Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Furaha Ambayo Nimepata kwa Kutoa

Furaha Ambayo Nimepata kwa Kutoa

NILIPOKUWA na umri wa miaka 12, niligundua kwa mara ya kwanza kwamba nilikuwa na kitu chenye thamani ninachoweza kutoa. Katika kusanyiko fulani, ndugu mmoja aliniuliza ikiwa ningependa kuhubiri. Ingawa sikuwahi kuhubiri, nilisema “Ndiyo.” Tulienda kwenye eneo, na akanipa vijitabu kadhaa kuhusu Ufalme wa Mungu. Aliniambia hivi: “Zungumza na watu upande ule wa mtaa, nami nitazungumza na wa upande huu.” Nikiwa mwenye wasiwasi, nilianza kuhubiri nyumba kwa nyumba, na muda si muda nilikuwa nimemaliza vijitabu vyote. Ilikuwa wazi kwamba watu wengi walitaka kile nilichokuwa nikiwapa.

Nilizaliwa mnamo 1923, huko Chatham, jimbo la Kent, nchini Uingereza, na nililelewa kati ya watu waliovunjika moyo. Vita Vikuu havikuwa vimeboresha maisha kama wengi walivyotazamia. Pia, wazazi wangu walikuwa wamekatishwa tamaa na viongozi wa dini ya Kibaptisti waliotaka tu kujifaidi. Nilipokuwa na miaka tisa hivi, mama yangu alianza kwenda kwenye jumba ambalo Mashahidi wa Yehova walifanyia mikutano yao. Dada mmoja alitufundisha sisi watoto masomo yaliyotegemea Biblia na kitabu The Harp of God. Nilifurahia mambo niliyokuwa nikijifunza.

KUJIFUNZA KUTOKA KWA NDUGU WENYE UMRI MKUBWA

Nilipokuwa tineja, nilifurahia kushiriki na watu tumaini lililo katika Neno la Mungu. Ingawa mara nyingi nilihubiri nyumba kwa nyumba nikiwa peke yangu, nilijifunza mengi pia kwa kuhubiri pamoja na wengine. Kwa mfano, siku moja tulipokuwa tukisafiri kwa baiskeli kuelekea kwenye eneo pamoja na ndugu fulani mwenye umri mkubwa, tulimpita kiongozi wa dini nami nikasema, “Ona huyo mbuzi!” Ndugu huyo alisimamisha baiskeli yake na kuniomba niketi pamoja naye kwenye gogo. Alisema hivi: “Ni nani aliyekupa mamlaka ya kumhukumu mtu kuwa mbuzi? Acha tufurahie kuwapatia watu habari njema na tumwachie Yehova kazi ya kuhukumu.” Nilijifunza mengi kuhusu furaha ya kutoa katika miaka hiyo.—Mt. 25:31-33; Mdo. 20:35.

Ndugu mwingine mwenye umri mkubwa alinifundisha kwamba ili kupata furaha ya kutoa, wakati mwingine tunahitaji kuvumilia tukiwa na subira. Mke wake hakuwapenda Mashahidi wa Yehova. Pindi moja ndugu huyo alinikaribisha kwake kwa ajili ya viburudisho. Kwa kuwa ndugu huyo alienda kuhubiri, mke wake alikasirika sana hivi kwamba akaanza kuturushia pakiti za majani ya chai. Badala ya kumkaripia, akiwa mwenye shangwe ndugu huyo alichukua pakiti hizo na kuzirudisha mahali pake. Miaka mingi baadaye, alithawabishwa kwa kuonyesha subira mke wake alipobatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

Tamaa yangu ya kuwapa wengine tumaini la wakati ujao iliendelea kukua, hivyo mimi na mama yangu tulibatizwa katika mji wa Dover, mnamo Machi 1940. Nilipokuwa na miaka 16, Uingereza ilitangaza vita dhidi ya Ujerumani mnamo Septemba 1939. Katika Juni 1940, niliona malori yaliyobeba maelfu ya wanajeshi waliovurugika na kuvunjika moyo yakipita mbele ya nyumba yetu. Walikuwa waokokaji wa Vita vya Dunkirk. Hawakuwa na tumaini lolote, na nilitamani kuwaeleza kuhusu Ufalme wa Mungu. Baadaye mwaka huo, Uingereza ilianza kurushiwa mabomu. Kila usiku, niliona ndege nyingi za kivita za Ujerumani zenye mabomu zikipita juu ya eneo letu. Tulisikia sauti ya mabomu yakiangushwa na kulipuka, na hilo liliongeza woga. Kila asubuhi tulipotoka nje, tungekuta eneo kubwa la nyumba zilizoharibiwa. Iliendelea kuwa wazi kwangu kwamba Ufalme ndio tumaini pekee la wakati ujao.

MAISHA YA KUTOA YANAANZA

Mwaka wa 1941, ndio mwaka nilioanza rasmi maisha ambayo yameniletea furaha tele. Nilikuwa nikifanya kazi katika Royal Dockyard iliyo Chatham nikizoezwa kuwa fundi wa meli, kazi ambayo ilitamaniwa na watu wengi na iliyokuwa na marupurupu mengi. Kwa muda mrefu, watumishi wa Yehova walikuwa wametambua kwamba Wakristo hawapaswi kupigania taifa lolote. Kufikia mwaka wa 1941, tulitambua kwamba hatupaswi kufanya kazi katika kampuni ya kutengeneza silaha. (Yoh. 18:36) Kwa kuwa kampuni iliyoniajiri ilikuwa ikitengeneza nyambizi, niliamua kuacha kazi na kuanza utumishi wa wakati wote. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa katika mji wa Cirencester, mji maridadi ulio kwenye eneo lenye vilima la Cotswolds.

Nilipofikisha umri wa miaka 18, nilifungwa gerezani kwa miezi tisa kwa kukataa kujiunga na jeshi. Niliogopa sana chumba changu cha gereza kilipofungwa na nikaachwa peke yangu. Lakini muda si muda, walinzi na wafungwa walianza kuuliza kwa nini nimefungwa, na kwa shangwe niliwaeleza imani yangu.

Nilipoachiliwa, niliombwa nijiunge na Leonard Smith * kuhubiri kwenye miji mbalimbali katika jimbo letu la Kent. Kuanzia mwaka wa 1944, ndege nyingi za kivita zilizojazwa makombora ziliangushwa katika eneo la Kent. Ndege hizo zilipita kwenye eneo letu lililokuwa katikati ya eneo la Wanazi na London. Ndege hizo ziliitwa doodlebugs. Ilikuwa kampeni ya kuwatia watu woga, kwa kuwa kila mara uliposikia ndege ikizima ikiwa hewani, ungejua kwamba itaanguka na kulipuka. Tuliongoza funzo fulani la Biblia na familia ya watu watano. Nyakati nyingine, tuliketi chini ya meza ya chuma, iliyokusudiwa kuwalinda ikiwa nyumba ingeangukiwa na makombora. Mwishowe, washiriki wote wa familia hiyo walibatizwa.

KUENEZA HABARI NJEMA NG’AMBO

Kutangaza kusanyiko nilipoanza upainia huko Ireland

Baada ya vita, nilifanya upainia kwa miaka miwili katika eneo la kusini mwa Ireland. Hatukujua kwamba Ireland ilitofautiana sana na Uingereza. Tulitafuta mahali pa kulala nyumba kwa nyumba, na kusema kwamba sisi ni wamishonari. Pia, tuliwaachia watu magazeti barabarani. Ni “upumbavu” sana kufanya hivyo katika nchi ya Kikatoliki! Mwanamume fulani alipotisha kututendea kijeuri, nilimweleza polisi ambaye alinijibu hivi: “Sasa, ulikuwa unatarajia nini?” Hatukutambua kiasi cha uvutano ambao makasisi walikuwa nao. Waliwafanya watu wafutwe kazi ikiwa wangechukua vitabu vyetu, na walifanya tufukuzwe kutoka mahali petu pa kulala.

Tuligundua kwamba baada ya kuhamia eneo jipya, tungepata matokeo mazuri zaidi kwa kusafiri hadi eneo lingine mbali na mahali petu pa kulala, na kuwahubiria watu ambao walikuwa na kasisi tofauti. Kisha, tulimalizia kwa kuwahubiria watu katika eneo letu. Tulipokuwa Kilkenny, tulijifunza na mwanamume kijana mara tatu kwa juma licha ya vitisho vya kushambuliwa na vikundi vya watu wenye jeuri. Nilifurahia sana kuwafundisha watu kweli za Biblia hivi kwamba nikajaza ombi la kuzoezwa kuwa mmishonari katika Shule ya Gileadi.

Tuliishi kwenye mashua iliyoitwa Sibia tangu mwaka wa 1948 hadi 1953

Baada ya kuzoezwa kwa miezi mitano huko New York, mimi na wenzangu watatu tulipewa mgawo wa kutumika katika visiwa vidogo vya Bahari ya Karibea. Katika Novemba mwaka wa 1948, tulisafiri kutoka jiji la New York City kwa mashua iliyoitwa Sibia yenye urefu wa mita 18. Sikuwahi kusafiri majini, kwa hiyo safari hiyo ilinisisimua. Ndugu mmoja kati yetu aliyeitwa Gust Maki, alikuwa nahodha mwenye uzoefu. Alitufundisha mambo ya msingi kuhusu jinsi ya kuongoza mashua, kama vile kuinua na kushusha matanga, jinsi ya kufuata mwelekezo wa dira, na jinsi ya kufunga ayari dhidi ya upepo. Kwa ustadi, Gust aliongoza mashua yetu kwa siku 30 kupitia dhoruba hatari mpaka tukafika eneo la Bahamas.

“KULITANGAZA KATI YA VISIWA”

Baada ya kuhubiri kwa miezi michache kwenye visiwa vya Bahamas, tulipanda mashua kuelekea Visiwa vya Leeward na Visiwa vya Windward, vilivyosambaa kwa umbali wa kilomita 800 kutoka Visiwa vya Virgin karibu na Puerto Riko hadi maeneo yaliyo karibu na Trinidad. Kwa miaka mitano, tulihubiri hasa katika visiwa vya mbali ambavyo havikuwa na Mashahidi. Tukiwa huko, nyakati nyingine hatukuweza kutuma au kupokea barua kwa majuma kadhaa. Lakini tulifurahia sana kulitangaza neno la Yehova kati ya visiwa!—Yer. 31:10.

Wamishonari wakiwa kwenye mashua Sibia (kuanzia kushoto hadi kulia): Ron Parkin, Dick Ryde, Gust Maki, na Stanley Carter

Tulipotia nanga, wenyeji walisisimuka sana kutuona na watu walikusanyika kwenye gati ili wajue sisi ni akina nani. Baadhi yao hawakuwahi kuona mashua au mzungu. Wenyeji wa visiwa hivyo walikuwa watu wenye urafiki, wa kidini, na waliijua Biblia vizuri. Mara nyingi, walitupatia samaki wabichi, maparachichi, na njugu-karanga. Ingawa chombo chetu kilikuwa kidogo, tulifaulu kulala, kupika, na kufua.

Tulitia nanga kwenye ufuo na kuwahubiria watu mchana kutwa. Tuliwaambia kwamba kutakuwa na hotuba ya Biblia. Kisha jioni ilipofika, tulipiga kengele ya mashua ili kuwaalika watu. Ilichangamsha sana kuona wakazi wakiwasili. Taa zao zilionekana kama nyota zikishuka juu ya milima. Nyakati nyingine tungekuwa na wahudhuriaji mia moja na wangeuliza maswali hadi usiku sana. Walipenda kuimba, hivyo tulichapisha na kuwapa maneno ya baadhi ya nyimbo za Ufalme. Sauti zao ziliungana vizuri sana na sauti zetu tulipowaongoza katika kuimba nyimbo hizo. Kwa kweli, tuna kumbukumbu nzuri sana za siku hizo!

Nyakati nyingine, baada ya kumaliza kujifunza Biblia, baadhi ya wanafunzi wangeandamana nasi mpaka kwenye funzo linalofuata na kujiunga nao ili tujifunze pamoja. Ingawa tuliishi kwenye eneo moja kwa majuma machache tu, mara nyingi tuliwaomba wale walioelewa Biblia zaidi waendelee kujifunza na wenzao hadi tutakaporudi. Ilipendeza sana kuona jinsi ambavyo baadhi yao walichukulia kwa uzito mgawo huo.

Leo, visiwa vingi kati ya hivyo vimejaa hoteli za kitalii, lakini siku hizo vilikuwa visiwa vilivyojitenga vyenye wangwa maridadi, fukwe zenye kuvutia, na miti ya mitende tu. Kwa kawaida tulisafiri usiku kutoka kisiwa kimoja hadi kingine. Pomboo waliogelea kuzunguka mashua yetu, na sauti pekee ambayo ungesikia ilikuwa ya mashua yetu ikisafiri juu ya maji. Na mwanga wa mwezi juu ya bahari tulivu ulionekana kama barabara kuu iliyonyooka kufikia upeo wa macho.

Baada ya kuhubiri kwa miaka mitano kwenye visiwa hivyo, tulienda Puerto Riko ili kubadilisha mashua yetu kwa mashua yenye injini. Tulipofika, nilikutana na dada mrembo mmishonari anayeitwa Maxine Boyd, na nikampenda. Alikuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii tangu utotoni. Baadaye, alitumika akiwa mmishonari katika Jamhuri ya Dominika mpaka alipofukuzwa na serikali hiyo ya Kikatoliki mwaka wa 1950. Kwa sababu nilikuwa baharia, nilipewa kibali cha kukaa nchini Puerto Riko kwa mwezi mmoja tu. Punde si punde ningesafiri kwenda visiwani na ningebaki huko kwa miaka kadhaa. Basi nikajiambia, ‘Ronald, ikiwa unampenda msichana huyu, lazima uchukue hatua mara moja.’ Baada ya majuma matatu, nilimwomba tuanze uchumba, na baada ya majuma sita tukaoana. Mimi na Maxine tulipewa mgawo wa kuwa wamishonari nchini Puerto Riko, kwa hiyo sikwenda kwenye mashua mpya.

Mwaka wa 1956, tulianza kazi ya kuzuru makutaniko nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Ndugu wengi walikuwa maskini lakini tulifurahia kuwatembelea. Kwa mfano, katika kijiji cha Potala Pastillo, kulikuwa na familia mbili za Mashahidi ambazo zilikuwa na watoto wengi, na nilipenda kuwapigia muziki kwa filimbi. Nilimwuliza mmoja wa wasichana wadogo anayeitwa Hilda, ikiwa angependa kwenda mahubiri pamoja nasi. Alisema hivi: “Ningependa kuandamana nanyi lakini sina viatu.” Tulimnunulia viatu, naye alijiunga nasi. Miaka mingi baadaye, katika mwaka wa 1972, mimi na Maxine tulipotembelea Betheli ya Brooklyn, dada fulani aliyehitimu kutoka Shule ya Gileadi alikuja kuzungumza nasi. Alikuwa karibu kwenda kwenye mgawo wake nchini Ekuado, naye alituambia hivi: “Sidhani kama mnanikumbuka. Mimi ni yule msichana mdogo kutoka Pastillo ambaye hakuwa na viatu.” Kumbe alikuwa Hilda! Tulifurahi sana mpaka tukatokwa na machozi!

Katika mwaka wa 1960, tuliombwa tutumikie kwenye ofisi ya tawi ya Puerto Riko, ambayo ilikuwa kwenye nyumba ndogo yenye orofa mbili huko Santurce, San Juan. Mwanzoni, mimi na Lennart Johnson tulifanya kati ya kazi nyingi zilizohusika. Yeye na mkewe walikuwa Mashahidi wa Yehova wa kwanza katika Jamhuri ya Dominika, nao walikuwa wamewasili nchini Puerto Riko mwaka wa 1957. Baadaye, Maxine alishughulikia maandikisho ya magazeti ambayo wakati mwingine yangekuwa zaidi ya elfu moja kwa juma. Alifurahia kufanya kazi hiyo kwa sababu aliwafikiria watu wote ambao wangepokea chakula hicho cha kiroho.

Ninafurahia kutumikia Betheli, kwa sababu ni kazi inayohusisha kutoa. Lakini haikosi changamoto. Kwa mfano, wakati wa kusanyiko la kimataifa la kwanza nchini Puerto Riko mwaka wa 1967, nilihisi kulemewa na majukumu mbalimbali. Nathan Knorr, aliyekuwa akiongoza kazi ya Mashahidi wa Yehova, alikuja nchini Puerto Riko. Alifikiri kimakosa kwamba sikuwa nimefanya mipango ya usafiri kwa ajili ya wamishonari ambao wangetutembelea, ingawa nilikuwa nimefanya hivyo. Baadaye, alinishauri vikali kuhusu kuwa mwenye utaratibu na akasema kwamba nimemtamausha. Sikutaka kubishana naye ingawa nilihisi kwamba hajanielewa, na hilo lilinikasirisha kwa kipindi fulani. Hata hivyo, miaka kadhaa baadaye tulipokutana na Ndugu Knorr, alitualika chumbani mwake na kutupikia.

Tukiwa Puerto Riko, tuliwatembelea watu wa familia yangu mara kadhaa. Baba hakuikubali kweli wakati mimi na mama tulipoanza kujifunza. Lakini wasemaji walipozuru kutoka Betheli, mara nyingi waliishi nyumbani kwetu. Baba aliona jinsi waangalizi hao wanyenyekevu walivyotofautiana na makasisi wa kidini, ambao miaka mingi mapema walimchukiza sana. Mwishowe, mwaka wa 1962 alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

Nikiwa na Maxine nchini Puerto Riko muda mfupi baada ya kufunga ndoa na tulipoadhimisha miaka 50 ya ndoa mwaka wa 2003

Mke wangu mpendwa, Maxine, alikufa mwaka wa 2011. Ninatazamia kwa hamu kumwona tena atakapofufuliwa. Ahadi hiyo hunitia moyo sana! Kwa miaka 58 tuliyoishi pamoja, mimi na Maxine tuliona idadi ya Mashahidi wa Yehova ikiongezeka nchini Puerto Riko kutoka 650 hivi hadi 26,000! Kisha mwaka wa 2013, ofisi ya tawi ya Puerto Riko iliunganishwa na ofisi ya Marekani, na niliombwa kutumikia huko Wallkill, New York. Baada ya miaka 60 katika kisiwa hicho, nilijihisi mwenyeji kama chura mdogo wa Puerto Riko anayeitwa coquí, ambaye huimba ko-kee, ko-kee akiwa kwenye miti saa za jioni. Lakini ulikuwa wakati wa kuhama.

“MUNGU HUMPENDA MTOAJI MCHANGAMFU”

Bado ninafurahia kumtumikia Mungu hapa Betheli. Sasa nina miaka zaidi ya 90, na kazi yangu ni kuwatia moyo washiriki wa familia ya Betheli. Nimeelezwa kwamba nimewatembelea watu zaidi ya 600 tangu nije Wallkill. Baadhi yao wanakuja kuzungumza kuhusu matatizo ya kibinafsi au ya familia. Wengine huomba ushauri kuhusu jinsi ya kufanikiwa katika utumishi wa Betheli. Na wengine waliooana karibuni hutafuta ushauri kuhusu ndoa. Wanabetheli fulani wamepewa mgawo wa kwenda shambani. Mimi huwasikiliza wote wanaokuja kuzungumza nami, na inapofaa ninawaambia, “‘Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.’ Hivyo furahia kazi yako. Unamfanyia Yehova.”—2 Kor. 9:7.

Ili uendelee kuwa mwenye furaha katika mgawo wako wa Betheli au mgawo mwingine wowote ni lazima ukazie fikira kwa nini mgawo wako ni muhimu. Kazi zote tunazofanya Betheli ni utumishi mtakatifu. Huchangia katika kumsaidia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kuandaa chakula cha kiroho kwa ajili ya ndugu ulimwenguni pote. (Mt. 24:45) Hata iwe tunatumikia Yehova tukiwa wapi, tuna nafasi nyingi za kumsifu. Acheni tufurahie kile ambacho ametuambia tufanye, kwa kuwa “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”

^ fu. 13 Simulizi la maisha la Leonard Smith lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2012.