Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Maoni Kama ya Yehova Kuhusu Haki?

Je, Una Maoni Kama ya Yehova Kuhusu Haki?

“Nitatangaza jina la Yehova . . . , Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.”KUM. 32:3, 4.

NYIMBO: 110, 2

1, 2. (a) Nabothi na wanawe walikabili ukosefu gani wa haki? (b) Tutachunguza sifa zipi mbili katika makala hii?

WAZIA tukio hili. Mwanamume fulani anahukumiwa kimakosa adhabu ya kifo. Watu wa familia na rafiki zake wanashtuka na kuhuzunika mwanamume huyo anapohukumiwa kwa msingi wa ushahidi wa uwongo uliotolewa na watu wasiofaa kitu. Watu wanaopenda haki wanahuzunika sana wanapoona mwanamume huyo asiye na hatia na wanawe wakiuawa. Hilo si simulizi la kuwaziwa. Jambo hilo lilimpata mtumishi mwaminifu wa Yehova aliyeitwa Nabothi ambaye aliishi wakati wa utawala wa Mfalme Ahabu wa Israeli.1 Fal. 21:11-13; 2 Fal. 9:26.

2 Katika makala hii, tutachunguza mfano wa Nabothi na pia wa mzee mwaminifu katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza ambaye alikosea. Tunapochunguza mifano hiyo ya Biblia, tutajifunza kwamba sifa ya unyenyekevu ni muhimu ikiwa tunataka kuonyesha kuwa tuna maoni ya Yehova kuhusu haki. Tutajifunza pia jinsi kuwa tayari kusamehe tunapoona ukosefu wa haki kutanikoni kunavyoonyesha maoni ya Yehova kuhusu haki.

HAKI YAPOTOSHWA

3, 4. Nabothi alikuwa mtu wa aina gani, na kwa nini alikataa kumuuzia Mfalme Ahabu shamba lake la mizabibu?

3 Nabothi alikuwa mwaminifu kwa Yehova wakati ambapo Waisraeli wengi walikuwa wanafuata mfano mbaya wa Mfalme Ahabu na mke wake mwovu Malkia Yezebeli. Waabudu hao wa Baali hawakumheshimu Yehova na kuthamini viwango vyake. Kwa upande mwingine, Nabothi alithamini uhusiano wake na Yehova hata kuliko uhai wake.

4 Soma 1 Wafalme 21:1-3. Ahabu alipotaka kununua shamba lake la mizabibu au kumpa shamba lingine bora zaidi la mizabibu, Nabothi alikataa. Kwa nini? Alisema hivi kwa heshima: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba mimi nikupe fungu la urithi la mababu zangu.” Msingi wa Nabothi wa kukataa kuuza shamba lake ulitokana na sheria ya Yehova kwa taifa la Israeli ambayo ilikataza mtu kuuza shamba la urithi milele. (Law. 25:23; Hes. 36:7) Ni wazi kwamba Nabothi alikuwa na maoni ya Yehova kuhusu mambo.

5. Yezebeli alihusikaje katika kifo cha Nabothi?

5 Kwa kusikitisha Nabothi alipokataa kuuuza shamba lake, Mfalme Ahabu na mke wake walifanya mambo mengi mabaya. Ili kupata shamba hilo la mizabibu kwa ajili ya mume wake, Yezebeli alipanga Nabothi ashtakiwe kwa uwongo, jambo lililofanya Nabothi na wanawe wauawe. Yehova angeshughulikiaje ukosefu huo mkubwa wa haki?

HUKUMU YA MUNGU YA UADILIFU

6, 7. Yehova alionyeshaje kwamba yeye hupenda haki, na kwa nini hilo lingewafariji watu wa familia ya Nabothi na rafiki zake?

6 Yehova alimtuma Eliya aende haraka kwa Ahabu. Eliya alimhukumu Ahabu kwa haki kuwa mwuaji na mwizi. Yehova alitoa hukumu gani katika kisa hicho? Ahabu, mke wake, na wanawe wangetendewa kama walivyowatendea Nabothi na wanawe.1 Fal. 21:17-25.

7 Ingawa watu wa familia na rafiki za Nabothi walihuzunika kutokana na matendo ya mauaji ya Ahabu, hapana shaka walifarijika kujua kwamba Yehova aliona ukosefu huo wa haki na alishughulikia jambo hilo haraka. Hata hivyo, unyenyekevu na imani yao kwa Yehova huenda ilijaribiwa na matukio yasiyotarajiwa ambayo yalifuata.

8. Ahabu aliitikiaje ujumbe wa hukumu kutoka kwa Yehova, na matokeo yalikuwa nini?

8 Ahabu aliposikia hukumu kali ya Yehova, “akayararua mavazi yake, akavaa nguo za magunia mwilini mwake; naye akaanza kufunga, akaendelea kulala katika nguo za magunia, akatembea kwa huzuni.” Ahabu alijinyenyekeza! Matokeo yalikuwa nini? Yehova alimwambia hivi Eliya: “Kwa sababu amejinyenyekeza kwa ajili yangu, sitauleta ule msiba katika siku zake. Katika siku za mwana wake nitauleta msiba ule juu ya nyumba yake.” (1 Fal. 21:27-29) Yehova, “mchunguzaji wa mioyo,” alimwonyesha Ahabu rehema.Met. 17:3.

UNYENYEKEVU NI ULINZI

9. Kwa nini sifa ya unyenyekevu ingeweza kuwalinda watu wa familia ya Nabothi na rafiki zake?

9 Uamuzi huo uliwaathirije wale waliojua kwamba Ahabu alikuwa amefanya uhalifu mkubwa hivyo? Kugeuzwa kwa hukumu hiyo huenda kulijaribu imani ya watu wa familia ya Nabothi na rafiki zake. Ikiwa wangehisi hivyo, unyenyekevu ungewalinda na kuwawezesha kumwabudu Yehova kwa uaminifu wakiwa na uhakika kwamba Mungu wao hawezi kutenda isivyo haki. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:3, 4.) Nabothi, wanawe, na familia zao watapata haki kamili Yehova atakapowafufua waadilifu. (Ayu. 14:14, 15; Yoh. 5:28, 29) Zaidi ya hilo, mtu mnyenyekevu hukumbuka kwamba “Mungu wa kweli ataleta kila kazi katika hukumu, kuhusiana na kila jambo lililofichwa, liwe jema au baya.” (Mhu. 12:14) Naam, anapotoa hukumu, Yehova huzingatia mambo ambayo hatujui. Hivyo, sifa ya unyenyekevu huwalinda watu wasio na hatia wasipatwe na msiba wa kiroho.

10, 11. (a) Maoni yetu kuhusu haki huenda yakajaribiwa chini ya hali gani? (b) Sifa ya unyenyekevu itatulinda kwa njia gani?

10 Utatendaje ikiwa wazee watafanya uamuzi ambao huelewi au labda hukubaliani nao? Kwa mfano, utafanya nini ikiwa wewe au mtu unayempenda anapoteza pendeleo analopenda la utumishi? Namna gani ikiwa mwenzi wako wa ndoa, mwana au binti yako, au rafiki yako wa karibu anatengwa na ushirika na hukubaliani na uamuzi huo? Vipi ikiwa unaamini kwamba mtenda dhambi ameonyeshwa rehema kimakosa? Hali kama hizo zinaweza kujaribu imani yetu kwa Yehova na mpango wake wa kitengenezo. Sifa ya unyenyekevu itakulindaje ikiwa utakabili jaribu kama hilo? Fikiria mambo haya mawili.

Utatendaje wazee wanapotangaza uamuzi ambao hukubaliani nao (Tazama fungu la 10 na 11)

11 Kwanza, sifa ya unyenyekevu itafanya tukubali kwamba hatujui habari zote zinazohusika. Hata iwe tunajua habari nyingi kadiri gani kuhusu hali fulani, Yehova pekee ndiye anayeweza kusoma moyo wa mfano. (1 Sam. 16:7) Kujua ukweli huo usioweza kupingwa kutatuchochea kuwa wanyenyekevu, kutambua mipaka yetu, na kubadili maoni yetu kuhusu jambo hilo. Pili, sifa ya unyenyekevu itatusaidia kujitiisha na kuwa wenye subira tunapomngojea Yehova arekebishe ukosefu wowote wa haki. Ni kama mwanamume mwenye hekima aliyeandika hivi: “Mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli . . . , lakini mambo hayatakuwa mema kwa mwovu, wala hatarefusha siku zake.” (Mhu. 8:12, 13) Kwa hakika, kuonyesha sifa ya unyenyekevu huwasaidia wote wanaohusika.Soma 1 Petro 5:5.

KISA CHA UNAFIKI

12. Tutachunguza simulizi gani, na kwa nini?

12 Wakristo wa karne ya kwanza waliokuwa Siria ya Antiokia walikabili hali fulani ambayo ilijaribu unyenyekevu wao na pia utayari wao wa kusamehe. Acheni tuchunguze simulizi hilo na tuone jinsi linavyoweza kutusaidia kuchunguza mtazamo wetu kuelekea kusamehe na kutusaidia kuelewa vizuri zaidi jinsi kusamehe kunavyohusiana na maoni ya Yehova kuhusu haki.

13, 14. Mtume Petro alifurahia mapendeleo gani, na alionyeshaje ujasiri?

13 Mtume Petro alikuwa mzee aliyejulikana sana katika kutaniko la Kikristo. Alikuwa mwandamani wa karibu wa Yesu na alipewa migawo muhimu. (Mt. 16:19) Kwa mfano, mwaka 36 W.K., Petro alikuwa na pendeleo la kushiriki habari njema na Kornelio na familia yake. Tukio hilo lilikuwa la pekee kwa kuwa Kornelio alikuwa Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa. Kornelio na familia yake walipopokea roho takatifu, Petro alisema hivi: “Je, mtu yeyote anaweza kuyakataza maji kwamba hawa wasibatizwe ambao wameipokea roho takatifu kama vile sisi tulivyoipokea?”Mdo. 10:47.

14 Katika 49 W.K., mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu walikutana ili kuchunguza ikiwa Watu wa Mataifa waliogeuza imani na kuwa Wakristo walipaswa kutahiriwa. Katika mkutano huo, Petro alizungumza kwa ujasiri akiwakumbusha akina ndugu kwamba miaka kadhaa mapema, Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walikuwa wamepokea zawadi ya roho takatifu. Ushahidi wa Petro kuhusu mambo aliyojionea ulisaidia sana baraza linaloongoza la karne ya kwanza kufanya uamuzi. (Mdo. 15 :6-11, 13, 14, 28, 29) Inaelekea kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa waliogeuza imani na kuwa Wakristo walithamini ujasiri wa Petro wa kuzungumzia mambo aliyojionea. Ilikuwa rahisi sana kwao kuwa na imani kuelekea mwanamume huyo mkomavu kiroho!Ebr. 13:7.

15. Petro alifanya kosa gani alipokuwa Siria ya Antiokia? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

15 Muda mfupi baada ya mkutano huo uliofanywa mwaka 49 W.K., Petro alitembelea Siria ya Antiokia. Alipokuwa huko, alishirikiana kwa uhuru na ndugu zake wa mataifa mengine. Bila shaka, walinufaika na ujuzi na uzoefu wa Petro. Hata hivyo, tunaweza kuwazia jinsi walivyoshangaa na kuvunjika moyo Petro alipoacha ghafula kula pamoja nao. Washiriki wengine waliokuwa Wayahudi kutanikoni, waliathiriwa na Petro, na wakaacha kushirikiana nao pia. Ni nini kilichomfanya mzee huyo mkomavu kuwa na maoni yasiyofaa ambayo yangeweza kugawanya kutaniko? Na jambo muhimu hata zaidi, tunaweza kujifunza nini kutokana na kosa la Petro ambalo linaweza kutusaidia ikiwa tutaumizwa na maneno au matendo ya mzee fulani wa kutaniko?

16. Petro alirekebishwaje, na ni maswali gani yanayozuka?

16 Soma Wagalatia 2:11-14. Petro alijiruhusu anaswe na mtego wa kuwaogopa wanadamu. (Met. 29:25) Ijapokuwa alifahamu vema maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo, Petro aliogopa maoni ya Wayahudi waliotahiriwa waliokuwa washiriki wa kutaniko la Yerusalemu. Mtume Paulo, ambaye pia alikuwa katika mkutano huo huko Yerusalemu mwaka 49 W.K., alimkabili Petro huko Antiokia na kufunua unafiki wake. (Mdo. 15:12; Gal. 2:13) Watu wa Mataifa waliogeuza imani na kuwa Wakristo ambao waliathiriwa kibinafsi na kosa la Petro wangetendaje kuelekea ukosefu huo wa haki? Je, wangekubali kukwazwa? Je, Petro angepoteza mapendeleo yenye thamani kwa sababu ya kosa lake?

UWE MWENYE KUSAMEHE

17. Petro alinufaikaje na msamaha wa Yehova?

17 Inaonekana Petro alikubali kwa unyenyekevu shauri la Paulo. Maandiko hayaonyeshi kwamba alipoteza mapendeleo yake. Hata baadaye aliongozwa na roho kuandika barua mbili zilizokuja kuwa sehemu ya Biblia. Jambo lenye kupendeza ni kwamba katika barua yake ya pili, Petro anamtaja Paulo kuwa “ndugu yetu mpendwa.” (2 Pet. 3:15) Ingawa kosa la Petro huenda liliwaumiza washiriki wa kutaniko waliokuwa Watu wa Mataifa, Yesu, ambaye ni kichwa cha kutaniko, aliendelea kumtumia. (Efe. 1:22) Kwa hiyo, washiriki wa kutaniko walikuwa na fursa ya kumwiga Yesu na Baba yake katika kusamehe. Tunatumaini kwamba hakuna yeyote aliyekubali kukwazwa na kosa la mwanamume huyo asiye mkamilifu.

18. Ni katika hali gani huenda tukahitaji kuonyesha maoni ya Yehova kuhusu haki?

18 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo pia hakuna wazee wakamilifu katika kutaniko la Kikristo, “kwa maana sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Huenda tunakubaliana na hilo, lakini tatizo huwa tunapoathiriwa moja kwa moja na kutokamilika kwa ndugu. Katika hali kama hiyo, je, tutakuwa na maoni ya Yehova kuhusu haki? Kwa mfano, utatendaje ikiwa mzee anataja jambo fulani linaloonyesha ameathiriwa kwa kiasi fulani na ubaguzi? Je, utakubali kukwazika ikiwa mzee anataja bila kufikiri jambo fulani linalokukasirisha au kukuumiza? Badala ya kukata kauli haraka kwamba ndugu huyo hastahili tena kuwa mzee, je, utamngojea kwa subira Yesu, aliye kichwa cha kutaniko? Je, utajitahidi kuona mambo yote yanayohusika, labda kwa kutafakari miaka mingi ambayo ndugu huyo ametumikia kwa uaminifu? Ikiwa ndugu aliyekutendea dhambi anaendelea kutumikia akiwa mzee au hata anapokea mapendeleo mengine ya ziada, je, utashangilia pamoja naye? Utayari wako wa kusamehe unaweza kuonyesha una maoni ya Yehova kuhusu haki.Soma Mathayo 6:14, 15.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Watu wanaopenda haki wanatazamia kwa hamu siku ambayo Yehova ataondoa kabisa ukosefu wote wa haki ambao Shetani na mfumo wake mwovu huwasababishia wanadamu. (Isa. 65:17) Kabla ya wakati huo, kila mmoja wetu na aazimie kuiga maoni ya Yehova kuhusu haki kwa kutambua kwa unyenyekevu mipaka yetu na kuwasamehe kwa hiari wale wanaotutendea dhambi.