Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | KUKABILIANA NA MAJANGA

Ugonjwa Hatari

Ugonjwa Hatari

Mwanamke anayeitwa Mabel, huko Argentina, alikuwa na afya nzuri na alikuwa mtaalamu wa viungo vya mwili. Mwaka 2007, alianza kujihisi mchovu na kuumwa sana na kichwa kila siku. Anasema hivi: “Nilienda kwa madaktari kadhaa na kujaribu matibabu mbalimbali lakini sikufanikiwa.” Hatimaye Mabel alipigwa picha ya MRI, iliyoonyesha alikuwa na uvimbe wa ubongo. Anasema: “Nilishtuka sana! Sikuamini kwamba nilikuwa na tatizo hilo.

“Hata hivyo, sikuelewa jinsi hali yangu ilivyokuwa mbaya hadi nilipofanyiwa upasuaji. Nilipoamka kwenye chumba cha wagonjwa mahututi sikuweza kusogea. Nilichofanya tu ni kutazama dari. Kabla ya hapo nilikuwa mwenye nguvu. Lakini ghafla sikuweza kufanya chochote. Muda wote niliokaa katika chumba cha wagonjwa mahututi nilisikia kelele za vifaa vya matibabu, ving’ora vya dharura, na vilio vya wagonjwa wengine. Nilijihisi nimezungukwa na ugonjwa na mateso.

“Kufikia sasa, nimepata nafuu. Ninaweza kutembea bila msaada na hata kwenda nje nikiwa peke yangu. Lakini nina matatizo ya kuona na pia hitilafu ya misuli.”

KUKABILIANA NA MAJANGA

Dumisha mtazamo mzuri. Biblia inasema kwenye Methali 17:22: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka huikausha mifupa.” Mabel anasema: “Nilipokuwa nikiugua nilikabili hali kama zile ambazo wagonjwa niliowahudumia walikabili. Mazoezi yaliniletea maumivu makali, na nyakati nyingine nilitamani kuacha. Nilijilazimisha kuondoa fikira zisizofaa, nikijua kwamba jitihada hizo zingeniletea matokeo mazuri.”

Kazia fikira mambo yatakayokupa tumaini. “Niliposoma Biblia nilijua kwa nini majanga hutokea,” anasema Mabel. “Lakini pia nilijua kwamba kadiri siku zinavyopita ndivyo tunavyokaribia wakati ambao maumivu hayatakuwepo tena.” *

Tambua kwamba Mungu anakujali wewe binafsi. (1 Petro 5:7) Mabel anakumbuka jinsi hilo lilivyomsaidia: “Nilipopelekwa kufanyiwa upasuaji, nilijionea ukweli wa maneno ya Isaya 41:10, ambapo Mungu anasema: ‘Usiogope, niko pamoja na wewe.’ Nilipata amani sana kujua kwamba Yehova Mungu ananijali.”

Je, wajua? Biblia inafundisha kwamba kuna wakati ambapo wanadamu hawatasumbuliwa tena na magonjwa.—Isaya 33:24; 35:5, 6.

^ fu. 8 Kwa habari zaidi, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kinapatikana katika Intaneti kwenye www.pr418.com/sw.