Hata hivyo, hakuna maandishi yanayoonyesha kwamba kuna mtu yeyote aliyethubutu kufanya hivyo.

Unabii wa 2: “Ee Bethlehemu Efratha, wewe uliye mdogo sana kuwa kati ya maelfu ya Yuda, kutoka kwako atanijia yeye atakayekuwa mtawala katika Israeli.”—Mika 5:2.

Utimizo: Yesu alizaliwa Bethlehemu. Kaisari Augusto alipoagiza watu wahesabiwe, baba mlezi wa Yesu, Yosefu, alilazimika kutoka Nazareti kwenda “Yudea [Yuda], kwenye jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu, kwa sababu alikuwa mshiriki wa nyumba na familia ya Daudi, ili apate kuandikishwa pamoja na Maria.” Wakiwa huko, Maria “akamzaa mwana wake,” Yesu.—Luka 2:1-7.

Historia inafunua nini?

● Vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinathibitisha kwamba Waroma waliwahesabu watu katika Mashariki ya Kati kwa kusudi la kukusanya kodi na kuwaandikisha watu jeshini. Uthibitisho wa kazi hiyo ya kuhesabu watu unaonekana katika agizo la gavana wa Roma huko Misri mnamo 104 W.K. Nakala ya agizo hilo, ambayo sasa inapatikana katika Maktaba ya Uingereza, inasema hivi: “Kwa kuwa wakati wa kuhesabiwa kwa watu kutoka nyumba hadi nyumba umefika, watu wote wanaoishi nje ya [wilaya] zao kwa sababu zozote zile wanashurutishwa warudi nyumbani kwao, ili waweze kuhesabiwa, na pia ili waweze kupalilia kwa bidii mashamba yao waliyogawiwa.”

● Wakati ambapo Yesu alizaliwa, kulikuwa na majiji mawili huko Israeli yaliyoitwa Bethlehemu. Jiji moja lilikuwa upande wa kaskazini karibu na Nazareti. Jiji lile lingine, ambalo hapo awali linaonekana kuwa liliitwa Efrathi (au Efratha) lilikuwa karibu na Yerusalemu huko Yuda. (Mwanzo 35:19) Yesu alizaliwa katika jiji hilo la Efratha, kama tu Mika alivyokuwa ametabiri karne nane hivi mapema.

Unabii wa 3: “Tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.”—Danieli 9:25.

Utimizo: Kipindi cha wakati kilichotajwa katika unabii wa Danieli kilikuwa na jumla ya vipindi 69 vya miaka 7 kila kimoja, au miaka 483. Kujengwa upya kwa Yerusalemu kulianza katika mwaka wa 455 K.W.K. Kama ilivyotabiriwa, miaka 483 (majuma 69 ya miaka) baadaye, katika mwaka wa 29 W.K., Yesu akawa Mtiwa-Mafuta, au Masihi, alipobatizwa na kutiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu. *Luka 3:21, 22.

Historia inafunua nini?

● Mapema katika karne ya kwanza W.K., “watu walikuwa wakitarajia” Masihi atokee. (Luka 3:15) Katika kitabu chake A History of Messianic Speculation in Israel, msomi Myahudi Abba Hillel Silver anaandika kwamba kipindi cha kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu “kilikuwa na msisimuko mwingi wa kumtarajia Masihi.” Pia anasema kwamba “Masihi alitarajiwa atokee katika robo ya pili ya karne ya kwanza.” Silver anaandika kwamba msisimuko huo wa Wayahudi, ulitegemea “mfuatano wa matukio yaliyotarajiwa wakati huo ambayo watu waliyafahamu vizuri.”

Unabii wa 4: “Atafanya kaburi lake liwe pamoja na waovu, na pamoja na jamii ya matajiri katika kifo chake.”—Isaya 53:9.

Utimizo: Yesu aliuawa kando ya wahalifu wawili waliokuwa wamehukumiwa, hata hivyo, alizikwa katika kaburi lililokuwa la mwamini tajiri—Yosefu wa Arimathea.—Mathayo 27:38, 57-60; Yohana 19:38.

Historia inafunua nini?

● Waandikaji wengi wa kale wasio Wakristo—kutia ndani mwanahistoria Myahudi Yosefu na mwanahistoria Mroma Tasito—wanathibitisha kwamba Yesu aliuawa kama mhalifu.

● Uchunguzi wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa huko Palestina umefunua makaburi ya kale yaliyo na vyumba au visanduku vilivyochimbwa katika mwamba. Kwa mtu tajiri na mwenye uvutano kama Yosefu wa Arimathea, haingekuwa vigumu kwake kuwa na kaburi lililokuwa tayari limechimbwa na linaloweza kutumiwa.

Unabii ambao umezungumziwa ni baadhi ya unabii mwingi wa Kimasihi ambao ulitimizwa na Yesu. Kwa wazi, hakuna mwanadamu anayeweza kuthibitisha kuwa utimizo wa unabii huo wenye mambo hususa ulikuwa uwongo. Utimizo wake hususa unaimarisha imani yetu kwamba Mungu ndiye Chanzo cha unabii huo na kwamba atahakikisha kuwa unabii mwingi uliotabiri kuhusu baraka zitakazoletwa na Masihi kwa ajili ya wanadamu watiifu utatimizwa.

Katika makala inayofuata ya mfululizo huu, tutazungumzia swali hili lenye kuchochea fikira: Ikiwa kwa kweli Yesu alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa, kwa nini alijiruhusu ateseke na kufa?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Kwa habari zaidi kuhusu unabii huo unaohusu wakati wa kutokea kwa Masihi, ona ukurasa wa 197-199 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 22, 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ORODHA YA MATUKIO YA UNABII FULANI KUMHUSU MASIHI

1 Masihi angekuwa mzao wa Mfalme Daudi

1070 K.W.K.

Daudi anakuwa mfalme wa Israeli yote

607 K.W.K.

Yerusalemu linaharibiwa na Wababiloni

455 K.W.K.

Amri inatolewa ya kurudi na kujenga upya Yerusalemu

2 Masihi angezaliwa katika Bethlehemu ya Yuda

2 K.W.K.

Yesu anazaliwa Bethlehemu ya Yuda katika nasaba ya Daudi

3 Masihi angewasili miaka 483 baada ya amri ya kujenga upya Yerusalemu kutolewa

29 W.K.

Yesu anabatizwa na kutiwa mafuta kuwa Masihi

4 Masihi angekufa na watenda-dhambi na angezikwa na matajiri

33 W.K.

Yesu anakufa kando ya wahalifu na kuzikwa na matajiri