Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Dini

Dini

Kwa nini kuna dini nyingi sana?

“Mnaiacha amri ya Mungu, na kuyashika sana mapokeo ya wanadamu.” Marko 7:8.

BIBLIA INASEMA NINI?

Kiasili watu wana “uhitaji wa kiroho” ambao unaweza kutoshelezwa kwa kumwabudu Mungu. (Mathayo 5:3) Kwa sababu hiyo, watu wameanzisha dini nyingi zinazotegemea mawazo ya wanadamu badala ya mawazo ya Mungu.

Kwa mfano, Biblia inasema hivi kuhusu wafuasi wa dini fulani katika karne ya kwanza: Walikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi; kwa maana, kwa sababu ya kukosa kujua uadilifu wa Mungu bali wakitafuta kujiwekea uadilifu wao wenyewe, hawakujitiisha kwa uadilifu wa Mungu.” (Waroma 10:2, 3) Vivyo hivyo, leo kuna dini nyingi ambazo “hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.”—Marko 7:7.

 Je, ni lazima uwe mfuasi wa dini fulani?

Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja.”—Waebrania 10:24, 25.

BIBLIA INASEMA NINI?

Andiko la Waebrania 10:25 linatumia maneno “bila kuacha kukusanyika pamoja.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba Mungu anataka watu wakusanyike ili kuabudu katika kikundi chenye utaratibu. Lakini je, kila mwabudu anapaswa kuwa na maoni yake kumhusu Mungu na sheria zake? La hasha. Biblia inasema kwamba waabudu wa kweli wa Mungu wanapaswa ‘kusema kwa upatano,’ na ‘kuunganishwa vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.’ (1 Wakorintho 1:10) Wanapaswa kushirikiana na makutaniko na ‘kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu’ ulimwenguni pote. (1 Petro 2:17; 1 Wakorintho 11:16) Ni jambo muhimu kumwabudu Mungu kwa njia hiyo yenye umoja na utaratibu.

Unawezaje kuitambua dini ya kweli?

• “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

BIBLIA INASEMA NINI?

Ikionyesha jinsi ya kuwatambua wafuasi wa dini ya kweli, Biblia inasema hivi: “Kwa matunda yao mtawatambua. Je, watu hukusanya zabibu kutoka kwenye miiba au tini kutoka kwenye michongoma?” (Mathayo 7:16) Huhitaji kuwa mtaalamu ili kutofautisha kati ya mti unaozaa tini na mti wenye miiba, vivyo hivyo huhitaji kuwa mtaalamu wa dini ili utofautishe dini ya kweli na ya uwongo. Ni nini baadhi ya matunda, au mambo yanayotambulisha dini ya kweli?

  • Dini ya kweli hufundisha ukweli wa Neno la Mungu, Biblia. (Yohana 4:24; 17:17) Haitegemei falsafa za wanadamu.

  • Dini ya kweli husaidia watu wamjue Mungu, kutia ndani kujua jina lake, Yehova.—Yohana 17:3, 6.

  • Dini ya kweli hutangaza kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu bali si serikali za wanadamu.—Mathayo 10:7; 24:14.

  • Wafuasi wa dini ya kweli wanapendana kikweli. (Yohana 13:35) Inawafundisha watu kuwaheshimu watu wa jamii zote, kutumia wakati na mali zao kuwasaidia wengine, na kutoshiriki katika vita.—Mika 4:1-4.

  • Dini ya kweli inahusu kila sehemu ya maisha, bali si kufuata tu desturi za kidini. Wafuasi wake wanatenda kulingana na yale wanayofundisha.—Waroma 2:21; 1 Yohana 3:18.

Mashahidi wa Yehova, ambao ni wachapishaji wa gazeti hili, wanajitahidi kumheshimu Mungu kupitia maneno na matendo yao. Tunakuomba uhudhurie mikutano katika Jumba la Ufalme ili ujionee mwenyewe.