Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini masimulizi ya Mathayo na Luka kuhusu maisha ya awali ya Yesu yanatofautiana?

Simulizi la Mathayo kuhusu matukio yanayohusiana na kuzaliwa kwa Yesu na maisha yake ya awali linatofautiana na simulizi la Luka kwa kiasi fulani kwa sababu waandikaji hao walikazia mambo tofauti.

Simulizi la Mathayo linakazia matukio yanayomhusu Yosefu. Linasimulia jinsi ambavyo Yosefu alitenda baada ya kujua kwamba Maria ana mimba, ndoto iliyomweleza kilichotukia, na jinsi alivyokubali maelezo hayo. (Mt. 1:19-25) Pia, Mathayo anaeleza kuhusu ndoto ya Yosefu ambayo katika hiyo malaika alimhimiza akimbilie Misri, safari yake pamoja na familia yake, ndoto ambayo malaika anamwagiza arudi nchi ya Israeli, safari ya kurudi, na uamuzi wake wa kuishi Nazareti pamoja na familia yake. (Mt. 2:13, 14, 19-​23) Katika sura za kwanza za Injili ya Mathayo, Yosefu anatajwa mara tisa, lakini Maria anatajwa mara tano tu.

Kwa upande mwingine, simulizi la Luka linamzungumzia Maria zaidi. Linatia ndani simulizi la malaika Gabrieli alipomtembelea Maria, Maria alipomtembelea mtu wa familia yake, Elisabeti, na maneno ya Maria ya kumsifu Yehova. (Luka 1:26-56) Luka anataja pia maneno ambayo Simeoni alimwambia Maria kuhusu jinsi Yesu angeteseka wakati ujao. Hata anaposimulia wakati ambapo familia hiyo ilienda hekaluni Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, Luka anataja maneno ya Maria, si ya Yosefu. Luka anataja pia kwamba Maria aliathiriwa sana na matukio hayo yote. (Luka 2:19, 34, 35, 48, 51) Katika sura mbili za kwanza za Injili ya Luka, Maria anatajwa mara 14, lakini Yosefu anatajwa mara 3 tu. Hivyo basi, Mathayo anaeleza zaidi kuhusu mahangaiko na utendaji wa Yosefu, ilhali Luka anataja mambo mengi zaidi kuhusu jukumu la Maria na mambo aliyopitia maishani.

Vivyo hivyo, waandikaji hao wa Injili wanatofautiana katika rekodi zao za ukoo wa Yesu. Mathayo anaorodhesha ukoo wa Yesu kupitia Yosefu na kuonyesha kwamba Yesu ndiye mrithi wa kisheria wa ufalme wa Daudi. Kwa nini? Kwa sababu Yosefu alikuwa mzao wa Mfalme Daudi kupitia Sulemani mwana wa Daudi. (Mt. 1:6, 16) Hata hivyo, inaelekea Luka anaorodhesha ukoo wa Yesu kupitia Maria na kuonyesha kwamba Yesu ndiye mrithi wa asili wa ufalme wa Daudi “kulingana na mwili.” (Rom. 1:⁠3) Kwa nini? Kwa sababu Maria alikuwa mzao wa Mfalme Daudi kupitia mwanawe, Nathani. (Luka 3:31) Lakini kwa nini Luka hamworodheshi Maria kupitia ukoo wa Heli, baba yake? Kwa sababu koo zilizotambuliwa kisheria ziliorodheshwa kupitia wanaume. Kwa hiyo, Luka anapomtaja Yosefu kuwa mwana wa Heli, ilieleweka kwamba Yosefu alikuwa mwana-mkwe wa Heli.​—Luka 3:23.

Orodha za ukoo zilizoandikwa na Mathayo na Luka zinathibitisha wazi kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Kwa hakika, ukweli kuhusu ukoo wa Yesu ulijulikana sana hivi kwamba hata Mafarisayo na Masadukayo hawangeweza kukana kwamba alikuwa wa ukoo huo. Leo, rekodi za koo zilizoandikwa na Mathayo na Luka ni sehemu ya msingi wa imani yetu na ushuhuda kuhusu uhakika wa ahadi za Mungu.