Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Sijaacha Kamwe Kujifunza

Sijaacha Kamwe Kujifunza

NINAMSHUKURU Yehova kwamba yeye ndiye ‘Mfundishaji wangu Mkuu.’ (Isa. 30:20) Anawafundisha waabudu wake kupitia Neno lake, Biblia; uumbaji wake maridadi; na tengenezo lake. Pia, anawatumia waabudu wenzetu, ndugu na dada zetu, ili kutusaidia. Ingawa ninakaribia umri wa miaka 100, ninaendelea kunufaika kutokana na maagizo ambayo Yehova anatupatia kupitia njia hizo zote. Acheni niwaeleze jinsi nilivyonufaika.

Nikiwa na familia yetu mwaka wa 1948

Nilizaliwa mwaka wa 1927 katika mji mdogo karibu na Chicago, Illinois, Marekani. Baba na Mama walikuwa na watoto watano—Jetha, Don, mimi, Karl, na Joy. Sote tulikuwa tumeazimia kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Jetha alihudhuria darasa la pili la Shule ya Gileadi mwaka wa 1943. Don, Karl, na Joy walianza kutumikia katika Betheli ya Brooklyn, New York; Don, mwaka wa 1944, Karl, mwaka wa 1947, na Joy, mwaka wa 1951. Mfano wao mzuri pamoja na ule wa wazazi wangu ulinichochea sana.

FAMILIA YETU INAJIFUNZA KWELI

Baba na Mama walikuwa wasomaji wa Biblia waliompenda Mungu, na walituchochea sisi pia tuwe na upendo huo. Hata hivyo, Baba aliacha kuheshimu makanisa na dini baada ya kutumikia akiwa mwanajeshi barani Ulaya wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Mama, akiwa na shukrani nyingi kwa sababu Baba alirudi salama kutoka vitani, alimwambia hivi: “Karl, twende kanisani kama ilivyokuwa kawaida yetu.” Baba alijibu hivi: “Nitakupeleka hapo, lakini sitaingia ndani.” Mama akamuuliza: “Kwa nini?” Baba akajibu: “Wakati wa vita, makasisi wa dini moja lakini waliotoka katika nchi mbili tofauti zilizokuwa zikipigana, waliwabariki wanajeshi wa nchi zao na silaha zao! Je, Mungu alikuwa akiunga mkono pande zote mbili?”

Baadaye, Mama alipokuwa kanisani, Mashahidi wawili walifika nyumbani kwetu. Walimpatia Baba mabuku mawili ya kitabu cha kujifunzia Biblia, Light, kilichozungumzia kitabu cha Ufunuo. Baba alipendezwa na akakubali kuvichukua. Mama alipoviona tu vitabu hivyo akaanza kuvisoma. Kisha, siku moja akaona tangazo katika gazeti likiwaalika watu waliopendezwa waende kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Light. Mama aliamua kwenda. Alipofika, mwanamke mwenye umri mkubwa alimfungulia mlango. Akiwa ameinua kitabu kimoja, Mama alimuuliza, “Mnajifunza kitabu hiki hapa?” Akamjibu, “Ndiyo mpendwa, karibu.” Juma lililofuata Mama alienda pamoja nasi watoto, na baada ya hapo tulienda kwa ukawaida.

Kwenye mkutano mmoja, aliyekuwa akiongoza aliniomba nisome Zaburi 144:​15, ambayo inasema kwamba wale wanaomwabudu Yehova wana furaha. Andiko hilo lilinivutia sana, na pia nilivutiwa na maandiko mengine mawili—1 Timotheo 1:​11, ambayo inasema Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” na Waefeso 5:​1, linalotuhimiza tuwe “waigaji wa Mungu.” Nilifikia mkataa kwamba ninapaswa kufurahia mambo ninayoweza kumfanyia Muumba wangu na kumshukuru kwa pendeleo la kumtumikia. Hayo ndiyo mambo mawili ambayo nimejitahidi kufanya katika maisha yangu yote.

Kutaniko la karibu zaidi lilikuwa katika jiji la Chicago, umbali wa kilomita 32. Hata hivyo, tulihudhuria mikutano hiyo, na ujuzi wangu wa Biblia uliongezeka. Ninakumbuka pindi moja yule aliyekuwa akiongoza alimchagua Jetha atoe maelezo. Niliposikiliza maelezo yake, nilijiambia: ‘Nilijua jibu hilo. Ningeweza kunyoosha mkono wangu na kutoa maelezo.’ Nilianza kutayarisha maelezo yangu mwenyewe. Na jambo muhimu zaidi, niliendelea kukua kiroho pamoja na ndugu na dada zangu. Nilibatizwa mwaka wa 1941.

KUFUNDISHWA NA YEHOVA KATIKA MAKUSANYIKO

Ninakumbuka hasa kusanyiko la mwaka wa 1942 jijini Cleveland, Ohio. Zaidi ya sehemu 50 nchini Marekani ziliunganishwa kwenye programu hiyo kupitia simu. Familia yetu ilikuwa kwenye mahema katika eneo la kupiga kambi (trailer city) ambalo akina ndugu waliandaa. Wakati huo, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vikiendelea, na upinzani kuelekea Mashahidi wa Yehova ulikuwa ukiongezeka. Wakati wa jioni, niliona kikundi cha akina ndugu wakiegesha magari yao huku taa za mbele zikiangalia nje ya kambi. Wote walikuwa wamekubaliana kwamba kuwe na mtu mmoja katika kila gari ambaye atakuwa mlinzi usiku wote. Ikiwa kungekuwa na dalili yoyote ya hatari, akina ndugu wangewasha taa za gari ili kuwapofusha washambuliaji na kupiga honi. Kisha, ndugu wengine wangekuja haraka ili kusaidia. Niliwaza hivi, ‘Watu wa Yehova wako tayari kwa kila jambo!’ Nikiwa nimepata uhakikisho huo, nililala fofofo, na hakukuwa na tatizo lolote.

Miaka mingi baadaye, nilipokuwa nikikumbuka matukio ya kusanyiko hilo, nilitambua kwamba mama yangu hakuonyesha dalili yoyote ya wasiwasi au woga. Alimtumaini kabisa Yehova na tengenezo lake. Sitasahau kamwe mfano wake bora.

Muda mfupi kabla ya kusanyiko hilo, Mama alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida. Hivyo, alisikiliza kwa makini hotuba zilizozungumzia utumishi wa wakati wote. Tulipokuwa tukirudi nyumbani, alisema, “Ningependa kuendelea kufanya upainia, lakini siwezi kufanya hivyo na wakati huohuo nitimize vizuri kazi za nyumbani.” Kisha, akatuuliza ikiwa tungependa kumsaidia. Tulijibu ndiyo, hivyo akatupatia kila mmoja wetu chumba kimoja au viwili vya kusafisha kabla ya kupata kiamsha kinywa. Tulipoenda shule, angehakikisha kwamba nyumba ilikuwa safi, kisha angeenda katika huduma. Alikuwa mama mwenye shughuli nyingi, lakini hakuwapuuza kamwe watoto wake. Tuliporudi nyumbani kwa ajili ya chakula cha mchana na baada ya shule, sikuzote alikuwa nyumbani. Siku nyingine baada ya kutoka shule, tungeenda pamoja naye katika huduma, jambo lililotusaidia kuelewa inamaanisha nini kuwa painia.

NAANZA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Nilianza upainia nikiwa na umri wa miaka 16. Ingawa wakati huo Baba hakuwa Shahidi, alipendezwa na maendeleo yangu. Jioni moja, nilimwambia kwamba licha ya kujitahidi sana, sikuwa nimepata mtu ambaye angependa kujifunza Biblia. Baada ya kutua kidogo, nilimuuliza, “Ungependa kujifunza Biblia pamoja nami?” Alitafakari kwa muda mfupi na akasema, “Siwezi kufikiria sababu yoyote nzuri ya kukataa kujifunza.” Naam, mwanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia alikuwa baba yangu. Hilo lilikuwa pendeleo kubwa sana!

Tulijifunza kwa kutumia kitabu “The Truth Shall Make You Free.” Kadiri tulivyoendelea kujifunza, nilitambua kwamba Baba alikuwa akinisaidia kuwa mwanafunzi na mwalimu bora. Kwa mfano, jioni moja baada ya kusoma fungu, alisema: “Ninaona kile ambacho kitabu kinasema. Lakini unajuaje kwamba kile kinachosemwa ni sahihi?” Sikuwa nimejitayarisha kujibu swali hilo, hivyo nilimwambia: “Siwezi kukuthibitishia kwa sasa, lakini katika funzo letu linalofuata, nitakuwa nimejitahidi kupata jibu.” Na nilifanya hivyo. Nilipata mistari ya Biblia ambayo iliunga mkono mambo tuliyokuwa tukizungumzia. Baada ya hapo, nilijitayarisha vizuri zaidi kwa ajili ya funzo letu kwa kujifunza kufanya utafiti. Hilo lilichangia katika ukuzi wetu wa kiroho. Baba alitumia mambo aliyokuwa akijifunza na akabatizwa mwaka wa 1952.

MALENGO MAPYA YALINISAIDIA KUENDELEA KUJIFUNZA

Niliondoka nyumbani nilipokuwa na umri wa miaka 17. Jetha a alikuwa mmishonari, na Don, alikuwa Mwanabetheli. Wote walipenda migawo yao, jambo ambalo lilinitia moyo sana. Hivyo, nilijaza ombi la kutumikia Betheli na la kuhudhuria Shule ya Gileadi na kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Matokeo yalikuwaje? Nilialikwa Betheli mwaka wa 1946.

Kwa miaka mingi, nimekuwa na migawo mingi mbalimbali ya Betheli, hivyo niliweza kujifunza mambo mengi mapya. Kwa kweli, katika miaka 75 ambayo nimetumikia Betheli, nilifundishwa jinsi ya kutengeneza vitabu na kufanya kazi ya uhasibu. Pia, nilijifunza jinsi ya kununua vitu vilivyohitajika Betheli na jinsi ya kusafirisha vitu muhimu nje ya nchi. Zaidi ya yote, ninafurahia elimu ya Biblia ambayo Betheli inaendelea kutoa kupitia ibada ya asubuhi na hotuba zinazotegemea Biblia.

Nikifundisha darasa la wazee wa kutaniko

Pia, nilijifunza kutoka kwa ndugu yangu mdogo, Karl, ambaye alikuja Betheli mwaka wa 1947. Alikuwa mwanafunzi na mwalimu bora wa Biblia. Pindi moja, nilimwomba anisaidie kutayarisha hotuba ambayo nilipaswa kutoa. Nilimwambia Karl kwamba nilikuwa nimekusanya habari nyingi, lakini sikujua jinsi ya kutumia habari hizo. Alinisaidia kupata suluhisho kwa kuniuliza swali moja, “Joel, kichwa cha hotuba yako ni kipi?” Mara moja nilielewa alikuwa akimaanisha nini—tumia tu habari unazohitaji na kuondoa usizohitaji. Sikuwahi kamwe kusahau somo hilo.

Ili utumikie Betheli kwa furaha, unahitaji kushiriki kikamili katika huduma, na hilo litafanya uwe na mambo mengi uliyojionea yenye kutia moyo. Kisa kimoja ninachokumbuka vizuri kilitokea mapema jioni moja eneo la Bronx, New York City. Mimi na ndugu mmoja tulimtembelea mwanamke fulani ambaye awali alikubali kuchukua gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Tulijitambulisha na kusema, “Jioni ya leo tunawasaidia watu kujifunza mambo yenye kujenga kutoka katika Biblia.” Akajibu, “Ikiwa mnazungumzia Biblia, karibuni.” Tulisoma na kuzungumzia maandiko kadhaa kuhusu Ufalme wa Mungu na ulimwengu mpya unaokuja. Ni wazi kwamba jambo hilo lilimvutia sana kwa kuwa aliwaalika marafiki wake kadhaa wajiunge nasi juma lililofuata. Baadaye, yeye na mume wake wakawa watumishi waaminifu wa Yehova.

KUJIFUNZA KUTOKA KWA MWENZI WANGU WA NDOA

Nilikuwa nikitafuta mwenzi wa ndoa kwa miaka 10 hivi kabla ya kukutana na mke wangu. Ni nini kilichonisaidia kupata mke anayefaa? Nilisali na kujiuliza, ‘Ninataka kufanya nini baada ya kufunga ndoa?’

Nikiwa na Mary katika kazi ya kuzungukia makutaniko

Baada ya kusanyiko la mwaka wa 1953 lililofanywa uwanja wa Yankee Stadium, nilikutana na dada anayeitwa Mary Aniol. Yeye na Jetha walikuwa katika darasa la pili la Gileadi, na Mary alikuwa mwandamani wa Jetha katika mgawo wao wa umishonari. Akiwa na shauku nyingi, Mary alinisimulia kuhusu mgawo wake wa umishonari katika visiwa vya Karibea na mafunzo ya Biblia aliyoongoza. Kadiri tulivyofahamiana zaidi, ndivyo tulivyotambua kwamba tulikuwa tukifuatia malengo ya kiroho yanayofanana. Upendo wetu ulizidi kukua, na Aprili 1955 tulifunga ndoa. Kwa njia nyingi, Mary alithibitika kuwa zawadi kutoka kwa Yehova na mfano wa kuiga. Alifurahia mgawo wowote ambao alipewa. Alifanya kazi kwa bidii, aliwajali watu kutoka moyoni, na sikuzote alitanguliza masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Tulitumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko kwa miaka mitatu, na katika mwaka wa 1958, tulialikwa Betheli tukiwa wenzi wa ndoa.

Nilijifunza mambo mengi kutoka kwa Mary. Kwa mfano, mwanzoni mwa ndoa yetu, tuliamua kusoma Biblia pamoja; tulisoma mistari 15 hivi kwa wakati mmoja. Baada ya mmoja wetu kusoma sehemu hiyo ya Biblia, tungetoa maelezo kuhusiana na mistari hiyo na kuzungumzia jinsi tunavyoweza kuitumia maishani. Mara nyingi, Mary alinisimulia mambo aliyojifunza akiwa Gileadi au katika utumishi wake wa umishonari. Mazungumzo hayo yalinipatia ufahamu na kunisaidia kuboresha hotuba zangu na kujua jinsi ya kuwatia moyo akina dada.—Met. 25:11.

Mke wangu mpendwa Mary alikufa mwaka wa 2013. Ninatazamia kwa hamu kumwona kwenye ulimwengu mpya! Kwa sasa, nimeazimia kuendelea kujifunza na kumtumaini Yehova kwa moyo wangu wote. (Met. 3:​5, 6) Ninafarijika na kufurahi ninapofikiria kuhusu mambo ambayo watu wa Yehova watafanya katika ulimwengu mpya. Bila shaka, hilo litatia ndani kujifunza mambo mapya kutoka kwa Mfundishaji wetu Mkuu na kujifunza kumhusu Mfundishaji wetu Mkuu! Naam, sina maneno yanayotosha kumshukuru Yehova kwa mambo yote aliyonifundisha na kwa jinsi alivyonionyesha fadhili nyingi sana zisizostahiliwa.

a Tazama simulizi la maisha la Jetha Sunal katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2003, uku. 23-29.