Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Yehova—Mungu Ambaye Hututia Moyo

Mwige Yehova—Mungu Ambaye Hututia Moyo

“Asifiwe Mungu . . . ambaye hututia moyo katika majaribu yetu yote.”​—2 KOR. 1:3, 4, maelezo ya chini.

NYIMBO: 7, 3

1. Ni maneno gani yenye kutia moyo ambayo Yehova alisema baada ya uasi kutokea katika bustani ya Edeni?

TANGU wanadamu walipotumbukia katika dhambi na kupoteza ukamilifu, Yehova amethibitika kuwa Mungu ambaye huwatia moyo viumbe wake. Mara tu baada ya uasi katika bustani ya Edeni, aliwapa wazao wa Adamu sababu ya kuwa na faraja. Wanadamu hawakuwa wamepoteza tumaini la wakati ujao. Kuelewa ahadi ya kinabii inayopatikana kwenye Mwanzo 3:15 kungewapa wanadamu tumaini kwamba hatimaye “yule nyoka wa zamani,” Shetani Ibilisi, pamoja na kazi zake zote za uovu zitaangamizwa.—Ufu. 12:9; 1 Yoh. 3:8.

YEHOVA ALIWATIA MOYO WATUMISHI WAKE WA ZAMANI

2. Yehova alimtiaje moyo Noa?

2 Noa, mtumishi wa Yehova, aliishi katika ulimwengu usiomwogopa Mungu ambapo yeye tu na familia yake ndio waliomwabudu Yehova. Akiwa amezungukwa na watu wakatili na wenye maadili mapotovu sana kingono, huenda Noa alivunjika moyo. (Mwa. 6:4, 5, 11; Yuda 6) Lakini Yehova alimpa habari fulani ambayo ilimpa ujasiri wa kuendelea ‘kutembea pamoja na Mungu.’ (Mwa. 6:9) Yehova alimwambia Noa kwamba angeuangamiza ulimwengu huo mwovu na akamwagiza jambo alilopaswa kufanya ili yeye na familia yake waokoke. (Mwa. 6:13-18) Katika kisa hiki, Yehova alithibitika kuwa Mungu ambaye huwatia moyo watumishi wake.

3. Yehova alimtiaje moyo Yoshua? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Baadaye, Yoshua alipewa kazi ngumu ya kuwagawia watu wa Mungu maeneo ya kuishi katika nchi ya ahadi. Kazi hiyo ilihusisha kuyashinda majeshi yenye nguvu ya mataifa yaliyomiliki eneo hilo. Yoshua alikuwa na kila sababu ya kuwa na wasiwasi. Yehova alijua jambo hilo, hivyo akamwambia Musa amtie moyo Yoshua. Mungu alimwambia hivi: “Nawe umweke Yoshua kuwa kiongozi, umtie moyo na kumwimarisha, kwa sababu yeye ndiye atakayewaongoza watu hawa kuvuka na kuwawezesha kuirithi nchi utakayoiona.” (Kum. 3:28) Kabla ya Yoshua kuanza kazi hiyo, Yehova alimtia moyo kwa maneno haya: “Je, si mimi niliyekuamuru uwe jasiri na imara? Basi uwe jasiri na imara. Usitetemeke wala kuogopa, kwa maana mimi Yehova Mungu wako nipo pamoja nawe mahali popote utakapoenda.” (Yos. 1:1, 9) Hayo yalikuwa maneno yenye kutia moyo kwelikweli!

4, 5. (a) Yehova aliwatiaje moyo watu wake wa kale? (b) Yehova alimtiaje moyo Mwana wake?

4 Si tu kwamba Yehova aliwatia moyo watu mmojammoja, bali pia aliwatia moyo watu wake wakiwa kikundi. Alisema kwa njia ya kiunabii maneno haya ambayo yangewafariji sana Wayahudi ambao walikuwa utekwani Babiloni: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isa. 41:10) Wakristo wa mapema walikuwa na uhakika huo pia, na ndivyo ilivyo kwa watu wa Mungu leo.—Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.

5 Yesu pia alitiwa moyo na Baba yake. Alipokuwa akibatizwa Yesu alisikia sauti kutoka mbinguni ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:17) Hapana shaka kwamba maneno hayo yalimwimarisha sana Yesu katika kipindi chote cha huduma yake duniani!

YESU ALIWATIA MOYO WENGINE

6. Mfano wa talanta unatutia moyo jinsi gani?

6 Yesu aliiga kielelezo cha Baba yake. Mfano wa talanta, unaopatikana kwenye unabii wa Yesu kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo, unatutia moyo kuwa waaminifu. Katika mfano huo bwana huyo aliwapongeza watumwa wake waaminifu kwa kuwaambia hivi: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Umekuwa mwaminifu katika mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi. Ingia katika shangwe ya bwana wako.” (Mt. 25:21, 23) Hayo ni maneno yenye kutia moyo kwelikweli yanayotuchochea tuendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu!

7. Yesu aliwatiaje moyo mitume wake, na hasa Petro?

7 Mitume wa Yesu walibishana mara nyingi kuhusu ni nani aliyekuwa mkuu zaidi miongoni mwao, lakini kwa subira Yesu aliwatia moyo wajinyenyekeze na kuwatumikia wengine badala ya kupiga ubwana. (Luka 22:24-26) Mtume Petro alikosea mara kadhaa na kumsikitisha Yesu. (Mt. 16:21-23; 26:31-35, 75) Badala ya kumwona Petro kuwa mtu asiyefaa kitu, Yesu alimtia moyo na hata akampa kazi ya kuwaimarisha ndugu zake.—Yoh. 21:16.

WALITIWA MOYO NYAKATI ZA KALE

8. Hezekia aliwatiaje moyo wakuu wa majeshi na watu wa Yuda?

8 Hata kabla ya Mwana wa Yehova kuja duniani na kutuwekea kielelezo kikamilifu cha kuwatia moyo wengine, tayari watumishi waaminifu wa Yehova walitambua umuhimu wa kufanya hivyo. Waashuru walipokuwa wakijitayarisha kuwavamia watu wa Yuda, Hezekia aliwakusanya wakuu wa majeshi na watu wa Yuda ili awatie moyo. “Basi watu wakaimarishwa na maneno [yake].”—Soma 2 Mambo ya Nyakati 32:6-8.

9. Kitabu cha Ayubu kinatufundisha nini kuhusu kuwatia moyo wengine?

9 Ingawa Ayubu mwenyewe alihitaji kufarijiwa, aliwafundisha ‘wale wafariji watatu wasumbufu’ somo kuhusu kuwatia wengine moyo. Aliwaambia kwamba ikiwa wangekuwa katika hali yake, ‘angewaimarisha kwa maneno ya kinywa chake, na kuwatuliza kwa faraja ya midomo yake.’ (Ayu. 16:1-5) Mwishowe, Ayubu alitiwa moyo na Elihu, na hata Yehova mwenyewe.—Ayu. 33:24, 25; 36:1, 11; 42:7, 10.

10, 11. (a) Kwa nini binti ya Yeftha alihitaji kutiwa moyo? (b) Ni nani leo wanaostahili kutiwa moyo?

10 Mtu mwingine wa nyakati za kale ambaye alihitaji kutiwa moyo ni binti ya Yeftha. Kabla ya kwenda kupigana na Waamoni, Mwamuzi Yeftha alimtolea Yehova nadhiri kwamba ikiwa angepata ushindi, mtu wa kwanza ambaye angetoka kuja kumpokea baada ya kutoka vitani angemtoa kwa Yehova ili atumikie katika mahali pake patakatifu. Ikatukia kwamba binti yake, mtoto pekee aliyekuwa naye, ndiye aliyekuja kumpokea ili kusheherekea ushindi aliopata. Yeftha alivunjika moyo sana. Hata hivyo, alitimiza nadhiri yake na kumpeleka binti yake huko Shilo ili atumikie katika hema la ibada maisha yake yote.—Amu. 11:30-35.

11 Ingawa huo ulikuwa uamuzi mgumu sana kwa Yeftha, ulikuwa mgumu hata zaidi kwa binti yake, ambaye aliunga mkono kwa hiari uamuzi wa baba yake. (Amu. 11:36, 37) Hivyo, hangefunga ndoa, kuwa na watoto, au kuendeleza jina na urithi wa familia. Ikiwa kuna mtu aliyehitaji faraja, ni binti ya Yeftha. Simulizi hilo la Biblia linasema hivi: “Kukawa na desturi hii katika Israeli: Kila mwaka, wasichana Waisraeli walienda kumpongeza binti ya Yeftha Mgileadi siku nne kwa mwaka.” (Amu. 11:39, 40) Je, si kweli kwamba Wakristo ambao hawajafunga ndoa, ambao wanatumia useja wao kuhangaikia zaidi “mambo ya Bwana” wanastahili pia kupongezwa na kutiwa moyo?—1 Kor. 7:32-35.

MITUME WALIWATIA MOYO NDUGU ZAO

12, 13. Petro aliwatiaje moyo ndugu zake?

12 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alimwambia hivi mtume Petro: “Simoni, Simoni, tazama! Shetani anataka kuwapata ninyi nyote ili awapepete kama ngano. Lakini nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isidhoofike; nawe utakaporudi, watie nguvu ndugu zako.”—Luka 22:31, 32.

Makutaniko ya karne ya kwanza yalitiwa moyo sana na barua za mitume, na bado zinatutia moyo mpaka leo hii (Tazama fungu la 12 hadi 17)

13 Petro alithibitika kuwa nguzo katika kutaniko la mapema la Kikristo. (Gal. 2:9) Aliwatia moyo ndugu zake kwa kielelezo chake cha ujasiri siku ya Pentekoste na hata baada ya hapo. Alipokuwa akikaribia mwisho wa huduma yake ya miaka mingi, aliwaandikia barua Wakristo wenzake. Alisema hivi kuhusu kusudi la kuwaandikia barua hiyo: “Nimewaandikia kwa maneno machache, ili kuwatia moyo na kutoa ushahidi kwa bidii kwamba hizi ndizo fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Simameni imara katika fadhili hizo.” (1 Pet. 5:12) Barua za Petro zilizoongozwa na roho zimekuwa zikiwatia moyo Wakristo kwa miaka hiyo yote mpaka leo hii. Tunahitaji sana maneno hayo yenye kutia moyo tunapongojea utimizo wa ahadi za Yehova.—2 Pet. 3:13.

14, 15. Barua za mtume Yohana zilizoongozwa na roho zimewatiaje moyo Wakristo kwa karne nyingi?

14 Mtume Yohana pia alikuwa nguzo katika kutaniko la mapema la Kikristo. Injili yake yenye kusisimua kuhusu huduma ya Yesu imekuwa ikiwatia moyo Wakristo kwa karne nyingi—mpaka sasa. Ni katika Injili yake pekee tunapopata maneno ya Yesu kwamba upendo ndiyo alama inayowatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu.—Soma Yohana 13:34, 35.

15 Barua tatu za Yohana zina hazina nyingine za kweli. Tunapolemewa na mzigo wa dhambi, je, hatufarijiki kusoma kwamba “damu ya Yesu . . . hutusafisha kutoka katika dhambi yote”? (1 Yoh. 1:7) Na ikiwa moyo wetu unaendelea kutuhukumu, je, hatutokwi na machozi tukiwa na shukrani tunaposoma kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu”? (1 Yoh. 3:20) Ni Yohana pekee aliyeandika kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8, 16) Barua yake ya pili na ya tatu inawapongeza Wakristo wanaoendelea “kutembea katika kweli.”—2 Yoh. 4; 3 Yoh. 3, 4.

16, 17. Mtume Paulo aliwatia moyo jinsi gani Wakristo wa mapema?

16 Katika karne ya kwanza, huenda Paulo ndiye mtume aliyefanya mengi zaidi kuwatia moyo ndugu zake. Inaelekea kwamba katika miaka ya mapema ya Ukristo, mitume wengi walikuwa wakiishi Yerusalemu, ambako baraza linaloongoza lilikuwa. (Mdo. 8:14; 15:2) Wakristo huko Yudea waliwahubiria kuhusu Kristo watu ambao kwa sababu ya mafundisho ya Kiyahudi waliamini kwamba kuna Mungu mmoja. Kwa upande mwingine, mtume Paulo aliongozwa na roho takatifu kwenda kuwahubiria watu wa mataifa walioishi katika maeneo yaliyokaliwa na Wagiriki na Waroma, ambao waliabudu miungu mingi.—Gal. 2:7-9; 1 Tim. 2:7.

17 Paulo alisafiri kwa mapana na marefu katika eneo ambalo sasa ni Uturuki, na vilevile alisafiri kwenda Ugiriki na Italia, akianzisha makutaniko ya Kikristo miongoni mwa watu ambao hawakuwa Wayahudi. Wakristo hao wageuzwa imani ‘waliteswa na wananchi wenzao’ na hivyo walihitaji kutiwa moyo. (1 The. 2:14) Karibu mwaka wa 50 W.K., Paulo aliliandikia hivi kutaniko lililokuwa limeanzishwa karibuni huko Thesalonike: “Sikuzote tunamshukuru Mungu tunapowataja nyote katika sala zetu, kwa maana tunaendelea kukumbuka kazi yenu ya uaminifu, kazi yenu ngumu ya upendo, na jinsi ambavyo mmevumilia.” (1 The. 1:2, 3) Pia aliwahimiza waimarishane, aliposema hivi: “Endeleeni kutiana moyo na kujengana.”—1 The. 5:11.

BARAZA LINALOONGOZA LILIWATIA MOYO WENGINE

18. Baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilimtiaje moyo Filipo?

18 Baraza linaloongoza la karne ya kwanza liliwatia moyo wale waliokuwa wakiongoza na Wakristo wote kwa ujumla. Mweneza-injili Filipo alipowahubiria Wasamaria kuhusu Kristo, washiriki wa baraza linaloongoza walimuunga mkono kikamili. Liliwatuma Petro na Yohana ambao walikuwa washiriki wa baraza hilo, wasali kwa ajili ya waamini wapya ili wapokee roho takatifu. (Mdo. 8:5, 14-17) Unaweza kuwazia jinsi Filipo na waamini hao wapya walivyotiwa moyo na utegemezo waliopata kutoka kwa baraza linaloongoza!

19. Barua ambayo Wakristo wa mapema walitumiwa na baraza linaloongoza ilikuwa na matokeo gani?

19 Baadaye, baraza linaloongoza lilihitaji kutoa uamuzi kuhusu ikiwa Wakristo wasio Wayahudi walipaswa kutahiriwa kama ilivyo desturi ya Wayahudi kulingana na Sheria ya Musa. (Mdo. 15:1, 2) Wakiongozwa na roho takatifu na baada ya kuchunguza Maandiko kwa kina, ndugu hao walifikia mkataa kwamba haikuwa lazima kwa Wakristo hao wasio Wayahudi kutahiriwa, kisha wakaandika barua kwa makutaniko ili kuyajulisha uamuzi huo. Wawakilishi wa baraza linaloongoza walitumwa kwa makutaniko hayo ili kupeleka barua hiyo. Ikawaje? “Baada ya kuisoma, wakashangilia kwa sababu ya kutiwa moyo.”—Mdo. 15:27-32.

20. (a) Leo, Baraza Linaloongoza huwatiaje moyo akina ndugu ulimwenguni pote? (b) Tutajibu swali gani katika makala inayofuata?

20 Leo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova huwatia moyo washiriki wa familia ya Betheli, watumishi wa pekee wa wakati wote walio shambani, na kwa kweli, ushirika mzima wa undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wa kweli. Na matokeo ni yaleyale—akina ndugu hushangilia kwa sababu ya kutiwa moyo! Zaidi ya hilo, katika mwaka wa 2015 Baraza Linaloongoza lilichapisha broshua Mrudie Yehova, ambayo imewatia moyo watu wengi ulimwenguni pote. Lakini je, ni wale tu wanaoongoza wanaopaswa kumwiga Yehova inapohusu kuwatia moyo wengine? Tutajibu swali hilo katika makala inayofuata.