Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”

“Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”

“Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.”YAK. 1:4.

NYIMBO: 135, 139

1, 2. (a) Tunajifunza nini kutokana na uvumilivu wa Gideoni na wanaume wake 300? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kulingana na Luka 21:19, kwa nini uvumilivu ni muhimu sana?

VITA vilikuwa vimepamba moto. Wanajeshi wa Israeli wakiongozwa na Mwamuzi Gideoni walikuwa wamewafuatilia adui zao, jeshi la Wamidiani na washirika wao, usiku kucha kwa umbali wa kilometa 32. Biblia inasimulia kilichotokea baadaye: “Gideoni akaja Yordani, akauvuka, yeye pamoja na wale wanaume mia tatu waliokuwa pamoja naye, wakiwa wamechoka.” Hata hivyo, Gideoni na wanaume wake bado hawakuwa wameshinda vita, kwa maana kulikuwa kungali na wanajeshi 15,000 hivi ambao walihitaji kupigana nao. Waisraeli walikuwa wamekandamizwa na Wamidiani kwa miaka mingi, hivyo walijua kwamba huo haukuwa wakati wa kurudi nyuma. Kwa hiyo, ili kuwaangamiza adui zao, ‘waliendelea kuwafuatilia’ nao wakawashinda Wamidiani.—Amu. 7:22; 8:4, 10, 28.

2 Sisi pia tunapambana vita vikali. Adui zetu ni pamoja na Shetani, ulimwengu wake, na udhaifu wetu. Baadhi yetu tumepambana kwa makumi ya miaka, na kwa msaada wa Yehova, tumefanikiwa kushinda. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda tukachoka kupambana na adui zetu na vilevile tukachoka kusubiri mwisho wa mfumo huu wa mambo. Bila shaka, bado hatujapata ushindi kamili katika pambano letu. Yesu alionya kuwa sisi tunaoishi katika siku za mwisho tungekabili majaribu makali na kutendewa kikatili, lakini pia alisema kwamba kupata ushindi kungetegemea uvumilivu wetu. (Soma Luka 21:19.) Uvumilivu ni nini? Ni nini kitakachotusaidia tuvumilie? Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa wale waliovumilia? Na tunawezaje kuacha “uvumilivu ukamilishe kazi yake”?—Yak. 1:4.

UVUMILIVU NI NINI?

3. Uvumilivu ni nini?

3 Kulingana na Biblia, uvumilivu unahusisha mengi zaidi ya kustahimili tu majaribu au hali ngumu. Uvumilivu unahusisha akili na moyo wetu, au namna tunavyotenda tunapokabili hali ngumu. Mtu anayevumilia anaonyesha sifa ya ujasiri, uimara, na subira. Kitabu kimoja kinasema kwamba uvumilivu ni ‘mtazamo unaomwezesha mtu kustahimili mambo, si kwa sababu tu hana la kufanya bali kwa sababu ana tumaini thabiti. Ni sifa inayomwezesha mtu kusimama imara huku akiendelea kukabili tatizo fulani. Ni sifa nzuri inayoweza kufanya jaribu kali sana lionekane kuwa jambo linaloleta utukufu kwa sababu ingawa kuna maumivu, bado kuna tumaini.’

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba upendo ndio hutuchochea tuvumilie?

4 Upendo ndio huwachochea Wakristo wavumilie. (Soma 1 Wakorintho 13:4, 7.) Kumpenda Yehova kunatuchochea tuvumilie jambo lolote analoruhusu litupate. (Luka 22:41, 42) Kuwapenda ndugu zetu kunatusaidia tuvumilie udhaifu wao. (1 Pet. 4:8) Kumpenda mwenzi wetu wa ndoa hutuwezesha kuvumilia “dhiki” ambazo hata wenzi wa ndoa wenye furaha hukabili na hutusaidia tuimarishe kifungo chetu cha ndoa.—1 Kor. 7:28.

NI NINI KITAKACHOKUSAIDIA UVUMILIE?

5. Kwa nini Yehova ndiye anayeweza kutupatia msaada bora zaidi ili tuvumilie?

5 Mwombe Yehova akupe nguvu. Yehova ni “Mungu anayetoa uvumilivu na faraja.” (Rom. 15:5) Yeye pekee ndiye anayeelewa kikamili matatizo tunayokabili na vilevile jinsi mazingira yetu, hisia, na chembe za urithi zinavyotuathiri. Hivyo, yeye ndiye anayeweza kutupatia msaada bora zaidi ili tuvumilie. Biblia inasema hivi: “Atawatimizia wale wanaomwogopa tamaa yao, naye atakisikia kilio chao cha kuomba msaada, naye atawaokoa.” (Zab. 145:19) Hata hivyo, Mungu hujibu jinsi gani tunapomwomba atupatie nguvu za kuvumilia?

6. Kama ilivyoahidiwa katika Biblia, Yehova ‘anafanyaje njia ya kutokea’ tunapokabili majaribu?

6 Soma 1 Wakorintho 10:13. Tunapomwomba Yehova msaada wa kukabiliana na majaribu, anaahidi kwamba ‘ataifanya njia ya kutokea.’ Je, Yehova anaingilia kati na kuondoa jaribu? Anaweza kufanya hivyo. Lakini katika visa vingi anafanya njia ya kutokea “kusudi [tuweze] kulivumilia.” Naam, Yehova hutuimarisha ili tuvumilie “kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Kol. 1:11) Kwa kuwa anaelewa vizuri sana uwezo wetu wa kimwili, kiakili, na kihisia, Yehova hataruhusu kamwe hali fulani iendelee kuwa ngumu sana hivi kwamba tushindwe kudumisha uaminifu.

7. Toa mfano unaoonyesha ni kwa nini tunahitaji chakula cha kiroho ili tuvumilie.

7 Imarisha imani yako kwa kujilisha kiroho. Ili kupanda Mlima Everest, ambao ni mlima mrefu zaidi duniani, kwa siku moja mpandaji anahitaji kula chakula ambacho kwa kawaida angekula kwa siku tatu au nne. Hilo litamsaidia avumilie na kutimiza lengo lake la kufika kileleni. Vivyo hivyo, ili tuvumilie katika maisha yetu ya Kikristo na kufikia lengo letu, tunapaswa kula kwa ukawaida chakula kingi cha kiroho. Tunahitaji kujitia nidhamu ili kutenga wakati wa kusoma, kujifunza, na kuhudhuria mikutano yetu ya Kikristo. Mambo hayo yanaimarisha imani yetu na kutupatia “chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele.”—Yoh. 6:27.

8, 9. (a) Kulingana na Ayubu 2:4, 5, ni jambo gani linalohusika tunapokabili majaribu? (b) Unaweza kuwazia tukio gani unapokabili majaribu?

8 Kumbuka suala la utimilifu. Mtumishi wa Yehova anapokuwa chini ya jaribu, kuna mambo mengi yanayohusika zaidi ya mateso anayokabili. Namna tunavyotenda tunapokabili majaribu, huonyesha ikiwa kweli tunamwona Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu. Shetani, adui wa enzi kuu ya Yehova, alimdhihaki Yehova kwa maneno haya: “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake. Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa [wa Ayubu] na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” (Ayu. 2:4, 5) Kulingana na Shetani, hakuna mwanadamu anayempenda na kumtumikia Yehova bila ubinafsi. Je, Shetani amebadilika tangu alipotoa dai hilo? La hasha! Karne nyingi baadaye, alipotupwa kutoka mbinguni, bado Shetani aliitwa “mshtaki wa ndugu zetu . . . , anayewashtaki mchana na usiku mbele za Mungu wetu!” (Ufu. 12:10) Shetani hajasahau suala la utimilifu. Anatamani sana kuona tukishindwa na majaribu na tukiacha kuunga mkono enzi kuu ya Mungu.

9 Kwa hiyo, unapokabili hali ngumu, wazia tukio hili. Shetani na roho wake waovu wako upande mmoja, wakikutazama jinsi unavyopambana na majaribu, nao wanadai kwamba utakata tamaa na mwishowe utashindwa. Upande mwingine yupo Yehova, Mwana wake anayetawala, watiwa mafuta waliofufuliwa, na maelfu ya malaika. Wanakutia moyo, nao wanafurahi sana kukuona kila siku ukivumilia na kuunga mkono enzi kuu ya Yehova. Kisha unamsikia Yehova akikuambia hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”—Met. 27:11.

10. Unaweza kumwigaje Yesu kwa kukazia fikira thawabu ya uvumilivu?

10 Kazia fikira thawabu ya kuendelea kuvumilia. Wazia kwamba unasafiri safari ndefu inayohusisha kupita kwenye sehemu ya barabara iliyo chini ya ardhi. Ukiwa katikati ya sehemu hiyo, unatazama huku na huku na kila mahali ni giza tititi. Hata hivyo, una uhakika kwamba ikiwa utaendelea kusafiri hadi mwisho, utaona tena mwanga. Vivyo hivyo, nyakati nyingine huenda ukahisi umelemewa na matatizo unayokabili. Hata Yesu angeweza kuhisi hivyo. Alikuwa shabaha ya ‘maneno yenye kupinga yaliyotolewa na watenda-dhambi,’ aliaibishwa, na hata aliuawa kikatili kwenye “mti wa mateso”; kwa kweli hicho kilikuwa kipindi cha giza zito zaidi katika maisha yake duniani! Hata hivyo, Yesu alivumilia yote hayo kwa sababu ya “shangwe iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2, 3) Alikazia fikira thawabu ambayo angepata kutokana na uvumilivu wake, hasa mchango wake katika kulitakasa jina la Mungu na kutetea enzi kuu ya Yehova. Giza, yaani majaribu ambayo Yesu alikabili yalikuwa ya muda mfupi, lakini utukufu wa thawabu yake ya mbinguni ungekuwa wa milele. Leo, majaribu unayokabili yanaweza kuwa makali sana na huenda yakakulemea. Lakini kumbuka kwamba dhiki zako katika barabara inayoelekea kwenye uzima wa milele ni za muda mfupi.

“WALE AMBAO WAMEVUMILIA”

11. Kwa nini tunapaswa kuchunguza mambo waliyopitia “wale ambao wamevumilia”?

11 Si sisi peke yetu tunaovumilia hali ngumu. Mtume Petro aliandika hivi ili kuwatia moyo Wakristo wavumilie hali ngumu zinazosababishwa na Shetani: “Chukueni msimamo mkampinge yeye, mkiwa imara katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu ulimwenguni.” (1 Pet. 5:9) Mambo waliyopitia “wale ambao wamevumilia” yanatusaidia tuendelee kusimama imara, yanatuhakikishia kuwa tunaweza kufanikiwa na kutukumbusha kwamba uaminifu wetu utathawabishwa. (Yak. 5:11) Acheni tuchunguze mifano michache. [1]

12. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa makerubi waliowekwa katika Edeni?

12 Makerubi. Mfano uliowekwa na baadhi ya viumbe wa roho wa kwanza kuonekana kwa wanadamu, unaweza kutufundisha kuwa wavumilivu tunapopata mgawo mgumu. Yehova Mungu “akaweka upande wa mashariki wa bustani ya Edeni makerubi na upanga unaowaka ambao ulikuwa unajizungusha-zungusha ili kuilinda njia ya kwenda kwenye ule mti wa uzima.” [2] (Mwa. 3:24) Ni wazi kwamba makerubi hao hawakuumbwa kwa kusudi la kupewa mgawo huo! Kwa kweli, dhambi na uasi haukuwa sehemu ya kusudi la Yehova kwa wanadamu. Hata hivyo, hatusomi popote kwamba makerubi, viumbe wa roho wenye cheo cha juu, walilalamika kwamba kazi waliyopewa ilikuwa ya hali ya chini sana. Hawakuchoka wala kukata tamaa. Badala yake, walishikamana kwa utiifu na mgawo wao na kuvumilia kwa zaidi ya miaka 1,600 hadi kazi yao ilipokwisha, labda wakati wa Gharika!

13. Ni nini kilichomsaidia Ayubu avumilie majaribu?

13 Mzee wa ukoo Ayubu. Ikiwa umevunjwa moyo na maneno yenye kuumiza ya rafiki au mshiriki wa familia yako, unasumbuliwa na ugonjwa mbaya, au unahuzunika kwa sababu ya kufiwa na mpendwa wako, unaweza kupata faraja kutokana na mfano wa Ayubu. (Ayu. 1:18, 19; 2:7, 9; 19:1-3) Ingawa hakujua ni nani aliyekuwa akimsababishia matatizo, Ayubu hakukata tamaa. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba alikuwa “mwenye kumwogopa Mungu.” (Ayu. 1:1) Ayubu aliazimia kumfurahisha Yehova chini ya hali zote, ziwe nzuri au mbaya. Mungu alimsaidia Ayubu atafakari mambo ya ajabu ambayo tayari Yehova alikuwa ameyafanya kupitia roho Yake takatifu. Ayubu akawa na uhakika zaidi kwamba Yehova angekomesha mateso yake kwa wakati unaofaa. (Ayu. 42:1, 2) Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. “Yehova akaigeuza hali ya mateka ya Ayubu . . .  na Yehova akaanza kumpa na kumwongezea Ayubu vyote vilivyokuwa vyake, kiasi cha mara mbili.” Ayubu aliishi miaka mingi naye akawa “mzee na mwenye kushiba siku.”—Ayu. 42:10, 17.

14. Kama 2 Wakorintho 1:6 inavyosema, uvumilivu wa Paulo uliwasaidiaje wengine?

14 Mtume Paulo. Je, unakabili upinzani mkali, au mateso, kutoka kwa maadui wa ibada ya kweli? Je, wewe ni mzee wa kutaniko au mwangalizi wa mzunguko na unahisi kwamba majukumu yako yanakulemea? Tafakari mfano wa Paulo. Alikabili ‘mambo mengi ya aina ya nje’ kutoka kwa watu waliomtesa vikali, na kila siku alikuwa na mkazo kwa sababu ya kuyahangaikia makutaniko. (2 Kor. 11:23-29) Hata hivyo, hakukata tamaa kamwe, na mfano wake uliwaimarisha wengine. (Soma 2 Wakorintho 1:6.) Unapovumilia hali ngumu, kumbuka kwamba mfano wako unaweza kuwatia moyo wengine waendelee kuvumilia.

JE, UVUMILIVU ‘UTAKAMILISHA KAZI YAKE’ KWAKO?

15, 16. (a) Ni “kazi” gani inayopaswa kukamilishwa na uvumilivu? (b) Toa mifano inayoonyesha jinsi tunavyoweza kuacha “uvumilivu ukamilishe kazi yake.”

15 Yakobo aliandika hivi chini ya mwongozo wa roho takatifu: “Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake.” Ni “kazi” gani inayopaswa kukamilishwa na uvumilivu? Uvumilivu unatusaidia tuwe “kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yak. 1:4) Mara nyingi, majaribu hufunua udhaifu na sifa za utu wetu ambazo tunahitaji kuboresha. Tunapovumilia majaribu hayo, utu wetu wa Kikristo unakuwa kamili au timamu zaidi. Kwa mfano, tunaweza kuwa na subira, shukrani, na huruma zaidi.

Tunapovumilia majaribu, utu wetu wa Kikristo unakuwa kamili zaidi (Tazama fungu la 15 na 16)

16 Kwa kuwa uvumilivu unakamilisha kazi muhimu sana ya kutufinyanga tukiwa Wakristo, usilegeze kamwe kanuni za Maandiko ili tu kukwepa majaribu unayokabili. Kwa mfano, vipi ikiwa unapambana na mawazo machafu? Badala ya kukubali kushawishika, mwombe Yehova akusaidie ili upinge tamaa hizo. Kufanya hivyo kutaimarisha sifa yako ya kujizuia. Je, unakabili upinzani kutoka kwa mshiriki wa familia ambaye si Shahidi? Badala ya kukubali kushinikizwa, azimia kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote. Ukifanya hivyo utaimarisha imani yako kwa Yehova. Kumbuka: Ili tupate kibali cha Mungu, ni lazima tuvumilie.—Rom. 5:3-5; Yak. 1:12.

17, 18. (a) Toa mfano unaoonyesha umuhimu wa kuvumilia mpaka mwisho. (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani mwisho unapokaribia?

17 Ni lazima tuvumilie, si kwa muda mfupi, bali hadi mwisho. Kwa mfano: Wazia meli inayozama. Ili abiria waokoke, ni lazima waogelee mpaka ufukweni. Abiria anayekata tamaa akiwa karibu tu kufika ufukweni atakufa maji sawa na yule aliyekata tamaa ya kuogelea mapema zaidi. Vivyo hivyo, tumeazimia kuvumilia hadi tufike kwenye ulimwengu mpya. Uhai wetu unategemea uvumilivu wetu. Tuna mtazamo kama ule wa mtume Paulo, ambaye mara mbili alisema hivi: “Hatufi moyo.”—2 Kor. 4:1, 16.

18 Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatusaidia tuvumilie mpaka mwisho. Tuna imani kama ya Paulo, ambaye aliandika hivi kwenye Waroma 8:37-39: “Tunatokea tukiwa tumeshinda kabisa kupitia yeye aliyetupenda. Kwa maana nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Ni kweli kwamba nyakati fulani tutachoka. Lakini acheni tuvumilie mpaka mwisho, ili hatimaye isemwe hivi kutuhusu sisi kama ilivyosemwa kwa Gideoni na wanaume wake: ‘Waliendelea kufuatilia.’—Amu. 8:4.

^ [1] (fungu la 11) Utatiwa moyo pia ukisoma masimulizi yanayohusu uvumilivu wa watu wa Mungu katika nyakati zetu. Kwa mfano, Kitabu cha Mwaka cha 1992, 1999, na 2008 kina ripoti za ndugu zetu kutoka Ethiopia, Malawi, na Urusi ambazo zinaimarisha sana imani.

^ [2] (fungu la 12) Biblia haisemi ni makerubi wangapi walipewa kazi hiyo.