Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Msimamo wa Kikristo Katika Ulimwengu Uliogawanyika

Dumisha Msimamo wa Kikristo Katika Ulimwengu Uliogawanyika

“Mlipeni . . . Mungu vitu vya Mungu.”—MT. 22:21.

NYIMBO: 33, 137

1. Tunawezaje kumtii Mungu na vilevile serikali za wanadamu?

NENO LA MUNGU linatuambia tuzitii serikali za wanadamu, lakini pia linatufundisha kwamba tunapaswa kumtii Mungu kuliko wanadamu. (Mdo. 5:29; Tito 3:1) Je, mafundisho hayo yanapingana? La hasha! Kanuni ya ujitiisho wa kadiri inatusaidia kuelewa na kutii amri hizo. Yesu alitoa kanuni ya kukata maneno aliposema hivi: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” [1] (Mt. 22:21) Tunaweza kufuata jinsi gani mwongozo wa Yesu? Tunajitiisha chini ya mamlaka za serikali kwa kutii sheria zake, kuwaheshimu maofisa, na kulipa kodi wanazodai. (Rom. 13:7) Hata hivyo, serikali za wanadamu zikituambia tumwasi Mungu, kwa heshima tutakataa kufanya hivyo.

2. Tunaonyeshaje kwamba hatuungi mkono upande wowote katika siasa za ulimwengu?

2 Kwa kadiri fulani tunamlipa Mungu vitu vya Mungu tunapodumisha msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. (Isa. 2:4) Kwa hiyo, hatupingi serikali yoyote ya kibinadamu ambayo Yehova ameruhusu iwepo; wala hatujihusishi na shughuli za kizalendo au za kitaifa. (Rom. 13:1, 2) Hatuwashawishi viongozi wa kisiasa wafanye mambo tunayotaka, hatupigi kura, hatugombei vyeo vya kisiasa, wala hatujaribu kubadili mifumo ya serikali.

3. Kwa nini hatupaswi kuunga mkono upande wowote?

3 Biblia inatueleza kwa nini Mungu hataki tuunge mkono upande wowote. Kwa mfano, tunafuata mafundisho na mfano wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, wa kutokuwa “sehemu ya ulimwengu,” kwa kuepuka siasa na vita. (Yoh. 6:15; 17:16) Tunapaswa kudumisha msimamo wetu wa Kikristo ili tuwe raia washikamanifu wa Ufalme wa Mungu. Vinginevyo, tungewezaje kuwa na dhamiri safi tunapowahubiria watu habari njema kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio unaoweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu? Isitoshe, tofauti na dini za uwongo zinazowagawanya waumini wake kwa kujihusisha katika siasa, ibada ya kweli inaendeleza undugu wetu wa kimataifa kwa kutusaidia kudumisha msimamo wetu wa Kikristo.—1 Pet. 2:17.

4. (a) Tunajuaje kwamba itazidi kuwa vigumu kudumisha msimamo wetu wa Kikristo? (b) Kwa nini tunapaswa kujitayarisha sasa kudumisha msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote?

4 Huenda hali ya kisiasa ni tulivu katika eneo letu na inaturuhusu kuendeleza ibada ya kweli. Hata hivyo, kadiri mfumo wa Shetani unavyokaribia mwisho, tunatazamia kwamba itakuwa vigumu zaidi kudumisha msimamo wa Kikristo. Ulimwengu umejaa watu “wasiotaka makubaliano yoyote” na “wenye vichwa vigumu,” hivyo utazidi kugawanyika. (2 Tim. 3:3, 4) Katika nchi fulani, tayari ndugu zetu wanakabili changamoto mbalimbali kwa kutounga mkono upande wowote kwa sababu ya mabadiliko makubwa ya hali ya kisiasa. Hiyo ndiyo sababu tunahitaji kuimarisha sasa azimio letu la kutounga mkono upande wowote. Tukisubiri mpaka tukabili hali ngumu, tunaweza kulegeza na kupoteza msimamo wetu. Basi tunaweza kujitayarishaje kudumisha msimamo wetu wa Kikristo katika ulimwengu huu uliogawanyika? Acheni tuzungumzie mambo manne yatakayotusaidia kufanya hivyo.

UWE NA MAONI KAMA YA YEHOVA KUHUSU SERIKALI ZA WANADAMU

5. Yehova anazionaje serikali za wanadamu?

5 Jambo la kwanza litakalotusaidia kudumisha msimamo wetu ni kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu mifumo ya kisiasa. Ingawa baadhi ya serikali zinaweza kuonekana zinazingatia haki, Yehova hakukusudia kamwe mwanadamu amtawale mwanadamu mwenzake. (Yer. 10:23) Serikali za wanadamu zinaendeleza utaifa, ambao unasababisha migawanyiko. Hata watawala bora zaidi wa kibinadamu hawawezi kusuluhisha matatizo yote ya wanadamu. Kwa kuongezea, tangu 1914, serikali za wanadamu zimepinga Ufalme wa Mungu, ambao hivi karibuni utatekeleza hukumu dhidi ya mataifa kwa kuyaangamiza.—Soma Zaburi 2:2, 7-9.

6. Tunapaswa kuwatendeaje wenye mamlaka serikalini?

6 Mungu ameruhusu serikali za wanadamu ziwepo kwa sababu zinadumisha hali ya amani kwa kadiri fulani, na hilo linatusaidia kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Rom. 13:3, 4) Mungu hata anatuagiza tusali kwa ajili ya wenye mamlaka, hasa ikiwa maamuzi yao yanaweza kuathiri ibada yetu. (1 Tim. 2:1, 2) Kama mtume Paulo, wakati mwingine tunakata rufaa kwa mamlaka za serikali ili tutendewe kwa haki. (Mdo. 25:11) Ingawa Biblia inasema kwamba mpinzani wa Mungu, Shetani, ana mamlaka juu ya mifumo ya kisiasa, haisemi kwamba anamwongoza moja kwa moja kila kiongozi au mtawala. (Luka 4:5, 6) Kwa hiyo, hatupaswi kutoa wazo linalodokeza kwamba mtawala fulani anaongozwa na Ibilisi. Badala yake, tunaposhughulika na “serikali na mamlaka,” tunaepuka ‘kusema vibaya juu ya yeyote.’—Tito 3:1, 2.

7. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani?

7 Tunamtii Mungu kwa kutompendelea kamwe mgombea au chama chochote cha kisiasa bila kujali ikiwa tunakubaliana na sera zake au la. Msimamo wetu unaweza kujaribiwa jinsi gani katika jambo hilo? Wazia kwamba kikundi fulani cha wanaharakati kinapinga serikali kwa sababu ya uonevu ambao umewaathiri hata watu wa Mungu. Ingawa hatutaandamana pamoja nao, je inawezekana moyoni mwetu tukawaunga mkono? (Efe. 2:2) Hatupaswi kuunga mkono upande wowote, si kwa maneno na matendo pekee, bali hata moyoni.

UWE MWENYE “KUJIHADHARI” LAKINI USIWE NA “HATIA”

8. Inapokuwa vigumu kudumisha msimamo wetu wa Kikristo, tunawezaje kuwa wenye “kujihadhari” na wakati huohuo kutokuwa na “hatia”?

8 Jambo la pili litakalotusaidia kudumisha msimamo wetu ni kuwa wenye “kujihadhari kama nyoka na hata hivyo wasio na hatia kama njiwa” tunapokabili hali ngumu. (Soma Mathayo 10:16, 17.) Tunachukua tahadhari kwa kutambua hatari mapema, na tunaepuka hatia kwa kutoruhusu hatari hizo zilegeze msimamo wetu. Fikiria changamoto kadhaa na jinsi tunavyoweza kukabiliana nazo.

9. Tunapaswa kujihadhari na nini tunapozungumza na wengine?

9 Mazungumzo. Tunapaswa kujihadhari watu wanapozungumzia masuala ya kisiasa. Kwa mfano, unapohubiri ujumbe wa Ufalme, epuka kusifia au kukosoa sera za chama au kiongozi fulani. Jaribu kuzungumzia jambo ambalo nyote mnakubaliana kwa kukazia fikira chanzo cha tatizo badala ya suluhisho lolote linalopendekezwa na viongozi wa kisiasa. Kisha, zungumzia Maandiko yanayoonyesha jinsi serikali ya Mungu itakavyoleta suluhisho kamili na la kudumu. Unapokumbana na masuala yanayozua ubishi kama vile ndoa za jinsia moja au kutoa mimba, tetea viwango vya Mungu na ueleze jinsi tunavyofuata viwango hivyo maishani mwetu. Unapozungumzia mambo hayo, usiunge mkono kamwe hoja yoyote ya kisiasa kuhusiana na mada hizo. Hatuungi mkono upande wowote inapohusu ni sheria gani inapaswa kutungwa, kufutwa, au kubadilishwa, na hatuwashinikizi wengine wakubali maoni yetu.

10. Tunapotazama au kusoma habari fulani, tunaweza kuhakikishaje kwamba hatuungi mkono upande wowote?

10 Vyombo vya habari. Mara nyingi habari hutolewa kwa njia ambayo inaunga mkono upande fulani. Wakati mwingine vyombo vya habari hutumiwa kwa faida ya wanasiasa. Katika nchi ambazo vyombo vya habari vinamilikiwa na serikali, habari zinazotolewa zinaweza kuegemea upande mmoja. Lakini hata Wakristo wanaoishi katika zile zinazoitwa nchi huru, wanapaswa kuwa waangalifu wasiunge mkono maoni ya wachambuzi. Jiulize hivi, ‘Je, mimi hufurahia kumsikiliza mtu fulani katika vyombo vya habari kwa sababu ninakubaliana na sera zake za kisiasa?’ Ikiwa ndivyo, basi jaribu kutafuta vyanzo vya habari visivyoegemea upande fulani. Vyovyote vile, ni busara kudhibiti habari tunazopata kutoka kwenye vyombo vya habari vinavyoendeleza mada za kisiasa, na tunahitaji kutumia “kielelezo cha maneno yenye afya,” kilicho katika Biblia, kupima habari tunazopokea.—2 Tim. 1:13.

11. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kudumisha msimamo wetu wa Kikristo ikiwa tunapenda sana mali zetu?

11 Vitu vya kimwili. Ikiwa tunapenda sana mali zetu, tunaweza kuwa katika hatari ya kulegeza msimamo wetu wa Kikristo tunapojaribiwa. Ruth, kutoka Malawi, alishuhudia Mashahidi kadhaa wakifanya hivyo walipokabili mateso katika miaka ya 1970. Anakumbuka hivi: “Hawakuwa tayari kuacha maisha yao ya starehe. Wengine walienda uhamishoni pamoja nasi lakini baadaye walijiunga na chama cha kisiasa na kurudi nyumbani kwa sababu hawakutaka kuvumilia maisha magumu katika kambi ya wakimbizi.” Tofauti na hilo, watumishi wengi wa Mungu wamedumisha msimamo wao wa Kikristo licha ya matatizo ya kiuchumi au kupoteza kila kitu walichokuwa nacho.—Ebr. 10:34.

12, 13. (a) Yehova anawaonaje wanadamu? (b) Tunaweza kujuaje ikiwa tumeanza kujivuna kwa sababu ya nchi yetu?

12 Majivuno. Mara nyingi watu hujivunia rangi, kabila, utamaduni, jiji, au taifa lao. Hata hivyo, kujivuna kwa sababu ya kabila, utamaduni, au taifa kutafanya tusiwe na maoni kama ya Yehova kuhusu utawala wa wanadamu na familia ya wanadamu. Bila shaka, Mungu hatarajii tukane utamaduni wetu. Kwa kweli, tofauti za kitamaduni zinaonyesha kwa njia yenye kuvutia jinsi familia ya wanadamu ilivyo na watu wa namna mbalimbali. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba watu wote ni sawa machoni pa Mungu.—Rom. 10:12.

13 Kujivuna kwa sababu ya mahali tulipozaliwa ni chanzo cha uzalendo, na inaweza kuwa hatua ya kwanza ya kulegeza msimamo wetu wa Kikristo. Wakristo pia wanaweza kuathiriwa na mtazamo huo, kwa kuwa hata baadhi ya washiriki wa kutaniko la karne ya kwanza waliwabagua ndugu zao kwa sababu ya taifa lao. (Mdo. 6:1) Mtu anaweza kujuaje ikiwa ameanza kuwa na majivuno? Wazia ikiwa ndugu au dada kutoka nchi nyingine anakupa pendekezo fulani. Je, utalikataa na kusema hivi moyoni, ‘Hapa kwetu sisi hufanya mambo vizuri zaidi kuliko wao’? Badala ya kufanya hivyo, tunahitaji kufuata ushauri huu: ‘Kwa unyenyekevu wa akili waoneni wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.’—Flp. 2:3.

TEGEMEA NGUVU ZA YEHOVA

14. Sala inaweza kutusaidiaje, na Biblia inathibitishaje jambo hilo?

14 Jambo la tatu litakalotusaidia kudumisha msimamo wetu ni kutegemea nguvu za Yehova. Omba roho takatifu, ambayo inaweza kukusaidia uwe na subira na sifa ya kujidhibiti. Sifa hizo zitakusaidia ikiwa serikali inatenda isivyo haki au kwa ufisadi. Pia, unaweza kumwomba Yehova akupe hekima ili utambue na ujue jinsi ya kushughulikia hali inayoweza kuhatarisha msimamo wako wa Kikristo. (Yak. 1:5) Ikiwa umefungwa gerezani au umeadhibiwa kwa njia nyingine yoyote kwa sababu ya msimamo wako thabiti katika ibada ya kweli, mwombe Yehova akupe nguvu za kutetea imani yako kwa ujasiri na kuvumilia mateso yoyote utakayokabili.—Soma Matendo 4:27-31.

15. Biblia inaweza kutusaidiaje tudumishe msimamo wetu? (Tazama pia sanduku lenye kichwa “Neno la Mungu Liliimarisha Azimio Lao.”)

15 Yehova anaweza kutumia Neno lake kukuimarisha. Tafakari maandiko yatakayokusaidia udumishe msimamo wako wa Kikristo chini ya majaribu. Yaweke katika kumbukumbu yako sasa kwa kuwa yatakusaidia wakati ujao ikiwa hutaweza kupata Biblia. Neno la Mungu linaweza pia kuimarisha tumaini lako la wakati ujao kuhusu baraka za Ufalme. Tunahitaji sana tumaini hilo ili tuvumilie mateso. (Rom. 8:25) Chagua maandiko yanayozungumzia baraka ambazo unatazamia kwa hamu sana, na uwazie jinsi utakavyofurahia baraka hizo katika Paradiso.

WAIGE WALE WALIODUMISHA MSIMAMO WAO

16, 17. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa watumishi waaminifu wa Mungu waliodumisha msimamo wao? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

16 Jambo la nne litakalotusaidia kudumisha msimamo wetu wa Kikristo ni kuwafikiria watumishi waaminifu wa Yehova. Mifano yao inaweza kutupatia hekima na nguvu tunazohitaji ili tuvumilie. Kwa mfano, Shadraki, Meshaki na Abednego walikataa kuabudu sanamu iliyowakilisha Serikali ya Babiloni. (Soma Danieli 3:16-18.) Kusoma kuhusu azimio lao kumewasaidia Mashahidi wengi leo wawe na ujasiri wa kukataa kuabudu bendera ya taifa. Pia, Yesu hakujihusisha kamwe na migogoro ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu. Akijua jinsi mfano wake unavyoweza kuwasaidia wengine, aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yoh. 16:33.

17 Mashahidi wengi wa Yehova leo wamedumisha msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Wengi wao wameteswa, wamefungwa gerezani, au kufa kwa sababu ya imani yao. Mifano yao inaweza kukusaidia kama ilivyomsaidia Barış, kutoka Uturuki, ambaye alisema hivi: “Franz Reiter alikuwa ndugu kijana ambaye aliuawa kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi la Hitler. Barua aliyomwandikia mama yake usiku wa kabla ya kifo chake inaonyesha alikuwa na uhakika na imani kubwa katika Yehova, na nilitaka kufuata mfano wake ikiwa ningekabili jaribu kama hilo.” [2]

18, 19. (a) Washiriki wa kutaniko lenu wanaweza kukusaidiaje udumishe msimamo wako wa Kikristo? (b) Umeazimia kufanya nini?

18 Ndugu na dada katika kutaniko lenu wanaweza kukusaidia pia. Waeleze wazee majaribu unayokabili kuhusu msimamo wako wa Kikristo, na uwaombe ushauri unaotegemea Biblia. Washiriki wa kutaniko wanaweza kukutia moyo ikiwa watajua changamoto unazokabili. Waombe wasali kwa niaba yako. Bila shaka, ikiwa tunataka ndugu zetu watusaidie na wasali kwa niaba yetu, tunapaswa kuwatendea vivyo hivyo pia. (Mt. 7:12) Makala yenye kichwa “Mashahidi wa Yehova Walio Gerezani kwa Sababu ya Imani Yao—Kulingana na Eneo” iliyo katika tovuti ya jw.org/sw, chini ya HABARI > MAMBO YA KISHERIA, inaweza kukusaidia utaje mambo hususa katika sala zako. Makala hiyo ina viunganishi vya makala zinazoorodhesha Mashahidi ambao sasa wako gerezani kwa sababu ya imani yao. Chagua majina kadhaa, na usali kwa niaba yao ili waendelea kuwa na ujasiri wa kudumisha msimamo wao.—Efe. 6:19, 20.

19 Kadiri serikali za wanadamu zinavyokaribia mwisho wake, hatutashangaa ikiwa zitaendelea kuchukizwa na ushikamanifu wetu kwa Yehova na Ufalme wake. Kwa hiyo, acheni tuimarishe sasa azimio letu la kudumisha msimamo wetu wa Kikristo katika ulimwengu huu uliogawanyika.

^ [1] (fungu la 1) Yesu alimtaja Kaisari, ambaye alikuwa kiongozi wa juu zaidi wakati huo, kuwakilisha wenye mamlaka au Serikali.

^ [2] (fungu la 17) Tazama kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 662, na sanduku lenye kichwa, “Alikufa kwa Sababu ya Kumheshimu Mungu” katika sura ya 14 ya kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala!.