Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho Yako ya Kujitolea na Imletee Yehova Sifa

Roho Yako ya Kujitolea na Imletee Yehova Sifa

“Kwa ajili ya watu kujitolea, mbarikini Yehova!”AMU. 5:2.

NYIMBO: 150, 10

1, 2. (a) Elifazi na Bildadi walidai nini kuhusu jinsi Mungu anavyoona utumishi wetu kwake? (b) Yehova alionyeshaje hisia zake?

“JE, MWANAMUME anaweza kuwa na faida kwa Mungu mwenyewe, kwamba mtu mwenye ufahamu awe na faida kwake? Je, Mweza-Yote anapendezwa kwa vyovyote kwa kuwa wewe ni mwadilifu, au kupata faida yoyote kwa kuwa wewe unafanya njia yako isiwe na lawama?” (Ayu. 22:1-3) Je, umewahi kuwazia majibu ya maswali kama hayo? Mwanzoni, Elifazi Mtemani alipomwuliza Ayubu maswali hayo, bila shaka Elifazi aliamini kwamba jibu lingekuwa hapana. Mwandamani wake Bildadi Mshua, hata alidai kwamba wanadamu hawawezi kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu.Soma Ayubu 25:4.

2 Wafariji hao wa uwongo walidai kwamba jitihada zetu za kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu hazina faida yoyote kwake, na kwamba thamani yetu kwa Mungu ni kama ya nondo, funza, au mnyoo. (Ayu. 4:19; 25:6) Huenda tukakata kauli kwa haraka kwamba Elifazi na Bildadi walionyesha mwelekeo wa unyenyekevu. (Ayu. 22:29) Kwa kweli, unapotazama chini ukiwa juu ya mlima mrefu au kupitia dirisha la ndege, huenda ukaona shughuli za wanadamu kuwa hazina thamani yoyote. Hata hivyo, kulingana na maoni ya Yehova yaliyokwezwa, je, hivyo ndivyo yeye huona mchango wetu katika kazi ya Ufalme anapotazama sayari yetu? Yehova alionyesha hisia zake alipowakaripia Elifazi, Bildadi, na Sofari kwa sababu walisema uwongo, lakini akapendezwa na Ayubu na kumwita, “mtumishi wangu.” (Ayu. 42:7, 8) Hivyo, kwa kweli mwanadamu anaweza “kuwa na faida kwa Mungu.”

“UNAMPA NINI?”

3. Elihu alisema nini kuhusu jitihada zetu za kumtumikia Yehova, naye alimaanisha nini?

3 Elihu hakurekebishwa na Yehova alipouliza hivi: “Ikiwa kweli uko upande wa haki, unampa [Mungu] nini, au je, yeye anapokea nini kutoka mkononi mwako?” (Ayu. 35:7) Je, Elihu alikuwa akidokeza kwamba jitihada zetu katika utumishi wa Mungu ni za bure? Hapana. Alikuwa akionyesha kwamba Yehova hategemei ibada yetu. Hana uhitaji wa kitu chochote. Hatuwezi kumfanya Yehova awe tajiri zaidi au mwenye nguvu zaidi. Badala yake, wema wowote, kipaji, au nguvu tulizo nazo tumepewa na Mungu, naye huzingatia jinsi tunavyozitumia.

4. Yehova hufananisha matendo yetu ya fadhili na nini?

4 Yehova huona matendo ya upendo mshikamanifu yanayoonyeshwa kwa watumishi wake kana kwamba anaonyeshwa yeye binafsi. Methali 19:17 inasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” Je, andiko hili linadokeza kwamba Yehova huzingatia matendo yote ya fadhili wanayotendewa watu wa hali ya chini? Je, tunaweza kukata kauli kwamba Muumba wa ulimwengu huwaona wanadamu wanaotenda kwa huruma kuwa wanamdai, na kwamba matendo yao huwa mikopo ambayo Yeye hulipa kwa kuwapa kibali na kuwabariki? Ndiyo, na jambo hilo lilionyeshwa wazi na mwana wa Mungu.Soma Luka 14:13, 14.

5. Tutachunguza maswali gani?

5 Yehova alimwalika nabii Isaya azungumze kwa niaba Yake, na kueleza jinsi anavyofurahia kuwaruhusu wanadamu waaminifu washiriki katika kutimiza kusudi Lake. (Isa. 6:8-10) Isaya alikubali kwa hiari mwaliko huo. Leo, watu wengi huonyesha roho kama hiyo ya “Mimi hapa! Nitume mimi” kwa kukubali migawo migumu katika utumishi wa Yehova. Lakini huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, jitihada zangu binafsi zinathaminiwa? Ingawa ni tendo la fadhili Yehova kuniruhusu nijitolee na kushiriki, je, hataandaa kile kinachohitajika ili kutimiza Neno lake haidhuru ninaamua kujitoa kadiri gani katika utumishi wake?’ Fikiria jinsi matukio yaliyotokea katika siku za Debora na Baraka yanavyojibu maswali hayo.

WALEMEWA NA HOFU KISHA WAIMARISHWA NA MUNGU

6. Kulikuwa na tofauti gani kati ya Waisraeli na jeshi la Yabini?

6 Waisraeli walikuwa ‘wamekandamizwa kwa ukali’ na Mfalme Yabini wa Kanaani kwa miaka 20. Hata waliogopa kuonekana hadharani. Kwa kufikiria mambo kwa njia ya kijeshi, hawakuwa na zana za kivita, wala silaha za kupigana au kujilinda ilhali maadui zao walikuwa na magari 900 ya vita yaliyokuwa na miundu ya chuma.Amu. 4:1-3, 13; 5:6-8. *

7, 8. (a) Mwanzoni Yehova alimpa Baraka maagizo gani? (b) Waisraeli walishindaje jeshi la Yabini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Hata hivyo, kupitia nabii wa kike Debora, Yehova alimpa Baraka amri hii iliyo wazi: “Nenda, usambae katika Mlima Tabori, nawe uchukue wanaume elfu kumi kutoka kwa wana wa Naftali na kutoka kwa wana wa Zabuloni. Nami hakika nitamvuta kwako Sisera mkuu wa jeshi la Yabini na magari yake ya vita na umati wake, kwenye bonde la mto la Kishoni, nami hakika nitamtia yeye mkononi mwako.”Amu. 4:4-7.

8 Ujumbe huo ulienea. Wajitoleaji wakakusanyika kwenye Mlima Tabori. Baraka akaanza mara moja kufuata maagizo ya Yehova. (Soma Waamuzi 4:14-16.) Wakati wa pigano kuu huko Taanaki, mvua kubwa ilinyesha ghafla na kufanya eneo hilo liwe na matope. Baraka akafuatilia jeshi la Sisera hadi Haroshethi, umbali wa kilomita 24. Alipokuwa akikimbia, Sisera aliacha gari lake la vita ambalo lilikuwa lenye kutisha, lakini wakati huu halikuwa na faida, na kukimbilia Saananimu, labda karibu na mji wa Kadeshi. Akajificha katika hema la Yaeli, mke wa Heberi Mkeni, na akakaribishwa na Yaeli. Kwa kuwa alikuwa amechoshwa na mapigano hayo, akalala usingizi. Hiyo ilikuwa fursa nzuri kwa Yaeli kutenda kwa ujasiri na kumwua Sisera. (Amu. 4:17-21) Adui wa Waisraeli alikuwa ameshindwa! *

MTAZAMO TOFAUTI-TOFAUTI KUELEKEA UTUMISHI WA KUJITOLEA

9. Kitabu cha Waamuzi 5:20, 21 kina habari gani kuhusu pigano dhidi ya Sisera?

9 Kitabu cha Waamuzi sura ya 4 na ya 5 zinapaswa kuchunguzwa pamoja, kwa kuwa kila sura hufunua habari tofauti. Kwa mfano, Waamuzi 5:20, 21 inasema hivi: “Nyota zilipigana zikiwa mbinguni, zikiwa kwenye mizunguko yao zilipigana na Sisera. Mto wa Kishoni ukawafagilia mbali.” Je, hilo linaonyesha kwamba walisaidiwa na malaika au vimondo fulani vilianguka? Simulizi hilo halijafafanua zaidi. Ni wazi kwamba ni kwa mwongozo wa Mungu tu mvua kubwa ilinyesha mahali na wakati fulani hususa, na hivyo kufagilia mbali magari 900 ya vita. Ushindi huo ulielekezwa kwa Yehova mara tatu, katika Waamuzi 4:14, 15. Hakuna hata mmoja kati ya wale wajitoleaji 10,000 Waisraeli ambaye angedai kwamba yeye ndiye ameleta ukombozi.

10, 11. “Merozi” ilikuwa nini, na kwa nini ililaaniwa?

10 Hata hivyo, inashangaza kwamba katikati ya wimbo wa ushindi wa Debora na Baraka wa kumsifu Yehova kwa sababu ya ushindi wa kimuujiza, waliimba hivi: “‘Laani Merozi,’ akasema malaika wa Yehova, ‘Walaani wakaaji wake bila kukoma, kwa sababu hawakuja kumsaidia Yehova, kumsaidia Yehova pamoja na wanaume wenye nguvu.’”Amu. 5:23.

11 Inaelekea Merozi ililaaniwa kikamili hivi kwamba ni vigumu kujua ilikuwa nini hasa. Je, inawezekana kwamba ni jiji ambalo wakaaji wake walikataa kuitikia mwito wa kujitolea? Ikiwa eneo hilo lilikuwa kati ya maeneo ambayo Sisera alipitia alipokuwa akivikimbia vita, je, watu wa eneo hilo walipata nafasi ya kumkamata na wakakataa kufanya hivyo? Je, ni kweli kwamba hawakusikia mwito wa kutafuta wajitoleaji? Watu elfu kumi katika eneo lao walikuwa wamekusanywa kwa ajili ya vita hivyo. Wazia watu wa Merozi wakimwona shujaa huyo mwenye kutisha akikimbia katikati ya mitaa yao akiwa peke yake bila tumaini la kuponyoka. Hiyo ingekuwa fursa nzuri ya kuendeleza kusudi la Yehova na kupata baraka zake. Hata hivyo, katika wakati huo muhimu walipohitaji kuchagua kati ya kutenda au kutotenda, je, waliliona kuwa jambo lisilo la maana? Hicho ni kinyume kabisa cha tendo la ujasiri la Yaeli linaloelezwa katika mistari inayofuata!Amu. 5:24-27.

12. Kuna tofauti gani ya mtazamo kati ya watu mbalimbali wanaotajwa katika Waamuzi 5:9, 10, na hilo linapaswa kutuathirije leo?

12 Katika andiko la Waamuzi 5:9, 10, tunaona tofauti nyingine ya mtazamo kati ya wale walioandamana na Baraka na wale waliokataa. Debora na Baraka waliwapongeza “viongozi wa Israeli, waliojitolea kati ya watu.” Walitofautiana sana na “wapandaji wa punda-jike wenye rangi nyekundu ya kimanjano,” waliokuwa na kiburi kingi hivi kwamba walikataa kushiriki, na wale “[waliokaa] kwenye mazulia yenye thamani,” waliopenda maisha ya starehe! Tofauti na wale “[waliotembea] barabarani,” wakipendelea njia rahisi, wale walioenda pamoja na Baraka walikuwa tayari kwenda vitani kwenye milima ya Tabori na mabonde ya vinamasi ya Kishoni! Wote waliopenda raha walihimizwa ‘waangalie!’ au watafakari. Naam, walihitaji kutafakari juu ya fursa waliyokosa ya kutimiza kusudi la Yehova. Hivyo ndivyo wale wanaoogopa kujitoa kikamili kumtumikia Mungu wanavyopaswa kufanya.

13. Mtazamo wa makabila ya Rubeni, Dani, na Asheri ulitofautianaje na ule wa Zabuloni na Naftali?

13 Wale waliojitolea walijionea jinsi Yehova alivyotetea enzi yake kuu. Walikuwa na jambo muhimu la kuzungumzia walipokuwa “[wakisimulia] matendo ya uadilifu ya Yehova.” (Amu. 5:11) Kwa upande mwingine, makabila ya Rubeni, Dani, na Asheri yalitajwa katika Waamuzi 5:15-17 kwa sababu ya kuzingatia zaidi vitu vyao vya kimwili, kama vile makundi ya mifugo, meli, na mahali pa kushukia pwani. Tofauti nao, Zabuloni na Naftali “[walidharau] nafsi zao karibu kufa” ili kuwaunga mkono Debora na Baraka. (Amu. 5:18) Tunajifunza somo muhimu kwa kuchunguza tofauti hiyo ya mitazamo kuelekea utumishi wa kujitolea.

“MBARIKINI YEHOVA!”

14. Tunaonyeshaje kwamba tunaunga mkono enzi kuu ya Yehova leo?

14 Leo, hatuambiwi twende vitani, lakini tuna pendeleo la kuonyesha ujasiri wetu kwa kuhubiri kwa bidii. Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, kuna uhitaji mkubwa sana wa wajitoleaji katika tengenezo la Yehova. Mamilioni ya ndugu, dada, na vijana wanajitolea katika utumishi mbalimbali wa wakati wote wakiwa mapainia, Wanabetheli, wajitoleaji wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme, na wajitoleaji katika makusanyiko. Pia, wafikirie wazee wanaobeba majukumu mazito katika Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, na kupanga makusanyiko. Uwe na uhakika kwamba Yehova anathamini sana roho yako ya kujitolea, na hataisahau.Ebr. 6:10.

Kabla ya kufanya uamuzi, tafakari matokeo yake juu ya familia yako na kutaniko (Tazama fungu la 15)

15. Tunaweza kutambuaje ikiwa tumeanza kupuuza umuhimu wa kazi ya Yehova?

15 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninaridhika tu kuwaacha wengine wafanye kazi yote? Je, ninaruhusu mambo ya kimwili yaingilie roho yangu ya kujitolea? Kama Baraka, Debora, Yaeli, na wale wajitoleaji 10,000, je, nina imani na ujasiri wa kutumia chochote nilicho nacho kutii amri ya Yehova iliyo wazi? Ikiwa ninafikiria kuhamia jiji au nchi nyingine kwa sababu za kiuchumi, je, ninatafakari na kusali kuhusiana na matokeo ya uamuzi huo juu ya familia yangu na kutaniko?’ *

16. Tunaweza kumpa Yehova nini ambacho hana?

16 Yehova anatupatia heshima kwa kuturuhusu kushiriki kuunga mkono enzi yake kuu. Tangu Ibilisi alipowashawishi wanadamu waunge mkono utawala wake dhidi ya utawala wa Yehova, unapounga mkono utawala wa Yehova unamwonyesha Shetani waziwazi kwamba unamtetea Yehova. Imani na utimilifu unaochochea roho yako ya kujitolea unampendeza Yehova. (Met. 23:15, 16) Anatumia mambo unayofanya kumuunga mkono kujibu dhihaka za Shetani. (Met. 27:11) Kwa hiyo, kwa kumtii Yehova kwa ushikamanifu unampa kitu chenye thamani, na anapata shangwe katika kukipokea.

17. Andiko la Waamuzi 5:31 linaashiria nini kuhusu wakati ujao?

17 Hivi karibuni, dunia itajawa na wale wanaopendelea enzi kuu ya Yehova kuliko utawala mwingine wowote. Tunatamani sana siku hiyo ifike! Tunajiunga na Debora na Baraka kuimba hivi: “Na waangamie hivyo adui zako wote, Ee Yehova, na wanaokupenda wawe kama wakati jua linaposonga katika nguvu zake.” (Amu. 5:31) Ombi hilo litajibiwa Yehova atakapoangamiza ulimwengu mwovu wa Shetani! Vita vya Har–Magedoni vitakapoanza, hakutakuwa na uhitaji wa wajitoleaji wa kibinadamu wa kupigana na adui. Utakuwa wakati wa ‘kusimama tuli, na kuuona wokovu wa Yehova.’ (2 Nya. 20:17) Lakini kwa sasa, tuna fursa nyingi za kuunga mkono kusudi la Yehova kwa ujasiri na bidii.

18. Matokeo yatakuwa nini kwa wale wanaonufaika na utumishi wako wa kujitolea?

18 “Kwa ajili ya watu kujitolea, mbarikini Yehova!” Hivyo, Debora na Baraka walianza wimbo wao wa ushindi kwa kumsifu Aliye Juu, bali si kusifu viumbe. (Amu. 5:1, 2) Vivyo hivyo leo, acha roho yako ya kujitolea iwachochee wale wote watakaonufaika nayo ‘kumbariki Yehova!’

^ fu. 6 Mundu ni upanga wenye ncha kali, mrefu, na nyakati nyingine huwa umejipinda. Miundu ingechomoza kutoka kwenye magari ya vita, huenda kwenye ekseli. Ni nani angethubutu kukaribia gari hilo lenye kutisha la kivita linalosonga?

^ fu. 8 Habari zaidi kuhusu simulizi hili lenye kusisimua zinapatikana kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2015, uku. 12-15.

^ fu. 15 Tazama makala “Mahangaiko Kuhusu Pesa” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2015.