Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fanya Kazi Pamoja na Yehova Kila Siku

Fanya Kazi Pamoja na Yehova Kila Siku

“Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.”—1 KOR. 3:9.

NYIMBO: 64, 111

1. Tunaweza kufanya kazi pamoja na Yehova katika njia zipi?

MUUMBA alikusudia kwamba wanadamu wakamilifu wangeshirikiana naye ili kutimiza mambo aliyokusudia. Licha ya kwamba wanadamu si wakamilifu, bado watu ambao ni waaminifu wanaweza kufanya kazi na Yehova kila siku. Kwa mfano, tunapohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi, tunakuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:5-9) Hebu fikiria jinsi lilivyo pendeleo kubwa kuwa miongoni mwa watu ambao Muumba mweza yote anawaona kuwa wanastahili kufanya kazi iliyo muhimu sana machoni pake! Hata hivyo, mbali na kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kuna njia nyingine ambazo tunaweza kufanya kazi pamoja na Yehova. Makala hii itazungumzia njia nyingine ambazo tunaweza kufanya kazi pamoja na Yehova, yaani, kwa kuwasaidia washiriki wa familia zetu na waabudu wenzetu, kwa kuwa wakarimu, kwa kujitolea katika miradi ya kitheokrasi, na kwa kupanua utumishi wetu mtakatifu.—Kol. 3:23.

2. Kwa nini si jambo la hekima kulinganisha mambo unayofanya ili kuendeleza makusudi ya Yehova na mambo ambayo wengine wanafanya?

2 Tunapochunguza habari hii, usilinganishe mambo unayoweza kumfanyia Yehova na mambo ambayo wengine wanaweza kumfanyia. Kumbuka kwamba umri, afya, hali, na uwezo wa watu hutofautiana. Mtume Paulo aliongozwa na roho takatifu kusema hivi: “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.”—Gal. 6:4.

WASAIDIE WATU WA FAMILIA YAKO NA WAABUDU WENZAKO

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba mtu yeyote anayeitunza familia yake anashirikiana na Mungu?

3 Yehova anatarajia watumishi wake watunze familia zao. Kwa mfano, huenda ukalazimika kufanya kazi ili upate pesa za kuwatunza wapendwa wako. Akina mama wengi hukaa nyumbani ili wawatunze watoto wao wadogo. Na baadhi ya watoto ambao tayari ni watu wazima huwatunza wazazi wao ambao ni wagonjwa. Hayo ni mambo ya lazima. Neno la Mungu linasema hivi: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji watu wake mwenyewe, hasa watu wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Tim. 5:8) Ikiwa una majukumu kama hayo, huenda usiwe na wakati wa kutosha wa kushiriki katika utendaji wa kitheokrasi kama ambavyo ungependa. Lakini usife moyo! Yehova hufurahi unapoiandalia familia yako.—1 Kor. 10:31.

4. Wazazi wanawezaje kutanguliza masilahi ya kiroho badala ya masilahi yao wenyewe, nao watapata matokeo gani?

4 Wazazi Wakristo hufanya kazi pamoja na Yehova wanapowawekea watoto wao malengo ya kiroho. Wazazi wengi ambao wamefanya hivyo baadaye wameona wana na binti zao wakiingia katika utumishi wa wakati wote na kukubali migawo mbali na nyumbani. Baadhi yao ni wamishonari; wengine ni mapainia wanaotumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri; na wengine ni Wanabetheli. Huenda isiwe rahisi kwa familia kuwa pamoja mara nyingi kadiri wapendavyo kwa sababu ya umbali. Ingawa hivyo, wazazi wanaojidhabihu kwa njia hiyo huwatia moyo watoto wao waendelee kushikamana na migawo yao. Kwa nini? Wanapata shangwe kubwa na furaha kwa kuwa wanajua kwamba watoto wao wanatanguliza Ufalme. (3 Yoh. 4) Wengi wa wazazi hao huhisi kama Hana, ambaye alisema kwamba ‘amemkabidhi’ Samweli mwanawe kwa Yehova. Wazazi hao huliona kuwa pendeleo kubwa kufanya kazi pamoja na Yehova kama Hana. Na hawangependa kamwe hali ibadilike.—1 Sam. 1:28.

5. Unaweza kufanya nini ili uwasaidie washiriki wa kutaniko lako? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

5 Ikiwa huna majukumu makubwa sana ya familia, je, unaweza kuwasaidia waabudu wenzako wanaowatunza wagonjwa, waabudu wenzako ambao ni wagonjwa, wenye umri mkubwa, au wanaohitaji msaada? Kwa nini usiangalie ni nani kutanikoni anayehitaji msaada? Labda unaweza kumsaidia dada Mkristo ambaye anawatunza wazazi wake waliozeeka ili apate nafasi ya kushughulikia mambo mengine. Au unaweza kujitolea kuwasaidia wale wanaohitaji usafiri ili wafike mikutanoni, kwenda kununua vitu, kwenda kufanya shughuli nyingine muhimu, au kumtembelea mgonjwa hospitalini. Ukifanya hivyo, huenda Yehova akakutumia kujibu sala ya mtu huyo na hivyo kufanya kazi pamoja na Yehova.—Soma 1 Wakorintho 10:24.

UWE MKARIBISHAJI WAGENI

6. Kuwaonyesha wengine ukaribishaji wageni kunahusisha nini?

6 Wafanyakazi wenzi wa Mungu wanajulikana kwa sifa ya ukaribishaji wageni. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, maneno ‘ukaribishaji wageni’ yanamaanisha “kuwaonyesha wageni fadhili.” (Ebr. 13:2; maelezo ya chini) Neno la Mungu lina masimulizi yanayotufundisha jinsi tunavyoweza kuonyesha upendo kama huo. (Mwa. 18:1-5) Tunaweza na tunapaswa kutumia fursa yoyote iliyopo kuwasaidia wengine kwa ukawaida, iwe ni “ndugu zetu katika imani” au la.—Gal. 6:10.

7. Kwa nini ungependa kujiwekea lengo la kuwakaribisha watumishi wa wakati wote wanaozuru?

7 Je, unaweza kufanya kazi pamoja na Mungu kwa kuwaonyesha ukaribishaji wageni watumishi wa wakati wote wanaozuru? (Soma 3 Yohana 5, 8.) Mara nyingi pindi kama hizo huandaa fursa za ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12) Fikiria kisa cha Olaf. Anakumbuka kwamba miaka mingi iliyopita mwangalizi wa mzunguko aliyekuwa mseja alizuru katika kutaniko lao na hakuna yeyote ambaye alikuwa na uwezo wa kumkaribisha ili alale nyumbani kwake. Olaf ambaye alikuwa kijana wakati huo aliwaomba wazazi wake ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova wamruhusu amkaribishe mwangalizi wa mzunguko ili alale nyumbani kwao. Wazazi wake walikubali lakini wakamwambia Olaf kwamba angelala kwenye kochi. Hajutii kamwe jambo hilo. Olaf anasema hivi: “Hilo lilikuwa juma zuri kwelikweli! Mimi pamoja na mwangalizi huyo tulikuwa tukiamka mapema kila siku na kuzungumzia mambo mengi yenye kufurahisha huku tukinywa kiamsha kinywa. Kitia-moyo nilichopokea kilinichochea niwe na hamu ya kuingia katika utumishi wa wakati wote.” Kufikia sasa, Olaf amekuwa akitumikia akiwa mmishonari katika nchi mbalimbali kwa miaka 40.

8. Tuna sababu zipi za kuwaonyesha wengine fadhili hata ikiwa mwanzoni huenda wasithamini? Toa mfano.

8 Unaweza kuwaonyesha wageni upendo katika njia nyingi hata ikiwa mwanzoni hawathamini. Fikiria kisa hiki. Dada mmoja kutoka Hispania alikuwa akijifunza Biblia na mwanamke aliyeitwa Yesica kutoka Ekuado. Siku moja walipokuwa wakijifunza Biblia mwanafunzi huyo alianza kulia. Dada huyo alimuuliza kwa nini alikuwa akilia. Yesica alimwambia kwamba kabla ya kuhamia Hispania alikuwa maskini sana hivi kwamba siku moja aliishiwa na chakula. Kitu pekee ambacho angeweza kumpa binti yake ni maji. Yesica alijitahidi kumbembeleza mtoto wake alale huku akisali ili apate msaada. Muda mfupi baadaye, Mashahidi wawili walimtembelea, lakini Yesica aliwatendea kwa ukali, naye akararua gazeti alilopewa na dada hao. Aliwauliza, “Hiki ndicho chakula mnachotaka nimpe binti yangu?” Dada hao walijitahidi kumtuliza lakini hawakufanikiwa. Baadaye, waliacha kikapu kilichokuwa na chakula mlangoni pake. Yesica aliguswa sana na tendo lao la fadhili na ndiyo sababu alikuwa akilia alipokumbuka kwamba hakumsikiliza Mungu alipojibu sala yake. Ingawa hivyo, sasa Yesica alikuwa ameazimia kumtumikia Yehova. Ukarimu wao ulileta matokeo mazuri sana!—Mhu. 11:1, 6.

JITOLEE KATIKA MIRADI YA KITHEOKRASI

9, 10. (a) Taja baadhi ya pindi katika nyakati za Biblia ambapo watu wa Mungu waliombwa wajitolee kwa sababu ya uhitaji uliokuwa umetokea. (b) Taja baadhi ya mambo ambayo hushughulikiwa na wanaume walio tayari kutumikia kutanikoni.

9 Pindi kadhaa katika historia ya kale ya taifa la Israeli, wajitoleaji walihitajika. (Kut. 36:2; 1 Nya. 29:5; Neh. 11:2) Leo, wewe pia una fursa nyingi za kutumia wakati wako, mali zako, na ujuzi wako kuwasaidia ndugu na dada zako. Ukifanya hivyo, utapata shangwe nyingi na baraka tele.

10 Neno la Mungu huwatia moyo wanaume kutanikoni wafanye kazi pamoja na Yehova kwa kujitahidi kufikia mapendeleo ya utumishi na ya uangalizi. (1 Tim. 3:1, 8, 9; 1 Pet. 5:2, 3) Wale wanaofanya hivyo wanatamani kuwasaidia wengine kiroho na katika mambo mengine pia. (Mdo. 6:1-4) Je, wazee wamekuuliza ikiwa uko tayari kufanya kazi ya ukaribishaji au kushughulikia machapisho, maeneo, udumishaji, au kazi nyingine kutanikoni? Wale wanaoshughulikia kazi hizo watakuambia kwamba ni jambo lenye kufurahisha sana kuwasaidia wengine.

Kujitolea katika miradi ya kitheokrasi hutupatia fursa nyingi za kupata marafiki wapya (Tazama fungu la 11)

11. Dada mmoja amenufaikaje na marafiki aliopata akiwa kwenye miradi ya kitheokrasi?

11 Kwa kawaida, wale ambao hujitolea kushughulikia miradi ya kitheokrasi hupata marafiki wapya. Fikiria mfano wa Margie, dada ambaye amejitolea katika miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme kwa miaka 18. Kwa miaka mingi, ameanzisha urafiki pamoja na dada kadhaa ili awazoeze. Amejionea kwamba kufanya hivyo ni njia bora sana ya kutiana moyo kiroho. (Rom. 1:12) Marafiki wapya aliopata alipokuwa akijitolea kwenye miradi ya ujenzi wamekuwa wakimtia moyo anapokabili hali ngumu. Je, umewahi kujitolea kufanya kazi katika miradi ya ujenzi? Je, unaweza kujitolea, iwe una ustadi fulani au la?

12. Unaweza kutoa msaada gani misiba inapotokea?

12 Misiba inapotokea, watu wa Mungu wana fursa ya kufanya kazi pamoja na Mungu kwa kuwapa ndugu zao msaada wanaohitaji. Kwa mfano, wao huwapa msaada wa kifedha wale walioathiriwa na misiba hiyo. (Yoh. 13:34, 35; Mdo. 11:27-30) Njia nyingine ya kutoa msaada unaohitajika ni kusafisha au kusaidia kukarabati majengo yaliyoharibika. Gabriela, dada kutoka Poland ambaye nyumba yake iliharibiwa kabisa na mafuriko, alifurahi sana akina ndugu kutoka makutaniko jirani walipokuja kumsaidia. Anaeleza hivi: “Sitaki kuzungumza kuhusu vitu nilivyopoteza—hivyo ni vitu vya kimwili tu. Badala yake, ninataka kuwaambia jinsi nilivyonufaika. Msaada niliopokea uliongeza uhakika wangu kwamba kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo ni pendeleo la pekee na chanzo cha shangwe na furaha.” Wengi ambao wamepokea msaada fulani baada ya msiba wanasema kwamba wameimarika zaidi. Na wale wanaofanya kazi pamoja na Yehova kutoa misaada kama hiyo hupata shangwe nyingi.—Soma Matendo 20:35; 2 Wakorintho 9:6, 7.

13. Kujitolea kunaweza kuimarishaje uhusiano wetu pamoja na Yehova? Toa mfano.

13 Stephanie na wahubiri wengine walipata shangwe ya kufanya kazi pamoja na Mungu kwa kuwasaidia Mashahidi waliohamia Marekani wakiwa wakimbizi kwa sababu ya vita. Walitafuta nyumba na fanicha kwa ajili ya familia hizo. Stephanie anasema hivi: “Shangwe na uthamini walioonyesha walipokuwa wakifurahia upendo wa undugu wetu wa ulimwenguni pote ulituchochea sana. Ndugu na dada hao wanafikiri kwamba sisi tumewasaidia, lakini kihalisi, wao ndio waliotusaidia zaidi. Mambo tuliyoshuhudia kama vile upendo, umoja, imani, na kumtegemea Yehova yamefanya upendo wetu kwa Yehova uongezeke, na hilo limetufanya tuthamini hata zaidi mambo yote tunayopokea kutoka katika tengenezo la Yehova.”

PANUA UTUMISHI WAKO

14, 15. (a) Nabii Isaya alionyesha roho ya aina gani? (b) Leo, wahubiri wa Ufalme huigaje mtazamo wake?

14 Je, ungependa kufanya kazi pamoja na Yehova kwa ukamili zaidi? Je, unaweza kuwa tayari kuhamia eneo lingine ili umtumikie mahali ambako kuna uhitaji mkubwa wa wahubiri katika tengenezo lake? Bila shaka, watumishi wa Mungu hawahitaji kusafiri mbali na nyumbani ili waonyeshe ukarimu. Lakini hali za ndugu na dada wengine zinawaruhusu kutumikia kwenye maeneo ya mbali. Mtazamo wao ni kama ule wa nabii Isaya. Yehova alipouliza, “Nimtume nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” Isaya alijibu: “Mimi hapa! Nitume mimi!” (Isa. 6:8) Je, una tamaa kama hiyo na je, hali yako inakuruhusu kujibu kama Isaya ili utosheleze mahitaji ya tengenezo? Kuna uhitaji gani?

15 Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Je, unaweza kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa, labda ukiwa painia? Au je, unaweza kumsaidia mwingine afanye hivyo? Ndugu na dada wengi wamehisi kwamba njia bora sana ya kumwonyesha Mungu na jirani zao upendo ni kutumikia wakiwa mapainia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kupanua au kuongeza utumishi wako? Utapata shangwe nyingi kwa kufanya hivyo.

16, 17. Taja fursa zilizopo ikiwa unatamani kufanya mengi zaidi katika utumishi wako kwa Yehova.

16 Je, uko tayari kutumikia Betheli au katika miradi ya ujenzi, iwe utajitolea kwa kipindi fulani, au siku moja au zaidi kila juma? Sikuzote kumekuwa na uhitaji mkubwa wa ndugu na dada walio tayari kumtumikia Yehova mahali popote penye uhitaji na kufanya kazi yoyote wanayopewa. Hivyo, wanaweza kuombwa wafanye kazi kwenye eneo lenye uhitaji wa pekee, ingawa huenda wana ustadi na uzoefu katika nyanja tofauti. Licha ya hilo, Yehova anawathamini sana ndugu na dada wanaoonyesha roho hiyo ya kujidhabihu kwa kuwa tayari kutumikia mahali popote palipo na uhitaji.—Zab. 110:3.

17 Je, unatamani kupokea mazoezi zaidi yatakayokusaidia uwe na vifaa kamili kwa ajili ya utumishi wako mtakatifu? Ikiwa ndivyo, unaweza kujaza ombi la kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Shule hiyo huwapa mazoezi wanaume na wanawake wa kiroho walio katika utumishi wa wakati wote ili wapanue masilahi ya Ufalme. Wale wanaoomba kuhudhuria shule hiyo wanahitaji kuwa tayari kukubali mgawo wowote baada ya kuhitimu. Je, uko tayari kujitahidi kutumia vizuri fursa hiyo ili ufikie mapendeleo mengi zaidi ya utumishi?—1 Kor. 9:23.

18. Utapata nini kwa kufanya kazi na Yehova kila siku?

18 Kila siku tukiwa watu wa Yehova tunachochewa kuonyesha ukarimu na kuhangaikia mahitaji ya wengine, jambo linaloonyesha kwamba sisi ni watu wema, wenye fadhili, na upendo. Tunapofanya hivyo, tunapata shangwe, amani, na furaha. (Gal. 5:22, 23) Hata iwe una hali gani maishani, unaweza kuwa na shangwe kwa kumwiga Yehova katika kuonyesha ukarimu na kwa kuwa miongoni mwa wafanyakazi wenye thamani wanaofanya kazi pamoja naye!—Met. 3:9, 10.