Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 33

Ufufuo Unafunua Upendo, Hekima, na Subira ya Mungu

Ufufuo Unafunua Upendo, Hekima, na Subira ya Mungu

“Kutakuwa na ufufuo.”—MDO. 24:15.

WIMBO 151 Ataita

MUHTASARI *

1. Kwa nini Yehova alianza kazi ya uumbaji?

KULIKUWA na wakati ambapo Yehova alikuwa peke yake. Lakini hakuwa mpweke. Alikuwa amekamilika katika kila njia. Lakini Mungu alitaka wengine wafurahie maisha. Akichochewa na upendo, Yehova alianza kazi ya uumbaji.—Zab. 36:9; 1 Yoh. 4:19.

2. Yesu na malaika walihisije kuhusu kazi za uumbaji za Yehova?

2 Kwanza, Yehova alimuumba mfanyakazi mwenzake. Kisha, “vitu vingine vyote viliumbwa” kupitia mwana wake wa kwanza, kutia ndani mamilioni ya malaika. (Kol. 1:16) Yesu alishangilia kupata fursa ya kufanya kazi pamoja na Baba yake. (Met. 8:30) Pia, wana wa kiroho wa Mungu walikuwa na sababu ya kushangilia. Walikuwa wakitazama wakati Yehova, pamoja na Yesu, mfanyakazi wake stadi, walipofanyiza mbingu na dunia. Malaika waliitikiaje? ‘Walianza kushangilia kwa sauti’ dunia ilipokuwa ikiumbwa, na bila shaka, waliendelea kushangilia kila kazi ya uumbaji ya Yehova kutia ndani kazi yake bora ya mwisho, yaani, wanadamu. (Ayu. 38:7; Met. 8:31) Uumbaji wote wa Yehova unafunua upendo na hekima yake.—Zab. 104:24; Rom. 1:20.

3. Kama inavyotajwa kwenye 1 Wakorintho 15:21, 22, dhabihu ya fidia ya Yesu inafanya jambo gani liwezekane?

3 Yehova alikusudia wanadamu wafurahie uzima wa milele katika sayari maridadi aliyokuwa ameumba. Lakini Adamu na Hawa walipomwasi Baba yao mwenye upendo, dhambi na kifo vikaenea katika dunia yote. (Rom. 5:12) Yehova alifanya nini? Mara moja, alieleza jinsi ambavyo angewakomboa wanadamu. (Mwa. 3:15) Yehova alifanya mpango wa kuandaa fidia ambayo ingefanya iwezekane kwa watoto wa Adamu na Hawa kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo. Kisha, angeweza kumruhusu kila mtu achague ikiwa anataka kumtumikia Yeye na kupata uzima wa milele.—Yoh. 3:16; Rom. 6:23; soma 1 Wakorintho 15:21, 22.

4. Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

4 Ahadi ya Mungu ya kuwafufua wafu inatokeza maswali kadhaa. Kwa mfano, huenda ufufuo utafanywa jinsi gani? Je, tutaweza kuwatambua wapendwa wetu watakapofufuliwa? Ufufuo utatuleteaje shangwe? Na kutafakari kuhusu ufufuo kunaimarishaje uthamini wetu kuelekea upendo, hekima, na subira ya Yehova? Acheni tuchunguze kila moja ya maswali hayo.

HUENDA UFUFUO UTAFANYWA JINSI GANI?

5. Kwa nini inapatana na akili kuamini kwamba ufufuo utafanyika kwa utaratibu, hatua kwa hatua?

5 Yehova atakapowafufua mamilioni ya watu kupitia mwana wake tunaweza kutarajia kwamba si watu wote watakaofufuliwa kwa wakati uleule. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu, ikiwa watu wataongezeka na kuwa wengi ghafla huenda hilo likasababisha vurugu. Na kamwe Yehova hafanyi jambo lolote bila mpangilio au utaratibu. Anajua kwamba ili amani idumu lazima utaratibu ufuatwe. (1 Kor. 14:33) Yehova Mungu alionyesha hekima na subira alipofanya kazi na Yesu kutayarisha dunia hatua kwa hatua kabla ya kuwaumba wanadamu. Vivyo hivyo, Yesu ataonyesha sifa hizo wakati wa Utawala wa Miaka Elfu atakapokuwa akifanya kazi na watu waliookoka Har–Magedoni kuitayarisha dunia ili kuwapokea wale watakaofufuliwa.

Wale watakaookoka Har–Magedoni watawafundisha wale watakaofufuliwa kuhusu Ufalme wa Mungu na matakwa ya Yehova (Tazama fungu la 6) *

6. Kulingana na Matendo 24:15, ni nani watakaokuwa miongoni mwa wale watakaofufuliwa na Yehova?

6 Jambo muhimu zaidi ni kwamba wale watakaookoka Har–Magedoni watahitaji kuwafundisha wale waliofufuliwa kuhusu Ufalme wa Mungu na matakwa ya Yehova. Kwa nini? Kwa sababu wengi kati ya wale watakaofufuliwa ni “wasio waadilifu.” (Soma Matendo 24:15.) Watahitaji kufanya mabadiliko mengi ili kufaidika na fidia ya Kristo. Wazia kazi itakayohusika kuwafundisha ukweli kumhusu Mungu mamilioni ya watu wasio na ujuzi wowote kumhusu Yehova. Je, kila mtu atakuwa na mwalimu wake kama tunavyoongoza mafunzo ya Biblia leo? Je, watu hao waliofufuliwa watapangiwa makutaniko na kuzoezwa kuwafundisha wale watakaofufuliwa baada yao? Itabidi tusubiri ili tujionee. Hata hivyo, tunajua kwamba kufikia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, “dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova.” (Isa. 11:9) Itakuwa miaka elfu moja yenye shughuli nyingi lakini yenye shangwe!

7. Kwa nini watu wa Mungu watakuwa na hisia mwenzi wanapowafundisha wale watakaofufuliwa?

7 Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo watoto wote wa Yehova wa duniani watahitaji kufanya mabadiliko ili kumpendeza yeye. Hivyo, wote watakuwa na hisia mwenzi ya kweli wanapowasaidia wale watakaofufuliwa kushinda mielekeo yao ya dhambi na kuishi kulingana na viwango vya Yehova. (1 Pet. 3:8) Bila shaka, wale watakaofufuliwa watakutana na watu wa Yehova walio wanyenyekevu ambao pia watakuwa ‘wakifanyia kazi wokovu wao wenyewe.’—Flp. 2:12.

JE, TUTAWEZA KUWATAMBUA WALE WATAKAOFUFULIWA?

8. Kwa nini inapatana na akili kufikia mkataa kwamba wale watakaowapokea watu waliofufuliwa wataweza kuwatambua wapendwa wao?

8 Kuna sababu kadhaa zinazofanya tuamini kwamba watu watakaofufuliwa wataweza kuwatambua wapendwa wao. Kwa mfano, kwa msingi wa ufufuo ambao umewahi kufanywa, inaelekea Yehova atawaumba upya watu ili waonekane, wazungumze, na kufikiri kwa njia ileile waliyokuwa nayo kabla ya kifo chao. Kumbuka kwamba Yesu alilinganisha kifo na usingizi, na ufufuo na kuamshwa kutoka kwenye usingizi. (Mt. 9:18, 24; Yoh. 11:11-13) Watu wanapoamka kutoka usingizini, sauti na mwonekano wao huwa uleule, kama ilivyokuwa walipoenda kulala nao hubaki na kumbukumbu yao ileile. Fikiria mfano wa Lazaro. Alikuwa amekufa kwa siku nne, hivyo, mwili wake ulikuwa umeanza kuoza. Hata hivyo, Yesu alipomfufua ni wazi kwamba dada zake walimtambua, na ni wazi kwamba Lazaro aliwakumbuka pia.—Yoh. 11:38-44; 12:1, 2.

9. Kwa nini wale watakaofufuliwa hawatakuwa na akili na miili mikamilifu?

9 Yehova anaahidi kwamba hakuna mtu atakayeishi chini ya utawala wa Kristo atakayesema: “Mimi ni mgonjwa.” (Isa. 33:24; Rom. 6:7) Hivyo, wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu wataumbwa upya wakiwa na miili yenye afya. Hata hivyo, hawatakuwa wakamilifu hapohapo baada ya ufufuo. Kwa kuwa huenda hilo lingefanya wapendwa wao wasiwatambue. Inaonekana kwamba wanadamu wote watafikia ukamilifu hatua kwa hatua wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Ni mwishoni tu mwa ile miaka elfu moja ndipo Yesu atakapomrudishia Baba yake Ufalme. Kisha, Ufalme utakuwa umekamilisha kazi yake kikamili. Kutia ndani kuwafanya wanadamu kuwa wakamilifu.—1 Kor. 15:24-28; Ufu. 20:1-3.

UFUFUO UTATULETEAJE SHANGWE?

10. Ufufuo utakufanya uhisije?

10 Wazia hali itakavyokuwa kukutana tena na wapendwa wako. Je, shangwe utakayohisi itakufanya ucheke au ulie? Je, utamwimbia Yehova nyimbo za sifa kwa sauti? Jambo moja ni hakika: utahisi upendo mkubwa kwa Baba yako anayekujali na mwana wake asiye na ubinafsi, kwa sababu ya zawadi ya pekee ya ufufuo.

11. Kulingana na maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Yohana 5:28, 29, wale watakaoishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu watapata nini?

11 Wazia shangwe ambayo wale watakaofufuliwa watahisi watakapouvua utu wao wa zamani na kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu. Wale wanaofanya mabadiliko hayo watapata ufufuo wa uzima. Kwa upande mwingine, wale watakaomwasi Mungu hawataruhusiwa kuvuruga amani ya Paradiso.—Isa. 65:20; soma Yohana 5:28, 29.

12. Yehova atawabariki watu wote duniani jinsi gani?

12 Chini ya utawala wa Ufalme, watu wote wa Mungu watajionea ukweli wa maneno ya Methali 10:22 inayosema: “Baraka ya Yehova ndiyo inayomtajirisha mtu, naye haichanganyi na maumivu.” Kwa msaada wa roho ya Yehova, watu wa Mungu watakuwa matajiri kiroho, yaani, watazidi kuwa kama Kristo, na hatua kwa hatua watafikia ukamilifu. (Yoh. 13:15-17; Efe. 4:23, 24) Kila siku miili yao itazidi kuwa na nguvu zaidi na watazidi kuwa watu bora. Maisha hayo yatakuwa yenye shangwe sana! (Ayu. 33:25) Hata hivyo, kutafakari kuhusu ufufuo kutakusaidiaje sasa?

THAMINI UPENDO WA YEHOVA

13. Andiko la Zaburi 139:1-4, linaonyeshaje kwamba Yehova anatujua sana, na ufufuo utathibitishaje hilo?

13 Kama tulivyozungumzia awali, Yehova atakapokuwa anawafufua watu atawarudishia kumbukumbu zao na utu wao uliowafanya wawe jinsi walivyo. Hebu wazia hilo linamaanisha nini. Yehova anakupenda sana hivi kwamba anaweka kumbukumbu ya mambo yote unayofikiria, unayohisi, kusema na kufanya. Hivyo, ikiwa atakufufua ataweza kukurudishia kwa urahisi kumbukumbu zako, mtazamo, na utu wako. Mfalme Daudi alitambua jinsi Yehova anavyopendezwa na kila mmoja wetu. (Soma Zaburi 139:1-4.) Kuelewa kwamba Yehova anatupenda sana kunaweza kufanya tuhisije?

14. Tunapaswa kuhisije tunapotafakari kuhusu jinsi Yehova anavyotujua sana?

14 Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotujua sana hatupaswi kuwa na wasiwasi. Kwa nini? Kumbuka kwamba Yehova anatujali sana. Anathamini sifa zetu zinazotufanya tuwe wa pekee. Anakumbuka mambo tunayopitia maishani yanayotufanya tuwe jinsi tulivyo. Wazo hilo linatia moyo kwelikweli! Kamwe tusihisi tuko peke yetu. Kila dakika inayopita katika siku, Yehova yuko kando yetu akitafuta fursa za kutusaidia.—2 Nya. 16:9.

THAMINI HEKIMA YA YEHOVA

15. Ufufuo unatuthibitishiaje hekima ya Yehova?

15 Hofu ya kifo ni silaha yenye nguvu. Wale wanaoongozwa na Shetani wanaitumia kuwalazimisha watu wawasaliti rafiki zao au wakane imani yao. Lakini tishio hilo halina nguvu kwetu. Tunajua kwamba ikiwa adui zetu watatuua, Yehova ataturudishia uhai wetu. (Ufu. 2:10) Tunasadiki kwamba hakuna jambo wanaloweza kufanya linaloweza kututenga na upendo wa Yehova. (Rom. 8:35-39) Yehova ameonyesha hekima ya pekee kwa kutupatia tumaini la ufufuo. Kupitia ufufuo, anamnyang’anya Shetani moja wapo ya silaha zake zenye matokeo makubwa zaidi, na wakati huohuo anatupatia ujasiri usioshindwa.

Je, maamuzi yetu yanaonyesha tunatumaini ahadi ya Yehova kwamba atatuandalia mahitaji yetu ya kimwili? (Tazama fungu la 16) *

16. Unahitaji kujiuliza maswali gani, na majibu yatakusaidiaje kujua unamtumaini Yehova kadiri gani?

16 Ikiwa maadui wa Yehova watatishia kukuua, je, utakuwa na uhakika kwamba Yehova atakufufua? Unaweza kujuaje kama utamtumaini Yehova wakati huo? Njia moja ni kujiuliza: ‘Je, maamuzi madogo ninayofanya kila siku yanathibitisha kwamba ninamtumaini Yehova?’ (Luka 16:10) Swali lingine linaweza kuwa: ‘Je, njia yangu ya maisha inathibitisha kwamba ninaamini ahadi ya Yehova kwamba ataniandalia mahitaji yangu ya kimwili ikiwa ninatanguliza Ufalme?’ (Mt. 6:31-33) Ikiwa majibu kwa maswali hayo mawili ni ndiyo, basi unathibitisha kwamba unamtumaini Yehova nawe utakuwa tayari kwa majaribu yoyote yatakayokuja.—Met. 3:5, 6.

THAMINI SUBIRA YA YEHOVA

17. (a) Ufufuo unaonyeshaje kwamba Yehova ni mwenye subira? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini subira ya Yehova?

17 Yehova amepanga siku na saa hususa ambayo ataleta mwisho wa mfumo huu mwovu. (Mt. 24:36) Hatakosa subira na kutenda kabla ya wakati huo. Anatamani kuwafufua wafu lakini yeye ni mwenye subira. (Ayu. 14:14, 15) Anangojea hadi wakati unaofaa ufike ili awafufue. (Yoh. 5:28) Tuna sababu nzuri za kuthamini subira ya Yehova. Hebu wazia: Kwa sababu Yehova ni mwenye subira, watu wengi, kutia ndani sisi tumepata nafasi ya ‘kufikia toba.’ (2 Pet. 3:9) Yehova anataka watu wengi, kadiri iwezekanavyo wapate fursa ya kupata uzima wa milele. Basi, acheni tuonyeshe kwamba tunathamini subira yake. Jinsi gani? Kwa kuwatafuta kwa bidii wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” na kuwasaidia wampende Yehova na kumtumikia. (Mdo. 13:48) Kisha, watafaidika kutokana na subira ya Yehova kama tu sisi tunavyofaidika.

18. Kwa nini tunapaswa kuwaonyesha subira wengine?

18 Yehova atangoja kwa subira hadi mwisho wa miaka elfu moja kabla ya kutarajia ukamilifu kutoka kwetu. Hadi wakati huo utakapofika, Yehova yuko tayari kutusamehe dhambi zetu. Hivyo, bila shaka tuna sababu ya kukazia mema ya wengine na kuwaonyesha subira. Fikiria mfano wa dada mmoja ambaye mume wake alipata ugonjwa wa kuwa na wasiwasi mwingi kupita kiasi na akaacha kuhudhuria mikutano. Dada huyo anasema hivi: “Jambo hilo liliniumiza sana. Mipango yetu ya wakati ujao tukiwa familia iliharibika.” Hata hivyo, katika kipindi hicho chote dada huyo mpendwa alimwonyesha subira mume wake. Alimtegemea Yehova naye hakukata tamaa kamwe. Kama Yehova, hakukazia fikira tatizo, bali mambo mema kumhusu mume wake. Anasema hivi: “Mume wangu ana sifa nzuri sana, naye anajitahidi kushinda tatizo lake hatua kwa hatua.” Ni jambo la muhimu sana tuwaonyeshe subira wale walio katika familia zetu au kutanikoni wanaojitahidi kushinda changamoto wanazokabili!

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Yesu na malaika walikuwa na shangwe dunia ilipoumbwa. Lakini, wazia jinsi watakavyofurahi watakapoona dunia imejaa watu wakamilifu wanaompenda na kumtumikia Yehova. Wazia shangwe ambayo wale walionunuliwa kutoka duniani kwenda mbinguni kutawala pamoja na Kristo watahisi watakapoona wanadamu wakifaidika kutokana na kazi yao. (Ufu. 4:4, 9-11; 5:9, 10) Na wazia kuishi wakati ambapo machozi ya shangwe yatachukua nafasi ya machozi ya huzuni, wakati magonjwa, majonzi, na kifo havitakuwapo tena milele. (Ufu. 21:4) Hadi wakati huo, azimia kumwiga Baba yako mwenye upendo, hekima na subira. Ikiwa utafanya hivyo, utadumisha shangwe yako licha ya majaribu yoyote utakayokabili. (Yak. 1:2-4) Tunamshukuru sana Yehova kwa ahadi yake kwamba “kutakuwa na ufufuo”!—Mdo. 24:15.

WIMBO 141 Muujiza wa Uhai

^ fu. 5 Yehova ni Baba mwenye upendo, hekima, na subira. Tunaweza kuona sifa hizo kupitia vitu vyote alivyoumba na kusudi lake la kuwarudishia wanadamu uhai wakati wa ufufuo. Makala hii itazungumzia baadhi ya maswali ambayo huenda tukawa nayo kuhusu ufufuo, na itakazia jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunathamini upendo, hekima, na subira ya Yehova.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Mwanamume mwenyeji wa asili wa Marekani aliyekufa mamia ya miaka iliyopita afufuliwa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Ndugu aliyeokoka Har–Magedoni anamfundisha mwanamume huyo aliyefufuliwa mambo anayohitaji kufanya ili afaidike kutokana na fidia ya Kristo.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Ndugu anamwambia mwajiri wake kwamba kuna siku kadhaa za katikati ya wiki ambazo hawezi kufanya kazi muda wa ziada. Anaeleza kwamba ametenga jioni hizo kwa ajili ya utendaji unaohusiana na ibada yake kwa Yehova. Hata hivyo, kunapokuwa na uhitaji wa lazima siku nyinginezo, atakuwa tayari kufanya kazi muda wa ziada.