Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini maadui wa Yesu waliona kunawa mikono kuwa jambo zito?

Hilo ni moja kati ya mambo yaliyofanya maadui wamkosoe Yesu pamoja na wanafunzi wake. Sheria ya Musa ilikuwa na amri nyingi zilizohusu kujitakasa kutokana na mtiririko wowote wa mwili, ukoma, maiti, na mizoga. Pia, ilitoa maagizo ya jinsi ya kuondoa uchafu. Hilo lingefanywa kupitia kutoa dhabihu, kusafisha, au kunyunyiza.​—Law., sura ya 11-15; Hes., sura ya 19.

Marabi wa Kiyahudi walifafanua kila kipengele cha sheria hizo. Kitabu kimoja kinasema kwamba kila kisa cha unajisi “kingechunguzwa ili kujua ni katika hali gani unajisi ulitokea, jinsi ambavyo ungesambazwa kwa wengine, vyombo ambavyo vingeathiriwa na vile ambavyo havingeathiriwa, na mwishowe, namna na utaratibu unaopaswa kufuatwa ili kutakasa kitu.”

Wapinzani wa Yesu walimwuliza hivi: “Kwa nini wanafunzi wako hawajiendeshi kulingana na mapokeo ya watu wa zamani, bali hula mlo wao kwa mikono iliyo najisi?” (Marko 7:5) Maadui hao wa kidini hawakuwa wakizungumzia kudumisha usafi kwa sababu za kiafya. Kidesturi, marabi walisema kwamba mtu alipaswa kumwagiliwa maji mikononi kabla ya kula. Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Pia, kulikuwa na mabishano kuhusu vyombo vilivyofaa kutumiwa kummwagilia mtu maji, maji yaliyofaa kutumiwa, nani aliyestahili kummwagia maji hayo, na ni sehemu kubwa kadiri gani ya mikono iliyopaswa kumwagiliwa maji.”

Maoni ya Yesu kuhusu sheria hizo yalikuwa wazi na rahisi kuelewa. Aliwaambia hivi viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza: “Isaya kwa kufaa alitoa unabii juu yenu wanafiki, kama ilivyoandikwa, ‘Watu hawa huniheshimu mimi kwa midomo yao, bali mioyo yao iko mbali nami [Yehova]. Wao huniabudu bure, kwa sababu wao hufundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’ Mnaiacha amri ya Mungu, na kuyashika sana mapokeo ya wanadamu.”​—Marko 7:6-8.