Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Johannes Rauthe akishiriki kazi ya kuhubiri, yaelekea katika miaka ya 1920

Kutoka Katika Hifadhi Ya Vitu Vyetu Vya Kale

“Ninapata Matokeo Yanayomtukuza Yehova”

“Ninapata Matokeo Yanayomtukuza Yehova”

GAZETI la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1915, lilisema hivi kuhusu vita vya kwanza vya ulimwengu, ambavyo mwishowe vilihusisha nchi 30 hivi: “Vita vyote vilivyopiganwa kipindi cha nyuma ni vidogo sana vinapolinganishwa na vita vikubwa vinavyoendelea barani Ulaya.” Kwa sababu ya uadui kati ya mataifa, gazeti hilo liliripoti hivi: “Utumishi [wa Ufalme] umezuiwa kwa kiasi fulani, hasa nchini Ujerumani na Ufaransa.”

Wanafunzi wa Biblia walikabiliwa na mapigano yaliyohusisha ulimwengu mzima lakini hawakuelewa kikamili kanuni ya Kikristo ya kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Hata hivyo, walikuwa wameazimia kutangaza habari njema. Wilhelm Hildebrandt alitaka kushiriki katika utumishi wa Ufalme, hivyo aliagiza nakala za trakti The Bible Students Monthly katika Kifaransa. Hakuwa nchini Ufaransa akiwa kolpota (mhubiri wa wakati wote) bali alikuwa mwanajeshi Mjerumani. Ingawa alipaswa kuwa adui, mwanamume huyo aliyevalia sare za kijeshi, aliwashangaza wapita-njia Wafaransa kwa kuwapa ujumbe wa amani.

Barua zilizochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi zinaonyesha kwamba baadhi ya Wanafunzi wa Biblia kutoka Ujerumani walihisi wana wajibu wa kushiriki habari njema za Ufalme walipokuwa katika utumishi wa kijeshi. Ndugu Lemke, aliyetumikia katika jeshi la wanamaji, aliripoti kwamba wanajeshi wenzake watano walipendezwa na ujumbe wa Ufalme. Aliandika hivi: “Hata katika meli hii, ninapata matokeo yanayomtukuza Yehova.”

Georg Kayser alienda vitani akiwa mwanajeshi na kurudi nyumbani akiwa mtumishi wa Mungu wa kweli. Ni nini kilichotokea? Alipata chapisho la Wanafunzi wa Biblia, akakubali kweli za Ufalme kwa moyo wote, na kuacha kuwa mwanajeshi. Kisha alianza kufanya kazi ambayo haikuhusisha kupigana. Baada ya vita, alitumika akiwa painia mwenye bidii kwa miaka mingi.

Wanafunzi wa Biblia hawakuelewa kikamili suala la kutounga mkono upande wowote, lakini mtazamo na matendo yao yalitofautiana sana na ya watu wengine waliounga mkono vita. Ingawa wanasiasa na viongozi wa kidini waliunga mkono vita, Wanafunzi wa Biblia walishikamana na “Mkuu wa Amani.” (Isa. 9:6) Baadhi ya Wakristo hao hawakudumisha kikamili msimamo wa kutounga mkono upande wowote, lakini bado walikuwa na imani ya msingi kama ya Mwanafunzi wa Biblia anayeitwa Konrad Mörtter, ambaye alisema hivi: “Nilitambua wazi kutoka kwenye Neno la Mungu kwamba Mkristo hapaswi kuua.”​—Kut. 20:13. *

Hans Hölterhoff alitumia gari hili la kukokota kutangaza gazeti la The Golden Age

Nchini Ujerumani, ambapo sheria haikumruhusu mtu akatae kushiriki vita kwa sababu ya dhamiri, Wanafunzi wa Biblia zaidi ya 20 walikataa kabisa kujihusisha na jeshi. Baadhi yao walionwa kuwa wana tatizo la kiakili, kama vile Gustav Kujath, ambaye alipelekwa kwenye hospitali ya wagonjwa wa akili na kupewa dawa. Hans Hölterhoff, ambaye pia alikataa kujiandikisha katika jeshi, alifungwa gerezani, ambapo alikataa kazi zozote zilizohusiana na vita. Walinzi walimvisha vazi rasmi lililombana mpaka mikono na miguu yake ikafa ganzi. Hilo lilipokosa kuvunja azimio lake, walinzi walifanya mipango ya kumwua ili kumtisha. Hata hivyo, Hans alibaki thabiti kipindi chote cha vita.

Ndugu wengine waliojiandikisha jeshini walikataa kubeba silaha na wakaomba kazi nyingine zisizohusisha kupigana. * Kwa mfano, Johannes Rauthe alifanya hivyo na akatumwa kufanya kazi kwenye shirika la reli. Konrad Mörtter alipewa kazi ya kuwasaidia wauguzi na madaktari, naye Reinhold Weber alifanya kazi akiwa muuguzi. August Krafzig alifurahi kwamba kazi yake haikuhusisha kwenda vitani. Wanafunzi hao wa Biblia na wengine kama wao walikuwa wameazimia kumtumikia Yehova kulingana na jinsi walivyoelewa maana ya kuonyesha upendo na ushikamanifu.

Kwa sababu ya mwenendo wao wakati wa vita, Wanafunzi wa Biblia walianza kuchunguzwa na serikali. Miaka iliyofuata Wanafunzi wa Biblia nchini Ujerumani walishtakiwa mara nyingi kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri. Ili kuwasaidia, ofisi ya tawi ya Ujerumani ilianzisha idara ya mambo ya kisheria katika Betheli ya Magdeburg.

Hatua kwa hatua, Mashahidi wa Yehova waliboresha uelewaji wao kuhusu msimamo wa Kikristo. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza, walidumisha msimamo wao kwa kutojihusisha hata kidogo na utumishi wa kijeshi. Hivyo, walionwa kuwa maadui wa Ujerumani, jambo lililofanya wateswe vikali. Lakini hiyo ni habari itakayozungumziwa katika makala nyingine kwenye mfululizo wa “Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale.”​—Kutoka katika hifadhi ya vitu vyetu vya kale ya Ulaya ya Kati.

^ fu. 7 Tazama similizi la Wanafunzi wa Biblia nchini Uingereza katika kipindi cha Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kwenye makala yenye kichwa, “Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale​—Walisimama Imara Katika ‘Saa ya Jaribu’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2013.

^ fu. 9 Jambo hilo lilipendekezwa katika Buku la VI la kitabu Millennial Dawn (1904) na pia katika toleo la Kijerumani la Zion’s Watch Tower la Agosti 1906. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1915 lilirekebisha maoni yetu na kupendekeza kwamba Wanafunzi wa Biblia wasijiunge na jeshi. Hata hivyo, makala hiyo haikuchapishwa kwenye toleo la Kijerumani.