Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | KWA NINI WATOTO HAWANA NIDHAMU?

Nidhamu Inayofaa

Nidhamu Inayofaa

NI WAZI kwamba kulea watoto ni kazi ngumu. Lakini kutomwadhibu mtoto anapokosea huifanya kazi hiyo iwe ngumu zaidi. Kwa nini? Kwa sababu bila kupewa nidhamu (1) watoto hukosa mwongozo, na hilo huwachosha sana wazazi, na (2) wazazi hutoa maagizo bila msimamo na hilo huwafanya watoto wachanganyikiwe.

Kwa upande mwingine, kumtia mtoto nidhamu yenye usawaziko na upendo, kunaweza kumzoeza kufikiri kwa njia nzuri na kuwa na tabia nzuri. Pia, hilo husaidia watoto wajiamini na wawe wenye kutegemeka wanapokuwa watu wazima. Hata hivyo, unaweza kupata wapi mwongozo wenye kutegemeka wa jinsi ya kutia nidhamu watoto wako?

Umuhimu wa Kanuni za Biblia

Wachapishaji wa gazeti hili, Mashahidi wa Yehova, wanaamini kwamba Biblia ni ‘yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu.’ (2 Timotheo 3:16) Biblia si kitabu tu chenye maagizo ya jinsi ya kulea mtoto wako; bali ina kanuni zinazotoa mwongozo unaofaa kwa ajili ya familia. Chunguza kanuni zifuatazo.

BIBLIA INASEMA: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.”—Methali 22:15.

Ingawa watoto hufikiria wengine na ni wenye fadhili, bado wao hutenda kwa njia isiyofaa. Hivyo, watoto wanahitaji kutiwa nidhamu. (Methali 13:24) Kutambua ukweli huo kutakusaidia kutimiza daraka lako ukiwa mzazi.

BIBLIA INASEMA: “Usimnyime mvulana nidhamu.”—Methali 23:13.

Usiogope kuwatia nidhamu watoto wako kwa usawaziko eti kwa sababu tu utawavunja moyo au watakuchukia watakapokuwa watu wazima. Badala yake, nidhamu inapotolewa kwa njia ya upendo, itawasaidia watoto wako kujifunza jinsi ya kukubali shauri kwa unyenyekevu, sifa itakayowafaa watakapokuwa watu wazima.—Waebrania 12:11.

BIBLIA INASEMA: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6: 7.

Kwa kawaida wazazi wanapenda kuwalinda watoto wao, na jambo hilo linafaa. Hata hivyo, unapaswa kuwa na usawaziko. Hutawasaidia watoto wako ikiwa utajaribu “kuwaokoa” wanapoadhibiwa kwa sababu ya makosa yao au kuwatetea mwalimu wao au mtu mwingine anapokueleza kuhusu tabia yao mbaya. Badala yake, unapaswa kuwaona watu hao kuwa rafiki zako. Unapofanya hivyo, unamfundisha mtoto wako kuheshimu mamlaka—kutia ndani yako.Wakolosai 3:20.

BIBLIA INASEMA: “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”—Methali 29:15.

Uwe mwenye upendo, mwenye msimamo, na mwenye usawaziko

Ingawa wazazi hawapaswi kuwa wakali kupita kiasi, wanapaswa kuepuka kuendekeza watoto wao. Kitabu The Price of Privilege kinasema hivi: “Watoto wanaoendekezwa na wazazi wao, huenda wakaanza kupuuza mamlaka ya watu wazima walio nyumbani.” Usipotumia mamlaka yako, huenda mtoto wako akahisi kwamba yeye ndiye mtawala. Hivyo, atafanya maamuzi yasiyofaa yatakayoleta madhara kwake na kwako pia.—Methali 17:25; 29:21.

BIBLIA INASEMA: “Mwanamume . . . atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.”—Mathayo 19:5.

Kulingana na Biblia, mwanamume na mwanamke wanapaswa kuwa wamefunga ndoa kabla ya kuanza kupata watoto na wanapaswa kuendelea kuwa pamoja hata baada ya watoto hao kuwa watu wazima na kuondoka nyumbani. (Mathayo 19:5, 6) Hilo linamaanisha kwamba unakuwa mwenzi wa ndoa kwanza, na mzazi baadaye. Ikiwa hutafanya hivyo, huenda mtoto wako akaanza ‘kujifikiria mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Waroma 12:3) Pia wenzi wa ndoa “wanaoendekeza mtoto wao,” wanaweza kudhoofisha ndoa yao.

Msaada kwa Wazazi

Ili utimize daraka lako ukiwa mzazi, unapaswa kumtia nidhamu mtoto wako kulingana na kanuni zifuatazo.

Uwe mwenye upendo. “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21.

Uwe na msimamo. “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”—Mathayo 5:37.

Uwe na usawaziko. “Nitakurekebisha kwa kiwango kinachofaa.”—Yeremia 30:11. *

^ fu. 21 Kwa habari zaidi, tembelea Tovuti ya jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > WENZI WA NDOA NA WAZAZI, kisha utapata makala kama vile “Kuwatia Watoto Nidhamu,” “Jinsi ya Kushughulika na Mtoto Mwenye Milipuko ya Hasira,” “Wafundishe Watoto Wako Maadili Mema,” na “Jinsi ya Kumtia Nidhamu Kijana Wako.”