Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yohana Mbatizaji—Mfano Mzuri wa Kudumisha Shangwe

Yohana Mbatizaji—Mfano Mzuri wa Kudumisha Shangwe

JE, UNATAMANI mgawo fulani kutanikoni ambao kwa sasa huwezi kuutimiza? Huenda ni jukumu ambalo mtu mwingine anafurahia. Au huenda ni mgawo wa utumishi, au pendeleo fulani, ambalo awali ulikuwa nalo. Lakini kwa sasa huenda umri, afya mbaya, matatizo ya kiuchumi, au majukumu ya kifamilia yanakuzuia kufanya mengi. Au huenda kwa sababu ya mabadiliko katika tengenezo, umelazimika kuacha mgawo ambao umefanya kwa muda mrefu. Haidhuru sababu ni nini, unaweza kuhisi kwamba hufanyi yote ambayo ungependa kutimiza katika utumishi wa Mungu. Katika hali kama hizo, inaeleweka kwamba huenda nyakati nyingine ukakata tamaa. Hata hivyo, unaweza kufanya nini ili hisia zisizofaa kama vile kuvunjika moyo, uchungu, au kinyongo zisitie mizizi moyoni mwako? Unaweza kudumishaje shangwe yako?

Tunaweza kujifunza jinsi ya kudumisha shangwe yetu kwa kuchunguza mfano wa Yohana Mbatizaji. Yohana alikuwa na mapendeleo ya pekee, lakini hakutarajia kwamba maisha yake katika utumishi wa Yehova yangechukua mkondo ambao yalichukua. Huenda hakuwazia kwamba angetumia muda mwingi zaidi gerezani kuliko aliotumia katika huduma yake. Lakini bado Yohana aliendelea kuwa na shangwe, na alidumisha mtazamo huo katika kipindi chote cha maisha yake. Ni nini kilichomsaidia? Na tunaweza kudumishaje shangwe yetu licha ya hali zinazovunja moyo?

MGAWO ULIOMLETEA SHANGWE

Katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 29 W.K., Yohana alianza mgawo wake akiwa mtayarishaji wa njia kwa ajili ya Masihi, akisema: “Tubuni, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 3:2; Luka 1:12-17) Watu wengi waliitikia vizuri. Hata umati mkubwa wa watu ulikuja kutoka maeneo ya mbali ili kusikia ujumbe wake, na wengi walichochewa kutubu dhambi zao na kubatizwa. Pia, Yohana aliwaonya kwa ujasiri viongozi wa kidini waliojiona kuwa waadilifu kuhusu hukumu iliyokuwa ikiwasubiri ikiwa hawangebadilika. (Mt. 3:5-12) Huduma yake ilifikia kilele alipombatiza Yesu wakati wa majira ya kupukutika, mwaka wa 29 W.K. Kuanzia wakati huo na kuendelea Yohana aliwaelekeza watu kwa Yesu, Masihi aliyeahidiwa.—Yoh. 1:32-37.

Kwa sababu ya mgawo wa pekee ambao Yohana alikuwa nao, Yesu angeweza kusema: “Kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mtu mkuu kuliko Yohana Mbatizaji.” (Mt. 11:11) Hapana shaka kwamba Yohana alishangilia kwa sababu ya baraka alizopata. Kama Yohana, watu wengi leo wamefurahia baraka nyingi. Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Terry. Yeye pamoja na Sandra, mke wake, wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 50. Terry anaeleza hivi: “Nimefurahia mapendeleo mengi sana yenye kusisimua. Nimetumikia nikiwa painia wa kawaida, Mwanabetheli, painia wa pekee, mwangalizi wa mzunguko, mwangalizi wa wilaya, na sasa tena nikiwa painia wa pekee.” Tunashangilia tunapopata mapendeleo ya kitheokrasi, lakini kama tutakavyojifunza kutokana na mfano wa Yohana, jitihada inahitajika ili tuendelee kuwa na shangwe hali zetu zinapobadilika.

ENDELEA KUWA MWENYE SHUKRANI

Jambo moja lililomfanya Yohana Mbatizaji aendelee kuwa mwenye shangwe ni kwamba aliendelea kuthamini mapendeleo aliyokuwa nayo. Fikiria mfano huu. Baada ya Yesu kubatizwa, huduma ya Yohana ilianza kupungua ilhali ya Yesu ilianza kuongezeka. Jambo hilo liliwahangaisha wanafunzi wa Yohana, nao wakamfikia na kumwambia: Angalia, huyu “anabatiza na watu wote wanaenda kwake.” (Yoh. 3:26) Yohana akawaambia: “Yule aliye na bibi harusi ndiye bwana harusi. Hata hivyo, rafiki ya bwana harusi, anaposimama na kumsikia, anashangilia sana kwa sababu ya sauti ya bwana harusi. Kwa hiyo shangwe yangu imekamilishwa.” (Yoh 3:29) Yohana hakushindana na Yesu; wala hakufikiri kwamba pendeleo alilokuwa nalo lilikuwa limepungua thamani eti kwa sababu Yesu alikuwa na jukumu kubwa kuliko lake. Badala yake, Yohana aliendelea kuwa na shangwe kwa sababu alithamini sana jukumu lake akiwa “rafiki ya bwana harusi.”

Mtazamo wa Yohana ulimsaidia aendelee kuridhika licha ya yote ambayo mgawo wake ulihusisha. Kwa mfano, Yohana alikuwa Mnadhiri tangu alipozaliwa, na hivyo hakupaswa kunywa kileo chochote. (Luka 1:15) Yesu alisema hivi kuhusu maisha ya kujinyima ya Yohana: “Yohana hakuja akila wala kunywa.” Kwa upande mwingine, Yesu na wanafunzi wake hawakuwa chini ya vizuizi hivyo na waliishi maisha ya kawaida. (Mt. 11:18, 19) Pia, ingawa Yohana hakufanya muujiza wowote, alijua kwamba wanafunzi wa Yesu, kutia ndani wale ambao awali walimfuata yeye, walikuwa wamepewa nguvu hizo. (Mt. 10:1; Yoh. 10:41) Badala ya kuruhusu tofauti hizo zimkengeushe, Yohana alishikamana kwa bidii na mgawo aliopewa na Yehova.

Ikiwa sisi pia tutathamini mgawo tulio nao kwa sasa katika utumishi wa Yehova, tutalinda shangwe yetu. Terry, ndugu aliyetajwa awali, anasema hivi: “Nilikazia uangalifu kila mgawo niliopewa.” Anasema hivi anapotafakari kuhusu maisha yake akiwa mtumishi wa wakati wote: “Sijutii chochote, bali nina kumbukumbu nyingi zenye kufurahisha.”

Tunaweza kufanya shangwe yetu katika utumishi wa Mungu izidi kuongezeka kwa kutafakari jambo linalofanya mgawo au jukumu lolote la kitheokrasi liwe na thamani kwelikweli. Jambo hilo ni pendeleo la kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Kama tu ambavyo kito chenye thamani tulichorithi kinavyoweza kuendelea kung’aa tunapoking’arisha, ndivyo kutafakari kuhusu heshima ya pekee tuliyo nayo ya kumtumikia Mungu, kunavyoweza kutulinda dhidi ya mawazo yasiyofaa yanayoweza kufanya shangwe yetu ififie. Tutaepuka kulinganisha mambo ambayo tumetimiza na yale ambayo wengine wametimiza. Hatutayaona mapendeleo yetu kuwa na thamani ndogo kwa kulinganisha na mapendeleo ambayo wengine wanayo.—Gal. 6:4.

KAZIA FIKIRA MAMBO YA KIROHO

Huenda Yohana alijua kwamba huduma yake haingedumu kwa muda mrefu, lakini huenda hakutambua kwamba ingefikia mwisho wake ghafla. (Yoh. 3:30) Katika mwaka wa 30 W.K., miezi sita hivi baada ya kumbatiza Yesu, Yohana alifungwa gerezani na Mfalme Herode. Lakini bado Yohana alifanya yote aliyoweza ili aendelee kutoa ushahidi. (Marko 6:17-20) Ni nini kilichomsaidia aendelee kuwa na shangwe licha ya mabadiliko aliyokabili? Aliendelea kukazia fikira mambo ya kiroho.

Yohana alipokuwa gerezani alipokea ripoti kuhusu huduma ya Yesu iliyokuwa ikiongezeka. (Mt. 11:2; Luka 7:18) Yohana alisadiki kwamba Yesu alikuwa Masihi lakini huenda alijiuliza jinsi ambavyo Yesu angetimiza mambo yote ambayo Maandiko yalisema Masihi angetimiza. Kwa kuwa Masihi angepokea mamlaka ya kifalme, je, Yesu angeanza kutawala hivi karibuni? Je, hilo lingefanya aachiliwe huru kutoka gerezani? Akiwa na hamu ya kuelewa vizuri jukumu la Yesu, Yohana aliwatuma wawili kati ya wanafunzi wake waende kwa Yesu na kumuuliza: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja, au tumtarajie mwingine?” (Luka 7:19) Waliporudi, lazima Yohana aliwasikiliza kwa makini walipokuwa wakimsimulia kwamba Yesu alikuwa akiwaponya watu kimuujiza na alikuwa amewatuma wamwambie hivi Yohana: “Vipofu wanaona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.”—Luka 7:20-22.

Bila shaka ripoti waliyomletea ilimwimarisha sana Yohana. Ilithibitisha kwamba Yesu alikuwa akitimiza unabii mbalimbali kumhusu Masihi. Ingawa kutokea kwa Yesu hakungemfanya Yohana aachiliwe huru kutoka gerezani, Yohana alijua kwamba utumishi wake haukuwa wa bure. Licha ya hali yake, alikuwa na sababu ya kuwa na furaha.

Kukazia fikira ripoti nzuri kuhusu kazi yetu ya kuhubiri ulimwenguni pote kunaweza kutusaidia tudumishe shangwe yetu

Kama Yohana, ikiwa tutakazia fikira mambo ya kiroho, tutafanikiwa kuvumilia kwa shangwe na subira. (Kol. 1:9-11) Tutafanikiwa kuvumilia ikiwa tutasoma Biblia na kutafakari kuhusu mambo tunayosoma, ambayo yatatukumbusha kwamba kazi yetu katika utumishi wa Mungu si ya bure. (1 Kor. 15:58) Sandra anasema hivi: “Kusoma sura moja ya Biblia kila siku kumefanya nimkaribie Yehova zaidi. Kumenisaidia nimkazie fikira Yehova badala kujikazia fikira.” Pia, tunaweza kukazia fikira ripoti kuhusu kazi ya Ufalme, na jambo hilo litatusaidia tusihangaike kupita kiasi kuhusu hali yetu, badala yake tukazie fikira mambo ambayo Yehova anatimiza. Sandra anasema hivi: “Programu za kila mwezi za JW Broadcasting® hutufanya tuhisi tukiwa karibu zaidi na tengenezo na zinatusaidia tudumishe shangwe katika mgawo wetu.”

Yohana Mbatizaji alitekeleza mgawo wake wa muda mfupi kwa “roho na nguvu za Eliya,” na kama Eliya, “alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu.” (Luka 1:17; Yak. 5:17) Tukiiga mfano wake wa kuonyesha uthamini na kukazia fikira mambo ya kiroho, sisi pia tutaendelea kuwa na shangwe katika utumishi wetu wa Ufalme, hata hali zetu maishani ziweje.