Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafuta Kitu Chenye Thamani Zaidi Kuliko Dhahabu

Tafuta Kitu Chenye Thamani Zaidi Kuliko Dhahabu

Je, umewahi kupata chembe ndogo ya dhahabu? Ni watu wachache sana ambao wamewahi kupata. Hata hivyo, mamilioni ya watu wamepata kitu bora kuliko dhahabu. Ni hekima kutoka kwa Mungu ambayo “dhahabu safi haiwezi kubadilishwa nayo.”​—Ayu. 28:12, 15.

KATIKA njia fulani, wanafunzi wanyoofu wa Biblia ni kama watu wanaotafuta dhahabu. Wanafunzi hao wanahitaji kuwa wenye bidii na kuendelea kuchunguza Maandiko ili wapate hekima yenye thamani. Tukiwa wanafunzi wa Biblia, tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi ambavyo dhahabu hutafutwa? Acheni tuchunguze njia tatu.

GHAFLA UNAPATA DHAHABU!

Wazia kwamba unatembea kando ya mto kisha unaona jiwe dogo liking’aa. Unainama na unafurahi unapogundua kwamba umepata chembe ya dhahabu. Ni ndogo kuliko kichwa cha njiti ya kiberiti lakini ni adimu kuliko almasi bora. Bila shaka, utatafuta kuona ikiwa kuna chembe zaidi katika eneo hilo.

Vivyo hivyo, ni kweli kwamba huwezi kusahau siku ambayo Shahidi wa Yehova alibisha mlangoni pako ili kuzungumzia ujumbe wa tumaini ulio katika Biblia. Huenda unakumbuka vizuri wakati ulipopata chembe yako ya kwanza ya dhahabu ya kiroho. Labda ni siku ambayo uliona jina la Mungu, Yehova, katika Biblia. (Zab. 83:18) Au ni wakati ulipojifunza kwamba unaweza kuwa rafiki ya Yehova. (Yak. 2:23) Ulitambua mara moja kwamba ulikuwa umepata kitu chenye thamani zaidi kuliko dhahabu! Na huenda ulitamani kupata chembe zaidi za kiroho.

UNAPATA DHAHABU ZAIDI!

Mara nyingine chembe ndogo za dhahabu hujikusanya kwenye vijito na mito. Nyakati nyingine, watafutaji wenye bidii wanaweza kupata marundo makubwa kama hayo yenye thamani ya pesa nyingi kwa miezi michache tu.

Ulipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, huenda ulihisi kama mtafutaji aliyepata rundo la dhahabu. Kutafakari andiko moja baada ya lingine kuliongeza ujuzi wako na kukuimarisha kiroho. Ulipotafakari kweli hizo zenye thamani za Biblia, ulijifunza jinsi unavyoweza kumkaribia Yehova na kujitunza katika upendo wake ili upate uzima wa milele.—Yak. 4:8; Yuda 20, 21.

Kama mtafutaji anayejitahidi kupata dhahabu, je, unajitahidi kujifunza kweli za Biblia zenye thamani?

Kama mtafutaji anavyotafuta marundo ya dhahabu, huenda ulikuwa na bidii nyingi ulipokuwa ukitafuta utajiri wa kiroho wenye thamani. Baada ya kujifunza kweli za msingi, inaelekea ulichochewa kufanya mabadiliko na kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa.​—Mt. 28:19, 20.

ENDELEA KUTAFUTA!

Huenda mtafutaji akapata dhahabu kidogo ndani ya mwamba. Baadhi ya miamba hiyo inaweza kuwa na dhahabu nyingi kiasi cha kumfanya mtafutaji achimbe na kuponda mwamba huo ili atoe dhahabu. Huenda isiwe rahisi kuona dhahabu iliyo ndani ya mwamba huo. Kwa nini? Kwa sababu mawe yenye madini yenye thamani kubwa yanaweza kuwa na gramu 10 tu za dhahabu katika mwamba wenye uzito wa tani moja! Hata hivyo, kwa mtafutaji huyo kiasi hicho kina thamani ya kutosha kufanya aichimbe.

Vivyo hivyo, jitihada zinahitajiwa hata baada ya mtu kujifunza “fundisho la msingi juu ya Kristo.” (Ebr. 6:1, 2) Unahitaji kufanya bidii kupata mambo mapya na masomo unayoweza kutumia maishani unapojifunza Biblia. Kwa hiyo, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba funzo lako la Biblia linaendelea kukujenga, hata ikiwa umejifunza Biblia kwa miaka mingi?

Endelea kuwa na hamu ya kujifunza. Zingatia mambo madogo-madogo. Endelea kujitahidi na utapata chembe zenye thamani za Maandiko zilizo na hekima na mwongozo wa Mungu. (Rom. 11:33) Ili uongeze ujuzi wako wa Maandiko, tumia vizuri vifaa vya utafiti vinavyopatikana katika lugha yako. Kwa subira tafuta mwongozo unaohitaji na majibu ya maswali yako ya Biblia. Waulize wengine ni maandiko gani na makala zipi ambazo hasa zimewanufaisha na kuwatia moyo. Waeleze wengine mambo yenye kufurahisha ambayo umegundua wakati wa funzo lako la Neno la Mungu.

Bila shaka, lengo lako si tu kuongeza ujuzi. Mtume Paulo alionya kwamba “ujuzi huleta majivuno.” (1 Kor. 8:1) Hivyo, jitahidi ili uendelee kuwa mnyenyekevu na mwenye imani yenye nguvu. Ibada ya familia na funzo la Biblia la kibinafsi la kawaida litakusaidia kuishi kulingana na viwango vya Yehova na litakuchochea kuwasaidia wengine. Zaidi ya yote, utashangilia kwa sababu utakuwa umepata kitu chenye thamani zaidi kuliko dhahabu.—Met. 3:13, 14.