Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Anayeweza Kuubadili Ulimwengu Wetu?

Ni Nani Anayeweza Kuubadili Ulimwengu Wetu?

Maoni Ya Biblia

Ni Nani Anayeweza Kuubadili Ulimwengu Wetu?

“Watu ulimwenguni wanataka majibu kutoka kwa viongozi wao. Wanatarajia kupata suluhisho, si jitihada nusunusu au udhuru.”—KATIBU MKUU WA UMOJA WA MATAIFA BAN KI-MOON.

TUNAISHI katika kipindi ambacho Biblia inakiita “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Vyombo vya habari vimejaa ripoti zenye kuogopesha kuhusu vita, ugaidi, matatizo ya kiuchumi, na tisho la kuharibiwa kwa mazingira.

Je, kuna tumaini lolote kwamba mambo yatabadilika na kuwa afadhali? Je, serikali za wanadamu zinaweza kutatua matatizo ya ulimwengu? Au tunahitaji kutafuta msaada kwingine?

Mataifa Mengi Yanadai Nini?

Mataifa mengi yanadai kwamba yanaungwa mkono na Mungu. Kwa mfano, katika Kiapo chake cha Uaminifu, Marekani inadai kuwa “taifa moja chini ya Mungu” (one nation under God) na sarafu na noti za nchi hiyo zina maneno “Tunamtumaini Mungu” (In God We Trust).

Bila shaka, watu wengi wanaoishi nchini Marekani hata hawaamini kwamba Mungu yupo, na ndivyo ilivyo katika nchi nyingine zinazodai kuwa zinaungwa mkono na Mungu. Hata watu wanaoamini kwamba Mungu yuko wana maoni yanayotofautiana kuhusu ni kwa kadiri gani anaingilia mambo ya wanadamu.

● Watu fulani husema kwamba Mungu hajishughulishi kabisa na mambo ya wanadamu na ameacha wanadamu wajitawale.

● Wengine husema kwamba Mungu anafanya kazi kupitia serikali za wanadamu na kwamba yeye anaweza kubariki jitihada zao za kuubadili ulimwengu.

Maoni yako ni gani kati ya hayo mawili?

Fikiria hili: Ikiwa maoni yaliyotajwa kwanza ni ya kweli, basi tungekuwa katika taabu kubwa. Ikiwa maoni yale ya pili yangekuwa ya kweli, basi tungelazimika kujiuliza: ‘Je, Mungu anapendelea taifa moja kuliko lingine? Mataifa mawili yanapoenda vitani na yote yasali kwa bidii na kwa unyofu ili Mungu awape ushindi, Mungu atakuwa upande wa nani?’ Je, inawezekana kwamba yeye haungi mkono upande wowote?

Yale Ambayo Biblia Inafundisha

1. Mwanadamu haukuumbwa ajitawale. Biblia inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Historia inathibitisha ukweli wa maneno hayo. Serikali za wanadamu zimeshindwa kuleta ulimwengu bora, hata viongozi wao wanapokuwa na sera na nia nzuri. Badala yake, “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.

2. Mungu anajali hali zinazotupata. Anajua na anajali kuhusu mambo yanayotupata. Isitoshe, atachukua hatua za kutusaidia. Jinsi gani? Kupitia Ufalme wake ambao “hautaharibiwa kamwe.”—Danieli 2:44.

3. Ufalme wa Mungu ni serikali halisi. Ufalme huo ndio ule ambao mamilioni ya watu wanyofu husali kuuhusu katika ile sala ya Baba Yetu, au Sala ya Bwana ambayo hurudiwa mara nyingi. Katika sala hiyo, watu humsihi Mungu hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ona kwamba Ufalme wa Mungu haushughuliki na mambo ya mbinguni tu; utafanya pia mapenzi ya Mungu yatimizwe duniani.

4. Mungu anaweza kuutumia Ufalme wake kuubadili ulimwengu wetu, naye atafanya hivyo. Ikiwa huamini hilo, fikiria yale ambayo Biblia inafundisha.

● Mungu aliwapa wanadamu mwanzo mkamilifu katika mazingira yenye amani.—Mwanzo 1:27-31.

● Licha ya matatizo tunayoona, Mungu hajatupilia mbali kusudi lake kwa dunia yetu.—Zaburi 37:11, 29.

● Tayari Mungu amechukua hatua za kurudisha dunia yetu—na wanadamu—katika hali aliyokuwa amekusudia.—Yohana 3:16.

Ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na jinsi utakavyobadili ulimwengu wetu? Mashahidi wa Yehova, ambao ndio huchapisha gazeti hili, watafurahi kukusaidia. Zungumza nao mambo yafuatayo watakapokutembelea tena nyumbani.

Ufalme wa Mungu ni nini?

Utaleta mabadiliko gani?

Ufalme wa Mungu utaleta mabadiliko hayo lini na jinsi gani?

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Kwa nini serikali za wanadamu haziwezi kuboresha ulimwengu?—Yeremia 10:23.

● Mungu ameonyeshaje kwamba anatujali?—Yohana 3:16.

● Ufalme wa Mungu utafanya nini kiwezekane kwa dunia na wale wanaoishi ndani yake?—Zaburi 37:11, 29.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Je, serikali za wanadamu zinaweza kusuluhisha matatizo ya ulimwengu? Au tutafute msaada kwingine?