Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 31

Je, Unangojea “Jiji Lililo na Misingi ya Kweli”?

Je, Unangojea “Jiji Lililo na Misingi ya Kweli”?

“Alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mbuni na mjenzi wake ni Mungu.”​—EBR. 11:10.

WIMBO 22 Ufalme Umesimamishwa​—Na Uje!

MUHTASARI *

1. Ndugu na dada wengi wamedhabihu mambo gani, na kwa nini?

LEO, mamilioni ya watu wa Mungu wamejidhabihu sana. Ndugu na dada wengi wameamua kubaki waseja. Wenzi wa ndoa wameahirisha kupata watoto. Familia zimerahisisha maisha yao. Wote hao wamefanya uamuzi huo kwa sababu moja muhimu—wanataka kufanya yote wawezayo ili kumtumikia Yehova kikamili. Wameridhika na wana uhakika kwamba Yehova atawaandalia vitu vyote ambavyo kwa kweli wanahitaji. Je, watatamaushwa? Hapana! Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo? Sababu moja ni kwamba Yehova alimbariki Abrahamu, “baba ya wale wote walio na imani.”—Rom. 4:11.

2. (a) Kulingana na Waebrania 11:8-10, 16, kwa nini Abrahamu alikuwa tayari kuondoka Uru? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Kwa hiari Abrahamu aliacha maisha mazuri aliyokuwa nayo katika jiji la Uru. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa akingojea “jiji lililo na misingi ya kweli.” (Soma Waebrania 11:8-10, 16.) Ni “jiji” gani hilo? Abrahamu alikabili changamoto gani alipokuwa akingojea jiji hilo lijengwe? Na tunaweza kumwigaje Abrahamu na wale wote katika siku zetu ambao wamefuata mfano wake?

“JIJI LILILO NA MISINGI YA KWELI” NI NINI?

3. Abrahamu alikuwa akingojea “jiji” gani?

3 Jiji ambalo Abrahamu alikuwa akingojea ni Ufalme wa Mungu. Ufalme huo unafanyizwa na Yesu Kristo, pamoja na Wakristo watiwa-mafuta 144,000. Paulo anauita Ufalme huo, “jiji la Mungu aliye hai, yaani, Yerusalemu la mbinguni.” (Ebr. 12:22; Ufu. 5:8-10; 14:1) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali kuhusu Ufalme huo, wakiomba kwamba uje ili mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.—Mt. 6:10.

4. Kulingana na Mwanzo 17:1, 2, 6, Abrahamu alijua mambo gani kuhusu jiji, au Ufalme ambao Mungu alikuwa ameahidi?

4 Je, Abrahamu alijua jinsi ambavyo Ufalme wa Mungu ungepangwa? Hapana. Kwa karne nyingi, habari kuhusu Ufalme zilikuwa “siri takatifu.” (Efe. 1:8-10; Kol. 1:26, 27) Lakini Abrahamu alijua kwamba baadhi ya wazao wake wangekuwa wafalme. Yehova alikuwa amempa ahadi hiyo kihususa. (Soma Mwanzo 17:1, 2, 6.) Abrahamu alikuwa na imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu, hivi kwamba ni kana kwamba alikuwa akimwona Mtiwa-Mafuta au Masihi ambaye angekuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, Yesu aliweza kuwaambia hivi Wayahudi katika siku zake: “Baba yenu Abrahamu alishangilia sana tazamio la kuona siku yangu, naye aliiona na kushangilia.” (Yoh. 8:56) Ni wazi kwamba Abrahamu alijua kuwa wazao wake wangefanyiza Ufalme ambao ungesimamishwa na Yehova, naye alikuwa tayari kumngojea Yehova atimize ahadi hiyo.

Abrahamu alionyeshaje imani katika ahadi za Yehova? (Tazama fungu la 5)

5. Tunajuaje kwamba Abrahamu alikuwa akingojea “jiji” ambalo mbuni wake ni Mungu?

5 Abrahamu alionyeshaje kwamba alikuwa akingojea Ufalme, au “jiji,” ambalo mbuni wake ni Mungu? Kwanza, Abrahamu hakuwa raia wa ufalme wowote hapa duniani. Alikuwa akihama-hama kutoka eneo moja kwenda lingine, hakuwa na eneo la kudumu la kuishi na hakumuunga mkono mfalme yeyote wa kibinadamu. Kwa kuongezea, Abrahamu hakuamua kuanzisha ufalme wake mwenyewe. Badala yake aliendelea kumtii Yehova, akimngojea atimize ahadi Yake. Kwa kufanya hivyo, Abrahamu alionyesha imani ya pekee katika Yehova. Acheni tuchunguze baadhi ya changamoto alizokabili na tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wake mzuri.

ABRAHAMU ALIKABILI CHANGAMOTO GANI?

6. Uru lilikuwa jiji la aina gani?

6 Jiji ambalo Abrahamu aliondoka lilikuwa salama na lenye kustarehesha. Jiji hilo lililindwa kwa kuta kubwa na handaki la maji lililozunguka pande tatu. Watu wa Uru walikuwa stadi katika uandishi na hesabu. Inaelekea jiji hilo lilikuwa kituo cha biashara; hati nyingi za biashara zimevumbuliwa katika eneo hilo. Nyumba za kibinafsi zilijengwa kwa matofali, kisha kuta zilipigwa lipu na kupakwa chokaa. Baadhi ya nyumba hizo zilikuwa na vyumba 13 au 14 vilivyozunguka ua uliosakafiwa kwa mawe.

7. Kwa nini Abrahamu alihitaji kuwa na hakika kwamba Yehova angemlinda yeye na familia yake?

7 Abrahamu alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemlinda yeye na familia yake. Kwa nini? Kumbuka kwamba Abrahamu na Sara walipoondoka jiji la Uru waliacha nyumba yenye usalama na yenye kustarehesha ili wakaishi kwenye mahema kwenye eneo la wazi katika nchi ya Kanaani. Abrahamu pamoja na familia yake hawakuwa wakilindwa tena na ukuta mkubwa na handaki la maji lenye kina kirefu. Sasa hawakuwa na ulinzi dhidi ya mashambulizi ya maadui.

8. Pindi moja Abrahamu alilazimika kukabiliana na nini?

8 Abrahamu alifanya mapenzi ya Mungu, lakini pindi moja hakuwa na chakula cha kutosha kwa ajili ya familia yake. Abrahamu alihitaji kukabiliana na njaa kali iliyopiga nchi ileile ambayo Yehova alikuwa amemtuma. Njaa hiyo ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Abrahamu aliamua kuhamisha familia yake kwa muda kwenda Misri. Hata hivyo alipokuwa Misri, Farao, mtawala wa nchi hiyo alimchukua mke wake. Wazia wasiwasi ambao lazima Abrahamu alikuwa nao hadi Farao alipomrudisha Sara kwa Abrahamu kwa mwongozo wa Yehova.—Mwa. 12:10-19.

9. Abrahamu alihitaji kukabiliana na changamoto gani za kifamilia?

9 Maisha ya familia ya Abrahamu yalikuwa magumu. Sara, mke wake mpendwa, hakuweza kupata watoto. Kwa miaka mingi walihitaji kukabiliana na hali hiyo yenye kuumiza. Mwishowe, Sara akamchukua Hagari, mtumishi wake, na kumpa Abrahamu ili awazalie Abrahamu na Sara watoto. Lakini Hagari alipopata mimba ya Ishmaeli, alianza kumdharau Sara. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Sara alimfukuza Hagari.—Mwa. 16:1-6.

10. Ni mambo gani yaliyomhusisha Ishmaeli na Isaka yaliyojaribu imani ya Abrahamu kumwelekea Yehova?

10 Hatimaye Sara alipata mimba na kumzalia Abrahamu mwana ambaye alimwita Isaka. Abrahamu aliwapenda wana wake wote wawili, Ishmaeli na Isaka. Lakini kwa sababu Ishmaeli alimtendea kwa njia mbaya Isaka, Abrahamu alilazimika kuwafukuza Ishmaeli na Hagari. (Mwa. 21:9-14) Baadaye, Yehova alimwomba Abrahamu amtoe Isaka kuwa dhabihu. (Mwa. 22:1, 2; Ebr. 11:17-19) Katika pindi hizo zote, Abrahamu alihitaji kuwa na uhakika kwamba mwishowe Yehova angetimiza ahadi yake kuhusu wana wake.

11. Kwa nini Abrahamu alihitaji kumngojea Yehova kwa subira?

11 Katika kipindi hicho chote Abrahamu alihitaji kujifunza kumngojea Yehova kwa subira. Inaelekea alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 70 alipoondoka Uru pamoja na familia yake. (Mwa. 11:31–12:4) Na kwa miaka mia moja hivi, aliishi kwenye mahema, akihama-hama katika nchi ya Kanaani. Abrahamu alikufa akiwa na umri wa miaka 175. (Mwa. 25:7) Lakini hakuona utimizo wa ahadi ya Yehova ya kuwapa wazao wake nchi aliyokuwa akiishi. Na hakuishi vya kutosha kuliona lile jiji, yaani, Ufalme wa Mungu ukisimamishwa. Hata hivyo, Abrahamu anafafanuliwa kuwa alikufa “akiwa amezeeka na kuridhika.” (Mwa. 25:8) Licha ya changamoto zote alizokabiliana nazo, Abrahamu aliendelea kuwa na imani yenye nguvu na aliridhika kumngojea Yehova. Kwa nini aliweza kuvumilia? Kwa sababu katika maisha yote ya Abrahamu, Yehova alimlinda na kumtendea kama rafiki.—Mwa. 15:1; Isa. 41:8; Yak. 2:22, 23.

Kama Abrahamu na Sara, watumishi wa Mungu wanaonyeshaje imani na subira? (Tazama fungu la 12) *

12. Tunangojea nini, na tutachunguza nini?

12 Kama Abrahamu, tunangojea jiji lililo na misingi ya kweli. Hata hivyo, hatungoji lijengwe. Ufalme wa Mungu ulisimamishwa mwaka wa 1914 na tayari unatawala kikamili mbinguni. (Ufu. 12:7-10) Lakini tunangojea ufalme huo utawale dunia yote. Tunapongojea hilo litokee kuna hali nyingi tunazokabiliana nazo ambazo zinafanana na zile ambazo Abrahamu na Sara walikabiliana nazo. Je, watumishi wa Yehova wa siku zetu wamefaulu kuiga mfano wa Abrahamu? Masimulizi ya maisha yanayochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi yanaonyesha kwamba kama Abrahamu na Sara, ndugu na dada wengi leo wanaonyesha subira. Acheni tuchunguze masimulizi machache kati ya hayo, na tuone mambo tunayoweza kujifunza.

WALIIGA MFANO WA ABRAHAMU

Bill Walden alikuwa tayari kujidhabihu, naye alijionea baraka za Yehova

13. Unajifunza nini kutokana na simulizi la Ndugu Walden?

13 Uwe tayari kujidhabihu. Ikiwa tunataka jiji la Mungu, yaani, Ufalme, uwe jambo muhimu zaidi maishani mwetu lazima tuwe kama Abrahamu, ambaye kwa hiari alijidhabihu ili kumpendeza Mungu. (Mt. 6:33; Marko 10:28-30) Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Bill Walden. * Katika mwaka wa 1942, Bill alipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alikuwa ahitimu kutoka chuo fulani nchini Marekani alichokuwa akisoma shahada ya uhandisi wa majengo. Profesa aliyekuwa anamfundisha Bill alikuwa amemtafutia kazi ambayo angefanya baada ya kuhitimu, lakini Bill aliikataa. Alimwambia kwamba ameamua kumtumikia Mungu kikamili zaidi badala ya kufanya kazi yenye mshahara mnono. Muda mfupi baadaye, Bill aliandikishwa katika utumishi wa kijeshi. Alikataa kwa heshima na matokeo yake alipigwa faini ya dola 10,000 za Marekani na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani. Aliachiliwa huru baada ya miaka mitatu. Baadaye, alialikwa kuhudhuria shule ya Gileadi, na alitumikia akiwa mmishonari barani Afrika. Kisha, Bill alimwoa Eva, nao wakatumikia pamoja barani Afrika, jambo ambalo lilihitaji kujidhabihu. Mwishowe, walirudi Marekani ili kumtunza mama ya Bill. Bill anamalizia hivi simulizi lake la maisha: “Machozi hunitoka ninapofikiria pendeleo kubwa la kumtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 70. Mara kwa mara ninamshukuru kwa kuniongoza katika utumishi wake.” Je, unaweza kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi kuu maishani mwako?

Eleni na Aristotelis Apostolidis walihisi kwamba Yehova aliwaimarisha

14-15. Unajifunza nini kutokana na simulizi la Ndugu na Dada Apostolidis?

14 Usitarajie kwamba hutakuwa na matatizo maishani. Mfano wa Abrahamu unatufundisha kwamba hata wale wanaotoa maisha yao yote ili kumtumikia Yehova lazima watakabili matatizo. (Yak. 1:2; 1 Pet. 5:9) Fikiria jinsi jambo hilo lilivyothibitika kuwa kweli katika kisa cha Aristotelis Apostolidis. * Alibatizwa mwaka wa 1946 nchini Ugiriki, na mwaka wa 1952 alimchumbia dada aliyeitwa Eleni, aliyekuwa na malengo kama yake. Hata hivyo, Eleni akawa mgonjwa na iligunduliwa kwamba alikuwa na uvimbe kwenye ubongo. Uvimbe uliondolewa, lakini miaka michache baada ya kufunga ndoa, uvimbe ulirudi. Madaktari walimfanyia upasuaji mwingine, lakini Eleni aliachwa akiwa amepooza sehemu fulani ya mwili na hangeweza kuzungumza vizuri. Aliendelea kuwa mhudumu mwenye bidii licha ya ugonjwa wake na mateso ya serikali wakati huo.

15 Aristotelis alimtunza mke wake kwa miaka 30. Katika kipindi hicho alitumikia akiwa mzee, katika halmashauri ya kusanyiko, na alisaidia katika ujenzi wa Jumba la Kusanyiko. Kisha katika mwaka wa 1987, Eleni alipata aksidenti na kuumia alipokuwa akihubiri. Alipoteza fahamu kwa miaka mitatu, na kisha akafa. Aristotelis anamalizia simulizi lake kwa kusema: “Katika miaka iliyopita, nimejitahidi kuwa na nguvu na ustahimilivu usio wa kawaida kwa sababu ya hali ngumu, matatizo na matukio yasiyotazamiwa. Hata hivyo, sikuzote Yehova amenipa nguvu ninazohitaji ili kushinda matatizo hayo.” (Zab. 94:18, 19) Yehova anawapenda sana wale wanaofanya yote wanayoweza kwa ajili yake licha ya majaribu!

Audrey Hyde aliendelea kuwa na mtazamo mzuri kwa kukazia fikira wakati ujao

16. Ndugu Knorr alimpa mke wake ushauri gani mzuri?

16 Kazia fikira wakati ujao. Abrahamu alikazia fikira thawabu za wakati ujao ambazo Yehova angempa na hilo lilimsaidia kushinda changamoto alizokabili wakati huo. Dada Audrey Hyde alijitahidi kuwa na mtazamo huohuo mzuri, ingawa mume wake Nathan H. Knorr, alikufa kwa kansa na mume wake wa pili, Glen Hyde, alipata ugonjwa unaoathiri ubongo, unaoitwa Alzheimer’s. * Dada huyo anaeleza kwamba jambo ambalo Ndugu Knorr alimwambia majuma machache kabla ya kifo chake, lilimsaidia sana. Anasema hivi: “Nathan alinikumbusha: ‘Baada ya kifo, tumaini letu huwa hakika, na hatutateseka tena.’ Kisha akanisihi: ‘Kaza macho mbele kwani huko ndiko kuna thawabu yako.’ . . . Akaongeza: ‘Uwe na mengi ya kufanya, yaani, jaribu kutumia maisha yako kufanya jambo fulani kwa ajili ya wengine. Hilo litakufanya uishi kwa furaha.’” Ni ushauri mzuri sana kuendelea kuwa na mengi ya kufanya kwa kuwatendea wengine mema na ‘kushangilia katika tumaini’!—Rom. 12:12.

17. (a) Kwa nini tuna sababu nzuri ya kazia fikira wakati ujao? (b) Kufuata maneno ya Mika 7:7 kutatusaidiaje kufurahia baraka za wakati ujao?

17 Leo, kuliko wakati mwingine wowote, tuna sababu kubwa ya kukazia fikira wakati ujao. Matukio ya ulimwengu yanaonyesha wazi kwamba tunaishi katika kipindi cha mwisho cha siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Hivi karibuni, hatutahitaji kulingojea jiji lenye misingi ya kweli, kuutawala kikamili ulimwengu wote. Miongoni mwa baraka nyingi tutakazofurahia ni kuwaona wapendwa wetu watakaofufuliwa. Wakati huo, Yehova atamthawabisha Abrahamu kwa kumfufua yeye na familia yake kwa sababu ya imani na subira yake. Je, utakuwepo wakati huo ili kuwakaribisha? Unaweza kuwepo ikiwa, kama Abrahamu, utakuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, ikiwa utaendelea kuwa na amani licha ya matatizo, na ikiwa utajifunza kumngojea Yehova kwa subira.—Soma Mika 7:7.

WIMBO 74 Shiriki Kuimba Wimbo wa Ufalme!

^ fu. 5 Kusubiri utimizo wa ahadi kunaweza kujaribu subira yetu na nyakati nyingine imani yetu. Tunaweza kujifunza mambo gani kutoka kwa Abrahamu ambayo yanaweza kuimarisha azimio letu la kungojea kwa subira utimizo wa ahadi za Yehova? Na baadhi ya watumishi wa Yehova wa siku zetu wametuwekea mfano gani mzuri?

^ fu. 13 Simulizi la maisha la Ndugu Walden limechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 2013, ukurasa wa 8-10.

^ fu. 14 Simulizi la maisha la Ndugu Apostolidis limechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2002, ukurasa wa 24-28.

^ fu. 16 Simulizi la maisha la Dada Hyde limechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2004, ukurasa wa 23-29.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa wakiendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu licha ya changamoto. Wanaendelea kuimarisha imani yao kwa kukazia fikira ahadi za Yehova za wakati ujao.