Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Watoto Wanaoomboleza

Kuwasaidia Watoto Wanaoomboleza

Kuwasaidia Watoto Wanaoomboleza

Si rahisi kumwambia mtu mzima kuhusu kifo cha mpendwa. Kwa hiyo, hebu wazia jinsi ilivyo vigumu kumweleza mtoto.

WATOTO wengi huchanganyikiwa—au hata kuogopa—wanapompoteza mtu wa familia au rafiki. Inakuwa vigumu sana kumsaidia mtoto kukabiliana na kipindi hicho, hasa kwa wazazi ambao pia wanaomboleza. Isitoshe, wazazi pia wanahitaji kufarijiwa.

Wazazi fulani hujaribu kufanya iwe rahisi kwa mtoto kukubali habari hizo kwa kumwambia kwamba mpendwa wao aliyekufa amewaacha au ameondoka. Hata hivyo, maneno kama hayo ni yenye kupotosha na ya uwongo. Basi, unawezaje kumweleza mtoto kuhusu kifo?

Renato na Isabelle walikabili tatizo kama hilo. Binti yao Nicolle mwenye umri wa miaka mitatu na nusu alipokufa, walihitaji kumsaidia mwana wao Felipe, aliyekuwa na umri wa miaka mitano akabiliane na kifo hicho.

Amkeni!: Mlimwelezaje Felipe kuhusu kifo cha Nicolle?

Isabelle: Tuliamua kusema kweli na hatukumficha chochote. Tulimtia moyo aulize maswali, na tulijitahidi kuyajibu kwa njia ambayo mtoto aliye na umri wake angeweza kuelewa. Nicolle alikufa kutokana na maambukizo ya bakteria, kwa hiyo tulimwambia kwamba mdudu mdogo sana alikuwa ameingia ndani ya mwili wake na madaktari hawakufaulu kuua mdudu huyo.

Amkeni!: Je, mlimweleza Felipe yale ambayo dini yenu inasema kuhusu kifo?

Renato: Sisi ni Mashahidi wa Yehova na tulijua kwamba tungemfariji Felipe kwa kumweleza mafundisho yetu yanayotegemea Biblia kuhusu kifo. Biblia inasema mambo waziwazi kabisa—inafundisha kwamba wafu hawajui lolote. (Mhubiri 9:5) Tulitambua kwamba kuzungumza na Felipe kuhusu jambo hilo, kungeondoa woga wowote anaoweza kuwa nao—kama vile, kuhusu kuachwa akiwa peke yake usiku.

Isabelle: Biblia pia inafundisha kwamba wale ambao wamekufa watafufuliwa waishi katika dunia iliyo paradiso. Tunaamini jambo hilo, na tulihisi kwamba imani hiyo ingemsaidia Felipe pia. Kwa hiyo, tulizungumza naye kuhusu kile ambacho Biblia inafundisha. Tulizungumza kuhusu simulizi la Biblia la Yesu kumfufua binti ya Yairo aliyekuwa na umri wa miaka 12. Kisha tukamweleza Felipe kwamba Nicolle atafufuliwa pia. Biblia inafundisha hivyo.—Marko 5:22-24, 35-42; Yohana 5:28, 29.

Amkeni!: Je, mnafikiri Felipe angeweza kuelewa habari hiyo yote?

Renato: Ndiyo, tuliamini angeelewa. Watoto huelewa na kuvumilia hali zinazohusiana na kifo wanapopewa habari ya kweli, sahihi, rahisi, na inayoeleweka vizuri. Hakuna haja ya kuficha chochote. Kifo ni kitu halisi. Inasikitisha kwamba bado kifo ni sehemu ya maisha. Kwa hiyo, wazazi wanahitaji kuwafundisha watoto wao jinsi ya kukabiliana na hisia zao mtu anapokufa, na baadaye tulifanya vivyo hivyo na mwana wetu mdogo Vinicius. *

Amkeni!: Je, mliandamana na Felipe kwenye mazishi?

Renato: Baada ya kuchunguza faida na madhara ya kufanya hiyo, tuliamua asije. Watoto walio na umri wake huathiriwa sana. Bila shaka, wazazi wengine huamua kuandamana na mtoto wao, na kila mtoto ni tofauti ikitegemea anaweza kukabiliana na hali jinsi gani. Ikiwa mtoto atapelekwa kwenye mazishi, ni vizuri kumweleza mambo yatakayotendeka huko.

Amkeni!: Lazima muwe mlikuwa na huzuni sana kipindi ambacho Nicolle alikufa. Je, mliogopa mwana wenu asiwaone mkilia?

Isabelle: Hatukujaribu kumficha Felipe hisia zetu. Ikiwa Yesu ‘alitokwa na machozi’ wakati mtu fulani aliyempenda alipokufa, kwa nini sisi tusifanye hivyo pia? (Yohana 11:35, 36) Na kwa nini Felipe asituone tukilia? Kuonyesha huzuni yetu waziwazi kulimwonyesha Felipe kwamba kutoa machozi si vibaya. Ni njia ya kuonyesha hisia. Tulitaka Felipe ahisi kwamba anaweza kuonyesha hisia zake pia, badala ya kuzifungia.

Renato: Familia inapokumbwa na msiba, watoto huhisi kwamba hawana usalama. Kwa hiyo, ikiwa sisi wazazi tunaonyesha hisia zetu kwa unyoofu, watoto pia watafanya hivyo. Baada ya kusikiliza kwa makini kinachowasumbua, tutaweza kuwategemeza na kupunguza wasiwasi wao.

Amkeni!: Je, mlipata msaada wowote kutoka kwa wengine?

Renato: Ndiyo, washiriki wa kutaniko letu walitutegemeza sana. Walipotutembelea, kutupigia simu, na kututumia kadi, Felipe angeweza kuona jinsi walivyotupenda na kutujali.

Isabelle: Watu wa familia yetu walitusaidia sana pia. Baada ya kifo cha Nicolle, baba yangu aliamua kuja kila asubuhi kula kiamsha-kinywa pamoja nasi. Ilikuwa njia yake ya kututegemeza kwa upendo. Na Felipe alitiwa moyo sana kuwa pamoja na babu yake.

Renato: Kitia-moyo cha kiroho ambacho tulipata katika mikutano ya Kikristo kilitusaidia sana. Tulijitahidi sana tusikose mikutano, hata ingawa nyakati nyingine tulishindwa kuzuia machozi. Kwa kweli, kuwa kwenye mikutano ya Kikristo kulitufanya tukumbuke pindi ambazo tulikuwa na Nicolle. Lakini tulijua kwamba lazima tuendelee kuwa imara, hasa kwa faida ya Felipe.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kwa habari zaidi, ona makala “Msaidie Mtoto Wako Akabiliane na Huzuni,” kwenye ukurasa wa 18-20 wa toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2008, na broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 14]

Vitabu vilivyoorodheshwa hapa chini, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova, vinaweza kuwafariji watu waliopoteza mpendwa katika kifo.

KWA WATU WAZIMA:

Biblia Inafundisha Nini Hasa?

Sura ya 6: Wafu Wako Wapi?

Sura ya 7: Tumaini Hakika kwa Wapendwa Wako Ambao Wamekufa

KWA WATOTO WACHANGA:

Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia

Hadithi ya 92: Yesu Anafufua Wafu

KWA WATOTO AMBAO BADO SI MATINEJA:

Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu

Sura ya 34: Inakuwaje Tunapokufa?

Sura ya 35: Tunaweza Kufufuliwa!

Sura ya 36: Ni Nani Watakaofufuliwa? Nao Wataishi Wapi?

KWA VIJANA WANAOBALEHE:

Maswali Ambayo Vijana Huuliza Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1

Sura ya 16: Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 15]

JINSI YA KUSAIDIA

● Mtie moyo aulize maswali. Onyesha kwamba uko tayari iwapo mtoto wako anataka kuzungumza kuhusu kifo na maana yake.

● Epuka kutumia maneno ya kijuujuu tu yasiyo na maana—kama vile, kusema kwamba aliyekufa “ametuacha” au “ameondoka.”

● Eleza kuhusu kifo kwa njia rahisi na ya moja kwa moja. Wengine husema kwamba mwili wa mpendwa “umeacha kufanya kazi” na “haukuweza kurekebishwa.”

● Mweleze mtoto mambo yatakayotukia kwenye mazishi; mweleze kwamba aliyekufa hataweza kuona au kusikia mambo yanayoendelea.

● Usifiche hisia zako. Kwa njia hiyo mtoto wako ataona kwamba ni jambo la kawaida kuomboleza.

● Kumbuka, hakuna njia “inayofaa” ya kuomboleza. Kila mtoto—na kila hali—ni tofauti.

[Hisani]

Chanzo: www.kidshealth.org

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kuanzia juu kushoto hadi kulia: Felipe, Renato, Isabelle, na Vinicius