Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 32

Upendo Wenu na Uwe Mwingi

Upendo Wenu na Uwe Mwingi

“Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi zaidi na zaidi.”—FLP. 1:9.

WIMBO 106 Kusitawisha Sifa ya Upendo

MUHTASARI *

1. Ni nani waliosaidia kuanzisha kutaniko la Filipi?

MTUME Paulo, Sila, Luka, na Timotheo walipowasili katika jiji la Filipi lililokuwa koloni la serikali ya Roma, walikuta watu wengi waliopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Ndugu hao wanne wenye bidii walisaidia kuanzisha kutaniko, na wanafunzi wote wakaanza kukutanika pamoja, huenda katika nyumba ya Lidia, mwamini aliyekuwa mkarimu.—Mdo. 16:40.

2. Muda si muda kutaniko hilo lilikabili hali gani ngumu?

2 Muda si muda, kutaniko hilo changa lilikabili hali fulani ngumu. Shetani aliwachochea maadui walioichukia kweli waipinge vikali kazi ya kuhubiri ya Wakristo hao waaminifu. Paulo na Sila walikamatwa, wakapigwa viboko, na kufungwa gerezani. Baada ya kuachiliwa huru kutoka gerezani, waliwatembelea wanafunzi hao wapya na kuwatia moyo. Kisha Paulo, Sila, na Timotheo wakaondoka katika jiji hilo lakini inaelekea kwamba Luka alibaki. Kutaniko hilo jipya lingeendeleaje? Kwa msaada wa roho ya Yehova, waamini hao wapya walisonga mbele kwa bidii katika utumishi wao kwa Yehova. (Flp. 2:12) Paulo alikuwa na kila sababu ya kujivunia ndugu hao!

3. Kama Wafilipi 1:9-11 inavyotaja, Paulo alisali kuhusu nini?

3 Miaka kumi hivi baadaye, Paulo aliliandikia barua kutaniko la Filipi. Unaposoma barua hiyo, ni rahisi kujionea jinsi Paulo alivyowapenda ndugu zake. Aliandika hivi: “[Ninatamani] kuwaona ninyi nyote kwa upendo mwororo kama alio nao Kristo Yesu.” (Flp. 1:8) Aliwaambia kwamba alikuwa akisali kwa ajili yao. Alimwomba Yehova awasaidie wawe na upendo mwingi, wahakikishe mambo yaliyo muhimu zaidi, wawe bila kasoro, waepuke kuwakwaza wengine, na waendelee kuzaa tunda la uadilifu. Bila shaka, utakubali kwamba sisi pia tunaweza kunufaika na maneno hayo ya Paulo ya kutoka moyoni. Basi acheni tusome maneno hayo ambayo Paulo aliwaandikia Wafilipi. (Soma Wafilipi 1:9-11.) Kisha tutachunguza mambo aliyotaja na kuzungumzia jinsi tunavyoweza kuyatumia.

IWENI NA UPENDO MWINGI

4. (a) Kulingana na 1 Yohana 4:9, 10, Yehova ameonyeshaje upendo wake kwetu? (b) Tunapaswa kumpenda Mungu kadiri gani?

4 Yehova alituonyesha upendo mkubwa alipomtuma Mwana wake duniani ili afe kwa ajili ya dhambi zetu. (Soma 1 Yohana 4:9, 10.) Upendo wa Mungu usio na ubinafsi unatuchochea tumpende. (Rom. 5:8) Tunapaswa kumpenda Mungu kadiri gani? Yesu alijibu swali hilo kwa kumwambia hivi Farisayo fulani: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mt. 22:36, 37) Hatungependa kumpenda Mungu kwa moyo nusu-nusu. Badala yake, tungependa upendo wetu kwa Mungu uzidi kuimarika siku baada ya siku. Paulo aliwaambia Wafilipi kwamba ‘upendo wao ulipaswa kuwa mwingi zaidi na zaidi.’ Tunaweza kufanya nini ili upendo wetu kwa Mungu uzidi kuimarika?

5. Ni nini kinachoweza kufanya upendo wetu uwe imara?

5 Ili kumpenda Mungu tunahitaji kumjua. Biblia inasema: “Yeyote ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Mtume Paulo alieleza kwamba upendo wetu kwa Mungu ungezidi kuimarika kadiri tunavyojipatia “ujuzi sahihi na utambuzi kamili” kumhusu Mungu. (Flp. 1:9) Tulipoanza kujifunza Biblia, tulianza kumpenda Mungu ingawa hatukuwa na ujuzi mwingi kuhusu sifa zake zenye kuvutia. Kisha, kadiri tulivyoendelea kujifunza kumhusu Yehova, ndivyo upendo wetu kwake ulivyozidi kuimarika. Hiyo ndiyo sababu sisi huona kujifunza Biblia kwa ukawaida na kutafakari Neno la Mungu kuwa miongoni mwa mambo muhimu zaidi maishani mwetu!—Flp. 2:16.

6. Kulingana na 1 Yohana 4:11, 20, 21, tunaweza kufanya nini ili upendo wetu uzidi kuwa mwingi?

6 Upendo mkubwa ambao Mungu anatuonyesha utatuchochea tuwapende ndugu zetu. (Soma 1 Yohana 4:11, 20, 21.) Huenda tukafikiri kwamba kuwapenda ndugu na dada zetu ni jambo lisilohitaji jitihada yoyote. Huenda tuna maoni hayo kwa sababu tunamwabudu Yehova na tunajitahidi kuiga sifa zake nzuri. Pia, tunaiga kielelezo cha Yesu ambaye alikuwa na upendo mkubwa sana hivi kwamba alitoa uhai wake kwa ajili yetu. Ingawa hivyo, nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kwetu kutii amri ya kuwapenda wengine. Fikiria kisa kilichotokea katika kutaniko la Filipi.

7. Tunajifunza nini kutokana na shauri ambalo Paulo aliwapa Euodia na Sintike?

7 Euodia na Sintike walikuwa dada wenye bidii waliotumikia “pamoja” na mtume Paulo. Hata hivyo, huenda waliruhusu hali ya kutoelewana kati yao iwatenganishe. Katika barua ambayo Paulo aliandikia kutaniko ambalo dada hao walikuwa wakitumikia, aliwataja kihususa Euodia na Sintike kwa majina na kuwapa shauri la moja kwa moja kwamba “wawe na akili moja.” (Flp. 4:2, 3) Pia, Paulo aliona umuhimu wa kulipatia kutaniko lote agizo hili: “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika wala kubishana.” (Flp. 2:14) Hapana shaka kwamba shauri hilo la moja kwa moja la Paulo liliwasaidia dada hao washikamanifu na pia ndugu na dada wengine kutanikoni kuimarisha kifungo cha upendo miongoni mwao.

Kwa nini tunapaswa kudumisha mtazamo unaofaa kuwahusu ndugu zetu? (Tazama fungu la 8) *

8. Ni nini kinachoweza kutuzuia kuwaonyesha upendo ndugu zetu, na tunaweza kushindaje kikwazo hicho?

8 Kama ilivyokuwa kwa Euodia na Sintike, huenda sisi pia tukakabili kikwazo kikubwa kinachotuzuia kuimarisha kifungo cha upendo kati yetu na wengine, yaani, mwelekeo wa kukazia fikira udhaifu wa wengine. Sisi sote hukosea kila siku. Ikiwa tutaendelea kukazia fikira makosa ya wengine, upendo wetu kuwaelekea utafifia. Kwa mfano, huenda tukaudhika ikiwa tunasafisha Jumba la Ufalme, kisha ndugu yetu anaacha kutusaidia na kufanya mambo mengine. Na ikiwa tutaanza kuorodhesha makosa yote mengine ambayo tunajua ndugu yetu amefanya, tutazidi kuudhika na upendo wetu kwake utazidi kufifia. Ukijikuta katika hali kama hiyo, ni vema kutafakari kuhusu ukweli huu: Yehova anaona udhaifu wetu na pia wa ndugu yetu. Lakini licha ya udhaifu huo, bado Yehova anampenda ndugu yetu na anatupenda sisi pia. Kwa sababu hiyo, tunahitaji kuiga upendo wa Yehova na kudumisha mtazamo mzuri kuwaelekea ndugu zetu. Tunapojitahidi kabisa kuwapenda ndugu zetu, tunaimarisha kifungo cha umoja miongoni mwetu.—Flp. 2:1, 2.

“MAMBO MUHIMU ZAIDI”

9. “Mambo muhimu zaidi” yanayotajwa na Paulo katika barua yake kwa Wafilipi yanatia ndani nini?

9 Paulo aliongozwa na roho takatifu kuwaambia akina ndugu na dada huko Filipi na Wakristo wote kwa ujumla kwamba ‘wahakikishe mambo yaliyo muhimu zaidi.’ (Flp. 1:10) Mambo hayo muhimu yanatia ndani kutetewa kwa jina la Yehova, kutimizwa kwa makusudi yake, na amani na umoja katika kutaniko. (Mt. 6:9, 10; Yoh. 13:35) Tunapoyatanguliza mambo hayo maishani mwetu, tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova.

10. Ni lazima tufanye nini ili Yehova atuone kuwa watu wasio na kasoro?

10 Pia, Paulo alisema kwamba ni lazima tuwe “bila kasoro.” Hilo halimaanishi kwamba ni lazima tuwe wakamilifu. Hatuwezi kuwa bila kasoro kwa kiwango kilekile kama Yehova. Lakini Yehova atatuona kuwa watu wasio na kasoro ikiwa tutajitahidi kadiri ya uwezo wetu kuimarisha upendo wetu na kuhakikisha mambo yaliyo muhimu zaidi. Njia moja ya kuonyesha kwamba tunawapenda ndugu zetu ni kuepuka kuwakwaza.

11. Kwa nini ni lazima tuepuke kuwakwaza wengine?

11 Kihalisi, agizo la kuepuka kuwakwaza wengine ni onyo zito. Tunaweza kuwakwazaje wengine? Huenda tukawakwaza kupitia burudani tunazochagua, mavazi yetu, au hata kazi za kimwili tunazochagua kufanya. Huenda jambo tunalochagua kufanya si kosa machoni pa Yehova. Lakini ikiwa mambo tunayochagua kufanya yanasumbua dhamiri ya ndugu au dada yetu na kusababisha akwazike, hilo ni jambo zito sana. Yesu alisema kwamba ingekuwa afadhali jiwe zito lifungwe shingoni petu na tutupwe baharini kuliko kumkwaza mmoja wa kondoo wake.—Mt. 18:6.

12. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa wenzi fulani wa ndoa mapainia?

12 Wenzi fulani wa ndoa mapainia walitii onyo la Yesu jinsi gani? Walitumikia katika kutaniko moja na wenzi wa ndoa waliokuwa wamebatizwa karibuni ambao walilelewa na wazazi wakali ambao waliwawekea vizuizi vingi. Wenzi hao wapya waliamini kwamba Wakristo hawapaswi kwenda kwenye majumba ya sinema—hata ikiwa wanaenda kutazama sinema inayofaa. Walishtuka sana waliposikia kwamba wale wenzi wa ndoa mapainia walikuwa wameenda kutazama sinema fulani. Baada ya wenzi hao wa ndoa mapainia kutambua jambo hilo, waliacha kwenda kwenye majumba ya sinema hadi ndugu na dada hao wapya walipozoeza dhamiri zao na kuwa wenye usawaziko zaidi. (Ebr. 5:14) Tendo hilo lisilo la ubinafsi la wenzi hao wa ndoa mapainia, lilithibitisha kwamba waliwapenda ndugu na dada hao wapya si kwa maneno tu, bali pia kwa matendo.—Rom. 14:19-21; 1 Yoh. 3:18.

13. Tunaweza kusababishaje ndugu au dada yetu atende dhambi?

13 Pia, huenda tukawakwaza wengine kwa kusababisha watende dhambi. Jinsi gani? Fikiria hali hii. Baada ya pambano la muda mrefu, hatimaye mwanafunzi wa Biblia anashinda uraibu wa kutumia pombe. Anatambua kwamba ni lazima aache kabisa kutumia pombe. Anafanya maendeleo upesi na kubatizwa. Baadaye, ndugu fulani asiye na nia mbaya ambaye amemwalika kwenye tafrija anamtia moyo ndugu yetu mpya anywe pombe. Anamwambia: “Wewe ni Mkristo sasa; una roho ya Yehova. Na sifa moja ya tunda la roho ni kujizuia. Ukiwa na sifa ya kujizuia, unaweza kunywa pombe kwa kiasi.” Bila shaka unaweza kuwazia jinsi matokeo yatakavyokuwa ikiwa ndugu yetu mpya ataamua kusikiliza ushauri huo usiofaa!

14. Mikutano ya Kikristo inatusaidiaje kutii maagizo yaliyo kwenye Wafilipi 1:10?

14 Mikutano yetu ya Kikristo hutusaidia kwa njia mbalimbali kutii maagizo tunayopata katika andiko la Wafilipi 1:10. Kwanza, programu iliyojaa chakula kingi kizuri cha kiroho hutukumbusha mambo ambayo Yehova huyaona kuwa muhimu zaidi. Pili, tunajifunza jinsi ya kutumia mambo tunayojifunza ili tuwe bila kasoro. Na tatu, tunachochewa “katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24, 25) Kadiri ndugu zetu wanavyoendelea kututia moyo, ndivyo upendo wetu kwa Yehova na kwa ndugu zetu utakavyozidi kuongezeka. Tunapompenda Mungu na ndugu zetu kwa moyo wetu wote, tutafanya kila tunaloweza tusiwakwaze ndugu zetu.

ENDELEENI ‘KUJAZWA TUNDA LA UADILIFU’

15. Maneno ‘kujazwa tunda la uadilifu’ yanamaanisha nini?

15 Paulo alisali kwa bidii kwamba Wafilipi ‘wajazwe tunda la uadilifu.’ (Flp. 1:11) Hapana shaka kwamba “tunda [hilo] la uadilifu” lilitia ndani kumpenda Yehova na watu wake. Pia, lilitia ndani kuzungumza na wengine kuhusu imani yao katika Yesu na kuhusu tumaini lao zuri la wakati ujao. Andiko la Wafilipi 2:15 linatumia mfano mwingine, yaani, “[kuangaza] kama mianga katika ulimwengu.” Mfano huo unafaa kwa sababu Yesu aliwaita wanafunzi wake “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14-16) Pia, aliwaamuru wafuasi wake ‘wakafanye wanafunzi,’ na alisema kwamba ‘wangekuwa mashahidi mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.’ (Mt. 28:18-20; Mdo. 1:8) Tunazaa “tunda la uadilifu” tunaposhiriki kwa bidii katika kazi hii muhimu sana.

Akiwa katika kifungo cha nyumbani jijini Roma, Paulo analiandikia barua kutaniko la Filipi. Katika kipindi hicho, Paulo anatumia vizuri fursa aliyo nayo kuwahubiria walinzi walio pamoja naye na wageni wanaomtembelea (Tazama fungu la 16)

16. Andiko la Wafilipi 1:12-14 linaonyeshaje kwamba tunaweza kuangaza kama mianga hata tunapokuwa chini ya hali ngumu? (Tazama picha kwenye jalada.)

16 Hata iwe tuna hali gani, tunaweza kuangaza kama mianga. Katika visa fulani, jambo tunaloona kuwa kikwazo kinachotuzuia kutangaza habari njema linaweza kutokeza fursa ya kuhubiri. Kwa mfano, mtume Paulo alikuwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma alipowaandikia Wafilipi barua. Lakini minyororo aliyokuwa amefungwa haikumzuia kuwahubiria walinzi na wageni waliomtembelea. Paulo alihubiri kwa bidii chini ya hali hizo, na jambo hilo liliwapa akina ndugu uhakika na uhodari mwingi wa “kulisema neno la Mungu bila woga.”—Soma Wafilipi 1:12-14; 4:22.

Sikuzote tafuta njia za kushiriki kikamili katika huduma (Tazama fungu la 17) *

17. Toa mfano wa ndugu na dada katika nyakati zetu wanaoendelea kuzaa matunda licha ya hali ngumu.

17 Ndugu na dada zetu wengi wana fursa ya kumwiga Paulo katika kuonyesha ujasiri. Wanaishi katika nchi ambazo hawawezi kuhubiri hadharani au nyumba kwa nyumba, hivyo wao hutafuta njia nyingine za kutangaza habari njema. (Mt. 10:16-20) Katika mojawapo ya nchi hizo, mwangalizi mmoja wa mzunguko alipendekeza kwamba kila mhubiri awe na “eneo” lake mwenyewe la kuhubiri linalotia ndani watu wa ukoo, majirani, wanafunzi wenzake, wafanyakazi wenzake, na watu wengine anaofahamiana nao. Katika kipindi cha miaka miwili, idadi ya makutaniko katika mzunguko huo iliongezeka kwa kiwango kikubwa. Huenda tunaishi katika nchi ambayo tunahubiri kwa uhuru. Hata hivyo, tunajifunza somo muhimu kutokana na mfano huo wa ndugu na dada zetu wabunifu: Sikuzote tafuta njia za kushiriki kikamili katika huduma, ukiwa na uhakika kwamba Yehova atakupa nguvu unazohitaji ili kushinda kizuizi chochote.—Flp. 2:13.

18. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

18 Katika nyakati hizi zenye kusisimua, acheni tuazimie kufuata shauri lililoongozwa na roho lililo katika barua ya Paulo kwa Wafilipi. Acheni tuhakikishe mambo yaliyo muhimu zaidi, tuwe bila kasoro, tuepuke kuwakwaza wengine, na tuzae tunda la uadilifu. Tukifanya hivyo, upendo wetu utakuwa mwingi na tutamletea heshima Yehova, Baba yetu anayetujali.

WIMBO 17 “Nataka”

^ fu. 5 Leo, kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji kuimarisha upendo wetu kwa ndugu na dada zetu. Barua kwa Wafilipi inatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kuwa na upendo mwingi, hata tunapokabili matatizo mbalimbali.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa usafi kwenye Jumba la Ufalme, ndugu mmoja anayeitwa Joe, anaacha kufanya usafi na kuanza kuongea na ndugu mwingine pamoja na mwanaye. Jambo hilo linamuudhi Ndugu Mike ambaye anasafisha zulia. Anajiambia, ‘Joe anapaswa kufanya usafi, si kuzungumza.’ Baadaye, Mike anamwona Joe akimsaidia kwa upendo dada mwenye umri mkubwa. Jambo hilo lenye kugusa moyo linamkumbusha Mike awe akikazia zaidi sifa nzuri za ndugu yake.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Katika nchi ambayo akina ndugu hawawezi kuhubiri hadharani, ndugu anatumia busara anaposhiriki ujumbe wa Ufalme pamoja na mtu wanayefahamiana. Baadaye, akiwa kazini wakati wa mapumziko, ndugu huyo anamhubiria mfanyakazi mwenzake.