Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uaminifu Hutuwezesha Kupata Kibali cha Mungu

Uaminifu Hutuwezesha Kupata Kibali cha Mungu

“Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—EBR. 6:12.

NYIMBO: 86, 54

1, 2. Yeftha na binti yake walikabili changamoto gani?

MWANAMKE kijana anafarijika sana kumwona baba yake akirudi kutoka vitani salama salimini. Alikuwa akimsubiri kwa wasiwasi sana. Sasa anamwona baba yake akirudi na ushindi mkubwa, naye anakimbia kwenda kumpokea huku akishangilia. Lakini badala ya kuimba na kucheza dansi pamoja naye, baba yake anayararua mavazi yake na kusema hivi: “Ole, binti yangu! Kwa kweli umenifanya niiname chini.” Kisha anamwambia binti yake maneno ambayo yatabadili kabisa maisha yake, na kuzima ndoto na matarajio yake ya kuishi maisha ya kawaida. Hata hivyo, binti huyo anakubali bila kusita maneno ya baba yake, na anamtia moyo atimize kile alichomwahidi Yehova. Maneno yake yanaonyesha wazi kwamba ana imani kubwa, na ana uhakika kwamba sikuzote Yehova anamtakia mema. (Amu. 11:34-37) Baba yake anajivunia sana jambo hilo kwa sababu anajua kwamba utayari wa binti yake utawawezesha kupata kibali cha Yehova.

2 Yeftha na binti yake aliyemwogopa Mungu walimtumaini Yehova na njia zake za kufanya mambo, hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. Walikuwa na uhakika kwamba kupata kibali cha Mungu ni bora kuliko dhabihu yoyote ile ambayo wangetoa.

3. Mfano wa Yeftha na binti yake unaweza kutusaidiaje leo?

3 Tunajua kuwa si rahisi siku zote kuwa waaminifu kwa Yehova. Ukweli ni kwamba tunahitaji kufanya “pigano kali kwa ajili ya imani.” (Yuda 3) Ili kutusaidia kufanya hivyo, acheni tuzungumzie changamoto ambazo Yeftha na binti yake walishinda. Walidumishaje uaminifu wao kwa Yehova?

KUDUMISHA UAMINIFU KATIKA ULIMWENGU MWOVU

4, 5. (a) Yehova aliwapa Waisraeli amri gani walipokaribia kuingia katika Nchi ya Ahadi? (b) Kulingana na Zaburi 106, Waisraeli walipatwa na nini walipokosa kutii?

4 Kila siku, Yeftha na binti yake walikuwa na fursa ya kutafakari matokeo mabaya sana ya kutokuwa waaminifu kwa Yehova. Miaka 300 hivi mapema, mababu zao waliamriwa wawaondolee mbali wakazi wapagani katika Nchi ya Ahadi. (Kum. 7:1-4) Waisraeli hawakutii, hivyo wengi wao waliiga mwenendo mpotovu wa Wakanaani, wakaabudu miungu ya uwongo na kufanya matendo mengine maovu.—Soma Zaburi 106:34-39.

5 Uasi huo ulifanya wapoteze kibali cha Yehova, hivyo wakakosa ulinzi wake. (Amu. 2:1-3, 11-15; Zab. 106:40-43) Fikiria jinsi ilivyokuwa vigumu kwa familia zilizomwogopa Mungu kudumisha uaminifu wakati huo. Hata hivyo, Biblia inafunua kwamba kulikuwa na watu waaminifu, kama vile Yeftha na binti yake na pia Elkana, Hana, na Samweli, ambao waliazimia kupata kibali cha Mungu.—1 Sam. 1:20-28; 2:26.

6. Ulimwengu wa leo ukoje, na tunapaswa kujitahidi kufanya nini?

6 Leo, tunaishi katika ulimwengu ambao watu wanafikiri na kutenda kama Wakanaani wa kale; wanatukuza ngono, jeuri, na kuwachochea watu wapende vitu vya kimwili. Yehova ametupatia maonyo yaliyo wazi, kama alivyofanya kwa Waisraeli, ili kutulinda dhidi ya mambo hayo maovu. Je, tutajifunza kutokana na makosa ya Waisraeli? (1 Kor. 10:6-11) Tunapaswa kujitahidi kuondoa mtazamo wowote unaofanana na ule wa Wakanaani. (Rom. 12:2) Je, tunajitahidi kwa uaminifu kufanya hivyo?

KUDUMISHA UAMINIFU TUNAPOKATISHWA TAMAA

7. (a) Yeftha alitendewaje na watu wa taifa lake? (b) Yeftha alitendaje?

7 Katika siku za Yeftha, kutotii kwa Waisraeli kulifanya wawe watumwa wa Wafilisti na Waamoni. (Amu. 10:7, 8) Hata hivyo, Yeftha hakukabili changamoto kutoka kwa mataifa adui pekee, bali pia kutoka kwa ndugu zake na viongozi wa Israeli. Wivu na chuki iliwafanya ndugu zake wa kambo wamfukuze, na kumnyang’anya haki yake ya urithi akiwa mzaliwa wa kwanza. (Amu. 11:1-3) Yeftha hakuruhusu ukatili wao uathiri mtazamo wake. Badala ya kuwachukia na kupuuza ombi la wanaume wazee wa Israeli, Yeftha alikubali kuwasaidia. (Amu. 11:4-11) Ni nini kilichomchochea Yeftha atende kwa njia hiyo iliyoonyesha ukomavu wa kiroho?

8, 9. (a) Ni kanuni gani zilizo katika Sheria ya Musa ambazo huenda zilimsaidia Yeftha? (b) Ni jambo gani lililokuwa muhimu zaidi kwa Yeftha?

8 Yeftha alikuwa mwanaume mwenye nguvu na shujaa, lakini pia alijua vizuri jinsi Mungu alivyoshughulika na watu Wake. Kuelewa kwa kina historia ya Waisraeli kulimsaidia sana atambue lililo sawa na lisilo sawa machoni pa Yehova. (Amu. 11:12-27) Kanuni za Mungu zilizo katika Sheria ya Musa zilifinyanga mtazamo na moyo wa Yeftha. Alijua kwamba Yehova hapendi watu waweke kinyongo, bali anataka watu Wake wapendane. Isitoshe, Sheria ilieleza kwamba mtu hapaswi kupuuza mahitaji ya wengine, hata wale ‘wanaomchukia.’—Soma Kutoka 23:5; Mambo ya Walawi 19:17, 18.

9 Huenda Yeftha alijifunza kutokana na mifano ya watu waaminifu, kama vile Yosefu ambaye aliwatendea kwa rehema ndugu zake hata ingawa ‘walianza kumchukia.’ (Mwa. 37:4; 45:4, 5) Inaelekea kutafakari mifano hiyo kulimsaidia Yeftha achague mwenendo unaomfurahisha Yehova. Bila shaka mwenendo wa ndugu zake ulimuumiza sana, lakini haukumzuia kumtumikia Yehova na watu Wake. (Amu. 11:9) Kupigania jina la Yehova kulikuwa muhimu zaidi kuliko hisia zake. Aliazimia kuwa mwaminifu kwa Yehova, na hilo lilimnufaisha yeye na watu wengine.—Ebr. 11:32, 33.

10. Kanuni za Mungu zinaweza kutusaidiaje tutende Kikristo?

10 Mfano wa Yeftha unatufundisha nini? Huenda tumevunjwa moyo au kutendewa isivyofaa na Wakristo wenzetu. Ikiwa ndivyo, hatupaswi kuruhusu changamoto hizo zituzuie kuhudhuria mikutano au kumtumikia Yehova na kushirikiana na kutaniko kwa ukamili. Tunaweza kumwiga Yeftha, kwa kuruhusu viwango vya Yehova vitusaidie kushinda hali zenye kuvunja moyo na kuendelea kutenda mema.—Rom. 12:20, 21; Kol. 3:13.

DHABIHU ZA HIARI HUFUNUA IMANI YETU

11, 12. Yeftha aliweka nadhiri gani, nayo ilihusisha nini?

11 Yeftha alitambua kwamba angehitaji msaada wa Yehova ili kuwakomboa Waisraeli mikononi mwa Waamoni. Alimwahidi Yehova kwamba ikiwa angeshinda, basi angemtoa mtu wa kwanza kuja kumpokea kutoka katika nyumba yake kama “toleo la kuteketezwa.” (Amu. 11:30, 31) Toleo hilo lilihusisha nini?

12 Kuwadhabihu wanadamu ni jambo lenye kuchukiza sana machoni pa Yehova. Hivyo, ni wazi kwamba Yeftha hakuwa na nia ya kumdhabihu mtu kihalisi. (Kum. 18:9, 10) Chini ya Sheria ya Musa, toleo zima la kuteketezwa lilitolewa kwa Yehova; kwa hiyo inaonekana Yeftha alimaanisha kwamba angemtoa mtu huyo wakfu kwa ajili ya utumishi wa Yehova pekee. Ahadi hiyo ilihusisha kutumikia daima katika maskani. Yehova alikubali ahadi ya Yeftha na alimbariki kwa kumpa ushindi mkubwa, naye akawapiga na kuwatiisha maadui. (Amu. 11:32, 33) Lakini ni nani angetolewa kama “toleo la kuteketezwa” kwa Mungu?

13, 14. Maneno ya Yeftha kwenye Waamuzi 11:35 yanafunua nini kuhusu imani yake?

13 Kumbuka simulizi tuliloanza nalo mwanzoni mwa makala hii. Yeftha aliporudi kutoka vitani, aliyeenda kumpokea si mwingine bali binti yake, mtoto wake wa pekee! Sasa Yeftha akakabili jaribu. Je, angetimiza ahadi yake kwa kumtoa binti yake ili akatumikie katika maskani kwa maisha yake yote?

14 Kwa mara nyingine tena, kanuni za Mungu zilimwongoza Yeftha afanye uamuzi unaofaa. Labda alikumbuka andiko la Kutoka 23:19, ambalo liliwaagiza watu wa Mungu wawe tayari kumpa Yehova kilicho bora. Isitoshe, Sheria ilionyesha wazi kwamba ahadi ni deni. Ilisema hivi: “Ikiwa mwanamume ataweka nadhiri kwa Yehova . . . , hapaswi kulivunja neno lake. Anapaswa kufanya kulingana na yote ambayo yametoka kinywani mwake.” (Hes. 30:2) Kama Hana, mwanamke mwaminifu ambaye huenda aliishi wakati mmoja na yeye, Yeftha alitimiza ahadi yake kwa kuwa alijua faida ambayo yeye na binti yake wangepata wakati ujao. Hakuwa na mtoto mwingine; binti yake pekee ndiye angeweza kuendeleza uzao na kuhifadhi urithi wake katika Israeli. (Amu. 11:34) Hata hivyo, andiko la Waamuzi 11:35 linamalizia kwa maneno haya ya Yeftha: “Nimemfungulia Yehova kinywa changu, nami siwezi kurudi nyuma.” Kuwa mwaminifu hata ilipomgharimu sana, kulimwezesha apate kibali na baraka za Mungu. Je, wewe ungefanya kama Yeftha alivyofanya?

15. Wengi wetu tumetoa ahadi gani, na tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni waaminifu?

15 Tulipoweka maisha yetu wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutafanya mapenzi yake kikamili. Tulijua kwamba tutahitaji kujidhabihu ili tutimize ahadi hiyo. Hata hivyo, utayari wetu unajaribiwa hasa tunapoagizwa tufanye mambo yaliyo kinyume na mapenzi yetu. Tunapojidhabihu na kumtumikia Yehova hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo, tunathibitisha kwamba sisi ni waaminifu. Baraka tunazopata ni nyingi sana kuliko dhabihu zozote tunazotoa, hata iwe zinatugharimu kadiri gani. (Mal. 3:10) Lakini vipi kuhusu binti ya Yeftha?

Tunaweza kuonyeshaje imani kama ya Yeftha na binti yake? (Tazama fungu la 16 na 17)

16. Binti ya Yeftha aliitikiaje ahadi ya baba yake? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

16 Haingekuwa rahisi kwa binti ya Yeftha kukubali kutimiza nadhiri ya baba yake. Nadhiri hiyo ilikuwa tofauti na ile ya Hana, aliyemtoa mwana wake akatumikie akiwa Mnadhiri katika maskani. (1 Sam. 1:11) Mnadhiri aliruhusiwa kufunga ndoa na kuwa na familia. Lakini binti ya Yeftha alitolewa kabisa kama “toleo la kuteketezwa”; hivyo hangeolewa wala kuwa na watoto. (Amu. 11:37-40) Akiwa binti ya mwanaume shujaa na kiongozi wa Israeli, binti ya Yeftha angeweza kuolewa na mwanaume bora sana nchini humo. Lakini katika maskani angetumikia akiwa mtumishi wa hali ya chini. Binti ya Yeftha alitendaje? Alionyesha kwamba kumtumikia Yehova ndilo jambo kuu maishani mwake kwa kusema hivi: “Baba yangu, ikiwa umemfungulia Yehova kinywa chako, nitendee kulingana na neno lililotoka katika kinywa chako.” (Amu. 11:36) Alidhabihu tamaa yake ya asili ya kuolewa na kuwa na watoto ili kuendeleza ibada safi. Tunaweza kuigaje mtazamo wake wa kujidhabihu?

17. (a) Tunaweza kuigaje imani ya Yeftha na binti yake? (b) Andiko la Waebrania 6:10-12 linakuchocheaje ujidhabihu?

17 Maelfu ya vijana Wakristo, wanawake kwa wanaume, wanadhabihu kwa hiari ndoa au watoto, angalau kwa sasa, ili wamtumikie Yehova kikamili. Pia, wale wenye umri mkubwa wanadhabihu wakati ambao wangetumia pamoja na watoto na wajukuu wao ili washiriki katika miradi ya ujenzi au kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme na kutumikia kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Wengine wanadhabihu mambo ya kibinafsi ili washiriki katika kampeni za pekee wakati wa majira ya Ukumbusho. Utumishi huo wa moyo wote unamfurahisha sana Yehova, naye hatasahau kamwe kazi na upendo wa watumishi wake. (Soma Waebrania 6:10-12.) Je, unaweza kujidhabihu zaidi ili umtumikie Yehova kikamili?

TUMEJIFUNZA NINI?

18, 19. Tumejifunza nini katika simulizi la Yeftha na binti yake, na tunaweza kuwaigaje?

18 Ingawa Yeftha alikabili changamoto nyingi maishani, alikubali kuongozwa na kanuni za Yehova katika maamuzi yake. Hakukubali kuathiriwa na watu waliomzunguka. Kukatishwa tamaa na watu wengine hakukudhoofisha azimio lake la kuendelea kuwa mwaminifu. Yeye na binti yake walijidhabihu kwa hiari, nao walipata baraka nyingi kwa kuwa Yehova aliwatumia kuendeleza ibada safi. Wengine walipoacha kufuata viwango vya Yehova, Yeftha na binti yake walishikamana navyo.

19 Biblia inatuhimiza tuwe “waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Ebr. 6:12) Acheni tumwige Yeftha na binti yake kwa kuishi kupatana na ukweli huu muhimu tunaojifunza kutokana na mfano wao: Uaminifu hutuwezesha kupata kibali cha Mungu.