Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 31

“Hatufi Moyo”!

“Hatufi Moyo”!

“Kwa hiyo, hatufi moyo.”​—2 KOR. 4:16.

WIMBO 128 Kuvumilia Mpaka Mwisho

MUHTASARI *

1. Wakristo wanapaswa kufanya nini ili wakamilishe mbio za uzima?

WAKRISTO wako katika mbio za uzima. Iwe tumeanza kukimbia hivi karibuni au tumekuwa tukikimbia kwa miaka mingi, tunahitaji kuendelea kukimbia hadi tuvuke mstari wa mwisho. Ushauri ambao mtume Paulo aliwapa Wakristo huko Filipi unaweza kutuchochea tumalize mbio hizo. Baadhi ya washiriki wa kutaniko hilo la karne ya kwanza walikuwa wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi Paulo alipowaandikia barua hiyo. Walikuwa wakikimbia vema, lakini Paulo aliwakumbusha kuhusu umuhimu wa kuendelea kukimbia kwa uvumilivu. Alitaka waendelee kufuata mfano wake kwa ‘kuendelea kujitahidi kuelekea ule mradi.’—Flp. 3:14.

2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ushauri wa Paulo kwa Wafilipi ulitolewa kwa wakati unaofaa?

2 Ushauri wa Paulo kwa Wafilipi ulitolewa kwa wakati unaofaa. Kutaniko la Filipi lilikuwa limekabili upinzani tangu lilipoanzishwa. Mambo yalianza Paulo na Sila walipokubali mwaliko wa ‘kuvuka kuingia Makedonia,’ nao wakafika huko Filipi karibu mwaka wa 50 W.K. (Mdo. 16:9) Huko walimkuta mwanamke aliyeitwa Lidia, ambaye “alikuwa akisikiliza, na Yehova akaufungua moyo wake wazi” ili asikilize habari njema. (Mdo. 16:14) Baada ya muda mfupi, yeye na watu wa familia yake wakabatizwa. Hata hivyo, Ibilisi hakuwa amelala. Wanaume wa jiji hilo waliwakokota Paulo na Sila na kuwapeleka mbele za mahakimu wa raia na kuwashtaki kwa uwongo kwamba walikuwa wakisababisha usumbufu. Hivyo, Paulo na Sila wakapigwa fimbo, wakafungwa gerezani, na baadaye wakalazimishwa kuondoka katika jiji hilo. (Mdo. 16:16-40) Je, walikufa moyo? La hasha! Na vipi kuhusu ndugu na dada katika kutaniko hilo jipya? Inafurahisha kwamba wao pia walivumilia! Bila shaka, walitiwa moyo sana na mfano mzuri ambao Paulo na Sila walikuwa wamewawekea.

3. Paulo alitambua nini, na tutazungumzia maswali gani?

3 Paulo aliazimia kutokufa moyo. (2 Kor. 4:16) Hata hivyo, alitambua kwamba ili akimbie mbio hizo hadi mwisho, angehitaji kukazia fikira mradi wake. Mfano wa Paulo unatufundisha nini? Tuna mifano gani ya imani katika siku zetu inayoonyesha kwamba tunaweza kuvumilia licha ya matatizo? Na tumaini letu la wakati ujao linaweza kuimarishaje azimio letu la kutokufa moyo kamwe?

JINSI MFANO WA PAULO UNAVYOTUNUFAISHA

4. Ni jambo gani lililomsaidia Paulo aendelee kuwa mwenye bidii licha ya hali zake?

4 Fikiria jinsi Paulo alivyokuwa akijitoa kabisa alipowaandikia Wafilipi. Alikuwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma. Alikuwa na uhuru mdogo sana wa kuhubiri. Ingawa hivyo, aliwatolea ushahidi kwa bidii wageni waliomtembelea na kuyaandikia barua makutaniko yaliyokuwa mbali. Leo pia, Wakristo wengi ambao hawawezi kutoka nyumbani hutumia vizuri kila fursa wanayopata kuwahubiria habari njema wale wanaokuja kuwatembelea. Pia, wanawaandikia barua zenye kutia moyo watu ambao si rahisi kukutana nao.

5. Kulingana na andiko la Wafilipi 3:12-14, ni nini kilichomsaidia Paulo kukazia fikira mradi wake?

5 Paulo hakujiruhusu akengeushwe na mambo mazuri aliyotimiza zamani au makosa aliyofanya. Isitoshe, alisema kwamba “kuyasahau mambo ya nyuma” ni hatua muhimu ili “kujinyoosha kuelekea mambo yaliyo mbele,” yaani, kukamilisha mbio kwa mafanikio. (Soma Wafilipi 3:12-14.) Paulo angeweza kukengeushwa na mambo gani? Kwanza, mambo aliyotimiza katika dini ya Kiyahudi yalikuwa makubwa. Hata hivyo, aliyaona mambo hayo kuwa “takataka nyingi.” (Flp. 3:3-8) Pili, hakuruhusu hatia ya kuwatesa Wakristo imfanye aache kumtumikia Yehova. Na tatu, hakufikiri kwamba mambo ambayo tayari alikuwa ametimiza yalitosha. Paulo alitimiza mengi katika huduma yake licha ya kufungwa gerezani, kupigwa fimbo, kupigwa mawe, kuvunjikiwa na meli, na vilevile kukosa chakula na mavazi. (2 Kor. 11:23-27) Hata hivyo, licha ya yote aliyotimiza na mateso aliyopitia, Paulo alijua kwamba ni lazima aendelee kujitahidi kumtumikia Yehova. Sisi pia tunapaswa kufanya vivyo hivyo.

6. Huenda tukahitaji kusahau ‘mambo gani ya nyuma’?

6 Tunaweza kumwigaje Paulo inapohusu “kuyasahau mambo ya nyuma”? Huenda baadhi yetu tukahitaji kushinda hisia za hatia zinazotokana na dhambi tulizofanya zamani. Ikiwa ndivyo, katika funzo lako la kibinafsi kwa nini usianze mradi wa kujifunza unaokazia dhabihu ya fidia ya Kristo? Ikiwa tutajifunza, kutafakari, na kusali kuhusu fundisho hilo lenye kutia moyo, huenda tukafaulu kupunguza kwa kiwango kikubwa hisia za hatia zisizo za lazima. Huenda hata tukaacha kujihukumu kwa sababu ya dhambi ambazo Yehova tayari ametusamehe. Fikiria somo lingine tunaloweza kujifunza kutoka kwa Paulo. Huenda wengine waliacha kazi zenye mshahara mnono ili wafuatie masilahi ya Ufalme. Ikiwa ndivyo, je, tunaweza kusahau mambo ya nyuma kwa kuacha kutamani fursa tulizotupilia mbali za kupata vitu vya kimwili? (Hes. 11:4-6; Mhu. 7:10) “Mambo ya nyuma” yanaweza kutia ndani hata mambo tuliyotimiza au hali ngumu tulizovumilia wakati uliopita. Bila shaka, kutazama nyuma na kuona jinsi Yehova alivyotubariki na kututegemeza kwa miaka mingi kunaweza kutusaidia kumkaribia zaidi Baba yetu. Hata hivyo, tusingependa kamwe kuridhika tukifikiri kwamba tumemaliza kazi yetu.—1 Kor. 15:58.

Katika mbio za uzima, tunapaswa kukazia fikira mradi wetu na kuepuka vitu vinavyoweza kutukengeusha (Tazama fungu la 7)

7. Kulingana na 1 Wakorintho 9:24-27, ili tushinde mbio za uzima, tunapaswa kufanya nini? Toa mfano.

7 Paulo aliyaelewa vizuri maneno haya ya Yesu: “Jitahidini sana.” (Luka 13:23, 24) Paulo alijua kwamba kama Kristo, yeye pia alipaswa kuendelea kujitahidi sana hadi mwisho. Hivyo, alilinganisha maisha ya Mkristo na mbio. (Soma 1 Wakorintho 9:24-27.) Mkimbiaji katika mbio hukazia fikira mstari wa mwisho na huepuka vitu vinavyoweza kumkengeusha. Kwa mfano, fikiria wale wanaokimbia kwenye shindano la mbio linalofanywa kwenye jiji lenye maduka mengi na mambo mengine yanayoweza kuwakengeusha. Je, unaweza kumwazia mkimbiaji akisimama na kuanza kutazama bidhaa zilizo madukani? Hawezi kufanya hivyo ikiwa anataka kushinda! Katika mbio za uzima, ni lazima sisi pia tuepuke vitu vinavyoweza kutukengeusha. Ikiwa tutakazia fikira lengo letu, na kujitahidi sana kama Paulo, tutashinda tuzo!

JINSI YA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO ZINAZOJARIBU IMANI YETU

8. Tutachunguza changamoto gani tatu?

8 Acheni tuchunguze changamoto tatu zinazoweza kutufanya tupunguze kasi yetu. Changamoto hizo ni matarajio yasiyotimia, kudhoofika kwa sababu ya umri kusonga, na majaribu ya muda mrefu. Tunaweza kufaidika kwa kujifunza kuhusu jinsi wengine walivyokabiliana na hali hizo.—Flp. 3:17.

9. Tunaweza kuathirikaje matarajio yetu yasipotimia?

9 Matarajio yasiyotimia. Kiasili tunatamani kuona utimizo wa mambo mazuri ambayo Yehova ameahidi. Isitoshe, nabii Habakuki alipomweleza Yehova jinsi alivyotamani kuona Yehova akikomesha mambo maovu yaliyokuwa yakitendeka nchini Yuda, Yehova alimwambia ‘aendelee kutarajia.’ (Hab. 2:3) Hata hivyo, matarajio yetu yanapoonekana ni kana kwamba yanakawia kutimia, huenda bidii yetu ikapungua. Hata tunaweza kuvunjika moyo. (Met. 13:12) Hali ilikuwa hivyo mwanzoni mwa karne ya 20. Wakati huo, Wakristo wengi watiwa-mafuta walitarajia kupokea tuzo yao ya kwenda mbinguni mwaka wa 1914. Jambo hilo lilipokosa kutimia, ndugu hao waaminifu walikabilianaje na hali hiyo?

Royal na Pearl Spatz hawakuona tumaini lao likitimizwa mwaka wa 1914, lakini waliendelea kuwa waaminifu kwa makumi ya miaka (Tazama fungu la 10)

10. Wenzi fulani wa ndoa walitendaje matarajio yao yalipokosa kutimia?

10 Fikiria mfano wa Wakristo wawili washikamanifu waliokabili changamoto kama hiyo. Ndugu Royal Spatz alibatizwa mwaka wa 1908 akiwa na umri wa miaka 20. Alikuwa na uhakika kabisa kwamba baada ya muda mfupi angepokea tuzo yake. Hata alipomchumbia mke wake mtarajiwa, Pearl, mwaka wa 1911, alimwambia: “Unajua vizuri kitakachotokea mwaka wa 1914. Ikiwa tunafunga ndoa, tufanye hivyo haraka!” Je, wenzi hao Wakristo walivunjika moyo na kujitoa katika mbio za uzima walipokosa kupokea tuzo yao ya kwenda mbinguni mwaka wa 1914? Hapana, kwa sababu lengo lao kuu lilikuwa kufanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu, na si tu kupokea tuzo. Walikuwa wameazimia kuendelea kukimbia mbio kwa uvumilivu. Na kwa kweli, Royal na Pearl waliendelea kuwa wahubiri wenye bidii na waaminifu hadi walipomaliza mwendo wao wa kidunia miaka mingi baadaye. Bila shaka, unatamani kuona Yehova akilitetea jina lake na enzi yake kuu na kutimiza ahadi zake zote. Uwe na hakika kwamba mambo hayo yote yatatimia kwa wakati hususa uliowekwa na Yehova. Hadi wakati huo, acheni tuendelee kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wetu kwa Mungu, na tusiruhusu kamwe matarajio yasiyotimia yatuvunje moyo au kutufanya tupunguze bidii yetu.

Hata alipozeeka, Arthur Secord alikuwa na tamaa ya kuendelea kusonga mbele. (Tazama fungu la 11)

11-12. Kwa nini tunaweza kuendelea kusonga mbele kiroho hata ikiwa tumedhoofika kwa sababu ya umri kusonga? Toa mfano.

11 Kudhoofika kwa sababu ya umri kusonga. Tofauti na wakimbiaji katika mbio halisi, mtu hahitaji kuwa na nguvu nyingi kimwili ili aendelee kuwa imara kiroho. Isitoshe, ndugu na dada wengi ambao wamedhoofika kwa sababu ya umri bado wamedumisha azimio lao thabiti la kuendelea kusonga mbele kiroho. (2 Kor. 4:16) Kwa mfano, akiwa na umri wa miaka 88 tayari Ndugu Arthur Secord * alikuwa ametumikia Betheli kwa miaka 55. Afya yake ilikuwa imedhoofika. Siku moja muuguzi alienda kumhudumia kitandani mwake. Muuguzi huyo alimtazama na kumwambia kwa upendo: “Ndugu Secord, mwili huu umetimiza mambo mengi sana katika utumishi wa Yehova.” Hata hivyo, Arthur, hakukazia fikira mambo aliyotimiza zamani. Alimtazama muuguzi, akatabasamu na kusema: “Ndiyo, ni kweli. Lakini jambo muhimu si yale tuliyotimiza. Jambo muhimu ni yale tunayofanya sasa na kuendelea.”

12 Huenda umemtumikia Yehova kwa miaka mingi na sasa afya yako inakuzuia kutimiza mengi kama ulivyokuwa ukifanya hapo awali. Ikiwa ndivyo, usivunjike moyo. Uwe na hakika kwamba Yehova anakumbuka utumishi wako wa uaminifu uliotimiza wakati uliopita. (Ebr. 6:10) Kwa sasa, kumbuka kwamba upendo wetu kwa Yehova haupimwi kwa wingi wa mambo tunayotimiza katika utumishi wake. Kinyume chake, tunafunua kina cha upendo wetu kwake kwa kuwa na mtazamo mzuri na kujitahidi kufanya yote tuwezayo kulingana na uwezo wetu. (Kol. 3:23) Yehova anaelewa udhaifu wetu na hatarajii tufanye mambo yanayopita uwezo wetu.—Marko 12:43, 44.

Anatoly na Lidiya Melnik walivumilia kwa uaminifu licha ya matatizo mengi (Tazama fungu la 13)

13. Mfano wa Anatoly na Lidiya unatutiaje moyo tuendelee kusonga mbele licha ya matatizo ya muda mrefu?

13 Matatizo ya muda mrefu. Baadhi ya watumishi wa Yehova wamevumilia hali ngumu na mateso kwa miaka mingi. Kwa mfano, Anatoly Melnik * alikuwa na umri wa miaka 12 tu baba yake alipokamatwa na kufungwa gerezani, na kisha kupelekwa uhamishoni Siberia, umbali wa zaidi ya kilomita 7,000 kutoka Moldova, ambako familia yao ilikuwa ikiishi. Mwaka mmoja baadaye, Anatoly, mama yake, pamoja na babu na bibi (nyanya) yake walipelekwa pia uhamishoni Siberia. Baada ya muda, walifanikiwa kuhudhuria mikutano katika kijiji kingine, lakini walihitaji kutembea kilomita 30 kwenye theluji, wakivumilia baridi kali sana. Baadaye, Ndugu Melnik alifungwa gerezani kwa miaka mitatu, akiwa mbali na Lidiya, mke wake na binti yao mwenye umri wa mwaka mmoja. Licha ya kuvumilia hali ngumu kwa miaka mingi, Anatoly na familia yake waliendelea kusonga mbele bila kutetereka. Sasa Anatoly ana umri wa miaka 82 na ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Asia ya Kati. Kama Anatoly na Lidiya, acheni tufanye yote tuwezayo katika utumishi wa Yehova, naam, tuendelee kuvumilia kama ambavyo tumekuwa tukifanya wakati uliopita.—Gal. 6:9.

TUNACHOCHEWA NA TUMAINI LETU LA WAKATI UJAO

14. Paulo alitambua alihitaji kufanya nini ili afikie mradi wake?

14 Paulo alikuwa na uhakika kwamba angemaliza mbio na kufikia mradi wake. Akiwa Mkristo mtiwa-mafuta, alitazamia kwa hamu kupokea “tuzo ya mwito wa Mungu wa kwenda juu.” Hata hivyo, alitambua kwamba ili afikie mradi huo alihitaji ‘kuendelea kujitahidi.’ (Flp. 3:14) Paulo alitumia mfano fulani wenye kuvutia ili kuwasaidia Wafilipi waendelee kukazia fikira mradi wao.

15. Paulo alitumiaje mfano kuhusu uraia kuwatia moyo Wakristo Wafilipi waendelee “kujitahidi” kufikia mradi wao?

15 Paulo aliwakumbusha Wafilipi kuhusu uraia wao wa mbinguni. (Flp. 3:20) Kwa nini walihitaji kukumbuka jambo hilo? Katika siku hizo, uraia wa Roma ulionwa kuwa wenye thamani sana. * Hata hivyo, Wakristo watiwa-mafuta walikuwa na uraia bora zaidi, uraia ambao ungewaletea faida nyingi zaidi. Uraia wa Roma ulikuwa na thamani ndogo sana kwa kulinganisha na uraia wa mbinguni! Hiyo ndiyo sababu Paulo aliwatia moyo Wafilipi “[wajiendeshe] kama raia kwa njia inayostahili habari njema kumhusu Kristo.” (Flp. 1:27, maelezo ya chini) Wakristo watiwa-mafuta leo huweka mfano mzuri wanapoendelea kujitahidi kuufikia mradi wao wa uzima wa milele mbinguni.

16. Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, tunapaswa kuendelea kufanya nini kama inavyotajwa kwenye Wafilipi 4:6, 7?

16 Iwe tuna tumaini la kupata uzima wa milele mbinguni au katika paradiso duniani, tunapaswa kuendelea kujitahidi kuufikia mradi wetu. Hata iwe tunakabili hali gani, hatupaswi kutazama vitu vilivyo nyuma; wala hatupaswi kuruhusu chochote kituzuie kufanya maendeleo. (Flp. 3:16) Huenda ukahisi kwamba matarajio yako yanakawia kutimia, au umedhoofika kwa sababu ya umri kusonga. Huenda umevumilia hali ngumu na mateso kwa miaka mingi. Hata hali ziweje, ‘usihangaike kuhusiana na jambo lolote.’ Badala yake, mjulishe Mungu maombi yako na dua zako, naye atakupa amani nyingi kuliko unavyoweza kuwazia.—Soma Wafilipi 4:6, 7.

17. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

17 Kama mkimbiaji anavyojikakamua kwa bidii anapokaribia mstari wa mwisho, acheni tuendelee kukazia fikira kikamili mradi wetu wa kukamilisha mbio za uzima. Kadiri nguvu na hali zetu zinavyoruhusu, acheni tujitahidi kabisa kusonga mbele kwa bidii kuelekea mambo mazuri ajabu yaliyo mbele yetu. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kujitahidi kukimbia kwenye njia iliyo sahihi na kwa mwendo unaofaa? Makala inayofuata itatusaidia kujua mambo tunayopaswa kutanguliza na jinsi tunavyoweza ‘kujihakikishia mambo yaliyo muhimu zaidi.’—Flp. 1:9, 10.

WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara

^ fu. 5 Hata iwe tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu kadiri gani, tukiwa Wakristo tungependa kuendelea kukua kiroho na kufanya maendeleo. Mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake wasife moyo kamwe! Barua yake kwa Wafilipi ina kitia-moyo kinachotuchochea tuvumilie tunapoendelea kukimbia katika mbio za uzima. Makala hii itatuonyesha jinsi tunavyoweza kutumia maishani maneno hayo ya Paulo yaliyoongozwa na roho.

^ fu. 11 Tazama simulizi la maisha la Ndugu Secord, “My Part in Advancing Right Worship,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi, Juni 15, 1965, la Kiingereza.

^ fu. 13 Tazama simulizi la maisha la Ndugu Melnik, “Nilifundishwa Kumpenda Mungu Tangu Utotoni,” katika gazeti Amkeni!, la Oktoba 22, 2004.

^ fu. 15 Kwa kuwa jiji la Filipi lilikuwa koloni la serikali ya Roma, wakaaji wa jiji hilo walipata haki fulani ambazo raia wa Roma walikuwa nazo. Hivyo, akina ndugu huko Filipi wangeweza kuelewa vizuri mfano wa Paulo.