Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 33

“Wale Wanaokusikiliza” Wataokolewa

“Wale Wanaokusikiliza” Wataokolewa

“Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Endelea kufanya mambo haya, kwa maana ukifanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.”—1 TIM. 4:16.

WIMBO 67 “Lihubiri Neno”

MUHTASARI *

1. Sisi sote tunatamani watu wetu wa ukoo wachukue hatua gani?

DADA mmoja anayeitwa Pauline * anasema hivi: “Tangu nilipojifunza kweli, nilitamani kila mtu katika familia yetu awe pamoja nami katika Paradiso. Nilitamani hasa mume wangu Wayne na mwana wetu mdogo wajiunge nami kumtumikia Yehova.” Je, una watu wa ukoo ambao bado hawajajifunza kumhusu Yehova na kuanza kumpenda? Huenda unahisi kama Pauline alivyohisi kuhusu watu wa familia yake.

2. Tutazungumzia maswali gani katika makala hii?

2 Hatuwezi kuwalazimisha watu wetu wa ukoo wakubali habari njema, lakini tunaweza kuwatia moyo wafungue akili na mioyo yao ili wasikilize ujumbe wa Biblia. (2 Tim. 3:14, 15) Kwa nini tunapaswa kuwahubiria watu wetu wa ukoo? Kwa nini tunapaswa kuwaonyesha hisia-mwenzi? Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu wetu wa ukoo wampende Yehova kama tunavyompenda? Na ndugu na dada wote kutanikoni wanaweza kutusaidiaje?

KWA NINI TUNAPASWA KUWAHUBIRIA WATU WA UKOO?

3. Kulingana na 2 Petro 3:9, kwa nini tunapaswa kuwahubiria watu wetu wa ukoo?

3 Hivi karibuni, Yehova atakomesha mfumo huu. Ni wale tu walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” watakaookolewa. (Mdo. 13:48) Sisi hutumia wakati na nguvu nyingi kuwahubiria watu tusiowafahamu, hivyo ni jambo la kawaida pia kutamani watu wetu wa ukoo wamtumikie Yehova pamoja nasi. Baba yetu mwenye upendo, Yehova, “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—Soma 2 Petro 3:9.

4. Huenda tukafanya kosa gani tunapowahubiria watu wetu wa ukoo?

4 Tunapaswa kuzingatia akilini kwamba kuna njia inayofaa na isiyofaa ya kushiriki pamoja na wengine ujumbe wa wokovu. Huenda tukatumia busara tunapomhubiria mtu tusiyemfahamu, lakini huenda tukazungumza waziwazi na bila busara tunapowahubiria watu wetu wa ukoo.

5. Tunapaswa kuzingatia nini akilini kabla ya kuwahubiria kweli watu wetu wa ukoo?

5 Huenda wengi wetu tunasikitika tunapofikiria jinsi tulivyowahubiria watu wetu wa ukoo kwa mara ya kwanza, na kutamani tungezungumza nao kwa njia tofauti. Mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Kol. 4:5, 6) Ni vema kukumbuka ushauri huo tunapowahubiria watu wetu wa ukoo. La sivyo, huenda tukawaudhi badala ya kufikia mioyo yao.

JINSI YA KUWASAIDIA WATU WETU WA UKOO

Sifa ya hisia-mwenzi na mwenendo wako ni mambo yanayoweza kutoa ushahidi mkubwa kwa wengine (Tazama fungu la 6 hadi 8) *

6-7. Toa mfano unaoonyesha umuhimu wa kumwonyesha mwenzi wa ndoa asiye mwamini hisia-mwenzi.

6 Waonyeshe hisia-mwenzi. Pauline, dada aliyetajwa awali, anasema hivi: “Mwanzoni nilitamani kuzungumza na mume wangu kuhusu mambo ya kiroho tu. Hatukuzungumzia mambo ya kawaida ya kila siku.” Hata hivyo, Wayne, mume wa Pauline, hakujua mengi kuhusu Biblia na hakuelewa mambo ambayo Pauline alikuwa akizungumzia. Kwa maoni yake, Wayne alihisi kwamba hakuna kingine ambacho mke wake alikuwa akifikiria isipokuwa dini yake. Alikuwa na wasiwasi kwamba mke wake alikuwa amejiunga na dhehebu hatari na alikuwa akipotoshwa.

7 Pauline anakiri kwamba kwa muda fulani alitumia wakati mwingi jioni na mwisho juma pamoja na ndugu na dada zake wa kiroho—kwenye mikutano, kazi ya kuhubiri, na kwenye tafrija. Pauline anasema: “Nyakati nyingine Wayne alipofika nyumbani hakumkuta yeyote, na alihisi upweke”. Ni wazi kwamba Wayne alimkosa sana mke wake na mwanaye. Hakuwafahamu watu walioshirikiana na mke wake, na alihisi kwamba marafiki hao wapya wa mke wake walikuwa muhimu zaidi kwake kuliko yeye. Wayne alitishia kumpa talaka Pauline. Je, umetambua ni kwa njia gani Pauline angeweza kumwonyesha mume wake hisia-mwenzi zaidi?

8. Kulingana na 1 Petro 3:1, 2, ni nini kinachoweza kuwachochea watu wetu wa ukoo waikubali kweli?

8 Acha mwenendo wako uhubiri. Kwa kawaida, watu wetu wa ukoo huona zaidi mambo tunayofanya kuliko yale tunayosema. (Soma 1 Petro 3:1, 2.) Mwishowe, Pauline alitambua ukweli huo. Anasema hivi: “Nilijua kwamba Wayne alitupenda na hakuwa na nia ya kunitaliki. Lakini alipotishia kunitaliki nilitambua kwamba nilihitaji kufanya mambo kulingana na njia ya Yehova. Badala ya kumhubiria tu, nilihitaji kuweka mfano mzuri kupitia mwenendo wangu.” Pauline aliacha kumlazimisha Wayne kuzungumzia mambo ya Biblia, na akaanza kuzungumza naye kuhusu mambo ya kawaida ya kila siku. Wayne aliona kwamba mke wake alianza kuwa mwenye kufanya amani zaidi, na mwana wao akawa mwenye adabu zaidi. (Met. 31:18, 27, 28) Wayne alipojionea matokeo mazuri ya ujumbe wa Biblia katika familia yake, alifungua akili na moyo wake na kusikiliza ujumbe wa Neno la Mungu.—1 Kor. 7:12-14, 16.

9. Kwa nini ni lazima tuendelee kujitahidi kuwasaidia watu wetu wa ukoo?

9 Endelea kujitahidi kuwasaidia watu wako wa ukoo. Yehova ametuwekea kielelezo bora. “Tena na tena” anawapa watu fursa ya kusikiliza habari njema na kupata uzima. (Yer. 44:4) Mtume Paulo alimwambia Timotheo aendelee kujitahidi kuwasaidia wengine. Kwa nini? Kwa sababu kwa kufanya hivyo, angejiokoa yeye mwenyewe na wale wanaomsikiliza. (1 Tim. 4:16) Tunawapenda watu wetu wa ukoo, hivyo tunatamani wajifunze kweli za Neno la Mungu. Mwishowe, maneno na matendo ya Pauline yalikuwa na matokeo mazuri kwa familia yake. Sasa anafurahia kumtumikia Yehova pamoja na mume wake. Wote wawili ni mapainia, na Wayne ni mzee wa kutaniko.

10. Kwa nini tunapaswa kuwa na subira?

10 Uwe na subira. Tunapoanza kuishi kulingana na viwango vya Mungu, huenda ikawa vigumu kwa watu wetu wa ukoo kukubali kwa urahisi imani yetu mpya na maisha yetu mapya. Mara nyingi, jambo la kwanza wanalotambua ni kwamba sasa hatushirikiani nao tena katika sherehe za kidini na hatujihusishi na mambo ya kisiasa. Mwanzoni, huenda baadhi ya watu wetu wa ukoo wakakasirika. (Mt. 10:35, 36) Lakini hatupaswi kukata tamaa na kuacha kuwasaidia. Ikiwa tutaacha kuwasaidia kuelewa mambo tunayoamini, kimsingi tutakuwa tumewahukumu kwamba hawastahili kupata uzima wa milele. Yehova hajatupatia kazi ya kuhukumu—amemkabidhi Yesu kazi hiyo. (Yoh. 5:22) Tukiwa na subira, huenda mwishowe watu wetu wa ukoo watakuwa tayari kusikiliza ujumbe wetu.—Tazama sanduku “ Tumia Tovuti Yetu Kufundisha.”

11-13. Unajifunza nini kutokana na jinsi Alice alivyoshughulika na wazazi wake?

11 Uwe thabiti lakini mwenye busara. (Met. 15:2) Fikiria mfano wa Alice. Alijifunza kumhusu Yehova alipokuwa akiishi mbali na wazazi wake, ambao hawakuamini kwamba kuna Mungu na walijihusisha sana na siasa. Alice alitambua kwamba alihitaji kuwajulisha wazazi wake haraka iwezekanavyo kuhusu mambo mazuri aliyokuwa akijifunza. Alice anasema: “Ukiruhusu muda mrefu upite ndipo uwaeleze watu wa familia yako kuhusu imani na utendaji wako, watapatwa na mshtuko mkubwa zaidi.” Aliwaandikia wazazi wake barua akitaka kujua maoni yao kuhusu mafundisho ya Biblia ambayo alihisi yangewavutia, kama vile upendo. (1 Kor. 13:1-13) Aliwashukuru wazazi wake kwa kumlea na kumtunza vizuri, na pia aliwatumia zawadi. Alipowatembelea nyumbani, alifanya yote awezayo kumsaidia mama yake kazi za nyumbani. Mwanzoni, wazazi wa Alice hawakuitikia vizuri alipowaeleza kuhusu imani yake mpya.

12 Alipokuwa nyumbani kwa wazazi wake, Alice alishikamana na ratiba yake ya kusoma Biblia. Anasema hivi: “Jambo hilo lilimsaidia mama yangu kuelewa jinsi Biblia ilivyokuwa muhimu sana kwangu.” Wakati huohuo, Baba ya Alice aliamua kujifunza mambo fulani kuhusu Biblia ili aweze kuelewa vizuri mambo yaliyomfanya binti yake abadili maoni yake; pia alikuwa na nia ya kuikosoa Biblia. Alice anasema: “Nilimpatia Biblia, na kumwandikia humo ujumbe mfupi wenye kugusa moyo.” Ikawaje? Baba yake hakupata jambo lolote la kukosoa, badala yake aliguswa sana na mambo aliyosoma katika Neno la Mungu.

13 Tunahitaji kuwa thabiti lakini wenye busara, hata tukilazimika kuvumilia majaribu. (1 Kor. 4:12b) Kwa mfano, Alice, alivumilia upinzani kutoka kwa mama yake. Anasema hivi: “Nilipobatizwa, Mama aliniita ‘binti mbaya.’” Alice alitendaje? Anasema hivi: “Badala ya kuogopa kuzungumzia dini yangu mpya, kwa heshima nilimweleza Mama kwamba nilikuwa nimeamua kuwa Shahidi wa Yehova na ningeshikamana na uamuzi huo. Nilijitahidi kumhakikishia Mama kwamba ninampenda sana. Sote tulilia, kisha nikampikia chakula kitamu. Tangu wakati huo, Mama alianza kutambua kwamba Biblia ilikuwa ikiboresha utu wangu.”

14. Kwa nini hatupaswi kamwe kuwaruhusu watu wetu wa ukoo watushinikize tuache kumtumikia Yehova?

14 Huenda muda mrefu ukapita kabla ya watu wetu wa ukoo kuelewa kikamili jinsi ibada yetu kwa Yehova ilivyo muhimu sana kwetu. Kwa mfano, Alice alipoamua kuwa painia badala ya kufuatia kazi ambayo wazazi wake walitaka afanye, mama yake alilia tena. Lakini Alice aliendelea kuwa thabiti. Anasema hivi: “Ukiruhusu familia yako ikushinikize kufanya jambo fulani, kuna uwezekano mkubwa watajaribu pia kukushinikiza ufanye mambo mengine. Hata hivyo, ukiwa thabiti lakini mwenye fadhili, huenda baadhi ya watu wa familia yako wakakusikiliza.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Alice. Wazazi wote wa Alice sasa ni mapainia, na baba yake ni mzee wa kutaniko.

JINSI WOTE KUTANIKONI WANAVYOWEZA KUKUSAIDIA

Kutaniko linaweza kuwasaidiaje watu wa familia yetu ambao si waamini? (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Kulingana na Mathayo 5:14-16 na 1 Petro 2:12, ‘matendo mema’ ya wengine yanaweza kuwasaidiaje watu wetu wa ukoo?

15 Yehova anawavuta watu kwake kupitia ‘matendo mema’ ya kutaniko la Kikristo. (Soma Mathayo 5:14-16; 1 Petro 2:12.) Ikiwa mwenzi wako si Shahidi wa Yehova, je, amewahi kukutana na ndugu na dada wa kutaniko lako? Pauline, dada aliyetajwa awali, aliwakaribisha ndugu na dada nyumbani ili Wayne, mume wake, aweze kufahamiana nao. Wayne anakumbuka jinsi ndugu mmoja alivyomsaidia kuwafahamu vizuri zaidi Mashahidi wa Yehova. Anaeleza hivi: “Alichukua likizo ya siku moja kutoka kazini ili tu tutazame mechi ya mpira tukiwa pamoja. Nikajiambia, ‘Kumbe yeye ni mtu wa kawaida tu!’”

16. Kwa nini tunapaswa kuwaalika watu wetu wa ukoo wahudhurie mikutano?

16 Njia moja nzuri ya kuwasaidia watu wetu wa ukoo ni kuwaalika kwenye mikutano ya kutaniko. (1 Kor. 14:24, 25) Mkutano wa kwanza ambao Wayne alihudhuria ulikuwa Ukumbusho—kwa sababu ulifanywa baada ya kazi na ulichukua muda mfupi. Wayne anasema hivi: “Sikuelewa vizuri hotuba iliyotolewa, lakini ninawakumbuka watu. Walinifuata na kunikaribisha vizuri, na kunipa mkono kwa uchangamfu. Nilitambua kwamba walikuwa watu wanyoofu.” Kulikuwa na ndugu mmoja na mke wake ambao walikuwa wakimwonyesha Pauline fadhili nyingi; walisaidia kumtunza mtoto wake mikutanoni na katika huduma. Hivyo, Wayne alipoamua kujifunza zaidi kuhusu mambo ambayo Pauline aliamini, alimwomba ndugu huyo ajifunze Biblia pamoja naye.

17. Hatupaswi kujilaumu kuhusu nini, na kwa nini hatupaswi kamwe kufikiri kwamba watu wetu wa ukoo hawawezi kubadilika?

17 Tunatumaini kwamba watu wetu wote wa ukoo watajiunga pamoja nasi kumtumikia Yehova. Hata hivyo, licha ya jitihada zetu zote za kuwasaidia watu wetu wa ukoo wawe watumishi wa Mungu, huenda wasiikubali kweli. Hali ikiwa hivyo, hatupaswi kujilaumu kwa uamuzi waliochukua. Isitoshe, hatuwezi kumlazimisha yeyote akubali mambo tunayoamini. Licha ya hilo, usipuuze kamwe jinsi shangwe yako ya kumtumikia Yehova inavyoweza kuwachochea watu wako wa ukoo. Sali kwa ajili yao. Zungumza nao kwa busara. Usiache kuwasaidia! (Mdo. 20:20) Uwe na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako. Na ikiwa watu wako wa ukoo watachagua kukusikiliza, wataokolewa!

WIMBO 57 Kuwahubiria Watu wa Namna Zote

^ fu. 5 Tungependa watu wetu wa ukoo wamjue Yehova, hata hivyo ni lazima waamue wao wenyewe ikiwa watamtumikia au la. Katika makala hii, tutachunguza mambo tunayoweza kufanya ili iwe rahisi kwa watu wetu wa ukoo kutusikiliza.

^ fu. 1 Baadhi ya majina yamebadilishwa. Katika makala hii, maneno “watu wa ukoo” yanarejelea watu wa familia ambao hawamtumikii Yehova.

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Ndugu kijana akimsaidia baba yake asiye mwamini kurekebisha gari lake. Kwa wakati unaofaa anamwonyesha video kwenye tovuti ya jw.org®.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Dada yetu akimsikiliza kwa makini mume wake asiye mwamini anapomweleza jinsi siku yake yenye mambo mengi ilivyokuwa. Baadaye, anafurahia tafrija pamoja na familia yake.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Dada huyo amewaalika nyumbani ndugu na dada wa kutaniko lake. Wanajitahidi kufahamiana na mume wake. Baadaye, mume huyo anahudhuria Ukumbusho pamoja na mke wake.