Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 34

“Onjeni” Wema wa Yehova—Jinsi Gani?

“Onjeni” Wema wa Yehova—Jinsi Gani?

“Onjeni mwone kwamba Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mtu anayemkimbilia.”—ZAB. 34:8.

WIMBO 117 Sifa ya Wema

MUHTASARI *

1-2. Kulingana na Zaburi 34:8, tunaweza kujifunzaje kuhusu wema wa Yehova?

WAZIA unapewa chakula ambacho hujawahi kula. Unaweza kujifunza mambo fulani kuhusu chakula hicho kwa kukitazama, kukinusa, kwa kupewa maelekezo ya jinsi ya kukipika, au kuwauliza wengine maoni yao kuhusu chakula hicho. Hata hivyo, njia pekee ya kujua ikiwa kwa kweli unakipenda chakula hicho, ni kukionja wewe mwenyewe.

2 Tunaweza kujifunza jambo fulani kuhusu wema wa Yehova kwa kusoma Biblia na machapisho yetu, na pia kwa kuwasikiliza wengine wanapozungumzia baraka walizopata kutoka kwa Yehova. Lakini tutaelewa kihalisi jinsi Yehova alivyo mwema ‘tunapoonja’ wema wake sisi wenyewe. (Soma Zaburi 34:8.) Acheni tuone mfano wa jinsi tunavyoweza kufanya hivyo. Tuseme tunataka kufanya aina fulani ya utumishi wa wakati wote, lakini ili tuweze kufikia lengo hilo, tunahitaji kurahisisha maisha yetu. Labda mara nyingi tumesoma ahadi ya Yesu kwamba ikiwa tutautanguliza Ufalme maishani, Yehova atatuandalia vitu ambavyo kwa kweli tunahitaji; lakini hatujawahi kujionea kibinafsi utimizo wa ahadi hiyo. (Mt. 6:33) Hata hivyo, tukiwa na imani katika ahadi ya Yesu, tunaamua kupunguza matumizi yetu, tunapunguza saa tunazotumia katika kazi ya kimwili, na kukazia fikira huduma yetu. Tunapofanya hivyo, tunajifunza kupitia mambo tunayojionea sisi wenyewe kwamba kwa kweli Yehova anatuandalia mahitaji yetu. ‘Tunaonja’ wema wa Yehova kibinafsi.

3. Kulingana na Zaburi 16:1, 2, ni nani wanaopokea wema wa Yehova?

3 Yehova ni “mwema kwa wote,” hata watu ambao hawamjui. (Zab. 145:9; Mt. 5:45) Lakini hasa wale wanaompenda Yehova na kumtumikia kwa nafsi yote wanapata baraka nyingi kutoka kwake. (Soma Zaburi 16:1, 2.) Fikiria baadhi ya njia ambazo tunanufaika kutokana na wema wa Yehova.

4. Yehova anawaonyeshaje wema wake wale wanaoanza kumkaribia?

4 Kila wakati tunapotumia mambo tunayojifunza kutoka kwa Yehova, tunajionea matokeo mazuri ya kutumia mambo hayo maishani. Tulipokuwa tukijifunza kumhusu na kuanza kumpenda, alitusaidia kushinda fikira na mazoea ambayo zamani yalitutenga naye. (Kol. 1:21) Na tulipojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, tulijionea wema wake hata zaidi alipotupatia dhamiri njema na kutuvuta ili tuwe na urafiki wa karibu pamoja naye.—1 Pet. 3:21.

5. Tunajionea wema wa Yehova katika huduma yetu jinsi gani?

5 Tunaendelea kujionea wema wa Yehova tunaposhiriki katika huduma. Je, wewe ni mwenye haya? Watu wengi wa Yehova ni wenye haya. Labda kabla hujawa mtumishi wa Yehova, hukuwahi kujiwazia ukigonga mlango wa mtu usiyemfahamu na kumweleza ujumbe wa Biblia. Lakini leo unafanya hivyo kwa ukawaida. Zaidi ya hilo, kwa msaada wa Yehova umejifunza kufurahia kazi ya kuhubiri! Umejionea utegemezo wa Yehova katika njia mbalimbali. Alikusaidia uendelee kuwa mtulivu mwenye nyumba alipokupinga. Pia, alikusaidia kukumbuka andiko lililofaa kabisa kumsomea mwenye nyumba aliyependezwa. Na alikupatia nguvu za kuendelea kuhubiri ulipokuwa kwenye eneo ambalo watu hawana upendezi.—Yer. 20:7-9.

6. Mazoezi ambayo Yehova huandaa yanathibitishaje wema wake?

6 Pia, Yehova ametuonyesha wema wake kwa kutuzoeza katika huduma. (Yoh. 6:45) Katika mkutano wetu wa katikati ya juma, tunasikiliza mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo yaliyotayarishwa vizuri, na tunatiwa moyo kuyatumia katika huduma. Mwanzoni, huenda tukawa na wasiwasi kuhusu kutumia njia fulani mpya, lakini tunapofanya hivyo, huenda tukaona kwamba njia hiyo mpya inawavutia watu katika eneo letu. Pia, kwenye mikutano na makusanyiko tunatiwa moyo kushiriki katika nyanja nyingine za huduma ambazo huenda hatujawahi kufanya. Kwa mara nyingine tena, hilo linamaanisha tutahitaji kufanya jambo ambalo hatukuzoea, lakini tunapofanya hivyo, tunampa Yehova kitu cha kubariki. Acheni tuchunguze baadhi ya baraka tunazoweza kupata tunapotafuta njia mpya za kumtolea Yehova kilicho bora, licha ya hali zetu. Kisha, tutazungumzia njia tunazoweza kupanua huduma yetu.

YEHOVA HUWABARIKI WALE WANAOMTUMAINI

7. Tunapata baraka gani tunapojitahidi kupanua huduma yetu?

7 Tunamkaribia hata zaidi Yehova. Fikiria mfano wa mzee wa kutaniko anayeitwa Samuel, * ambaye anatumikia pamoja na mke wake nchini Kolombia. Wenzi hao wa ndoa walifurahia kufanya upainia katika kutaniko lao la nyumbani, lakini walitaka kupanua huduma yao kwa kulisaidia kutaniko lenye uhitaji mkubwa. Ili kufikia lengo hilo, walihitaji kudhabihu mambo fulani. Samuel anasema hivi: “Tulitumia kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 6:33, na kuacha kununua vitu visivyo vya lazima. Lakini jambo gumu zaidi lilikuwa kuacha nyumba yetu. Ilikuwa imebuniwa kwa njia iliyotufaa kabisa na hatukuwa tukidaiwa mkopo wa nyumba.” Katika mgawo wao mpya, walitambua kwamba wangeweza kuishi kwa kutumia tu asilimia 17 hivi ya kipato chao cha awali. Samuel anasema hivi: “Tumejionea jinsi Yehova anavyoongoza hatua zetu na kujibu sala zetu. Tunahisi anatuonyesha kibali na upendo wake kwa njia ambayo hatukuwahi kujionea awali.” Je, unaweza kupanua huduma yako kwa njia fulani? Ikiwa ndivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba utamkaribia zaidi Yehova, na kwamba atakutunza.—Zab. 18:25.

8. Unajifunza nini kutokana na maelezo ya Ivan na Viktoria?

8 Tunapata shangwe katika huduma yetu. Fikiria maelezo ya Ivan na Viktoria, wenzi wa ndoa wanaotumikia wakiwa mapainia nchini Kyrgyzstan. Walirahisisha maisha yao ili waweze kujitolea katika mgawo wowote, kutia ndani miradi ya ujenzi. Ivan anasema hivi: “Tulijitoa kadiri tuwezavyo katika kila mradi. Jioni ilipofika tulikuwa tumechoka, lakini tulikuwa wenye amani na tumeridhika, tukijua kwamba tumetumia nguvu zetu katika kazi ya Ufalme. Pia, tulipata shangwe kubwa kwa sababu ya marafiki wapya na kumbukumbu nzuri tulizopata.”—Marko 10:29, 30.

9. Dada fulani anayekabili changamoto amefanya nini ili kupanua huduma yake, na amepata matokeo gani?

9 Tunapata shangwe katika utumishi wa Yehova hata wakati tunapokabili changamoto. Kwa mfano, Mirreh, dada mjane ambaye umri wake umesonga na anayeishi Afrika Magharibi, alistaafu kazi yake ya udaktari na kuanza kufanya upainia. Mirreh anasumbuliwa na ugonjwa wa Yabisi Kavu unaomletea maumivu makali, na anaweza tu kufanya utumishi wa nyumba kwa nyumba kwa vipindi vya saa moja. Lakini anaweza kutumia muda mwingi zaidi katika mahubiri ya hadharani. Ana ziara nyingi za kurudia na mafunzo ya Biblia, na baadhi yao anawasiliana nao kwa simu. Ni nini kilichomchochea Mirreh ajitoe ili kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova? Anasema hivi: “Moyo wangu umejaa upendo kwa ajili ya Yehova na Kristo Yesu. Na mara kwa mara ninasali kwamba Yehova anisaidie kufanya mengi kadiri ninavyoweza katika utumishi wake.”—Mt. 22:36, 37.

10. Kama andiko la 1 Petro 5:10, linavyoonyesha, wale wanaojitahidi kujitoa ili kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova, wanapata nini kutoka kwake?

10 Tunapata mazoezi zaidi kutoka kwa Yehova. Kenny, painia anayetumikia nchini Mauritius, alijionea ukweli huo. Alipojifunza kweli, aliacha masomo ya chuo kikuu, akabatizwa, na kuanza utumishi wa wakati wote. Anasema hivi: “Nilijitahidi kuishi kulingana na maneno ya nabii Isaya aliyesema hivi: ‘Mimi hapa! Nitume mimi!’” (Isa. 6:8) Kenny ameshiriki katika miradi kadhaa ya ujenzi na pia amesaidia kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha yake ya mama. Kenny anasema hivi: “Nilipata mazoezi yaliyonipatia ustadi niliohitaji ili kutimiza migawo yangu.” Lakini alijifunza mengi zaidi ya jinsi ya kufanya tu kazi. Anaongezea hivi: “Nilijifunza kuhusu mapungufu yangu na sifa nilizohitaji kusitawisha ili kuwa mtumishi mzuri zaidi wa Yehova.” (Soma 1 Petro 5:10.) Kwa nini usichunguze hali zako ili uone kama unaweza kufanya mabadiliko fulani na hivyo kuwa na fursa zaidi za kupata mazoezi kutoka kwa Yehova?

Wenzi wa ndoa wakihubiri kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri; dada kijana akifanya kazi kwenye ujenzi wa Jumba la Ufalme; wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa wakishiriki katika mahubiri ya simu. Wote wanapata shangwe kubwa kutokana na huduma yao (Tazama fungu la 11)

11. Akina dada nchini Korea Kusini walifanya jitihada gani ili washiriki zaidi katika huduma ya shambani, na wamepata matokeo gani? (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Hata Mashahidi wenye uzoefu wanahitaji mazoezi wanapojaribu njia mpya ya utumishi. Wakati wa janga la COVID-19, wazee wa kutaniko katika kutaniko moja nchini Korea Kusini, waliandika hivi: “Baadhi ya wahubiri ambao walikuwa hawawezi kutoka na kuhubiri kwa muda mrefu kwa sababu ya afya, sasa wanaweza kuhubiri kwa ukawaida kwa njia ya video. Akina dada watatu wenye umri wa zaidi ya miaka 80, walijifunza teknolojia hiyo mpya na sasa wanahubiri kila siku.” (Zab. 92:14, 15) Je, ungependa kupanua huduma yako na kuonja wema wa Yehova hata zaidi? Fikiria baadhi ya hatua unazoweza kuchukua zitakazokusaidia kufikia lengo hilo.

JINSI UNAVYOWEZA KUJITOA ILI KUFANYA MENGI ZAIDI

12. Yehova anawaahidi nini wale wanaomtegemea yeye?

12 Jifunze kumtegemea Yehova. Anaahidi kutumwagia baraka tunapomtumaini na kumpa kilicho bora. (Mal. 3:10) Dada anayeitwa Fabiola, kutoka nchini Kolombia, alijionea jinsi Yehova alivyotimiza ahadi hiyo. Alitaka kutumikia akiwa painia wa kawaida mara tu baada ya kubatizwa. Hata hivyo, mume wake na watoto wake watatu walitegemea kipato chake. Hivyo, alipofikia umri ambao angeweza kustaafu, alisali kwa Yehova kwa bidii ili amsaidie. Anasema hivi: “Kwa kawaida inachukua muda mrefu sana ili kupata malipo ya kustaafu, lakini katika kisa changu ilichukua mwezi mmoja tu. Ilikuwa kama muujiza!” Miezi miwili baadaye, alianza upainia. Sasa ana umri wa zaidi ya miaka 70 na amekuwa painia kwa zaidi ya miaka 20. Katika kipindi hicho, amewasaidia watu wanane kufikia hatua ya ubatizo. Anasema hivi: “Ingawa nyakati nyingine ninahisi nikiwa dhaifu, Yehova hunisaidia kila siku kushikamana na ratiba yangu.”

Abrahamu na Sara, Yakobo, na makuhani waliovuka Mto Yordani walionyeshaje kwamba walimtumaini Yehova? (Tazama fungu la 13)

13-14. Ni mifano gani inayoweza kukusaidia kumtumaini Yehova na kujitoa ili kufanya mengi zaidi?

13 Nufaika kutokana na mifano ya wale waliomtegemea Yehova. Biblia ina mifano mingi ya watu waliojitahidi sana katika utumishi wa Yehova. Katika visa vingi, watumishi hao wa Yehova walihitaji kuchukua hatua ya kwanza kabla ya kupokea baraka za pekee kutoka kwa Yehova. Kwa mfano, ni baada tu ya Abrahamu kuhama kutoka nyumbani—“ingawa hakujua mahali alipokuwa akienda”—ndipo Yehova alipombariki. (Ebr. 11:8) Ni baada tu ya Yakobo kupigana mweleka na malaika, ndipo alipopokea baraka ya pekee. (Mwa. 32:24-30) Taifa la Israeli lilipokuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi, watu waliweza kuvuka Mto Yordani uliokuwa umefurika baada tu ya makuhani kutumbukiza miguu yao kwenye mto huo.—Yos. 3:14-16.

14 Pia, unaweza kunufaika kutokana na mifano ya Mashahidi wa Yehova wa siku zetu ambao wamemtegemea Yehova na kujitoa ili kufanya mengi zaidi. Kwa mfano, ndugu anayeitwa Payton na Diana, mke wake, walifurahia kusoma masimulizi ya ndugu na dada ambao wamepanua utumishi wao kwa Yehova, kama wale wanaozungumziwa kwenye mfululizo, “Walijitoa Wenyewe kwa Hiari.” * Payton anasema hivi: “Tuliposoma masimulizi yao tulihisi kana kwamba tunamtazama mtu fulani anayefurahia mlo mtamu. Kadiri tulivyotazama, ndivyo tulivyotamani hata zaidi ‘kuonja na kujionea kwamba Yehova ni mwema.’” Mwishowe, Payton na Diana walihama ili wakatumikie kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa. Je, umesoma mfululizo huo? Na je, umetazama video Kuhubiri Katika Eneo la Mbali—Australia na Kuhubiri Katika Eneo la Mbali—Ireland zinazopatikana kwenye tovuti ya jw.org? Habari hizo huenda zikakusaidia kupata njia za kupanua utumishi wako.

15. Marafiki wanaofaa wanaweza kutusaidiaje?

15 Chagua marafiki wanaofaa. Kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kufurahia mlo fulani mpya, ikiwa watu tulio pamoja nao wanaufurahia pia. Vivyo hivyo, ikiwa tunashirikiana na watu ambao wanatanguliza utumishi wa Yehova maishani mwao, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba sisi pia tutatafuta njia za kupanua utumishi wetu kwa Mungu. Kent na Veronica, ambao ni wenzi wa ndoa, walijionea ukweli wa jambo hilo. Kent anasema hivi: “Marafiki na watu wa familia yetu walitutia moyo tujaribu njia mpya za utumishi. Tulitambua kwamba kushirikiana na wale wanaotafuta kwanza Ufalme maishani mwao, kulitupatia ujasiri wa kujaribu aina mpya ya utumishi.” Kent na Veronica sasa wanatumikia wakiwa mapainia wa pekee nchini Serbia.

16. Kama mfano wa Yesu kwenye Luka 12:16-21 unavyoonyesha, kwa nini tunapaswa kuwa tayari kujidhabihu?

16 Jidhabihu kwa ajili ya Yehova. Hatuhitaji kujinyima kila jambo tunalofurahia, ili kumpendeza Yehova. (Mhu. 5:19, 20) Hata hivyo, ikiwa tutasita kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Mungu kwa sababu tunataka kuepuka kudhabihu mambo fulani ya kibinafsi, tunaweza kufanya kosa kama la yule mwanamume katika mfano wa Yesu aliyefanya kazi kwa bidii na kuwa na vitu vingi vizuri lakini akampuuza Mungu. (Soma Luka 12:16-21.) Ndugu anayeitwa Christian, anayeishi nchini Ufaransa, anasema hivi: “Nilikuwa simpi Yehova na familia yangu kilicho bora ilipohusu muda na nguvu zangu.” Yeye na mke wake waliamua kufanya upainia. Lakini ili kufikia lengo hilo, walihitaji kuacha kazi zao. Ili kujitegemeza, walianzisha biashara ndogo ya kufanya usafi, na walijifunza kuridhika na mambo machache. Je, dhabihu yao ilikuwa ya bure? Christian anasema hivi: “Sasa tunafurahia zaidi huduma yenye matokeo na tunafurahia kuona wanafunzi wetu wa Biblia na watu tunaowarudia wakijifunza kumhusu Yehova.”

17. Ni jambo gani linaloweza kufanya tusite kujaribu njia mpya katika huduma yetu?

17 Uwe tayari kujaribu aina mpya za utumishi. (Mdo. 17:16, 17; 20:20, 21) Shirley, painia wa kawaida nchini Marekani, alihitaji kubadilisha njia aliyokuwa akifanya utumishi wakati wa janga la COVID-19. Mwanzoni, alisita kufanya mahubiri kwa njia ya simu. Hata hivyo, alipopata mazoezi wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko, alianza kufanya aina hiyo ya utumishi kwa ukawaida. Anasema hivi: “Mwanzoni niliogopa, lakini sasa ninafurahia sana. Tunawafikia watu wengi zaidi kuliko tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba! ”

18. Ni nini kinachoweza kutusaidia kukabiliana na changamoto tunapojitahidi kupanua huduma yetu?

18 Jiwekee lengo na ujitahidi kulitimiza. Tunapokabili changamoto, tunasali na kufanya yote tuwezayo ili tutumie uwezo wetu wa kufikiri kutambua jambo tunalohitaji kufanya. (Met. 3:21) Sonia, anayetumikia akiwa painia wa kawaida kwenye kikundi cha lugha ya Romani barani Ulaya, anasema hivi: “Ninapenda kuandika malengo yangu kwenye karatasi na kuiweka mahali ninapoweza kuiona. Kwenye meza yangu nina picha ya barabara zinazopishana kwenye njia panda. Ninapotaka kufanya uamuzi, ninaangalia barabara hizo mbili na kufikiria ikiwa uamuzi wangu utaniongoza kwenda upande utakaonifikisha kwenye malengo yangu au la.” Sonia anajitahidi kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu changamoto anazokabili. Anasema hivi: “Kila hali mpya ninayokabili inaweza kulinganishwa na ukuta unaoweza kunizuia au daraja linaloweza kunisaidia—inategemea mtazamo wangu.”

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Yehova anatubariki katika njia nyingi. Tunaweza kuonyesha jinsi tunavyothamini baraka hizo kwa kufanya yote tunayoweza ili kumletea sifa. (Ebr. 13:15) Hilo linaweza kutia ndani kutafuta njia mpya za kupanua huduma yetu, kisha tutampa Yehova nafasi ya kutubariki hata zaidi. Acheni kila siku, tutafute njia za ‘kuonja na kujionea kwamba Yehova ni mwema.’ Kisha tutakuwa kama Yesu, aliyesema: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kuimaliza kazi yake.”—Yoh. 4:34.

WIMBO 80 “Onjeni Mwone Kwamba Yehova Ni Mwema”

^ fu. 5 Yehova ndiye Chanzo cha wema. Anawaandalia mambo mazuri watu wote—hata watu waovu. Lakini anapenda hasa kuwatendea mema waabudu wake waaminifu. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi Yehova anavyowaonyesha wema watumishi wake. Pia, tutachunguza jinsi ambavyo wale wanaopanua huduma yao wanaweza kujionea wema wa Yehova kwa njia ya pekee.

^ fu. 7 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 14 Awali mfululizo huo ulikuwa ukichapishwa kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi, sasa unapatikana kwenye jw.org. Tafuta kwenye KUTUHUSU > MASIMULIZI > KUFIKIA MIRADI YA KIROHO.