Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Je, Sisi Ni Marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 2

Je, Sisi Ni Marafiki Tu—Au Ninavutiwa Naye Kimahaba?, Sehemu ya 2

KATIKA TOLEO LILILOPITA, tulichunguza mambo mawili ya hakika kuhusu maisha.

● Unapoanza kuvutiwa kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa, utaumia hisia.—Methali 6:27.

● Unapoanza kuvutiwa kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa, unaweza kupoteza rafiki mzuri. *Methali 18:24.

KATIKA TOLEO HILI, tutazungumzia

● Jambo la tatu la hakika kuhusu kuvutiwa na mtu kimahaba

● Jinsi unavyoweza kujua ikiwa urafiki wako na mtu wa jinsia tofauti umepita mipaka

UKWELI WA MAMBO: Unapoanza kuvutiwa kimahaba kabla ya kuwa tayari kuoa au kuolewa, unaweza kujiharibia sifa. Mia * anasema: “Nimewaona wavulana ambao wana marafiki wengi wasichana. Kwa kusema kweli, wao huwachezea tu. Wasichana wenyewe wanafikiri kwamba mvulana huyo anavutiwa nao, lakini kumbe yeye anafurahia tu kwamba wasichana wengi wanavutiwa naye.”

Jambo la kufikiria:

● Iwe wewe ni mvulana au msichana, kuwa na urafiki wa karibu sana na watu wa jinsia tofauti kunawezaje kukuharibia sifa?

“Kuwatumia ujumbe mfupi watu wa jinsia tofauti ni kujiletea shida. Unaanza polepole kutuma ujumbe kwa mtu mmoja, lakini baadaye unajikuta ukituma ujumbe kwa watu wengi. Bila hata kujua, unakuwa umeanzisha urafiki wa karibu na wavulana watatu wakati uleule, na kila mmoja wao anafikiri kuwa ni yeye tu unayevutiwa naye. Wanapojua ukweli wa mambo, wanaumia hisia—na unapata sifa mbaya ya kuwa mtu anayewachezea wengine kimahaba.”—Lara.

Biblia inasema hivi: “Kwa matendo yake, mvulana [au msichana] hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.”—Methali 20:11.

Jambo kuu: Si vibaya kuchagamana na watu wa jinsia tofauti. Lakini usipojiwekea mipaka, unaweza kujiumiza, kuharibu urafiki mzuri, na kujiharibia sifa.

Unawezaje kujua ikiwa umevuka mipaka? Njia moja ni kwa kujiuliza hivi, ‘Je, rafiki huyo amekuwa ndiye mtu pekee ninayemwambia siri zangu?’ Msichana anayeitwa Erin anasema hivi: “Kama mvulana fulani kwa kweli ni rafiki tu, hapaswi kuwa ndiye mtu wa kwanza unayetaka kuongea naye kila siku au awe ndiye wa kwanza kumjulisha habari muhimu. Bila shaka hapaswi kuwa ndiye mtu unayemweleza hisia zako za ndani.”

Jambo la kufikiria:

● Kwa nini huenda ikaonekana kuwa inavutia kumweleza mtu wa jinsia tofauti mambo yako ya siri? Lakini kuna hatari gani?

“Sina urafiki wa karibu sana pamoja na wavulana ninaowafahamu. Siongei nao kwa muda mrefu kwenye simu kama vile ninavyoongea na rafiki yangu wa kike. Na kuna mambo fulani ambayo siwezi kuongea na wavulana.”—Rianne.

Biblia inasema hivi: “Achungaye mdomo wake huyahifadhi maisha yake, anayeropoka ovyo hujiletea maangamizi.”—Methali 13:3, Biblia Habari Njema.

Fikiria hili: Je, kuna hatari yoyote ya kumfunulia mtu wa jinsia tofauti mambo mengi? Namna gani mkiacha kuwa marafiki wa karibu? Je, utajuta kwamba ulimfunulia mambo yote hayo?

Tineja anayeitwa Alexis anasema hivi kwa ufupi: “Usimwepuke mtu kwa sababu tu ni wa jinsia tofauti. Kwa upande mwingine, usijidanganye na kusema kwamba nyinyi ni marafiki tu ikiwa hilo si kweli. Dhibiti hisia zako, na utaepuka maumivu mengi ya kihisia.”

Unaweza kupata makala zaidi za “Vijana Huuliza” katika Tovuti ya www.watchtower.org/ype

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi, ona Amkeni! la Juni 2012, ukurasa wa 15-17.

^ fu. 9 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

SIMULIZI HALISI: “Nilikuwa na rafiki mvulana, na tulikuwa na uhusiano mzuri sana. Lakini nikagundua kwamba mazungumzo yetu yalianza kuwa marefu zaidi na yalihusu mambo ya kibinafsi zaidi. Nilijua kwamba uhusiano wetu umeanza kuwa wa karibu zaidi kwa sababu angeniambia mahangaiko yake yote. Kisha siku moja akanitumia barua pepe na kuniambia kwamba ananipenda. Sikujua nimwambie nini. Kwa njia fulani nilisisimuka—inafurahisha unapojua kwamba mtu fulani anavutiwa na wewe. Lakini nilikuwa na wasiwasi. Nilijua hatungeweza kuendelea kuwa “marafiki tu” kwa sababu ni wazi kwamba alifikiria tuna uhusiano wa kimahaba. Nilijua kwamba nikimwambia kuwa sisi ni wachanga mno na hatuwezi kuanzisha urafiki wa kimahaba, ataumia hisia. Niliwaeleza wazazi wangu kila kitu, na walikazia jinsi ilivyokuwa muhimu kwetu wawili kupunguza mawasiliano yetu. Kisa hicho kilinifanya nitambue kwamba ni rahisi sana kwa jambo dogo tu linalofanywa kwa nia nzuri kugeuka kuwa jambo zito sana. Na tangu wakati huo, nimejiwekea mipaka ya jinsi ninavyoshughulika na watu wa jinsia tofauti, hasa ninapotuma ujumbe mfupi. Pia, ni afadhali kuchangamana mkiwa kikundi badala ya kuwa na mtu yuleyule wa jinsia tofauti kila wakati. Kwa njia hiyo, mazungumzo yenu hayatahusu sana mambo ya kibinafsi na hutajiingiza katika uhusiano wa karibu na mtu huyo.”—Elena.

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Waulize wazazi wako maoni yao kuhusu maswali mawili yaliyo chini ya kichwa “Jambo la kufikiria” katika makala hii. Je, maoni yao yanatofautiana na yako? Ikiwa ndivyo, yanatofautianaje? Unaona maoni yao yanaweza kukufaidi jinsi gani?​—Methali 1:8.

[Picha katika ukurasa wa 18]

MAMBO AMBAYO VIJANA WENZAKO WANASEMA

Andre—Kadiri unavyotumia wakati mwingi zaidi na msichana, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kuanza kuwa na hisia kumwelekea na ndivyo mtu huyo anavyozidi kufikiri kwamba una hisia za kimahaba kumwelekea. Kama una miradi ambayo unataka kutimiza kabla ya kuanzisha uchumba, basi usifanye ionekane kana kwamba unataka kuuanzisha.

Cassidy—Mimi ni mtu mwenye urafiki sana, na kwa sababu nililelewa pamoja na wavulana, mimi hujihisi nikiwa huru kabisa ninapokuwa nao—jambo ambalo nyakati nyingine huleta matatizo. Si vizuri kumtendea mvulana sawa na unavyomtendea msichana—anaweza kupata picha mbaya. Mimi huwatendea wavulana sawa na jinsi ambavyo ningemtendea ndugu yangu.

[Picha katika ukurasa wa 19]

TAARIFA KWA WAZAZI

Katika hali zinazofaa, si vibaya kwa vijana kuchangamana na wenzao wa jinsia tofauti. Lakini wale ambao hawako tayari kuoa au kuolewa wanapaswa kujiwekea mipaka. * Kwa vijana kama hao, urafiki pamoja na watu wa jinsia tofauti unapaswa kuwa na mipaka.

Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa watu wawili ambao hawako tayari kuoa au kuolewa wanaanza kuwa na hisia za kimahaba? Mwanzoni, huenda wakasisimuka lakini baadaye huenda wakavunjika moyo. Ni kama kupanda gari ambalo halina magurudumu. Baada ya muda, mvulana au msichana anagundua kwamba uhusiano wao hausongi mbele. Wengine wanaweza kuanza kuchumbiana kisiri—hali ambayo inaweza kuleta matatizo mengi ya kiadili. Wengine huvunja uhusiano wao—hatua ambayo inaweza kuwaacha wote wakihisi kwamba wamedanganywa, wameumizwa, na hata kufadhaishwa. Unawezaje kumsaidia kijana wako aepuke kuanzisha urafiki wa kimahaba akiwa mchanga?—Mhubiri 11:10.

Jambo la maana zaidi unaloweza kufanya ni kuwa na mawasiliano mazuri pamoja na kijana wako kuhusiana na urafiki pamoja na watu wa jinsia tofauti. Kwa njia hiyo, utajua—na utaweza kusaidia—endapo urafiki utaanza kupita mipaka.

Bila kujua, wazazi fulani huwazuia vijana wao wasizungumze nao kuhusu mahusiano yao pamoja na watu wa jinsia tofauti. Fikiria mambo ambayo vijana fulani walimwambia mwandishi wa Amkeni!

“Nilitaka sana kumwambia mama yangu kuhusu mtu niliyevutiwa naye, lakini sikuweza kwa sababu nilifikiri atakasirika sana.”—Cara.

“Nilipomwambia mama yangu kwamba nilivutiwa na mvulana fulani, alisema, ‘Usitarajie kuniona kwenye arusi yenu!’ badala ya kuniambia ‘Hebu niambie, rafiki yako ni mtu wa aina gani. Kwa nini unavutiwa naye?’ Ikiwa mama angeniuliza maswali kama hayo, ningefuata mashauri yake.”—Nadeine.

Kinyume na hilo, hebu ona matokeo mazuri wakati wazazi wanaposikiliza kwa subira na kutoa mwongozo unaofaa.

“Wazazi wangu hawakukasirika nilipowaambia kuhusu kijana niliyevutiwa naye. Walisema mambo niliyohitaji kusikia, lakini walielewa hisia zangu. Kwa sababu hiyo, inakuwa rahisi kwangu kusikiliza mashauri yao na kuwafunulia mawazo na hisia zangu.”—Corrina.

“Wazazi wangu waliponieleza kuhusu watu waliovutiwa nao walipokuwa wachanga—hata wakaniambia kwa nini mahusiano fulani hayakufaulu—ilinisaidia kutambua kwamba haikuwa vibaya kuongea na wazazi wangu kuhusu hisia zangu kumwelekea mtu fulani.”—Linette.

Pia, kumbuka kwamba wakati mwingine huenda kuna sababu nyingine zinazoweza kufanya kijana aanzishe uhusiano wa kimahaba akiwa mchanga.

“Nilimchumbia kijana fulani kisiri kwa sababu alinifanya nifurahi na alinisikiliza.”Annette.

“Kuna mvulana mmoja ambaye kila mara nilifurahia kuwa naye. Alionyesha kuwa anapendezwa nami na huo ndio udhaifu wangu. Mimi hufurahi watu wanapopendezwa nami, iwe inafaa au la.”Amy.

“Wazazi wangu wanaponiambia kwamba mimi ni mrembo au vazi fulani linapendeza ninapolivaa, mimi huhisi sihitaji tena mvulana fulani aniambie jambo hilo.”Karen.

Jiulize hivi:

Ninawezaje kuwa mwenye kufikika zaidi kwa kijana wangu?—Wafilipi 4:5.

Je, mimi ni “mwepesi kuhusu kusikia, [na] si mwepesi wa kusema”?—Yakobo 1:19.

Ninaweza kufanya nini ili kijana wangu asishawishiwe kutafuta upendo na kibali kutoka kwa watu nje ya familia?—Wakolosai 3:21.

Jambo kuu: Msaidie kijana wako ajifunze kudumisha urafiki unaofaa pamoja na watu wa jinsia tofauti ambao hautaleta matatizo. Jambo hilo litamsaidia atakapokuwa mtu mzima.—Wakolosai 3:5; 1 Wathesalonike 4:3-6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 37 Ona makala iliyotangulia na pia makala ya “Vijana Huuliza” katika Amkeni! la Juni 2012.

[Chati katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MIPAKA

FANYA

changamaneni na wengine mkiwa kikundi

fahamianeni

furahieni mazungumzo

EPUKA

X kuwa na mtu yuleyule wa jinsia tofauti kila wakati

X kuongea mambo ya siri

X kuchezeana kimahaba

[Mchoro katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KUCHANGAMANA

KUCHEZEANA KIMAHABA

KUGUSANA-GUSANA

KUSHIKANA MIKONO

KUPIGANA BUSU

KUGUSANA-GUSANA

KUSHIKANA MIKONO

KUPIGANA BUSU