Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaona Umuhimu wa Kuwazoeza Wengine?

Je, Unaona Umuhimu wa Kuwazoeza Wengine?

“Nitawapa ninyi mafundisho mema.”​—MET. 4:2.

NYIMBO: 93, 96

1, 2. Kwa nini tunapaswa kuwazoeza wengine wajitahidi kutimiza migawo ya kitheokrasi?

MGAWO muhimu zaidi katika maisha ya Yesu ulikuwa kutangaza habari njema ya Ufalme. Hata hivyo, alitumia muda kuwazoeza wengine wawe wachungaji na walimu. (Mt. 10:5-7) Ingawa Filipo alikuwa mweneza-injili mwenye shughuli nyingi, aliwasaidia binti zake wanne wawe wahubiri wenye matokeo wa kweli za Kimaandiko. (Mdo. 21:8, 9) Mazoezi ya aina hiyo ni muhimu kadiri gani leo?

2 Ulimwenguni pote, idadi ya watu wanaokubali habari njema inaongezeka. Wanafunzi ambao hawajabatizwa wanahitaji kutambua umuhimu wa funzo la Biblia la kibinafsi. Pia, wanapaswa kufundishwa jinsi ya kuwahubiria wengine habari njema na kuwafundisha kweli. Katika makutaniko yetu, ndugu wanahitaji kutiwa moyo wajitahidi ili wastahili kuwa watumishi wa huduma na wazee. Kupitia “mafundisho mema,” Wakristo wakomavu wanaweza kuwasaidia wapya wafanye maendeleo ya kiroho.​—Met. 4:2.

WASAIDIE WAPYA WAJUE JINSI YA KUJIFUNZA BIBLIA

3, 4. (a) Paulo alihusianishaje funzo la Biblia na huduma yenye matokeo? (b) Kabla ya kuwatia moyo wanafunzi wetu wajifunze Biblia kibinafsi, sisi wenyewe tunapaswa kuwa na mazoea gani?

3 Funzo la Biblia la kibinafsi ni muhimu kadiri gani? Tunapata jibu la swali hilo katika maneno ya Paulo kwa Wakristo Wakolosai. Aliandika hivi: “Hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba kwamba mjazwe ujuzi sahihi wa mapenzi [ya Mungu] katika hekima yote na utambuzi wa kiroho, ili mtembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” (Kol. 1:9, 10) Ujuzi huo sahihi ungewasaidia Wakristo Wakolosai “[kutembea] kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.” Hilo lingewawezesha kuendelea “kuzaa matunda katika kila kazi njema,” hasa katika kuhubiri habari njema. Ili amtumikie Mungu ifaavyo, mwabudu wa Yehova anapaswa kufuata ratiba ya kujifunza Biblia. Inafaa tuwasaidie wanafunzi wa Biblia waelewe jambo hilo.

4 Kabla ya kuwasaidia wengine kuona manufaa ya kujifunza Biblia kibinafsi, lazima tusadiki kwamba funzo hilo ni lenye thamani. Kwa kweli, sisi wenyewe tunapaswa kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza Biblia. Kwa hiyo, unaweza kujiuliza hivi: ‘Wenye nyumba wanapotoa maoni yanayopingana na mafundisho ya Biblia au wanapouliza maswali magumu, je, ninaweza kutoa majibu yanayotegemea Biblia? Ninaposoma kuhusu jinsi Yesu, Paulo, na wengine walivyovumilia katika huduma, je, mimi hutafakari jinsi uvumilivu wao unavyoweza kuathiri utumishi wangu kwa Yehova?’ Sote tunahitaji ujuzi na ushauri kutoka katika Neno la Mungu. Na tunapowaambia wengine jinsi ambavyo tumenufaika na funzo la Biblia la kibinafsi, tunawatia moyo wapate manufaa kama hayo kwa kuwa wanafunzi wenye bidii wa Maandiko.

5. Toa pendekezo la jinsi ya kuwasaidia wapya wawe na mazoea ya kujifunza Biblia kibinafsi.

5 Huenda ukajiuliza hivi: ‘Ninaweza kumzoezaje mwanafunzi wangu awe na mazoea ya kujifunza Biblia?’ Unaweza kuanza kwa kumwonyesha jinsi ya kujitayarisha kwa ajili ya funzo lenu. Huenda ukapendekeza asome nyongeza kwenye kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na maandiko yaliyotajwa. Msaidie atayarishe mikutano akiwa na lengo la kutoa maelezo. Mtie moyo asome kila nakala ya gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ikiwa Watchtower Library au Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO inapatikana katika lugha yake, unaweza kumwonyesha jinsi ya kuitumia kujibu maswali ya Biblia. Ukimsaidia kwa njia hiyo, inaelekea kwamba baada ya muda mfupi, mwanafunzi wako wa Biblia ataanza kufurahia kujifunza Neno la Mungu kibinafsi.

6. (a) Unaweza kumsaidiaje mwanafunzi wako aipende Biblia kutoka moyoni? (b) Huenda mwanafunzi wa Biblia akahisije baada ya kukuza tamaa ya kujifunza Biblia?

6 Bila shaka hatupaswi kumshinikiza mtu yeyote asome au ajifunze Biblia. Badala yake, acheni tutumie vifaa vilivyoandaliwa na tengenezo la Yehova kumsaidia mwanafunzi apende kujifunza Biblia. Baada ya muda, huenda mwanafunzi ambaye ni mnyoofu akahisi kama mtunga zaburi aliyeimba hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (Zab. 73:28) Roho takatifu ya Yehova itamchochea mwanafunzi huyo wa Biblia mwenye bidii na anayethamini Maandiko.

WAZOEZE WANAFUNZI KUHUBIRI NA KUFUNDISHA

7. Yesu aliwazoezaje watangazaji wa habari njema? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Katika Mathayo sura ya 10, tunasoma maagizo ambayo Yesu aliwapa mitume wake 12. Hakuzungumzia mambo kwa ujumla, alizungumzia mambo hususa. [1] Mitume walimsikiliza Yesu alipowafundisha jinsi ya kuhubiri kwa njia yenye matokeo. Kisha wakaenda shambani. Kwa kuwa walikuwa wameona njia ya Yesu ya kuhubiri, baada ya muda mfupi wakawa walimu stadi wa kweli za Biblia. (Mt. 11:1) Tunaweza kuwazoeza wanafunzi wetu wa Biblia wawe wahubiri wa habari njema wenye matokeo. Acheni sasa tuchunguze mambo mawili tunayoweza kuwazoeza wafanye.

8, 9. (a) Yesu alitumia mbinu zipi kuwahubiria watu? (b) Tunaweza kuwasaidiaje wahubiri wapya kuzungumza na watu kama Yesu alivyofanya?

8 Kuwa na mazungumzo pamoja na watu. Mara nyingi Yesu alizungumza na watu kuhusu Ufalme. Kwa mfano, alikuwa na mazungumzo mazuri na yenye matokeo pamoja na mwanamke fulani kando ya kisima cha Yakobo karibu na jiji la Sikari. (Yoh. 4:5-30) Pia, alizungumza na Mathayo Lawi, mkusanya kodi. Vitabu vya Injili havina habari nyingi kuhusu mazungumzo hayo, lakini Mathayo alikubali kuwa mfuasi wa Yesu. Mathayo na watu wengine walimsikiliza Yesu akizungumza kwa muda mrefu katika sherehe iliyofanywa kwenye nyumba ya Mathayo.—Mt. 9:9; Luka 5:27-39.

9 Katika pindi nyingine, Yesu alizungumza kwa urafiki na Nathanaeli, ambaye alikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu watu wa Nazareti. Hata hivyo, Nathanaeli alichochewa kubadili maoni yake. Aliamua kujifunza mengi zaidi kuhusu mafundisho ya Yesu, mwanamume kutoka Nazareti. (Yoh. 1:46-51) Hivyo, tuna sababu nzuri ya kuwazoeza wahubiri wapya wazungumze na watu kwa urafiki na kwa njia yenye kustarehesha. [2] Tunapowasaidia katika njia hiyo, inaelekea watafurahi kuona jinsi watu wenye mioyo minyoofu wanavyokubali kusikiliza habari njema tukizungumza nao kwa fadhili na kuwaonyesha upendo.

10-12. (a) Yesu alichocheaje upendezi ambao watu walionyesha katika habari njema? (b) Tunaweza kuwasaidiaje wahubiri wapya waboreshe ustadi wao wakiwa walimu wa kweli za Biblia?

10 Kuchochea upendezi. Yesu alikuwa na muda mfupi wa kutimiza huduma yake. Hata hivyo, alitumia muda kuchochea upendezi ambao watu walionyesha katika habari njema. Kwa mfano, Yesu alifundisha umati akiwa kwenye mashua. Katika pindi hiyo, alimsaidia kimuujiza Petro kupata samaki wengi kisha akamwambia hivi: “Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” Maneno na matendo ya Yesu yalikuwa na matokeo gani? Petro na wenzake “wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu, wakamfuata [Yesu].”​—Luka 5:1-11.

11 Nikodemo, mshiriki wa Sanhedrini, alipendezwa na mafundisho ya Yesu. Alitaka kujifunza mengi lakini aliogopa kile ambacho watu wangesema ikiwa wangemwona akizungumza na Yesu hadharani. Yesu alikuwa tayari kubadilikana na kuwa pamoja na watu wakati wowote; alikubali kukutana na Nikodemo usiku, wakati ambapo hakukuwa na watu. (Yoh. 3:1, 2) Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo? Mwana wa Mungu alitenga wakati wa kuimarisha imani ya watu. Je, hatupaswi kuwa na bidii ya kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na watu wanaopendezwa?

12 Inaelekea wahubiri wapya watakuwa walimu stadi wa kweli za Biblia ikiwa tutahubiri pamoja nao. Tunaweza kuwasaidia wawarudie hata watu ambao hawakupendezwa sana na ujumbe wetu. Tunaweza kuwaomba wahubiri wapya waandamane nasi katika ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia. Tunapowazoeza na kuwatia moyo kwa njia hiyo, bila shaka wahubiri wapya watakuwa na tamaa ya kuchochea upendezi wa watu na kuongoza mafunzo ya Biblia. Pia, watajifunza kuwa na subira na ustahimilivu katika huduma badala ya kukata tamaa haraka.​—Gal. 5:22; tazama sanduku lenye kichwa “ Ustahimilivu Ni Muhimu.”

WAZOEZE WAPYA WAWATUMIKIE WAAMINI WENZAO

13, 14. (a) Una maoni gani kuhusu masimulizi ya Biblia ya watu waliojidhabihu sana kwa niaba ya wengine? (b) Unaweza kufanya mambo gani ili uwazoeze wahubiri wapya na watoto wawapende ndugu na dada zao?

13 Masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba tuna pendeleo la kuonyesha “upendo wa kindugu” na kuwatumikia wengine. (Soma 1 Petro 1:22; Luka 22:24-27.) Mwana wa Mungu alitoa kila kitu, kutia ndani uhai wake, ili awahudumie wengine. (Mt. 20:28) Dorkasi “alizidi katika matendo mema na zawadi za rehema.” (Mdo. 9:36, 39) Maria, dada aliyeishi Roma, ‘alifanya kazi nyingi’ kwa niaba ya washiriki wa kutaniko. (Rom. 16:6) Tunaweza kuwasaidiaje wapya watambue umuhimu wa kuwasaidia ndugu na dada zao?

Wazoeze wapya wawapende waamini wenzao (Tazama fungu la 13, 14)

14 Mashahidi wakomavu wanaweza kuwaalika wapya waandamane nao wanapowatembelea ndugu na dada wagonjwa na waliozeeka. Ikiwa inafaa, wazazi wanaweza kuandamana na watoto wao katika ziara hizo. Wazee wanaweza kuwashirikisha wengine kuhakikisha kwamba ndugu zetu wapendwa ambao wamezeeka wanapata chakula kizuri na nyumba zao zinatunzwa na kurekebishwa. Katika njia hizo, watoto na wapya watajifunza kuwaonyesha wengine fadhili. Alipokuwa akihubiri katika eneo lake la vijijini, mzee mmoja alizoea kuwatembelea kifupi Mashahidi walioishi katika eneo hilo na kuwajulia hali. Ndugu fulani kijana aliyeandamana naye mara nyingi, alijifunza kwamba wote kutanikoni wanapaswa kuhisi kuwa wanapendwa.​—Rom. 12:10.

15. Kwa nini ni muhimu wazee wapendezwe na maendeleo ya wanaume kutanikoni?

15 Kwa kuwa Yehova anawatumia wanaume kama walimu kutanikoni, ni muhimu ndugu wajitahidi kuwa wasemaji wazuri. Ikiwa wewe ni mzee, je, unaweza kumsikiliza mtumishi wa huduma akifanya mazoezi ya hotuba yake? Kwa msaada wako, anaweza kuboresha ustadi wake akiwa mwalimu wa Neno la Mungu.​—Neh. 8:8. [3]

16, 17. (a) Paulo alionyeshaje kwamba anapendezwa na maendeleo ambayo Timotheo alifanya? (b) Wazee wanaweza kuwazoezaje kwa njia yenye matokeo ndugu watakaotumikia wakiwa wachungaji kutanikoni?

16 Kuna uhitaji mkubwa wa wachungaji katika kutaniko la Kikristo, na wale watakaofanya kazi hiyo wakati ujao wanahitaji kuendelea kuzoezwa. Paulo alitaja mambo ya msingi kuhusu jinsi ya kuwazoeza wengine, alipomwambia Timotheo hivi: “Wewe mtoto wangu, endelea kujipatia nguvu katika fadhili zisizostahiliwa ambazo ni kuhusiana na Kristo Yesu, na mambo uliyoyasikia kutoka kwangu kwa uthibitisho wa mashahidi wengi, mambo hayo uwakabidhi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:1, 2) Timotheo alijifunza kwa kufanya kazi pamoja na mtume huyo mwenye umri mkubwa. Kisha Timotheo alitumia mbinu za Paulo katika huduma yake na katika sehemu nyingine za utumishi mtakatifu.​—2 Tim. 3:10-12.

17 Paulo alitumia muda mwingi pamoja na Timotheo kwa sababu alitaka kuhakikisha kwamba amezoezwa vizuri. Kwa hiyo, alimwalika wasafiri pamoja. (Mdo. 16:1-5) Inapofaa, wazee wanaweza kuiga mfano wa Paulo kwa kuandamana na watumishi wa huduma wanaostahili kwenye ziara za uchungaji. Hivyo, wazee wanawapa ndugu hao nafasi ya kujionea ufundishaji, imani, subira, na upendo ambao wazee Wakristo wanahitaji kuonyesha. Kufanya hivyo kunachangia kuwazoeza wachungaji wa wakati ujao wa “kundi la Mungu.”​—1 Pet. 5:2.

UMUHIMU WA KUWAZOEZA WENGINE

18. Kwa nini ni muhimu kuwazoeza wengine katika utumishi wa Yehova?

18 Kuwazoeza wengine ni muhimu sana kwa sababu ya uhitaji mkubwa na nafasi zinazoongezeka za kumtumikia Yehova. Mifano ya jinsi Yesu na Paulo walivyowazoeza wengine inafaa hata leo. Yehova anataka watumishi wake leo wazoezwe vizuri kwa ajili ya migawo yao ya kitheokrasi. Mungu anatupatia pendeleo la kuwasaidia wasio na uzoefu kukuza ustadi wao wa kufanya kazi zinazohitajiwa kutanikoni. Kadiri hali zinavyozorota ulimwenguni na nafasi za kuhubiri zinavyoongezeka, ni muhimu kuwazoeza wengine na tunapaswa kufanya hivyo bila kukawia.

19. Kwa nini unapaswa kuwa na uhakika kwamba jitihada zako za kuwazoeza wengine katika utumishi wa Yehova zitafanikiwa?

19 Bila shaka, jitihada na muda unahitajiwa kuwazoeza wengine. Lakini Yehova na Mwana wake mpendwa watatutegemeza na kutupatia hekima ili tuwazoeze. Tunashangilia tunapowaona wale tunaowasaidia wakiendelea ‘kufanya kazi kwa bidii na kujikaza wenyewe.’ (1 Tim. 4:10) Acheni tuendelee kufanya maendeleo ya kiroho katika kumtolea Yehova utumishi mtakatifu.

^ [1] (fungu la 7) Yafuatayo ni baadhi ya mambo ambayo Yesu alizungumzia: (1) Hubiri ujumbe unaofaa. (2) Ridhika na maandalizi ya Mungu. (3) Epuka kubishana na wenye nyumba. (4) Mtegemee Mungu unapokabiliana na wapinzani. (5) Usiogope.

^ [2] (fungu la 9) Kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 62-64, kina madokezo mazuri ya jinsi ya kuwa na mazungumzo pamoja na watu katika huduma ya shambani.

^ [3] (fungu la 15) Kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 52 hadi 61, kinaeleza sifa zinazohitajiwa ili kuwa msemaji mzuri.