Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 32

Tembea kwa Unyenyekevu na kwa Kiasi na Mungu Wako

Tembea kwa Unyenyekevu na kwa Kiasi na Mungu Wako

“Utembee kwa kiasi na Mungu wako!”—MIKA 6:8.

WIMBO 31 Tembea Pamoja na Mungu!

MUHTASARI *

1. Daudi alisema nini kuhusu unyenyekevu wa Yehova?

JE, KWELI tunaweza kusema kwamba Yehova ni mnyenyekevu? Ndiyo, tunaweza. Daudi aliandika hivi: “Wewe hunipa ngao yako ya wokovu, na unyenyekevu wako hunifanya niwe mkuu.” (2 Sam. 22:36; Zab. 18:35) Huenda Daudi alikuwa akifikiria siku ambayo nabii Samweli alienda katika nyumba ya baba ya Daudi kumtia mafuta mfalme wa Israeli ambaye angefuata. Daudi alikuwa mwenye umri mdogo zaidi kati ya wavulana nane, hata hivyo, yeye ndiye aliyechaguliwa na Yehova kuchukua nafasi ya Mfalme Sauli.—1 Sam. 16:1, 10-13.

2. Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Bila shaka, Daudi angekubaliana na maneno yafuatayo yaliyosemwa na mtunga zaburi kumhusu Yehova: “Huinama chini ili atazame mbingu na dunia, akimwinua mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini. Humwinua juu maskini . . . ili amketishe pamoja na viongozi.” (Zab. 113:6-8) Katika makala hii, kwanza tutazungumzia baadhi ya mambo tunayojifunza kuhusu unyenyekevu kwa kuchunguza pindi ambazo Yehova alionyesha sifa hiyo. Kisha, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kuhusu sifa ya kiasi kutoka kwa Mfalme Sauli, nabii Danieli, na Yesu.

TUNAWEZA KUJIFUNZA NINI KUTOKA KWA YEHOVA?

3. Yehova anashughulika nasi jinsi gani, na hilo linathibitisha nini?

3 Yehova anathibitisha kwamba yeye ni mnyenyekevu kwa jinsi anavyoshughulika na wanadamu wasio wakamilifu. Hakubali tu ibada yetu, bali pia anatuona kuwa rafiki zake. (Zab. 25:14) Ili tuweze kuwa marafiki wake, Yehova alichukua hatua ya kwanza kwa kumtoa Mwana wake kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu. Kwa kweli, Yehova ametuonyesha rehema na huruma ya pekee sana!

4. Yehova ametupatia nini, na kwa nini?

4 Fikiria njia nyingine inayoonyesha kwamba Yehova ni mnyenyekevu. Akiwa Muumba, Yehova angeweza kutuumba bila uwezo wa kuchagua maisha tunayopenda kuishi. Lakini hakufanya hivyo. Alituumba kwa mfano wake na kutupatia uhuru wa kuchagua. Anataka sisi wanadamu wa hali ya chini tumtumikie kutoka moyoni kwa sababu tunampenda na tunatambua faida za kumtii yeye. (Kum. 10:12; Isa. 48:17, 18) Tunathamini sana kwamba Yehova ni mnyenyekevu!

Yesu anaonyeshwa akiwa mbinguni. Waliosimama kando yake ni baadhi ya watawala wenzake. Kwa pamoja wanatazama kundi kubwa la malaika. Baadhi ya malaika wanashuka duniani kwenda kutekeleza migawo yao. Yehova amewakabidhi majukumu wote walioonyeshwa kwenye picha (Tazama fungu la 5)

5. Yehova anatufundishaje kuwa wanyenyekevu? (Tazama picha kwenye jalada.)

5 Yehova anatufundisha tuwe wanyenyekevu kwa jinsi anavyoshughulika nasi. Yehova ndiye Mtu mwenye hekima zaidi katika ulimwengu wote. Ingawa hivyo, yuko tayari kukubali mapendekezo kutoka kwa wengine. Kwa mfano, Yehova alimruhusu mwana wake amsaidie alipokuwa akiumba vitu vyote. (Met. 8:27-30; Kol. 1:15, 16) Ingawa Yehova ni Mweza-Yote, anawapa wengine majukumu mbalimbali. Kwa mfano, amemweka rasmi Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme, Naye atawapatia mamlaka ya kadiri wale wanadamu 144,000 ambao watakuwa watawala pamoja na Yesu. (Luka 12:32) Hapana shaka, Yehova alimzoeza Yesu kuwa Mfalme na Kuhani Mkuu. (Ebr. 5:8, 9) Pia, anawazoeza wale watakaotawala pamoja na Yesu, lakini hawapatii mgawo huo na kisha kuingilia kila jambo dogo wanalofanya. Badala yake, anaamini kwamba watafanya mapenzi yake.—Ufu. 5:10.

Tunaweza kumwiga Yehova tunapowazoeza wengine na kuwapa majukumu (Tazama fungu la 6 na 7) *

6-7. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni inapohusu kuwapatia wengine majukumu?

6 Ikiwa Baba yetu wa mbinguni—ambaye hahitaji msaada kutoka kwa wengine—anawapatia wengine majukumu, sembuse sisi! Kwa mfano, je, wewe ni kichwa cha familia au mzee kutanikoni? Iga mfano wa Yehova kwa kuwapa wengine majukumu na kisha kutoingilia au kufuatilia kila jambo dogo wanalofanya. Unapomwiga Yehova, hautatimiza tu kazi unayotaka kufanya, bali pia utawazoeza wengine na kuwasaidia wajiamini zaidi. (Isa. 41:10) Wale waliopewa mamlaka ya kadiri, wanaweza kujifunza jambo gani lingine kutoka kwa Yehova?

7 Biblia inaonyesha kwamba Yehova anapendezwa na maoni ya wana wake wa mbinguni. (1 Fal. 22:19-22) Wazazi, mnaweza kuigaje mfano wa Yehova? Inapofaa, waulizeni watoto wenu maoni yao kuhusu jinsi kazi fulani inavyoweza kufanywa. Na hali zinaporuhusu, fuateni mapendekezo yao.

8. Yehova aliwaonyeshaje subira Abrahamu na Sara?

8 Pia, Yehova anaonyesha unyenyekevu wake kupitia subira yake. Kwa mfano, Yehova anawaonyesha subira watumishi wake wanapomuuliza maswali kwa heshima kuhusu maamuzi fulani aliyofanya. Alimsikiliza Abrahamu alipokuwa akieleza hangaiko lake kuhusu uamuzi wa Yehova wa kuangamiza Sodoma na Gomora. (Mwa. 18:22-33) Na kumbuka jinsi Yehova alivyoshughulika na Sara, mke wa Abrahamu. Hakukwazika au kukasirika Sara alipocheka aliposikia ahadi yake kwamba angepata mimba katika umri wake wa uzeeni. (Mwa. 18:10-14) Badala yake, alimtendea kwa heshima.

9. Wazazi na wazee wa makutaniko wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova?

9 Enyi wazazi na wazee wa makutaniko, mnaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova? Fikiria jinsi unavyoitikia wakati wale walio chini ya mamlaka yako hawakubaliani na maamuzi yako. Je, jambo la kwanza unalofanya ni kuwasahihisha? Au, je, unajitahidi kuelewa maoni yao? Kwa hakika, familia na makutaniko yanafaidika wakati wale walio na mamlaka wanamwiga Yehova. Kufikia hapa, tumezungumzia mambo tunayoweza kujifunza kuhusu unyenyekevu kutoka kwa Yehova. Sasa, acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kuhusu sifa ya kiasi kutokana na mifano iliyoandikwa katika Neno la Mungu.

TUNAWEZA KUJIFUNZA NINI KUTOKA KWA WENGINE?

10. Yehova anatumiaje mifano ya wengine ili kutufundisha?

10 Akiwa ‘Mfundishaji wetu Mkuu,’ Yehova ametuandalia mifano katika Neno lake ili kutufundisha. (Isa. 30:20, 21) Tunajifunza tunapotafakari masimulizi ya Biblia kuhusu wale walioonyesha sifa zinazompendeza Mungu kutia ndani sifa ya kiasi. Pia, tunajifunza tunapochunguza mambo yaliyowapata wale walioshindwa kuonyesha sifa hizo nzuri.—Zab. 37:37; 1 Kor. 10:11.

11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano mbaya wa Sauli?

11 Fikiria kuhusu mambo yaliyompata Mfalme Sauli. Mwanzoni alikuwa kijana mwenye sifa ya kiasi. Alikuwa anatambua mipaka yake na hata alisita kukubali majukumu zaidi. (1 Sam. 9:21; 10:20-22) Hata hivyo, baadaye Sauli alianza kuwa na kimbelembele. Alianza kuonyesha sifa hiyo mbaya punde tu baada ya kuwa Mfalme. Pindi moja, alikosa subira alipokuwa akimngojea nabii Samweli. Badala ya kuonyesha sifa ya kiasi na kuwa na uhakika kwamba Yehova angetenda kwa niaba ya watu wake, Sauli alitoa dhabihu ya kuteketezwa ingawa hakuwa na mamlaka ya kufanya hivyo. Matokeo ni kwamba Sauli alipoteza kibali cha Yehova na mwishowe ufalme. (1 Sam. 13:8-14) Tutakuwa wenye hekima ikiwa tutajifunza kutokana na mfano huo wa kuonya na kuepuka kutenda kwa kimbelembele.

12. Danieli alionyeshaje sifa ya kiasi?

12 Tofauti na mfano mbaya wa Sauli, fikiria mfano mzuri wa nabii Danieli. Katika maisha yake yote, Danieli aliendelea kuwa mtumishi wa Mungu mnyenyekevu na mwenye kiasi ambaye sikuzote alitafuta mwongozo wa Yehova. Kwa mfano, Yehova alipomtumia kufafanua ndoto ya Nebukadneza, Danieli hakudai kwamba alifafanua ndoto hiyo kwa uwezo wake. Badala yake, alionyesha sifa ya unyenyekevu na kiasi kwa kumpa utukufu Yehova. (Dan. 2:26-28) Tunajifunza nini? Ikiwa akina ndugu wanafurahia kusikiliza hotuba zetu au tunapata matokeo mazuri katika huduma, tunapaswa kukumbuka kumpa utukufu wote Yehova. Tunapaswa kutambua kwamba hatungefaulu kufanya mambo hayo bila msaada wa Yehova. (Flp. 4:13) Tunapokuwa na mtazamo huo, tunaiga mfano mzuri wa Yesu. Jinsi gani?

13. Tunajifunza nini kuhusu sifa ya kiasi kutokana na maneno ya Yesu kwenye Yohana 5:19, 30?

13 Ingawa alikuwa mwana mkamilifu wa Mungu, Yesu alimtegemea Yehova. (Soma Yohana 5:19, 30.) Kamwe, hakujaribu kumnyang’anya Baba yake wa mbinguni mamlaka. Wafilipi 2:6 inatuambia kwamba Yesu “hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.” Akiwa mwana anayejitiisha, Yesu alitambua mipaka yake na aliheshimu mamlaka ya Baba yake.

Yesu alijua na kuheshimu mipaka ya mamlaka yake (Tazama fungu la 14)

14. Yesu alitendaje alipoombwa kufanya jambo ambalo hakuwa na mamlaka nalo?

14 Fikiria jinsi ambavyo Yesu aliitikia wakati Yakobo, Yohana, pamoja na mama yao walipomwendea Yesu na kumwomba awapatie pendeleo ambalo hakuwa na mamlaka ya kutoa. Bila kusita, Yesu alisema kwamba Baba yake wa mbinguni tu ndiye anayeweza kuamua ni nani atakayeketi upande wake wa kuume na upande wake wa kushoto katika Ufalme. (Mt. 20:20-23) Yesu alionyesha kwamba alitambua mipaka yake. Alikuwa mwenye kiasi. Kamwe hakufanya mambo ambayo Yehova hakumwamuru afanye. (Yoh. 12:49) Tunaweza kuigaje mfano mzuri wa Yesu?

Tunaweza kuigaje mfano wa Yesu wa kuonyesha sifa ya kiasi? (Tazama fungu la 15 na 16) *

15-16. Tunaweza kutumiaje shauri la Biblia linalopatikana katika 1 Wakorintho 4:6?

15 Tunaweza kuiga mfano wa Yesu wa kuwa na sifa ya kiasi kwa kutumia shauri la Biblia linalopatikana katika 1 Wakorintho 4:6. Hapo tunaambiwa hivi: “Msipite mambo yaliyoandikwa.” Hivyo, tunapoombwa ushauri, tusingependa kamwe kusisitiza maoni yetu au kusema tu jambo la kwanza linalokuja akilini mwetu. Badala yake, tunapaswa kufuata shauri linalopatikana katika Biblia au machapisho yetu yanayotegemea Biblia. Kwa njia hiyo, tunaonyesha kwamba tunatambua mipaka yetu. Tukiwa na sifa ya kiasi tutazisifu ‘amri za uadilifu’ za Mweza-Yote.—Ufu. 15:3, 4.

16 Zaidi ya kumheshimu Yehova, tuna sababu nyingine nzuri za kuonyesha sifa ya kiasi. Sasa tutaona jinsi sifa ya unyenyekevu na ya kiasi zinavyoweza kutuletea shangwe na kutusaidia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine.

JINSI TUNAVYONUFAIKA KWA KUWA WANYENYEKEVU NA WENYE KIASI

17. Kwa nini watu wanyenyekevu na wenye kiasi wana shangwe?

17 Tunapokuwa wanyenyekevu na wenye kiasi kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba tutakuwa wenye shangwe. Kwa nini? Tunapotambua mipaka yetu, tutathamini na kufurahia msaada wowote tunaopata kutoka kwa wengine. Kwa mfano, fikiria wakati Yesu alipowaponya watu kumi wenye ukoma. Ni mmoja tu kati yao aliyerudi kumshukuru Yesu kwa kumponya ugonjwa huo mbaya sana, jambo ambalo mtu huyo hangeweza kamwe kufanya yeye mwenyewe. Mwanamume huyo mnyenyekevu na mwenye sifa ya kiasi alishukuru kwa msaada aliopata na alimtukuza Mungu kwa jambo hilo.—Luka 17:11-19.

18. Unyenyekevu na sifa ya kiasi hutusaidiaje kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine? (Waroma 12:10)

18 Kwa kawaida, watu wanyenyekevu na wenye kiasi wana uhusiano mzuri na wengine na wana uwezekano mkubwa wa kuwa na marafiki wa karibu. Kwa nini? Wako tayari kukubali kwamba wengine wana sifa nzuri na wanawatumaini. Watu wanyenyekevu na wenye kiasi wanafurahi wengine wanapofanikiwa katika migawo yoyote wanayopata na wako tayari kuwapongeza na kuwaonyesha heshima.—Soma Waroma 12:10.

19. Kwa nini tunapaswa kuepuka kiburi?

19 Tofauti na hilo, watu wenye kiburi huona ni vigumu kuwapongeza wengine na wanapendelea zaidi kupongezwa wao wenyewe. Wana mwelekeo mkubwa zaidi wa kujilinganisha na wengine na kuchochea roho ya mashindano. Badala ya kuwazoeza wengine na kuwapa majukumu, wanapendelea kusema, “Ukitaka jambo lifanywe kwa njia iliyo sahihi,” yaani, njia inayowapendeza wao, “unapaswa kulifanya mwenyewe.” Mara nyingi mtu mwenye kiburi anapenda makuu na ni mwenye wivu. (Gal. 5:26) Ni vigumu kwa watu wa namna hiyo kuwa na urafiki wa kudumu. Ikiwa tutagundua kwamba tuna tatizo la kuwa wenye kiburi, tunapaswa kusali kwa unyoofu kwa Yehova ili atusaidie kufanya upya akili yetu, ili sifa hiyo mbaya isikite mizizi ndani ya moyo wetu.—Rom. 12:2.

20. Kwa nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye sifa ya kiasi?

20 Tunamshukuru sana Yehova kwa kutuwekea mfano mzuri! Tunaona unyenyekevu wake kupitia jinsi anavyoshughulika na watumishi wake na tungependa kumwiga. Pia, tungependa kuiga mifano mizuri inayopatikana katika Biblia ya watu wenye sifa ya kiasi ambao walikuwa na pendeleo la kutembea pamoja na Mungu. Acheni sikuzote tumheshimu Yehova na kumpa utukufu anaostahili. (Ufu. 4:11) Kisha, sisi pia tutastahili kutembea pamoja na Baba yetu wa mbinguni ambaye anawapenda watu wanyenyekevu na wenye sifa ya kiasi.

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi kwa Ushikamanifu

^ fu. 5 Mtu mnyenyekevu ni mwenye rehema na huruma. Hivyo, kwa usahihi tunaweza kusema Yehova ni mnyenyekevu. Kama makala hii itakavyoonyesha, tunaweza kujifunza unyenyekevu kutokana na mfano wa Yehova. Pia, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kuhusu sifa ya kiasi kutoka kwa Mfalme Sauli, nabii Danieli, na Yesu.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Mzee wa kutaniko anatumia muda wake kumzoeza ndugu kijana kushughulikia maeneo ya kutaniko. Baadaye, mzee huyo haingilii kazi ya ndugu huyo kijana, bali anamruhusu atimize mgawo wake yeye mwenyewe.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Dada anamuuliza mzee ikiwa itafaa kukubali mwaliko wa kuhudhuria ndoa itakayofungwa kanisani. Mzee huyo hatoi maoni yake, bali anapitia pamoja naye baadhi ya kanuni za Biblia.