Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Usafi

Usafi

Je, usafi wa miili yetu ni muhimu kwa Mungu?

“Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.”2 Wakorintho 7:1.

BIBLIA INASEMA NINI?

Muumba wetu anatupenda na angependa tuwe na afya bora na tuishi maisha mazuri na marefu. Anasema hivi: “Moyo wako upate kushika amri zangu, kwa sababu utaongezewa urefu wa siku na miaka ya uzima na amani.” (Methali 3:1, 2) Sheria hususa kuhusu usafi ambazo Mungu aliwapa Waisraeli, zilionyesha kwamba anawapenda wanadamu. (Kumbukumbu la Torati 23:12-14) Waisraeli walipofuata sheria hizo ambazo hazikuwa ngumu, waliboresha afya na hawakupata magonjwa yaliyowapata watu wa mataifa mengine, kama vile Misri, ambao hawakuwa na sheria kama waliyopewa Waisraeli. —Kumbukumbu la Torati 7:12, 15.

Leo pia, watu ‘wanaojisafisha wenyewe kila unajisi wa mwili na roho’ unaotia ndani mazoea yenye kuchafua kama vile kuvuta sigara, ulevi, na kutumia dawa za kulevya, hupunguza uwezekano wa kupata magonjwa ya kimwili na kiakili au kufa mapema. Kwa kuwa hatuishi peke yetu, tunapofuata viwango vya Mungu vya usafi, tunaonyesha tunawajali wengine.—Marko 12:30, 31.

 Je, Mungu anataka watu wawe safi kiadili na kiroho?

“Viueni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo ghadhabu ya Mungu inakuja.”—Wakolosai 3:5, 6.

BIBLIA INASEMA NINI?

Kama tulivyoona, Biblia inatuhimiza “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.” Katika nyakati za Yesu Kristo, watu wengi, kutia ndani viongozi wa dini ya Kiyahudi walijitahidi sana kuwa safi kimwili lakini walipuuza usafi wa kiadili na kiroho. (Marko 7:1-5) Yesu alisahihisha maoni hayo aliposema: “Hakuna chochote kutoka nje kinachoingia ndani ya mtu ambacho kinaweza kumtia unajisi, kwa kuwa hicho hupita na kuingia, . . . ndani ya matumbo yake, nacho hutoka nje na kuingia ndani ya shimo la choo.” Tena akasema: “Kile ambacho hutoka ndani ya mtu ndicho humtia mtu unajisi; kwa maana kutoka ndani, kutoka katika moyo wa watu, hutoka mawazo mabaya: uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, kutamani, matendo ya uovu, udanganyifu, mwenendo mpotovu, jicho lenye wivu, . . . na ukosefu wa akili. Mambo hayo yote maovu . . . humtia mtu unajisi.”—Marko 7:18-23.

Kulingana na Yesu, watu wanaojitahidi sana kuwa wasafi kimwili lakini wakati uleule wanapuuza viwango vya Mungu vya kiadili na kiroho ni kama vikombe vilivyosafishwa nje lakini ndani ni vichafu.—Mathayo 23:25, 26.

Je, viwango vya Biblia ni vigumu sana?

“Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” —1 Yohana 5:3.

BIBLIA INASEMA NINI?

Andiko la Mika 6:8, linasema hivi: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?” Je, kweli ni vigumu kufanya hivyo? Isitoshe, Muumba wetu anataka tumtii kwa hiari. Tunapofanya hivyo, tunapata furaha sana. (Zaburi 40:8) Vilevile, tunapokosea, tunaweza kufarijiwa na rehema ya Mungu. “Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi,” yaani tuna udhaifu na dhambi.—Zaburi 103:13, 14.

Kwa ufupi, viwango vya Mungu vya usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho vinaonyesha wema na upendo wake kwetu. Tunapofuata viwango hivyo kwa hiari, tunaonyesha tuna hekima na tunampenda.