Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Upendo

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Upendo

KANUNI YA BIBLIA: “Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”Wakolosai 3:14.

FAIDA: Upendo unaotajwa mara nyingi katika Biblia si ule wa kimahaba au kimapenzi. Bali, Biblia huzungumzia zaidi kuhusu upendo unaoongozwa na kanuni, wenye sifa kama vile huruma, kusamehe, unyenyekevu, fadhili, upole, na subira. (Mika 6:8; Wakolosai 3:12, 13) Tofauti na hisia za kimahaba ambazo mara nyingi hufifia kadiri muda unavyopita, upendo huo huendelea kukua daima dawamu.

Brenda, mwanamke ambaye amekuwa katika ndoa kwa karibu miaka 30, anasema hivi: “Upendo kati ya watu waliofunga ndoa karibuni hauwezi kulinganishwa na kina cha upendo ambacho mume na mke huonyeshana kadiri muda unavyopita.”

Sam, mume ambaye amekuwa katika ndoa kwa zaidi ya miaka 12, anasema hivi: “Sikuzote mimi na mke wangu tumefurahia na hata kushangazwa na jinsi mashauri ya Biblia yalivyo rahisi kueleweka, na jinsi ambavyo kuyatumia huleta matokeo mazuri. Unapoyatumia, mambo yanakuwa shwari. Hata ingawa ningependa kusema kwamba nafuata mashauri ya Biblia nyakati zote, kuna wakati ambapo ninashindwa kufanya hivyo. Kwa mfano, ninapokuwa katika hali ya kuudhika upesi, kutaka kufanya nipendavyo, au ninapokuwa nimechoka. Nyakati kama hizo mimi humwomba Yehova anisaidie kushinda hisia zozote zisizofaa. Kisha ninamkumbatia mke wangu, na baada ya muda mfupi, hali inakuwa shwari kana kwamba hakuna jambo lolote baya lililotendeka!”

“Hekima huonyeshwa kwa matendo yake”

Yesu Kristo alisema “hekima huonyeshwa kwa matendo yake.” (Mathayo 11:19) Kwa msingi wa maneno hayo, ni Biblia pekee yenye hekima ya kweli. Imethibitika kwamba viwango na mafundisho yake huwanufaisha watu sikuzote. Viwango na mafundisho yake huwanufaisha watu wa nchi na tamaduni zote. Biblia inaelezea kwa kina kuhusu tabia za asili za wanadamu na hilo halishangazi kwa sababu Mtungaji wa Biblia ni Muumba wetu—Yehova Mungu. Hata hivyo, kufuata mafundisho ya Biblia kutatuthibitishia kwamba yeye ndiye chanzo cha viwango hivyo. Kwa hiyo, Biblia inatualika tufuate na kutumia viwango na mafundisho ya Yehova inaposema “onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” (Zaburi 34:8) Je, utakubali mwaliko huo?