Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya mwaka huu? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Yehova ametuwekea kielelezo gani cha jinsi ya kuwatendea wanawake?

Anawatendea bila ubaguzi, wala hawaoni wanaume kuwa bora kuliko wanawake. Mungu anawasikiliza wanawake, anajali kuhusu jinsi wanavyohisi na matatizo wanayokabili. Anawaamini na anajua kwamba watatimiza kazi yake.—w24.01, uku. 15-16.

Tunawezaje kutumia andiko la Waefeso 5:​7, linalosema: “Msishirikiane nao”?

Mtume Paulo alikuwa akituonya tusishirikiane na watu ambao watafanya iwe vigumu kwetu kushikamana na viwango vya Mungu. Watu hao wanatia ndani wale tunaokutana nao uso kwa uso pamoja na wale tunaowasiliana nao kwenye mitandao ya kijamii.—w24.03, uku. 22-23.

Tunahitaji kujilinda dhidi ya habari gani za uwongo?

Tunahitaji kujihadhari na habari ambazo hazijathibitishwa kutoka kwa marafiki wenye nia nzuri, barua-pepe kutoka kwa watu tusiowafahamu, na waasi-imani wanaojifanya wanapendezwa na ujumbe wetu.—w24.04, uku. 12.

Tunajua nini na hatujui nini kuhusu jinsi Yehova atakavyomhukumu Mfalme Sulemani na wale waliokufa katika majiji ya Sodoma na Gomora na katika Gharika?

Hatuna uhakika kwamba Yehova aliwahukumu watu hao wote uharibifu wa milele. Hata hivyo, tunajua kwamba Yehova ana habari kamili na ni mwenye rehema nyingi.—w24.05, uku. 3-4.

Mungu kuwa “Mwamba” kunatuhakikishia nini? (Kum. 32:4)

Tunaweza kutafuta kimbilio kwa Yehova. Yeye anategemeka, sikuzote anatimiza ahadi zake. Na Yehova ni imara na habadiliki, utu wake na kusudi lake haliwezi kamwe kubadilika.—w24.06, uku. 26-28.

Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuzoea kutaniko jipya?

Mtegemee Yehova, ambaye atakusaidia kama alivyowasaidia watumishi wake wa zamani. Epuka kulinganisha kutaniko lako la zamani na jipya. Uwe na mengi ya kufanya katika kutaniko lako jipya, na ujitahidi kutafuta marafiki wapya.—w24.07, uku. 26-28.

Tunajifunza masomo gani kupitia mifano mitatu inayopatikana kwenye Mathayo sura ya 25?

Mfano wa kondoo na mbuzi unakazia umuhimu wa kuwa waaminifu na washikamanifu. Mfano wa mabikira wenye busara na mabikira wapumbavu unakazia uhitaji wa kuwa tayari na kukaa macho. Na mfano wa talanta unakazia umuhimu wa kuwa wenye bidii.—w24.09, uku. 20-24.

Ukumbi wa hekalu la Sulemani ulikuwa na kimo gani?

Kwenye andiko la 2 Mambo ya Nyakati 3:​4, baadhi ya hati za Biblia za kale zinataja “120” katika mstari huo, na hivyo kufanya ukumbi huo uwe na kimo cha mita 53. Lakini hati nyingine zinazotegemeka zinataja “mikono 20,” na kufanya ukumbi huo uwe na kimo cha mita 9. Maelezo hayo ya mwisho yanaunga mkono wazo la kwamba kimo hicho kingeweza kutegemezwa na upana wa kuta za hekalu.—w24.10, uku. 31.

Mtumishi wa huduma kuwa ‘mume wa mke mmoja’ kunamaanisha nini? (1 Tim. 3:12)

Inamaanisha kwamba anapaswa kufunga ndoa na mwanamke mmoja na hapaswi kufanya uasherati. Zaidi ya hayo, hapaswi kuwakazia fikira wanawake wengine kwa njia isiyofaa.—w24.11, uku. 19.

Kwa nini tunaweza kusema kwamba maneno ya Yohana 6:53 si kielelezo cha kufuatwa wakati wa Mlo wa Jioni wa Bwana?

Yohana 6:53 inazungumzia uhitaji wa kula mwili wa Yesu na kunywa damu yake. Yesu alizungumza maneno hayo mwaka wa 32 W.K., huko Galilaya, kwa Wayahudi ambao bado walihitaji kumwamini. Hata hivyo, Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa mwaka mmoja baadaye jijini Yerusalemu. Hapo Yesu alizungumza na wale ambao wangetawala pamoja naye mbinguni.—w24.12, uku. 10-11.