Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 34

Una Sehemu Yako Katika Kutaniko la Yehova!

Una Sehemu Yako Katika Kutaniko la Yehova!

“Kama vile mwili ni mmoja lakini una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili huo, ingawa ni vingi, ni mwili mmoja, ndivyo pia alivyo Kristo.”—1 KOR. 12:12.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

MUHTASARI *

1. Tunafurahia pendeleo gani?

NI PENDELEO kubwa sana kuwa sehemu ya kutaniko la Yehova! Tuko katika paradiso ya kiroho ambayo imejaa watu wenye amani na furaha. Unatimiza sehemu gani katika kutaniko?

2. Mtume Paulo alitumia mfano gani katika barua zake zilizoongozwa na roho?

2 Tunaweza kujifunza mengi kuhusu sehemu yetu katika kutaniko kutokana na mfano ambao mtume Paulo alitumia katika barua zake mbalimbali zilizoongozwa na roho ya Mungu. Katika kila moja ya barua hizo, Paulo alilinganisha kutaniko na mwili wa binadamu. Pia, aliwalinganisha watu kutanikoni na sehemu mbalimbali za mwili.—Rom. 12:4-8; 1 Kor. 12:12-27; Efe. 4:16.

3. Tutajifunza mambo gani katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutachunguza mambo matatu muhimu ambayo tunaweza kujifunza kutokana na mfano ambao Paulo alitumia. Kwanza, tutajifunza kwamba kila mmoja wetu ana sehemu yake katika kutaniko la Yehova. Pili, tutachunguza mambo tunayoweza kufanya ikiwa hatujui vizuri sehemu * yetu katika kutaniko. Na tatu, tutazungumzia kwa nini tunahitaji kuwa na mengi ya kufanya ili kutimiza kazi ambayo Mungu amempatia kila mmoja wetu kutanikoni.

KILA MMOJA WETU ANA JUKUMU LA KUTIMIZA KATIKA KUTANIKO LA YEHOVA

4. Andiko la Waroma 12:4, 5 linatufundisha nini?

4 Jambo la kwanza tunaloweza kujifunza kutokana na mfano ambao Paulo alitumia ni kwamba kila mmoja wetu ana sehemu muhimu katika familia ya Yehova. Paulo anaanza mfano wake kwa kusema hivi: “Kama vile tulivyo na viungo vingi katika mwili mmoja, lakini viungo hivyo havifanyi kazi ileile, ndivyo sisi, ingawa tuko wengi, ni mwili mmoja katika muungano na Kristo, lakini kila mmoja wetu ni kiungo cha mwingine.” (Rom. 12:4, 5) Paulo alikuwa akimaanisha nini? Kila mmoja wetu ana jukumu tofauti kutanikoni, lakini kila mmoja wetu ana thamani.

Tunatimiza sehemu mbalimbali katika kutaniko, lakini kila mmoja wetu ni mwenye thamani (Tazama fungu la 5 hadi 12) *

5. Yehova amelipatia kutaniko “zawadi” gani?

5 Unapofikiria wale walio na sehemu katika kutaniko, huenda mara moja ukawafikiria wale wanaoongoza kutanikoni. (1 The. 5:12; Ebr. 13:17) Ni kweli kwamba kupitia Kristo, Yehova ametoa “wanaume kuwa zawadi” katika kutaniko Lake. (Efe. 4:8) ‘Wanaume hao walio zawadi’ wanatia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza, wasaidizi wa Baraza Linaloongoza waliowekwa rasmi, washiriki wa Halmashauri za Tawi, waangalizi wa mzunguko, wanaofundisha shule za Biblia, wazee wa makutaniko, na watumishi wa huduma. Wanaume hao wote wanawekwa rasmi kwa roho takatifu ili kuwatunza kondoo wenye thamani wa Yehova na kuliimarisha kutaniko.—1 Pet. 5:2, 3.

6. Kulingana na 1 Wathesalonike 2:6-8, ndugu wanaowekwa rasmi kwa roho takatifu wanajitahidi kufanya nini?

6 Akina ndugu huwekwa rasmi kwa roho takatifu ili kutimiza majukumu mbalimbali. Kama tu ambavyo viungo mbalimbali vya mwili, kama vile mikono na miguu, vinavyofanya kazi ili kunufaisha mwili mzima, ndugu wanaowekwa rasmi kwa roho takatifu wanafanya kazi kwa bidii ili kulinufaisha kutaniko zima. Hawajitafutii utukufu wao wenyewe. Badala yake, wanajitahidi kuwajenga na kuwaimarisha ndugu na dada zao. (Soma 1 Wathesalonike 2:6-8.) Tunamshukuru Yehova kwa wanaume hao wa kiroho wanaostahili na wasio na ubinafsi!

7. Watumishi wengi wa wakati wote hufurahia baraka gani?

7 Baadhi ya ndugu na dada kutanikoni wanaweza kuwekwa rasmi kutumikia wakiwa wamishonari, mapainia wa pekee, au mapainia wa kawaida. Isitoshe, ndugu na dada ulimwenguni pote wameifanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kuwa kazi kuu maishani mwao. Kwa kufanya hivyo, wamewasaidia wengi kuwa wanafunzi wa Kristo Yesu. Ingawa kwa kawaida waeneza injili hao wa wakati wote wana vitu vya kimwili vichache, Yehova amewathawabisha kwa baraka nyingi maishani. (Marko 10:29, 30) Tunawathamini sana ndugu na dada hao wapendwa, na tunashukuru kwamba wao ni sehemu ya kutaniko!

8. Kwa nini kila mhubiri wa habari njema ni mwenye thamani kwa Yehova?

8 Je, wanaume waliowekwa rasmi na wale walio katika utumishi wa wakati wote ndiyo pekee walio na sehemu katika kutaniko? Hapana! Kila mhubiri wa habari njema ana thamani kwa Mungu na kutanikoni. (Rom. 10:15; 1 Kor. 3:6-9) Hiyo ni kwa sababu mojawapo ya malengo muhimu zaidi ya kutaniko ni kufanya wanafunzi wa Bwana wetu Yesu Kristo. (Mt. 28:19, 20; 1 Tim. 2:4) Wale wote wanaoshirikiana na kutaniko, wahubiri waliobatizwa na ambao hawajabatizwa, wanajitahidi kutanguliza kazi hiyo maishani mwao.—Mt. 24:14.

9. Kwa nini tunawathamini dada zetu Wakristo?

9 Yehova huwapatia dada Wakristo sehemu yenye kuheshimika kutanikoni. Anawathamini dada hao ambao ni wake, akina mama, wajane, na dada waseja wanaomtumikia kwa ushikamanifu. Mara kwa mara, Maandiko yanawataja wanawake wa pekee waliompendeza Mungu. Wanapongezwa kwa kuwa mifano mizuri katika hekima, imani, bidii, ujasiri, ukarimu, na kazi njema. (Luka 8:2, 3; Mdo. 16:14, 15; Rom. 16:3, 6; Flp. 4:3; Ebr. 11:11, 31, 35) Tunamshukuru sana Yehova kwa kuwa na wanawake Wakristo katika makutaniko yetu wenye sifa hizohizo maridadi!

10. Kwa nini tunawathamini ndugu na dada zetu wenye umri mkubwa?

10 Pia, tumebarikiwa kuwa na ndugu na dada wengi wenye umri mkubwa kutanikoni. Baadhi ya makutaniko yana ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao wamemtumikia Yehova kwa ushikamanifu katika maisha yao yote. Wengine wenye umri mkubwa, wamejifunza kweli hivi karibuni. Vyovyote vile, ndugu na dada zetu wenye umri mkubwa huenda wanapambana na matatizo mbalimbali ya kiafya yanayosababishwa na umri kusonga. Matatizo hayo huenda yakaathiri utendaji wao kutanikoni na katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, ndugu na dada hao wenye umri mkubwa wanafanya yote wawezayo katika utumishi wa shambani, na wanatumia nguvu zao zote kuwatia moyo na kuwazoeza wengine! Nasi tunafaidika kutokana na uzoefu wao. Kwa kweli, wao ni maridadi machoni pa Yehova na kwetu pia.—Met. 16:31.

11-12. Vijana katika kutaniko lako wamekutiaje moyo?

11 Fikiria pia kuhusu vijana wetu. Huenda wakakabili changamoto nyingi wanapoendelea kukua katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani Ibilisi na falsafa zake zenye uovu. (1 Yoh. 5:19) Ingawa hivyo, sote tunatiwa moyo tunapowaona vijana wetu wakitoa maelezo mikutanoni, wakishiriki katika huduma, na wakitetea imani yao kwa ujasiri. Naam, enyi vijana mna sehemu muhimu katika kutaniko la Yehova!—Zab. 8:2.

12 Hata hivyo, si rahisi kwa baadhi ya ndugu na dada zetu kuamini kwamba wana sehemu muhimu katika kutaniko. Ni nini kinachoweza kumsaidia kila mmoja wetu ahisi kwamba ana sehemu muhimu katika kutaniko? Acheni tuone.

TAMBUA SEHEMU YAKO KATIKA KUTANIKO

13-14. Kwa nini huenda baadhi ya ndugu na dada wakahisi kwamba hawana thamani kutanikoni?

13 Fikiria jambo la pili tunaloweza kujifunza kutokana na mfano ambao Paulo alitumia. Anakazia uangalifu tatizo ambalo wengi wanalo leo; ni vigumu kwao kuamini kwamba wana thamani kutanikoni. Paulo anaandika hivi: “Ikiwa mguu ungesema, ‘Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si sehemu ya mwili,’ hilo halifanyi usiwe sehemu ya mwili. Na ikiwa sikio lingesema, ‘Kwa kuwa mimi si jicho, mimi si sehemu ya mwili,’ hilo halilifanyi lisiwe sehemu ya mwili.” (1 Kor. 12:15, 16) Paulo alikuwa akitufundisha nini?

14 Ikiwa utajilinganisha na wengine kutanikoni, huenda usione thamani yako kutanikoni. Huenda baadhi ya watu kutanikoni wakawa walimu stadi, wenye uwezo wa kupanga mambo vizuri, au wachungaji stadi. Labda unahisi kwamba huna zawadi hizo kwa kiwango kilekile kama wengine. Jambo hilo linaonyesha kwamba wewe ni mnyenyekevu na mwenye kiasi. (Flp. 2:3) Lakini uwe mwangalifu. Ikiwa mara kwa mara unajilinganisha na wale walio na uwezo fulani wa pekee utavunjika moyo. Huenda ukahisi, kama Paulo alivyosema, kwamba hutimizi sehemu yoyote katika kutaniko. Ni nini kinachoweza kukusaidia kukabiliana na hisia hizo?

15. Kulingana na 1 Wakorintho 12:4-11, tunahitaji kutambua nini kuhusu vipawa vyovyote tulivyo navyo?

15 Fikiria jambo hili: Yehova aliwapa baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza zawadi za kimuujiza za roho takatifu, lakini si Wakristo wote waliopokea zawadi ileile. (Soma 1 Wakorintho 12:4-11.) Yehova aliwapatia zawadi na uwezo tofauti-tofauti, lakini kila Mkristo alikuwa mwenye thamani. Leo, hatuna zawadi za kimuujiza za roho takatifu. Lakini bado tunaweza kutumia kanuni hii: Huenda tusiwe na vipawa vinavyofanana, lakini sote ni wenye thamani machoni pa Yehova.

16. Tunahitaji kutumia shauri gani kutoka kwa mtume Paulo?

16 Badala ya kujilinganisha na Wakristo wengine, tunahitaji kutumia shauri hili lililoongozwa na roho la mtume Paulo: “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.”—Gal. 6:4.

17. Tutafaidikaje kwa kufuata shauri la Paulo?

17 Ikiwa tutafuata shauri la mtume Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu na kuchunguza matendo yetu, huenda tukaanza kuona kwamba sisi pia tuna zawadi na uwezo mbalimbali wa pekee. Kwa mfano, huenda mzee asiwe na uwezo mkubwa wa kufundisha jukwaani, lakini huenda akawa na matokeo mazuri sana katika kazi ya kufanya wanafunzi. Au huenda hawezi kupanga mambo vizuri kama baadhi ya wazee kutanikoni, lakini huenda akawa anajulikana kutanikoni kuwa mchungaji mwenye upendo ambaye wahubiri wanajihisi huru kumfikia kwa ajili ya ushauri mzuri wa Kimaandiko. Au huenda anajulikana kuwa mkarimu. (Ebr. 13:2, 16) Tunapotambua wazi uwezo na zawadi tulizo nazo, tutakuwa na sababu ya kuridhika kutokana na kile tunachoweza kuchangia kutanikoni. Na itakuwa vigumu kuwaonea wivu wale walio na zawadi tofauti na zetu.

18. Tunaweza kuboreshaje uwezo wetu mbalimbali?

18 Haidhuru sehemu tunayotimiza katika kutaniko, sote tunapaswa kuwa na tamaa ya kuboresha utumishi wetu na uwezo mbalimbali tulio nao. Ili kutusaidia kuboresha uwezo wetu, Yehova anaandaa mazoezi mazuri sana kupitia tengenezo lake. Kwa mfano, katika mikutano ya katikati ya juma, tunapata mwongozo wa jinsi ya kuwa na matokeo zaidi katika huduma. Je, unanufaika kikamili na programu hiyo ya mazoezi?

19. Unaweza kufikiaje lengo la kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme?

19 Programu nyingine nzuri ya mazoezi ni Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Shule hii ni kwa ajili ya ndugu na dada walio katika utumishi wa wakati wote, na wenye umri kati ya miaka 23 na 65. Huenda ukahisi kwamba huwezi kamwe kufikia lengo hilo. Lakini badala ya kuorodhesha sababu zinazoweza kukufanya usihudhurie, orodhesha mambo yanayokufanya utake kuhudhuria. Kisha, weka mikakati itakayokusaidia kufikia sifa za kustahili kuhudhuria. Kwa msaada wa Yehova, na bidii yako, unaweza kutimiza mambo ambayo huenda mwanzoni ulidhani hayawezekani.

TUMIA ZAWADI ULIZO NAZO KULIJENGA KUTANIKO

20. Tunaweza kujifunza nini kutokana na andiko la Waroma 12:6-8?

20 Jambo la tatu tunaloweza kujifunza kutokana mfano ambao Paulo alitumia linapatikana kwenye Waroma 12:6-8. (Soma.) Hapo, kwa mara nyingine tena Paulo anaonyesha kwamba wale walio kutanikoni wana zawadi zinazotofautiana. Lakini sasa, anakazia kwamba tunapaswa kutumia zawadi yoyote tuliyo nayo kulijenga na kuliimarisha kutaniko.

21-22. Tunajifunza nini kutoka kwa Robert na Felice?

21 Fikiria mfano wa ndugu tutakayemwita Robert. Baada ya kutumikia kwenye nchi ya kigeni, alipata mgawo wa kutumikia kwenye Betheli iliyo nchini kwao. Ingawa alihakikishiwa kwamba badiliko la mgawo wake halikuwa kwa sababu alikuwa na mapungufu fulani, alisema hivi: “Nilikuwa na maoni mabaya kujihusu, nilihisi kwamba nimeshindwa kutimiza mgawo wangu, na nilibaki na mawazo hayo kwa miezi mingi. Kuna nyakati nilitamani kuacha utumishi wa Betheli.” Robert alipataje tena shangwe yake? Mzee mwenzake alimkumbusha kwamba Yehova ametuzoeza katika migawo yetu iliyopita ili tuweze kutumiwa kwa njia nzuri zaidi katika mgawo wetu wa sasa. Robert alitambua kwamba alihitaji kuacha kukazia mambo yaliyopita na kuanza kukazia fikiria mambo ambayo angeweza kufanya sasa.

22 Ndugu Felice Episcopo alikabili changamoto kama hiyo. Yeye na mke wake walihitimu Shule ya Gileadi mwaka wa 1956 na walitumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko nchini Bolivia. Mwaka wa 1964 walipata mtoto. Felice anasema hivi: “Ilikuwa changamoto kwetu kuacha mgawo tulioupenda sana. Lazima nikiri kwamba nilipoteza mwaka mzima nikijisikitikia. Lakini kwa msaada wa Yehova, nilibadili mtazamo wangu na kukazia fikira jukumu langu jipya la kuwa mzazi.” Je, unahisi kama Robert au Felice? Je, umevunjika moyo kwa sababu sasa huna mapendeleo yaleyale uliyokuwa nayo wakati uliopita. Ikiwa ndivyo, utafurahi zaidi ikiwa utabadili mtazamo wako na kukazia fikira mambo unayoweza kufanya sasa unapomtumikia Yehova na ndugu zako. Endelea kuwa na mengi ya kufanya ukitumia zawadi na uwezo mbalimbali ulio nao kuwasaidia wengine, nawe utapata shangwe unapoendelea kulijenga kutaniko.

23. Tunapaswa kutenga wakati wa kufanya nini, na tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

23 Kila mmoja wetu ni mwenye thamani machoni pa Yehova. Anataka tuwe sehemu ya familia yake. Ikiwa tutatumia muda kutafakari mambo tunayoweza kufanya ili kuwajenga ndugu na dada zetu na kujitahidi kutimiza mambo hayo, haitakuwa rahisi kuhisi kwamba hatutimizi sehemu yoyote katika kutaniko! Lakini namna gani kuhusu jinsi tunavyowaona wengine kutanikoni? Tunaweza kuwaonyeshaje kwamba tunawathamini? Katika makala inayofuata, tutachunguza jambo hilo muhimu.

WIMBO 24 Njooni Kwenye Mlima wa Yehova

^ fu. 5 Sote tungependa kuhisi kwamba tuna thamani machoni pa Yehova. Lakini nyakati nyingine huenda tukajiuliza, Yehova anaweza kunitumiaje? Makala hii itatusaidia kuona kwamba kila mmoja wetu ana sehemu muhimu katika kutaniko.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Sehemu tuliyo nayo katika kutaniko la Yehova inarejelea jukumu tunalotimiza katika kujenga na kuliimarisha kutaniko. Sehemu yetu katika kutaniko, haitegemei rangi yetu, kabila, hali yetu ya kiuchumi, kijamii, utamaduni wetu, au elimu tuliyo nayo.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Picha hizi tatu zinaonyesha mambo ambayo hufanyika kabla, wakati, na baada ya mikutano ya kutaniko. Picha ya 1: Mzee wa kutaniko anamsalimu kwa uchangamfu mgeni, ndugu kijana anashughulikia mfumo wa sauti, na dada fulani anazungumza na dada mwenye umri mkubwa. Picha ya 2: Vijana kwa wazee wanajitahidi kutoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Picha ya 3: Wenzi wa ndoa wanasaidia kusafisha Jumba la Ufalme. Mama anamsaidia mtoto wake kuweka mchango kwenye kisanduku cha michango. Ndugu kijana anashughulikia machapisho, na ndugu fulani anamtia moyo dada mwenye umri mkubwa.