Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 35

Heshimu Sehemu ya Wengine Katika Kutaniko la Yehova

Heshimu Sehemu ya Wengine Katika Kutaniko la Yehova

“Jicho haliwezi kuuambia mkono, ‘Sikuhitaji wewe,’ au tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, ‘Siwahitaji ninyi.’”​—1 KOR. 12:21.

WIMBO 124 Washikamanifu Sikuzote

MUHTASARI *

1. Yehova amewapatia nini watumishi wake wote waaminifu?

KWA upendo, Yehova amewapatia watumishi wake wote waaminifu sehemu katika kutaniko lake. Ingawa tunatimiza sehemu tofauti-tofauti, sote tuna thamani na kila mmoja anamhitaji mwenzake. Mtume Paulo anatusaidia kutambua somo hilo muhimu. Jinsi gani?

2. Kulingana na Waefeso 4:16, kwa nini tunahitaji kuthaminiana na kufanya kazi kwa umoja?

2 Kama andiko la msingi la makala hii linavyoonyesha, Paulo anakazia kwamba hakuna anayeweza kumtazama mtumishi mwenzake wa Yehova na kusema: “Sikuhitaji wewe.” (1 Kor. 12:21) Ili tuwe na amani kutanikoni, ni lazima tuthaminiane na kufanya kazi pamoja. (Soma Waefeso 4:16.) Tunapofanya kazi kwa umoja, kutaniko linasitawi na linajengwa katika upendo.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Tunaweza kuwaonyesha heshima Wakristo wenzetu kutanikoni katika njia zipi? Katika makala hii, tutajifunza jinsi wazee wa kutaniko wanavyoweza kuwaonyesha heshima wazee wenzao. Kisha, tutazungumzia jinsi sisi sote tunavyoweza kuonyesha kwamba tunawathamini ndugu na dada zetu ambao ni waseja. Na mwishowe, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunawathamini wale ambao hawawezi kuzungumza lugha yetu kwa ufasaha.

WAHESHIMU WAZEE WENZAKO WA KUTANIKO

4. Wazee wanapaswa kufuata shauri gani la Paulo lililotajwa kwenye Waroma 12:10?

4 Wazee wote wa kutaniko wanawekwa rasmi kwa roho takatifu ya Yehova. Hata hivyo, kila mmoja ana zawadi na uwezo tofauti. (1 Kor. 12:17, 18) Wengine wanaweza kuwa wamewekwa rasmi hivi karibuni na hawana uzoefu mwingi. Wengine hawawezi kufanya mengi kwa sababu ya umri na hali yao ya kiafya. Licha ya hivyo, hakuna mzee wa kutaniko anayepaswa kuhisi hivi kumhusu mzee mwenzake: “Sikuhitaji wewe.” Badala yake, kila mzee wa kutaniko anapaswa kufuata shauri la Paulo linalotajwa katika Waroma 12:10.—Soma.

Wazee wa kutaniko wanaonyesha kwamba wanawaheshimu wazee wenzao kwa kuwasikiliza kwa makini (Tazama fungu la 5 na 6)

5. Wazee wa kutaniko wanaonyeshaje kwamba wanawaheshimu wazee wenzao, na kwa nini ni muhimu wafanye hivyo?

5 Wazee wa kutaniko wanaonyesha kwamba wanawaheshimu wazee wenzao kwa kuwasikiliza kwa makini. Jambo hilo ni muhimu hasa wazee wa kutaniko wanapokutana pamoja wakiwa baraza ili kuzungumzia mambo mazito. Kwa nini? Ona yale ambayo gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1988 la Kiingereza lilisema: “Wazee wa kutaniko watatambua kwamba Kristo, kupitia roho takatifu, anaweza kumwongoza mzee yeyote katika baraza la wazee kutoa kanuni ya Biblia inayohitajika ili kukabiliana na hali yoyote au kufanya uamuzi muhimu. (Mdo. 15:6-15) Roho takatifu huwasaidia wazee wote wa kutaniko, si mzee mmoja peke yake.”

6. Wazee wa kutaniko wanaweza kufanyaje kazi kwa umoja, na kutaniko linafaidikaje wanapofanya hivyo?

6 Mzee wa kutaniko anayewaheshimu wazee wenzake, hatajaribu siku zote kuzungumza kwanza kwenye mkutano wa wazee. Hatawali mazungumzo na haamini kwamba siku zote maoni yake ndiyo sahihi. Badala yake, anatoa maoni yake kwa unyenyekevu na kuonyesha sifa ya kiasi. Anasikiliza kwa makini maelezo ya wazee wengine. Jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba yuko tayari kushiriki na wengine kanuni za Kimaandiko na kufuata mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Wazee wanapoonyeshana upendo na heshima wanapojadili mambo ya kutaniko, roho takatifu ya Mungu itakuwa pamoja nao, nayo itawaongoza ili wafanye maamuzi yatakayoliimarisha kutaniko.—Yak. 3:17, 18.

WAHESHIMU WAKRISTO AMBAO NI WASEJA

7. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu useja?

7 Leo, kutaniko linatia ndani wenzi wa ndoa na familia zenye watoto. Hata hivyo, linatia ndani pia ndugu na dada wengi ambao hawajafunga ndoa. Tunapaswa kuwaonaje wale ambao ni waseja? Fikiria mtazamo wa Yesu kuhusu useja. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu hakuoa. Alibaki akiwa mseja na kutumia muda wake kukazia fikira mgawo wake. Yesu hakufundisha kamwe kwamba ilikuwa lazima kufunga ndoa ama kubaki mseja. Hata hivyo, alisema kwamba baadhi ya Wakristo wangeamua kutofunga ndoa. (Mt. 19:11, 12) Yesu aliwaheshimu waseja. Hakuwaona waseja kuwa duni au kwamba wamepungukiwa kwa njia fulani.

8. Kulingana na andiko la 1 Wakorintho 7:7-9, Paulo aliwatia moyo Wakristo wafikirie nini?

8 Kama Yesu, mtume Paulo alifanya huduma yake akiwa mseja. Paulo hakufundisha kamwe kwamba lingekuwa kosa kwa Mkristo kufunga ndoa. Alitambua kwamba hilo lilikuwa jambo la kibinafsi. Hata hivyo, Paulo aliwatia moyo Wakristo wafikirie ikiwa wangeweza kumtumikia Yehova wakiwa waseja. (Soma 1 Wakorintho 7:7-9.) Kwa hakika, Paulo hakuwadharau Wakristo waseja. Isitoshe, alimchagua kijana Timotheo, ndugu mseja, kushughulikia migawo mizito. * (Flp. 2:19-22) Hivyo, ni wazi kwamba lingekuwa kosa kufikiri kuwa ndugu ana sifa za kustahili au hana kwa msingi tu wa kwamba amefunga ndoa au la.—1 Kor. 7:32-35, 38.

9. Tunaweza kusema nini kuhusu ndoa na useja?

9 Yesu na Paulo hawakufundisha kwamba ni lazima kwa Mkristo kufunga ndoa ama kubaki mseja. Hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu ndoa na useja? Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 1, 2012, ulieleza jambo hilo kwa njia nzuri uliposema: “Kwa kweli, useja na ndoa unaweza kuonwa kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. . . . Yehova hauoni [useja] kuwa chanzo cha aibu na huzuni.” Tukiwa na hilo akilini, tunahitaji kuheshimu sehemu ya ndugu na dada waseja kutanikoni.

Kwa sababu tunaheshimu hisia za ndugu na dada waseja, tunapaswa kuepuka kufanya nini? (Tazama fungu la 10)

10. Tunaweza kuwaonyeshaje heshima ndugu na dada zetu waseja?

10 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaheshimu hisia na tunaelewa hali za ndugu na dada zetu waseja? Ni vema kukumbuka kwamba baadhi ya Wakristo waseja wamefanya uamuzi wa kibinafsi wa kuendelea kubaki wakiwa waseja. Wakristo wengine waseja wangependa kufunga ndoa, lakini ni kwa sababu tu hawajafanikiwa kumpata mtu anayewafaa. Ilhali wengine huenda wamepoteza wenzi wao katika kifo. Vyovyote vile, je, ingefaa kwa wale walio katika kutaniko kuwauliza Wakristo waseja kwa nini hawajafunga ndoa, au kujitolea kuwasaidia wapate mwenzi? Hapana shaka kwamba huenda baadhi ya Wakristo waseja wakaomba msaada kama huo. Lakini ikiwa hawajaomba msaada huo, ndugu au dada yetu mseja atahisije utakapompendekezea kwamba unataka kumsaidia apate mwenzi? (1 The. 4:11; 1 Tim. 5:13) Acheni tuzungumzie baadhi ya maelezo kutoka kwa ndugu na dada zetu waaminifu walio waseja.

11-12. Huenda tukawavunjaje moyo waseja?

11 Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliye mseja na ambaye ana matokeo mazuri katika mgawo wake anahisi kwamba kuna faida nyingi za kuwa mseja. Hata hivyo alisema kwamba linaweza kuwa jambo lenye kuvunja moyo wakati ndugu na dada ambao hawana nia mbaya wanapomuuliza: “Kwa nini hujaoa?” Ndugu mmoja mseja anayetumikia katika ofisi ya tawi anasema: “Nyakati nyingine ndugu na dada hufanya nihisi kwamba waseja ni watu wa kusikitikiwa. Jambo hilo linaweza kufanya useja uonekane kuwa tatizo badala ya zawadi.”

12 Dada mmoja mseja anayetumikia Betheli alisema hivi: “Baadhi ya wahubiri wanadhani kwamba waseja wote wanatafuta wenzi wa ndoa au kwamba wanaona kila kikusanyiko cha watu kuwa fursa ya kupata mwenzi. Pindi moja niliposafiri kwenda eneo lingine kwa ajili ya mgawo wangu wa Betheli, nilifika siku ya mkutano. Dada aliyekuwa amenikaribisha nyumbani kwake aliniambia kuna ndugu wawili katika kutaniko hilo ambao walikuwa wa umri wangu. Alinihakikishia kwamba hakuwa akijaribu kunisaidia kupata mwenzi. Lakini mara tu tulipoingia ndani ya Jumba la Ufalme alinivuta kando ili nikutane na ndugu hao wawili. Kusema kweli, lilikuwa jambo la kuaibisha kwangu na kwa wale ndugu wawili.”

13. Dada fulani mseja alitiwa moyo na mfano wa nani?

13 Dada mwingine mseja anayetumikia Betheli anasema: “Ninawajua mapainia waseja wenye umri mkubwa ambao wamesawazika, wana malengo hususa, wamejidhabihu, na wameridhika na utumishi wao na ambao wana mchango mkubwa katika kutaniko. Wana maoni yaliyosawazika kuhusu useja wao, hawahisi wao ni bora kwa sababu wamebaki wakiwa waseja, au kwamba wamepungukiwa kwa sababu hawana mwenzi wa ndoa na familia.” Inapendeza sana wakati wote kutanikoni wanapohisi wanaheshimiwa na kuthaminiwa. Hujihisi kuwa unasikitikiwa au kuonewa wivu, wala huhisi kuwa unapuuzwa au kukwezwa. Unahisi ukiwa sehemu ya kutaniko.

14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini waseja?

14 Ndugu na dada zetu waseja watafurahi sana ikiwa tutapima thamani yao kwa msingi wa sifa zao nzuri na si kwa sababu wameoa au kuolewa au la. Badala ya kuwasikitikia, ni vema tukawathamini kwa sababu ya uaminifu wao. Matokeo ni kwamba ndugu na dada zetu waseja hawatahisi kamwe kuwa ni kana kwamba tunawaambia: ‘Hatuwahitaji ninyi.’ (1 Kor. 12:21) Badala yake, watajua kwamba tunawaheshimu na kuthamini sehemu yao katika kutaniko.

WAHESHIMU WALE AMBAO HAWAZUNGUMZI LUGHA YAKO KWA UFASAHA

15. Baadhi ya ndugu na dada wamefanya mabadiliko gani ili kupanua huduma yao?

15 Katika miaka ya karibuni, wahubiri wengi wamejiwekea lengo la kujifunza lugha nyingine ili kupanua huduma yao. Ili kufanya hivyo wanahitaji kufanya mabadiliko fulani. Ndugu na dada hao wamehama makutaniko yao ambayo yanatumia lugha yao ya mama ili kwenda kutumikia katika kutaniko linalotumia lugha nyingine na lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. (Mdo. 16:9) Huo ni uamuzi wa kibinafsi ambao Wakristo hao wanafanya ili kuendeleza masilahi ya Ufalme. Ingawa huenda ikawachukua miaka mingi ili waweze kuzungumza lugha hiyo mpya kwa ufasaha, wanatimiza mambo mengi mazuri. Sifa zao nzuri na uzoefu wao huliimarisha na kulitegemeza kutaniko. Tunawathamini ndugu na dada hao wenye kujidhabihu!

16. Wazee wanapaswa kuzingatia nini wanapochunguza sifa za kustahili kwa akina ndugu kutumikia wakiwa wazee au watumishi wa huduma?

16 Baraza la wazee halipaswi kusita kumpendekeza ndugu kutumikia akiwa mzee au mtumishi wa huduma kwa sababu tu hazungumzi lugha ya kutaniko kwa ufasaha. Wazee watachunguza sifa za ndugu kwa kuzingatia sifa za Kimaandiko kwa ajili ya wazee na watumishi wa huduma, na si jinsi wanavyozungumza lugha ambayo kutaniko linatumia.—1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9.

17. Baadhi ya familia zinakabili changamoto gani zinapohamia nchi nyingine?

17 Baadhi ya familia za Kikristo zimehamia nchi nyingine kwa sababu ya matatizo yaliyo kwenye nchi yao au ili kutafuta ajira. Katika hali kama hizo, huenda watoto wakaenda katika shule zinazotumia lugha kuu ya nchi hiyo. Huenda pia wazazi wakahitaji kujifunza lugha kuu ya nchi hiyo ili kutafuta kazi. Vipi ikiwa kuna kutaniko au kikundi kinachotumia lugha yao ya mama? Je, familia hiyo ihudhurie kutaniko lipi? Je, wahudhurie kutaniko linalotumia lugha kuu ya nchi hiyo au kutaniko linalotumia lugha yao ya mama?

18. Kulingana na Wagalatia 6:5, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaheshimu uamuzi wa kichwa cha familia?

18 Ni lazima kichwa cha familia aamue kutaniko ambalo familia yake itahudhuria. Kwa kuwa hilo ni jambo la kibinafsi, ni lazima afikirie uamuzi ambao utainufaisha familia yake. (Soma Wagalatia 6:5.) Tunapaswa kuheshimu uamuzi wa kichwa cha familia. Acheni tukubali uamuzi wowote atakaofanya na tuikaribishe familia hiyo ikiwa sehemu yenye thamani ya kutaniko letu.—Rom. 15:7.

19. Vichwa vya familia wanapaswa kutafakari kwa makini na kusali kuhusu nini?

19 Katika visa vingine, huenda familia ikatumikia katika kutaniko linalotumia lugha ya mama ya wazazi, lakini huenda watoto wasizungumze kwa ufasaha lugha hiyo. Ikiwa kutaniko liko mahali ambapo lugha kuu ya nchi waliyohamia inazungumzwa, inaweza kuwa changamoto kwa watoto kuelewa mikutano na kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa nini? Kwa sababu huenda watoto wakawa wanahudhuria shule inayotumia lugha kuu ya nchi hiyo na si lugha ya mama ya wazazi wao. Katika visa hivyo, vichwa vya familia wanapaswa kufikiria kwa makini na kusali kuhusu kile wanachohitaji kufanya ili kuwasaidia watoto wao kumkaribia zaidi Yehova na watu wake. Watahitaji kuwasaidia watoto wao wazungumze kwa ufasaha lugha yao ya mama au watahitaji kufikiria kuhamia kutaniko linalotumia lugha ambayo watoto wao wanaelewa vizuri. Haidhuru uamuzi ambao kichwa cha familia atafanya, kutaniko ambalo ataamua kushirikiana nalo linapaswa kumfanya yeye na familia yake wahisi wanaheshimiwa na kuthaminiwa.

Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini wale ambao wanajifunza lugha mpya? (Tazama fungu la 20)

20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawathamini ndugu na dada zetu wanaojifunza lugha mpya?

20 Kutokana na sababu zote ambazo tumezungumzia, katika makutaniko mengi kutakuwa na ndugu na dada ambao wanapambana ili kujifunza lugha mpya. Huenda ikawa vigumu kwao kujieleza. Lakini ikiwa hatutakazia fikira uwezo wao wa kuzungumza lugha mpya, tutaona upendo wao kwa Yehova na tamaa yao ya kumtumikia. Ikiwa tutaona sifa hizo nzuri, tutawathamini na kuwaheshimu sana ndugu na dada hao. Hatutawaambia, ‘Hatuwahitaji ninyi,’ eti kwa sababu hawazungumzi kwa ufasaha lugha yetu.

SISI NI WENYE THAMANI MACHONI PA YEHOVA

21-22. Tuna pendeleo gani zuri sana?

21 Yehova ametupatia pendeleo zuri sana la kuwa na sehemu katika kutaniko lake. Iwe sisi ni wanaume au wanawake, waseja au tumefunga ndoa, vijana au wazee au tunazungumza lugha fulani vizuri au hatuijui hata kidogo, tuna thamani machoni pa Yehova na machoni pa ndugu na dada zetu.—Rom. 12:4, 5; Kol. 3:10, 11.

22 Acheni tuendelee kutumia mambo mengi mazuri ambayo tumejifunza kutokana mfano wa Paulo wa mwili wa mwanadamu. Kwa njia hiyo, tutatafuta fursa nyingi hata zaidi za kuonyesha kwamba tunathamini sehemu yetu na ile ya wengine katika kutaniko la Yehova.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

^ fu. 5 Watu wa Yehova wanatoka katika malezi mbalimbali na wanatimiza sehemu tofauti-tofauti katika kutaniko. Makala hii itatusaidia kuona kwa nini ni muhimu kumheshimu kila mtu katika familia ya Yehova.

^ fu. 8 Hatuwezi kusema kwa hakika kwamba Timotheo hakuoa kamwe.