Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Visababishi Vya Jeuri

Visababishi Vya Jeuri

Visababishi Vya Jeuri

NI VIGUMU kueleza ni nini kinachosababisha jeuri. Na mara nyingi jeuri haisababishwi na jambo moja tu, kama vile marafiki, burudani, au mazingira ya kijamii. Huenda mambo mengi yakahusika, kutia ndani mambo yafuatayo.

Kuvunjika moyo na kukata tamaa. Nyakati nyingine watu hutenda kwa jeuri wanapokandamizwa, kubaguliwa, kutengwa na jamii, au kwa sababu ya umaskini au wanapoona kwamba hawawezi kujitegemeza.

Kufuata umati. Kama inavyoonekana mara nyingi katika michezo mingi, watu wanapokuwa katika vikundi au umati, wanashindwa kujizuia wasitende kwa njia isiyofaa. Kwa nini? “Huenda wakasahau viwango vyao vya maadili na yaelekea watatenda kwa jeuri au ukatili wanapochochewa,” kinasema kitabu Social Psychology. Kitabu kingine kinasema kwamba huenda watu kama hao wakaongozwa kutenda bila kufikiri na wakati huo “wakahisi kwamba hawawajibiki kwa jamii.”

Chuki na wivu. Mauaji ya kwanza kutajwa katika historia ya wanadamu yalifanywa na mtu anayeitwa Kaini. (Mwanzo 4:​1-8) Akichochewa na wivu wenye chuki, Kaini alimwua ndugu yake​—hata ingawa Mungu alikuwa amemwonya adhibiti hisia zake na akaahidi kumbariki ikiwa angefanya hivyo. Hilo linathibitisha ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya”!​—Yakobo 3:16.

Matumizi mabaya ya kileo na dawa za kulevya. Matumizi mabaya ya vileo huharibu afya ya kimwili na ya kiakili na pia huathiri sehemu mbalimbali za ubongo zinazodhibiti utendaji wa mwili. Kwa sababu hiyo, ni rahisi sana kwa mtu ambaye ametumia dawa za kulevya kutenda kwa jeuri na kwa ukatili anapochokozwa.

Uzembe katika mifumo ya kutekeleza sheria. “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya,” inasema Mhubiri 8:11. Mifumo ya sheria iliyo dhaifu, isiyo na uwezo wa kutekeleza kazi yake, au iliyo na ufisadi huchangia jeuri kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja.

Dini ya uwongo. Mara nyingi dini huhusianishwa na jeuri, kutia ndani jeuri ya kidini na ugaidi. Lakini si watu wanaoshikilia sana maoni yao, wenye msimamo mkali wa kidini, na washupavu peke yao wanaopaswa kulaumiwa. Wakati wa vile vita viwili vya ulimwengu, washiriki wa dini kuu​—“za Kikristo” na zisizo za Kikristo​—walichinjana wakiungwa mkono na viongozi wao wa kidini. Matendo kama hayo humchukiza Mungu.​—Tito 1:16; Ufunuo 17:​5, 6; 18:24.

Kwa kuwa kuna mambo mengi ambayo huchochea au kutukuza jeuri, je kweli mtu anaweza kuwa mwenye kufanya amani katika ulimwengu wa leo? Ndiyo, kama tutakavyoona katika makala inayofuata.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

JEURI HUANZIA MOYONI

Hata ingawa huenda jeuri ikasababishwa na mambo mengi, chanzo chake kikuu hutoka moyoni. Jinsi gani? Yesu Kristo ambaye aliujua vizuri moyo wa mwanadamu, alisema hivi: “Kutoka katika moyo wa watu, hutoka mawazo mabaya: uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, kutamani, matendo ya uovu, udanganyifu, mwenendo mpotovu, jicho lenye wivu, makufuru, majivuno, ukosefu wa akili.” (Marko 7:​21, 22) Tunachochea mielekeo hiyo mibaya tunapotazama, kusikiliza, au kufikiria mambo mabaya mara kwa mara.​—Yakobo 1:​14, 15.

Kwa upande mwingine, tunapolisha akili zetu mambo yanayofaa, kama yale yanayotajwa katika makala iliyo kwenye ukurasa wa 8, ‘tunaua’ tamaa mbaya na kukuza zile nzuri. (Wakolosai 3:5; Wafilipi 4:8) Tukifanya hivyo, Mungu atatusaidia ‘tufanywe kuwa na uwezo katika mtu tuliye kwa ndani.’​—Waefeso 3:16.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

JEURI HUWATATANISHA WATAALAMU

Kwa nini katika nchi fulani visa vya uuaji viko juu mara 60 zaidi ya nchi nyingine? Kwa nini vita na matendo mengine ya jeuri yamekuwapo siku zote katika historia ya mwanadamu? Kuna maswali mengi yenye kutatanisha; lakini majibu yenye kusadikisha ni machache.

Wachunguzi fulani wanasema kwamba umaskini na ukosefu wa usawa husababisha jeuri. Takwimu fulani zinaonyesha kwamba karibu asilimia 90 hivi ya vifo vyote vinavyosababishwa na jeuri kutia ndani kujiua, vimetukia katika mataifa maskini ulimwenguni, na maeneo ya majijini wanamoishi watu maskini ndiyo yenye uhalifu mwingi. Lakini, je, ni kweli kwamba watu maskini ni wajeuri zaidi? Au je, wanateseka sana kutokana na jeuri kwa sababu hawawezi kulipia gharama za kupata ulinzi? Katika maeneo mengi kama vile huko Calcutta, India, mamilioni ya watu ni maskini hohehahe. Hata hivyo, Calcutta ni mojawapo ya majiji yaliyo na visa vichache sana vya mauaji ulimwenguni.

Wengine husema kwamba bunduki zinapopatikana kwa urahisi, hilo husababisha kuongezeka kwa jeuri katika jamii. Kwa kweli, bunduki hufanya watu wenye jeuri wawe hatari sana. Lakini wataalamu wana maoni yanayopingana kuhusu kinachofanya jamii fulani ziwe na idadi kubwa ya watu wenye jeuri.