Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Hawana Subira?

Kwa Nini Watu Hawana Subira?

UKOSEFU wa subira si jambo geni. Si ajabu kuwaona watu wakikosa subira wanapokuwa katika msongamano wa magari au wanapongoja kwenye foleni. Lakini wataalamu fulani wanasema kwamba watu leo wamekosa subira zaidi kuliko ilivyokuwa zamani​—na huenda sababu zinazowafanya wakose subira zikakushangaza.

Wachanganuzi fulani wanasema kwamba katika miaka ya hivi karibuni teknolojia ndiyo imewafanya watu wakose subira. Kulingana na gazeti The Gazette la Montreal, Kanada, watafiti fulani wanasema kwamba “teknolojia kama vile simu za mkononi, kamera, barua-pepe, na iPod zinabadili maisha yetu . . . Matokeo ya papo kwa hapo tunayopata kutoka kwa teknolojia hizo yamefanya tutake kutimiziwa haraka mahitaji yetu katika sehemu nyingine za maisha.”

Baada ya kufanya uchunguzi, Mwanasaikolojia, Dakt. Jennifer Hartstein, anasema kwamba “tumekuwa jamii ambayo inataka mahitaji yake yatimizwe papo hapo, na tunatazamia mambo yafanywe haraka, kwa njia bora na kwa njia tunayotaka. Mambo yasipofanywa kwa njia hiyo, sisi huudhika na kukasirika, [dalili] ya kukosa subira.” Anaongezea kusema, “Tumepoteza uwezo wa kutulia na kufurahia maisha.”

Watu fulani wanaamini kwamba barua-pepe zinapoteza umaarufu wake na hivi karibuni zitaacha kutumiwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu watu wengi wanaoandika barua-pepe hawana subira ya kungojea jibu kwa saa nyingi, au hata kwa dakika kadhaa. Pia, lazima mtu aanze kwa salamu na kumaliza kwa salamu anapoandika barua na barua-pepe. Lakini watu wengi wanaona jambo hilo kuwa linachosha na linapoteza wakati. Wanapendelea kuandika ujumbe wa haraka ambao hauhitaji mtu afuate adabu zinazohitajika kama anapoandika barua-pepe. Inaonekana kwamba watu wengi hawana wakati wa kupoteza wa kuandika salamu. Watu wengi hawatengi wakati wa kupitia yale waliyoandika ili kuyasahihisha. Kwa sababu hiyo, watu wanapokea barua na barua-pepe ambazo hazikukusudiwa kwa ajili yao au zilizo na makosa mengi ya kisarufi na ya maandishi.

Watu wengi hawana subira ya kusoma habari ndefu zilizochapishwa

Si teknolojia tu inayofanya watu watake kupata matokeo ya haraka. Inaonekana kwamba watu wanapoteza uwezo wa kusubiri katika sehemu nyingine za maisha. Kwa mfano, je, wewe hujipata ukizungumza haraka sana, ukila haraka sana, ukiendesha gari kwa kasi sana, au ukitumia pesa haraka sana? Kwa watu fulani, dakika chache ambazo lazima wasubiri ili lifti ije, taa za barabarani zibadilike rangi, au kompyuta ifunguke zinaweza kuonwa kuwa muda mrefu sana.

Wataalamu wamegundua kwamba watu wengi hawana subira ya kusoma habari ndefu zilizochapishwa. Kwa nini? Kwa sababu wamezoea kupitia haraka-haraka kurasa kwenye Intaneti, wakiruka kutoka jambo moja kuu hadi lingine wakitafuta jambo kuu wanalotaka.

Kwa nini watu hawana subira? Wataalamu hawajui sababu zote zinazowafanya watu wakose subira. Lakini inaonekana kwamba kuna uthibitisho wenye nguvu unaoonyesha kwamba kukosa subira kunaweza kuleta madhara. Makala zinazofuata zinazungumzia baadhi ya hatari za kukosa subira na mambo unayoweza kufanya ili uwe mwenye subira zaidi.

Watu wengi wamezoea kupitia haraka-haraka kurasa kwenye Intaneti, wakiruka kutoka jambo moja kuu hadi lingine