Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumikie Yehova, Mungu wa Uhuru

Mtumikie Yehova, Mungu wa Uhuru

“Mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” —2 KOR. 3:17.

NYIMBO: 49, 73

1, 2. (a) Kwa nini watu katika siku za mtume Paulo walihangaikia sana suala la utumwa na uhuru? (b) Paulo alisema Chanzo cha uhuru wa kweli ni nani?

WAKRISTO wa mapema waliishi katika Milki ya Roma, na watu katika milki hiyo walijivunia sana sheria zao, mfumo wao wa utekelezaji haki, na uhuru waliokuwa nao. Hata hivyo, watumwa ndio waliochangia kwa kiasi kikubwa kuifanya milki hiyo iwe na nguvu na utukufu mwingi. Pindi moja, asilimia 30 hivi ya idadi ya watu walikuwa watumwa. Hapana shaka kwamba watu wa kawaida na vilevile Wakristo, walizungumzia sana mambo yaliyohusu utumwa na uhuru.

2 Barua za mtume Paulo zinasema mengi kuhusu uhuru. Hata hivyo, kusudi kuu la huduma yake halikuwa kuleta mabadiliko ya kijamii au ya kisiasa, jambo ambalo watu wengi walitamani. Badala ya kutegemea mtawala au kikundi fulani kilete uhuru, Paulo na Wakristo wenzake walijitahidi sana kuwasaidia wengine wajifunze kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu na dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo ambayo thamani yake haiwezi kulinganishwa na kitu chochote. Paulo aliwaonyesha waamini wenzake Chanzo cha uhuru wa kweli. Kwa mfano, katika barua yake ya pili kwa Wakristo huko Korintho, aliwaambia hivi waziwazi: “Yehova ni Roho, na mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.”—2 Kor. 3:17.

3, 4. (a) Paulo alizungumzia nini katika mistari iliyotangulia andiko la 2 Wakorintho 3:17? (b) Ni lazima tufanye nini ili tufurahie uhuru unaotoka kwa Yehova?

3 Mapema katika barua hiyo kwa Wakorintho, Paulo alizungumzia utukufu ambao Musa alikuwa nao aliposhuka Mlima Sinai baada ya kuzungumza na malaika wa Yehova. Watu walipomwona Musa, waliogopa sana, hivyo, Musa akaufunika uso wake kwa kitambaa. (Kut. 34:29, 30, 33; 2 Kor. 3:7, 13) Paulo alieleza hivi: “Lakini mtu anapomgeukia Yehova, kitambaa huondolewa.” (2 Kor. 3:16) Maneno hayo ya Paulo yanamaanisha nini?

4 Kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, ni Yehova pekee, Muumba wa vitu vyote, aliye na uhuru kamili na usio na mipaka. Hivyo ni wazi kwamba mahali ambapo Yehova yupo na “mahali palipo na roho ya Yehova,” pana uhuru. Hata hivyo, ili tupate uhuru huo na kunufaika nao ni lazima ‘tumgeukie Yehova,’ yaani, tusitawishe uhusiano wa karibu pamoja naye. Waisraeli walipokuwa nyikani hawakuwa na mtazamo wa kiroho kuhusu jinsi Yehova alivyoshughulika nao. Ni kana kwamba akili zao na mioyo yao ilikuwa imefunikwa kwa kitambaa na kufanywa kuwa migumu, wakikazia tu jinsi watakavyotumia uhuru waliopata baada ya kutoka Misri kutosheleza tamaa zao za kimwili.—Ebr. 3:8-10.

5. (a) Roho ya Yehova hutupatia uhuru wa aina gani? (b) Tunajuaje kwamba mtu anaweza kuwa na uhuru ambao Yehova hutoa licha ya kwamba amefungwa gerezani au ni mtumwa? (c) Tutachunguza maswali gani?

5 Uhuru ambao roho ya Yehova hutoa unahusisha mengi zaidi ya kumkomboa mtu kutokana na utumwa halisi. Roho ya Yehova humweka mtu huru kutokana na utumwa wa dhambi na kifo, na vilevile kutokana na ibada ya uwongo na mazoea yake, jambo ambalo haliwezi kamwe kutimizwa kwa jitihada za wanadamu. (Rom. 6:23; 8:2) Huo ni uhuru mzuri ajabu! Iwe mtu amefungwa jela au ni mtumwa anaweza kufurahia manufaa yanayotokana na uhuru huo. (Mwa. 39:20-23) Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Ndugu Harold King, ambaye alivumilia miaka mingi gerezani kwa sababu ya imani yake. Unaweza kutazama simulizi lake kwenye JW Broadcasting. (Tafuta kwenye MAHOJIANO NA MAMBO YALIYOONWA > KUVUMILIA MAJARIBU.) Sasa acheni tuchunguze maswali mawili. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini uhuru wetu? Na tunaweza kufanya nini ili tutumie kwa hekima uhuru huo?

KUTHAMINI UHURU AMBAO MUNGU AMETUPATIA

6. Waisraeli walionyeshaje kwamba hawakuthamini uhuru ambao Yehova aliwapa?

6 Tunapotambua thamani halisi ya zawadi yenye gharama kubwa tuliyopewa, tunachochewa kumwonyesha shukrani yule aliyetupatia zawadi hiyo. Waisraeli hawakuthamini uhuru ambao Yehova aliwapa alipowakomboa kutoka utumwani nchini Misri. Miezi michache baada ya kukombolewa, walianza kutamani sana vyakula na vinywaji walivyokuwa wakifurahia nchini Misri na kulalamika kuhusu maandalizi ya Yehova, hata walitaka kurudi Misri. Hebu wazia, Waisraeli waliona ‘samaki, matango, matikiti, vitunguu vya majani, vitunguu maji, na vitunguu saumu,’ kuwa vitu vya muhimu zaidi kuliko uhuru waliopewa wa kumwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Haishangazi kwa nini Yehova aliwakasirikia sana watu wake. (Hes. 11:5, 6, 10; 14:3, 4) Hilo ni somo kubwa kwetu!

7. Paulo alionyeshaje kwamba aliishi kulingana na shauri alilotoa kwenye 2 Wakorintho 6:1, na tunaweza kumwigaje?

7 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wote wasichukulie kivivihivi uhuru ambao Yehova kwa fadhili ametupatia kupitia Yesu Kristo, Mwana wake. (Soma 2 Wakorintho 6:1.) Kumbuka jinsi dhamiri ya mtume Paulo ilivyomtesa na kumsababishia maumivu mengi kwa sababu alijiona kuwa mtumwa wa dhambi na kifo. Hata hivyo, alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” Kwa nini? Aliwaeleza hivi Wakristo wenzake: “Kwa maana sheria ya roho ambayo hutokeza uzima katika muungano na Kristo Yesu imewaweka ninyi huru kutoka katika sheria ya dhambi na kifo.” (Rom. 7:24, 25; 8:2) Kama mtume Paulo, sisi pia hatupaswi kamwe kuchukulia kivivihivi uhuru ambao Yehova ametupatia kwa kutukomboa kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo. Kwa msingi wa fidia, tunaweza kumtumikia Mungu wetu tukiwa na dhamiri safi na kufurahia kwelikweli kufanya hivyo.—Zab. 40:8.

Je, unatumia uhuru wako wa kuchagua kuendeleza masilahi ya Ufalme au masilahi yako? (Tazama fungu la 8 hadi 10)

8, 9. (a) Mtume Petro alitoa onyo gani kuhusu jinsi tunavyopaswa kutumia uhuru wetu? (b) Tunakabili hatari gani leo?

8 Hata hivyo, zaidi ya kuonyesha shukrani kwa uhuru wenye thamani ambao tumepewa, tunapaswa kuwa waangalifu tusiutumie vibaya. Mtume Petro alionya dhidi ya kutumia uhuru wetu kama kisingizio cha kutosheleza tamaa zetu za kimwili. (Soma 1 Petro 2:16.) Je, onyo hilo halikukumbushi mambo yaliyowapata Waisraeli walipokuwa nyikani? Sisi pia tunakabili hatari hiyo, na labda tunakabili hatari kubwa zaidi kuliko wao. Shetani na ulimwengu wake unaendelea zaidi na zaidi kutushawishi kupitia mavazi na mapambo, chakula na vinywaji, tafrija na burudani, na mambo mengine chungu nzima. Mara nyingi matangazo ya biashara yaliyotayarishwa kwa ujanja mwingi hutumia watu wenye kuvutia ili kutushawishi tuone kwamba ni lazima tununue vitu ambavyo kwa kweli hatuvihitaji. Ni rahisi sana kunaswa na mitego hiyo na kutumia vibaya uhuru wetu!

9 Onyo la mtume Petro linahusu pia mambo muhimu ya maisha, kama vile elimu, ajira, au kazi tunayochagua kufanya. Kwa mfano, vijana wengi walio shuleni wanashinikizwa wasome kwa bidii ili wastahili kujiunga na taasisi maarufu za elimu ya juu. Wanashawishiwa kuamini kwamba elimu ya juu itawasaidia wapate kazi zenye mshahara mnono na zinazoheshimika katika jamii, nao huonyeshwa tofauti iliyopo kati ya mishahara ya waliohitimu kutoka katika taasisi hizo na wale waliopata elimu ya kawaida. Kwa kuwa vijana wanahitaji kufanya maamuzi yatakayoathiri maisha yao yote, mambo hayo yanaweza kuwavutia sana. Vijana hao pamoja na wazazi wao wanapaswa kukumbuka nini?

10. Tunapaswa kukumbuka jambo gani tunapotumia uhuru wetu kufanya maamuzi ya kibinafsi?

10 Huenda baadhi ya watu wakahisi kwamba kwa kuwa mambo hayo ni ya kibinafsi, wana uhuru wa kujiamulia wanachotaka maadamu dhamiri yao inawaruhusu. Labda jambo linalofanya wafikiri hivyo ni maneno haya ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo huko Korintho kuhusu chakula: “Kwa nini uhuru wangu uhukumiwe na dhamiri ya mtu mwingine?” (1 Kor. 10:29) Ingawa ni kweli kwamba tuna uhuru wa kujiamulia mambo yanayohusu elimu na kazi, tunapaswa kukumbuka kwamba uhuru wetu una mipaka na kwamba maamuzi yote tunayofanya huwa na matokeo mazuri au mabaya. Kwa sababu hiyo, Paulo alitangulia kusema hivi: “Mambo yote ni halali [au, “yanakubalika,” maelezo ya chini], lakini si mambo yote yaliyo na faida. Mambo yote ni halali, lakini si mambo yote yanayojenga.” (1 Kor. 10:23) Ni wazi kwamba hilo linatusaidia tutambue kwamba kuna mambo muhimu zaidi tunayopaswa kuzingatia kuliko mapendezi yetu wenyewe inapohusu kutumia uhuru wetu wa kibinafsi katika nyanja zote za maisha yetu.

KUTUMIA KWA HEKIMA UHURU WETU KUMTUMIKIA MUNGU

11. Tumewekwa huru kwa kusudi gani?

11 Petro alipowaonya Wakristo dhidi ya kutumia vibaya uhuru wao, aliwaonyesha pia kusudi la uhuru huo. Alituhimiza tutumie uhuru wetu “kama watumwa wa Mungu.” Hivyo, sababu hasa iliyomfanya Yehova, kupitia Yesu, atuweke huru kutoka katika sheria ya dhambi na kifo ni ili tumtumikie kikamili “kama watumwa wa Mungu.”

12. Noa na familia yake walituwekea mfano gani?

12 Njia bora kabisa itakayotulinda dhidi ya kutumia uhuru wetu vibaya, na hivyo kuepuka kuwa watumwa wa tamaa ya ulimwengu huu ya kujitafutia makuu na tamaa nyinginezo, ni kujishughulisha kikamili katika utendaji wa kiroho. (Gal. 5:16) Fikiria mfano wa Noa na familia yake. Waliishi katika ulimwengu uliokuwa umejaa ukatili na ukosefu wa maadili. Hata hivyo, hawakujihusisha wala kuathiriwa na tamaa na malengo ya watu waliowazunguka. Ni nini kilichowasaidia? Walichagua kujishughulisha kabisa na mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewaamuru—kujenga safina, kuhifadhi chakula kwa ajili yao na kwa ajili ya wanyama, na kuwatangazia onyo wanadamu wenzao. “Noa akafanya kulingana na mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwa. 6:22) Ikawaje? Noa na familia yake waliokoka ulimwengu huo ulipoangamizwa.—Ebr. 11:7.

13. Yesu alikabidhiwa kazi gani ambayo aliwaagiza wafuasi wake wafanye?

13 Yehova ametuamuru tufanye nini leo? Tukiwa wanafunzi wa Yesu, tunajua vizuri kazi ambayo Mungu ametukabidhi. (Soma Luka 4:18, 19.) Leo, watu wengi bado wamepofushwa na mungu wa mfumo huu wa mambo na ni watumwa wa dini ya uwongo, mfumo wa kibiashara, na mfumo wa kisiasa wa ulimwengu huu. (2 Kor. 4:4) Tuna pendeleo la kufuata hatua za Yesu kwa kuwasaidia watu wamjue na kumwabudu Yehova, Mungu wa uhuru. (Mt. 28:19, 20) Hiyo si kazi rahisi, na ina changamoto nyingi. Katika nchi fulani, watu ambao hawapendezwi na mambo ya kiroho wanazidi kuongezeka, na baadhi yao huwa wakali tunapowahubiria. Swali ambalo kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza ni, ‘Je, ninaweza kutumia uhuru wangu kufanya mengi zaidi ili kutegemeza kazi ya Ufalme?’

14, 15. Watu wa Yehova wameamua kufanya nini inapohusu kazi ya kuhubiri? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

14 Ni jambo linalotia moyo sana kuona kwamba wengi wametambua uharaka wa nyakati tunazoishi nao wamerahisisha maisha yao ili wawe watumishi wa wakati wote. (1 Kor. 9:19, 23) Baadhi yao wanatumikia katika eneo la kutaniko lao na wengine wamehamia katika maeneo yenye uhitaji. Ripoti inaonyesha kwamba katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, zaidi ya ndugu na dada 250,000 walianza upainia wa kawaida, hivyo sasa kuna zaidi ya mapainia wa kawaida 1,100,000 ulimwenguni pote. Hayo ni matokeo yenye kupendeza kwelikweli ya kutumia kwa hekima uhuru wetu kumtumikia Yehova!—Zab. 110:3.

15 Ni nini kilichowasaidia ndugu na dada hao watumie kwa hekima uhuru wao? Fikiria mfano wa John na Judith, ambao wametumikia katika nchi mbalimbali kwa miaka 30. Wanakumbuka kwamba Shule ya Utumishi wa Painia ilipoanzishwa mwaka wa 1977, wanafunzi walitiwa moyo kuwa tayari kuhamia na kutumikia katika maeneo yenye uhitaji. Ili kufikia lengo hilo, John anasema kwamba alihitaji kubadilisha mara kadhaa kazi aliyofanya ili awe na maisha rahisi. Mwishowe, walipohamia katika nchi ya kigeni, walitambua kwamba kusali kwa Yehova na kumtegemea kuliwasaidia kushinda vizuizi vya kujifunza lugha mpya, kuzoea utamaduni mpya, na kuvumilia hali mbalimbali za hewa. Wanahisije kuhusu miaka hiyo yote ya utumishi wao? John anasema hivi: “Nilihisi nilikuwa nimezama katika kazi bora zaidi kuliko zote nilizowahi kufanya. Yehova akawa halisi zaidi kwangu kama baba mpendwa. Nilielewa vizuri zaidi maana ya andiko la Yakobo 4:8: ‘Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.’ Nilitambua kwamba nimepata kile nilichokuwa nikitafuta, kusudi lenye kuridhisha maishani.”

16. Licha ya hali zao, maelfu ya watu wametumiaje uhuru wao kwa hekima?

16 Tofauti na wenzi hao, hali za ndugu na dada wengine huwaruhusu wafanye utumishi wa wakati wote kwa muda mfupi tu. Ingawa hivyo, wengi wao hujitolea kwenye ujenzi wa miradi mbalimbali ya kitheokrasi ulimwenguni pote. Kwa mfano, makao makuu ya ulimwenguni pote yalipokuwa yakijengwa huko Warwick, New York, ndugu na dada 27,000 hivi walijitolea—baadhi yao kwa majuma mawili, wengine kwa miezi kadhaa, na wengine kwa mwaka mmoja au zaidi. Wengi wao waliacha shughuli zao ili wakatumikie huko. Ndugu na dada hao ni mifano mizuri sana ya watu wanaotumia uhuru waliopewa kumsifu na kumheshimu Yehova, Mungu wa uhuru!

17. Wale wanaotumia kwa hekima uhuru waliopewa na Mungu wanatazamia nini wakati ujao?

17 Tunashukuru kwamba tunamjua Yehova na tunaweza kufurahia uhuru tunaopata katika ibada ya kweli. Acheni maamuzi tunayofanya yaonyeshe kwamba tunauthamini sana uhuru huo. Badala ya kuutumia vibaya, acheni tutumie uhuru wetu na fursa zinazotokana na uhuru huo kumtumikia Yehova kikamili kadiri iwezekanavyo. Tukifanya hivyo, tunaweza kutazamia kupata baraka ambazo Yehova ameahidi wakati maneno ya unabii huu yatakapotimia: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.