Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika “Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” ya 2013 iliyorekebishwa, Zaburi 144:12-15 inawahusu watu wa Mungu. Katika tafsiri ya awali, Zaburi hiyo iliwahusu wageni waovu wanaotajwa katika mstari wa 11. Kwa nini maneno hayo yalirekebishwa?

Mpangilio wa maneno ya Kiebrania katika Zaburi hiyo yanaweza kutokeza maana zote mbili. Hivyo basi, mpangilio wa maneno katika toleo lililorekebishwa unategemea mambo yafuatayo:

  1. Msamiati na sarufi ya Kiebrania inaunga mkono marekebisho hayo. Uhusiano kati ya Zaburi 144:12-15 na mistari iliyotangulia unategemea maana ya neno la kwanza katika mstari wa 12, ambalo ni asher katika Kiebrania. Neno asher linaweza kutafsiriwa kwa njia kadhaa. Kwa mfano, linaweza kuwa kiwakilishi kibainishi, kama vile “ambao.” Katika tafsiri ya awali, neno “wanaosema” [ambao wanasema] ndilo lililotumiwa. Hivyo, mambo mema yanayotajwa katika mstari wa 12 hadi 14 yaliwahusu waovu, ambao wanatajwa katika mistari inayotangulia. Hata hivyo, neno asher linaweza pia kumaanisha matokeo ya jambo fulani na linaweza kutafsiriwa “hivyo,” “ili,” au “ndipo.” Neno “ndipo” ndilo ambalo limetumiwa katika tafsiri ya 2013 iliyorekebishwa na katika tafsiri nyingine za Biblia.

  2. Mpangilio mpya wa maneno unapatana kabisa na mistari mingine ya zaburi hiyo. Matumizi ya neno “ndipo” katika mstari wa 12 yanatusaidia kuelewa kwamba baraka zinazotajwa katika mstari wa 12 hadi 14 zinawahusu waadilifu—wale wanaoomba ‘waokolewe na kunusuriwa’ kutoka mikononi mwa waovu (mstari wa 11). Rekebisho hilo pia linaungwa mkono na mstari wa 15, ambapo neno “furaha” linalopatikana mara mbili kwenye mstari huo, linawahusu pia waadilifu. Hivyo, katika visa vyote viwili furaha inayotajwa inahusu kikundi kilekile cha watu—watu “ambao Mungu wao ni Yehova!” Zingatia pia kwamba maandishi ya awali ya Kiebrania hayakuwa na alama za vituo, kama vile alama za kunukuu. Hivyo, watafsiri wanapaswa kuamua maana sahihi, wakizingatia mitindo ya kishairi ya lugha ya Kiebrania, muktadha, na maandiko mengine ya Biblia yanayohusika.

  3. Mpangilio mpya wa maneno unapatana na maandiko mengine katika Biblia yanayoahidi baraka za Mungu kwa watu wake waaminifu. Kwa kuwa tafsiri ya neno asher imerekebishwa, sasa zaburi hiyo inaunga mkono tumaini thabiti ambalo Daudi alikuwa nalo kwamba baada ya Mungu kuwaokoa Waisraeli kutoka kwa maadui wao, Mungu angewabariki watu wake kwa kuwapa furaha na ufanisi. (Law. 26:9, 10; Kum. 7:13; Zab. 128:1-6) Kwa mfano, andiko la Kumbukumbu la Torati 28:4 linasema hivi: “Watoto wenu watabarikiwa na pia mazao ya ardhi yenu na watoto wa mifugo yenu, ng’ombe wenu wachanga na wanakondoo wenu.” Kwa kweli, chini ya utawala wa Sulemani mwana wa Daudi, taifa la Israeli lilifurahia amani na ufanisi ambao haukuwahi kuonekana kabla yake. Zaidi ya hilo, mambo fulani yanayohusu utawala wa Sulemani yanaonyesha jinsi mambo yatakavyokuwa chini ya utawala wa Masihi.—1 Fal. 4:20, 21; Zab. 72:1-20.

Kwa ufupi, mpangilio mpya wa maneno ya Zaburi 144 haubadili uelewaji wetu wa mafundisho ya Biblia. Badala yake, unafanya zaburi hiyo yote ionyeshe wazi zaidi tumaini ambalo watumishi wa Yehova wamekuwa nalo kwa muda mrefu—hukumu ya Mungu dhidi ya waovu na baada ya hapo amani na ufanisi wa kudumu kwa ajili ya waadilifu.—Zab. 37:10, 11.