Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kutiana Moyo “na Kufanya Hivyo Zaidi”

Endeleeni Kutiana Moyo “na Kufanya Hivyo Zaidi”

“Na acheni tufikiriane . . . , tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.”—EBR. 10:24, 25.

NYIMBO: 90, 87

1. Kwa nini mtume Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania waendelee kutiana moyo “na kufanya hivyo zaidi”?

KWA nini tunapaswa kuzidisha jitihada zetu za kuwatia moyo wengine? Katika barua aliyowaandikia Wakristo Waebrania, mtume Paulo anatupatia sababu ya kufanya hivyo. Aliwaambia hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Miaka mitano hivi baadaye, Wakristo Wayahudi walioishi Yerusalemu walitambua kwamba “siku ya Yehova” ilikuwa ikikaribia na kujionea ishara ambayo Yesu alikuwa amewapa ili wakimbie kutoka katika jiji hilo ili kuokoa uhai wao. (Mdo. 2:19, 20; Luka 21:20-22) Siku hiyo ya Yehova ilifika katika mwaka wa 70 W.K. Waroma walipotekeleza hukumu ya Yehova dhidi ya jiji la Yerusalemu.

2. Kwa nini sisi pia tunapaswa kuzidisha jitihada zetu za kuwatia moyo wengine?

2 Leo, tuna kila sababu ya kuamini kwamba ile siku ya Yehova iliyo ‘kuu na yenye kuogopesha sana’ iko karibu. (Yoe. 2:11) Nabii Sefania alisema hivi: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu! Iko karibu, nayo inakuja haraka sana!” (Sef. 1:14) Onyo hilo la kinabii linahusu pia nyakati zetu. Hivyo, kwa kuwa siku ya Yehova imekaribia sana, Paulo anatuambia “tuhangaikiane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24, maelezo ya chini) Kwa hiyo, tunapaswa kupendezwa zaidi na zaidi na ndugu zetu, ili tuweze kuwatia moyo wakati wowote ule.

NI NANI WANAOHITAJI KUTIWA MOYO?

3. Mtume Paulo alisema nini kuhusu kuwatia moyo wengine? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 “Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.” (Met. 12:25) Maneno hayo yanatuhusu sisi sote. Kila mmoja wetu anahitaji kutiwa moyo mara kwa mara. Paulo alionyesha kwamba hata wale walio na jukumu la kuwatia moyo wengine wanahitaji kutiwa moyo. Aliwaandikia hivi Wakristo walioishi Roma: “Ninatamani kuwaona ninyi ili niwape zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au badala yake, tutiane moyo, kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia.” (Rom. 1:11, 12) Naam, hata Paulo mwenyewe ambaye aliwatia moyo wengine kwa njia ya pekee, alihitaji pia kutiwa moyo pindi fulani.—Soma Waroma 15:30-32.

4, 5. Ni nani tunaoweza kuwatia moyo, na kwa nini?

4 Ndugu na dada wanaoishi maisha ya kujidhabihu wanapaswa kupongezwa. Miongoni mwao ni mapainia waaminifu. Wengi wao wamejidhabihu sana ili watumikie wakiwa mapainia. Na ndivyo ilivyo pia kwa wamishonari, Wanabetheli, waangalizi wa mzunguko na wake zao, na wale wanaofanya kazi katika ofisi za utafsiri. Wote hao wamedhabihu mambo fulani ili watumie muda mwingi zaidi katika utumishi mtakatifu. Hivyo, wanapaswa kutiwa moyo. Pia, wale ambao kwa sababu fulani walilazimika kuacha utumishi wa wakati wote lakini bado wanatamani kuwa katika utumishi huo, wanathamini sana wanapotiwa moyo.

5 Ndugu na dada ambao ni waseja kwa sababu wanataka kutii himizo la kuoa au kuolewa “katika Bwana tu,” ni miongoni mwa wale ambao pia wanahitaji kutiwa moyo. (1 Kor. 7:39) Vivyo hivyo, mke anayetimiza majukumu yake kwa bidii huthamini sana mume wake anapomwambia maneno yenye kutia moyo. (Met. 31:28, 31) Pia, Wakristo wanaodumu wakiwa waaminifu licha ya mateso au magonjwa wanahitaji kutiwa moyo. (2 The. 1:3-5) Yehova na Kristo huwafariji Wakristo hao wote waaminifu.—Soma 2 Wathesalonike 2:16, 17.

WAZEE HUJITAHIDI KUWATIA MOYO WENGINE

6. Kulingana na Isaya 32:1, 2 wazee wana jukumu gani?

6 Soma Isaya 32:1, 2Yesu Kristo anawatumia ndugu zake watiwa mafuta na pia “wakuu” walio sehemu ya kondoo wengine kuwatia moyo na kuwapa mwongozo watu waliovunjika moyo na kukata tamaa katika kipindi hiki kigumu. Hivyo ndivyo inavyopaswa kuwa, kwa sababu wazee si “mabwana” wa imani ya wengine lakini ni “wafanyakazi [wenzao]” kwa ajili ya shangwe ya ndugu zao.—2 Kor. 1:24.

7, 8. Mbali na kuwatia moyo wengine kwa maneno, ni nini kingine ambacho wazee wanaweza kufanya ili kuwajenga?

7 Mtume Paulo alituwekea kielelezo kizuri cha kuiga. Aliwaandikia hivi Wakristo waliokuwa wakiteswa huko Thesalonike: “Tulikuwa na upendo mwororo kwenu, tulijitahidi kuwapa habari njema ya Mungu na hata uhai wetu wenyewe, kwa sababu tuliwapenda sana.”—1 The. 2:8.

8 Akionyesha kwamba haitoshi tu kuwatia moyo wengine kwa maneno yetu, Paulo aliwaambia hivi wazee huko Efeso: “Ni lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’” (Mdo. 20:35) Paulo alikuwa tayari kuwatia moyo ndugu zake na hata “[kutumia vyote alivyo navyo] na kutumiwa kabisa kwa ajili” yao. (2 Kor. 12:15) Vivyo hivyo, wazee wanapaswa kuwatia moyo na kuwafariji ndugu zao, si tu kwa maneno bali pia wanapaswa kuwajenga kwa kuonyesha kwa matendo kwamba wanapendezwa nao kibinafsi.—1 Kor. 14:3.

9. Wazee wanaweza kutoaje shauri kwa njia itakayowatia moyo wengine?

9 Nyakati nyingine kuwajenga wengine huhusisha kuwapa shauri, lakini hata wanapofanya hivyo, wazee wanapaswa kufuata kielelezo kilichowekwa katika Maandiko kuhusu jinsi ya kuwashauri wengine kwa njia itakayowatia moyo. Yesu aliweka mfano mzuri sana kuhusu hilo baada ya kufufuliwa. Alihitaji kuyashauri kwa uthabiti makutaniko fulani yaliyokuwa Asia Ndogo lakini ona jinsi alivyofanya hivyo. Kabla ya kuyashauri makutaniko yaliyokuwa Efeso, Pergamamu, na Thiatira, Yesu aliyapongeza kwa uchangamfu. (Ufu. 2:1-5, 12, 13, 18, 19) Aliliambia hivi kutaniko lililokuwa Laodikia: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu. Basi uwe mwenye bidii na utubu.” (Ufu. 3:19) Wazee hujitahidi kuiga kielelezo cha Kristo wanapohitaji kuwashauri wengine.

SI JUKUMU LA WAZEE PEKE YAO

Wazazi, je, mnawazoeza watoto wenu kuwatia moyo wengine? (Tazama fungu la 10)

10. Sisi sote tunaweza kufanya nini ili kujengana?

10 Kuwatia moyo wengine si jukumu la wazee peke yao. Paulo aliwahimiza Wakristo wote waseme “neno jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwanufaishe” wengine. (Efe. 4:29) Kila mmoja wetu anapaswa kuwa macho kutambua “uhitaji” ambao wengine wanao. Paulo aliwashauri hivi Wakristo Waebrania: “Imarisheni mikono inayolegea na magoti yaliyo dhaifu, nanyi endeleeni kuifanyia miguu yenu mapito yaliyonyooka, ili kile ambacho ni kilemavu kisiteguke, badala yake, kiponywe.” (Ebr. 12:12, 13) Sisi sote, kutia ndani watoto, tunaweza kujengana kwa maneno yenye kutia moyo.

11. Marthe alipata msaada gani aliposhuka moyo?

11 Marthe, * dada ambaye wakati fulani alikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo (sonona), aliandika hivi: “Siku moja nilipokuwa nikisali ili nitiwe moyo, nilikutana na dada fulani mwenye umri mkubwa ambaye alinionyesha upendo na huruma, mambo ambayo niliyahitaji hasa wakati huo. Pia, alinisimulia mambo aliyopitia ambayo yalifanana kabisa na hali yangu, na hilo lilifanya nione kwamba si mimi peke yangu niliyepitia hali hiyo.” Huenda dada huyo mwenye umri mkubwa hakutambua jinsi maneno yake yalivyomsaidia sana Marthe.

12, 13. Ni katika njia zipi tunaweza kutumia ushauri unaopatikana katika Wafilipi 2:1-4?

12 Paulo aliwapa ushauri huu washiriki wote wa kutaniko la Filipi: “Basi, ikiwa kuna jambo lolote la kutia moyo katika Kristo, ikiwa kuna faraja yoyote ya upendo, ikiwa kuna ushirika wowote wa kiroho, ikiwa kuna upendo mwororo na huruma zozote, fanyeni shangwe yangu ijae kwa kuwa na akili ileile na kuwa na upendo uleule, mkiwa mmeunganishwa kabisa, mkiwa na wazo moja akilini. Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”—Flp. 2:1-4.

13 Naam, ili kuwatia moyo ndugu na dada zetu, sote tunapaswa kujitahidi kuangalia faida za wengine, kutoa “faraja . . . ya upendo,” kuwa na “ushirika . . . wa kiroho” pamoja nao, na kuwaonyesha “upendo mwororo na huruma.”

MAMBO YANAYOWEZA KUWATIA MOYO WENGINE

14. Ni jambo gani linaloweza kuwatia moyo wengine?

14 Habari kuhusu uaminifu wa wale tuliowasaidia kujifunza kweli wakati uliopita zinaweza kututia moyo sana. Hivyo ndivyo alivyohisi mtume Yohana, aliyeandika hivi: “Sina shangwe kubwa kuliko hii: kwamba nisikie watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.” (3 Yoh. 4) Mapainia wengi wanaweza kuthibitisha jinsi wanavyotiwa moyo sana kujua kwamba baadhi ya watu waliowafundisha kweli miaka mingi iliyopita bado ni waaminifu na huenda hata wanatumikia wakiwa mapainia. Kumkumbusha painia aliyevunjika moyo kuhusu mambo yenye kufurahisha aliyotimiza wakati uliopita kunaweza kumfariji sana.

15. Tunaweza kufanya nini ili kuwatia moyo wale wanaotumikia kwa uaminifu?

15 Waangalizi wengi wa mzunguko wameeleza jinsi wao na wake zao walivyotiwa moyo baada ya kupokea hata barua fupi ya kuwashukuru kwa ziara waliyofanya kutanikoni. Vivyo hivyo pia, wazee, wamishonari, mapainia, na washiriki wa familia ya Betheli hutiwa moyo wengine wanapowashukuru kwa sababu ya utumishi wao wa uaminifu.

JINSI SISI SOTE TUNAVYOWEZA KUWATIA MOYO WENGINE

16. Ni jambo gani rahisi tunaloweza kufanya ili kumtia mtu moyo?

16 Ni makosa kufikiri kwamba hatuwezi kuwatia moyo wengine eti kwa sababu sisi si wazungumzaji sana. Hatuhitaji kufanya mambo mengi ili kuwatia moyo wengine—huenda tabasamu changamfu tu ikatosha tunapowasalimu. Ikiwa tunayemsalimu hatatabasamu, huenda anahangaishwa na tatizo fulani. Hivyo, tunaweza kumfariji kwa kumsikiliza kwa makini.—Yak. 1:19.

17. Ndugu mmoja kijana alisaidiwaje alipovunjika moyo?

17 Henri, ndugu kijana, alivunjika moyo sana wakati watu wake wa karibu wa ukoo, kutia ndani baba yake ambaye alikuwa mzee wa kutaniko aliyeheshimika, walipoiacha kweli. Henri alitiwa moyo na mwangalizi wa mzunguko ambaye alimpeleka kwenye mkahawa fulani na kumpa fursa ya kueleza yaliyo moyoni mwake. Henri alitambua kwamba njia pekee ya kuisaidia familia yake irudi katika kweli ni kuvumilia kwa uaminifu. Alipata faraja kubwa kwa kusoma Zaburi 46; Sefania 3:17; na Marko 10:29, 30.

Sisi sote tunaweza kujengana na kutiana moyo (Tazama fungu la 18)

18. (a) Mfalme Sulemani aliandika nini kuhusu kuwatia moyo wengine? (b) Mtume Paulo alitoa pendekezo gani?

18 Mfano wa Marthe na Henri unaonyesha kwamba tunaweza kumtia moyo ndugu au dada anayehitaji faraja. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Neno linalosemwa wakati unaofaa—ni jema sana! Kumtupia mtu jicho kwa uchangamfu huufanya moyo ushangilie; habari njema huitia nguvu mifupa.” (Met. 15:23, 30, maelezo ya chini) Zaidi ya hilo, mtu aliyevunjika moyo anaposoma habari fulani katika gazeti la Mnara wa Mlinzi au katika Tovuti yetu, anaweza kupata nguvu tena. Paulo anaonyesha kwamba mtu anapoimba wimbo wa Ufalme pamoja na wengine anaweza kutiwa moyo. Aliandika hivi: “Endeleeni kufundishana na kutiana moyo kwa zaburi, sifa kwa Mungu, nyimbo za kiroho zinazoimbwa kwa shukrani, mkimwimbia Yehova mioyoni mwenu.”—Kol. 3:16; Mdo. 16:25.

19. Kwa nini itakuwa muhimu hata zaidi kutiana moyo katika siku zijazo, na tunapaswa kufanya nini?

19 Kadiri siku ya Yehova inavyozidi ‘kukaribia,’ ndivyo itakavyokuwa muhimu hata zaidi kutiana moyo. (Ebr. 10:25) Acheni tufuate himizo hili ambalo Paulo aliwapa Wakristo wa siku zake: “Endeleeni kutiana moyo na kujengana, kama vile kwa kweli mnavyofanya.”—1 The. 5:11.

^ fu. 11 Baadhi ya majina yamebadilishwa.