Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kupata Uhuru wa Kweli

Jinsi ya Kupata Uhuru wa Kweli

“Mwana akiwaweka ninyi huru, kwa kweli mtakuwa huru.” —YOH. 8:36.

NYIMBO: 54, 36

1, 2. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wanafanya jitihada nyingi ili wawe huru? (b) Jitihada hizo zimekuwa na matokeo gani?

LEO, watu wengi ulimwenguni hupenda kuzungumza kuhusu usawa, uhuru, na kujikomboa. Katika sehemu nyingi za ulimwengu watu wanatamani kuwa huru kutokana na ukandamizaji, ubaguzi, na umaskini. Wengine hudai haki ya kuwa na uhuru wa kusema, wa kuchagua, na wa kujiamulia watakavyo. Inaonekana watu kila mahali wanatamani sana kujiamulia jinsi watakavyoishi na mambo wanayotaka kufanya.

2 Hata hivyo, wanakabili changamoto kubwa sana katika jitihada za kupata uhuru huo. Inapohusu masuala ya kijamii na ya kisiasa, watu wengi huamua kufanya maandamano, migomo, vurugu, au hata mapinduzi. Lakini je, jitihada zao hutimiza lengo lililokusudiwa? Sivyo hata kidogo, badala yake mara nyingi jitihada hizo husababisha matatizo chungu nzima na hata watu hupoteza uhai wao. Mambo hayo yote yanathibitisha ukweli wa maneno haya yaliyoongozwa na roho ambayo Mfalme Sulemani aliandika: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.”—Mhu. 8:9.

3. Tunaweza kufanya nini ili turidhike na kuwa na furaha ya kweli?

3 Mwanafunzi Mkristo Yakobo alionyesha jinsi tunavyoweza kupata furaha ya kweli na kuridhika maishani. Aliandika hivi: “Anayechunguza sheria kamilifu ambayo ni ya uhuru na kudumu katika hiyo . . . atafurahia kile anachofanya.” (Yak. 1:25) Yehova, ambaye ametupatia sheria hiyo kamilifu, anajua vizuri sana mambo ambayo wanadamu wanahitaji ili waridhike na kuwa na furaha kamili. Aliwapa wenzi wa ndoa wa kwanza kila kitu walichohitaji ili wawe na furaha—kutia ndani uhuru wa kweli.

WANADAMU WALIPOKUWA NA UHURU WA KWELI

4. Adamu na Hawa walifurahia uhuru wa aina gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Tunaposoma sura mbili za kwanza za kitabu cha Mwanzo, tunaona wazi kwamba Adamu na Hawa walifurahia uhuru ambao leo ni ndoto tu—walikuwa na kila kitu walichohitaji, hakuna chochote kilichowatia woga, na hakuna yeyote aliyewakandamiza. Wenzi hao wa kwanza hawakuwa na mahangaiko yoyote kuhusu chakula, kazi, magonjwa, au kifo. (Mwa. 1:27-29; 2:8, 9, 15) Je, hilo linamaanisha kwamba uhuru ambao Adamu na Hawa walifurahia haukuwa na mipaka? Acheni tuone.

5. Kinyume na maoni ya watu wengi leo, ni nini kinachohitajika ili watu wawe huru?

5 Watu wengi leo hufikiri kwamba mtu aliye na uhuru wa kweli ni yule anayeweza kufanya jambo lolote apendalo bila kujali matokeo ya matendo yake. Kitabu The World Book Encyclopedia kinafafanua uhuru kuwa “uwezo wa kuchagua mambo unayotaka kufanya na kuyatekeleza.” Hata hivyo, kinasema hivi pia: “Kisheria, watu wako huru ikiwa hawawekewi mipaka inayowakandamiza, isiyo ya lazima, au inayopita kiasi.” Hilo linadokeza kwamba kihalisi, ni muhimu kuwe na mipaka fulani ili kila mtu katika jamii anufaike na uhuru unaotolewa. Hivyo basi tunaweza kujiuliza hivi: Ni nani aliye na haki ya kuamua ni mipaka gani isiyowakandamiza watu, iliyo ya lazima, na isiyopita kiasi?

6. (a) Kwa nini ni Yehova pekee aliye na uhuru kamili? (b) Wanadamu wanaweza kufurahia uhuru wa aina gani, na kwa nini?

6 Tunapozungumza kuhusu uhuru, tunapaswa kukumbuka jambo hili muhimu kwamba ni Yehova pekee aliye na uhuru kamili na usio na mipaka. Kwa nini? Kwa sababu yeye ndiye Muumba wa vitu vyote, mweza yote, na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. (1 Tim. 1:17; Ufu. 4:11) Kumbuka maneno yenye kuvutia ambayo Mfalme Daudi anatumia kufafanua cheo cha pekee na kilichokwezwa sana ambacho ni Yehova pekee aliye nacho. (Soma 1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12.) Hivyo basi, viumbe wote mbinguni na duniani wana uhuru ulio na mipaka. Ni lazima watambue kwamba Yehova Mungu pekee ndiye aliye na mamlaka ya kuamua ni mipaka gani isiyokandamiza, iliyo ya lazima, na isiyopita kiasi. Na ukweli wa mambo ni kwamba Yehova Mungu aliwawekea wanadamu mipaka hiyo tangu alipowaumba.

7. Ni baadhi ya mambo gani ambayo sisi hufanya kiasili yanayotuletea furaha?

7 Ingawa mwanzoni Adamu na Hawa walikuwa huru katika njia mbalimbali, uhuru wao ulikuwa na mipaka. Mungu aliwaumba wakiwa na mipaka fulani ya asili. Kwa mfano, wazazi wetu wa kwanza walijua kwamba ili waendelee kuishi walihitaji kupumua, kula, kulala, na kadhalika. Je, kufanya mambo hayo kungewafanya wahisi kwamba wamenyimwa uhuru? La hasha, kwa sababu Yehova alihakikisha kwamba wangeridhika na kufurahia kufanya mambo hayo ya kila siku. (Zab. 104:14, 15; Mhu. 3:12, 13) Ni nani asiyefurahia kuvuta hewa safi, kula chakula anachokipenda, au kulala usingizi mnono? Tunafurahia kufanya mambo hayo ya lazima bila kuhisi kwamba tumebanwa au ni mzigo kwetu. Hapana shaka kwamba Adamu na Hawa walihisi hivyo pia.

8. Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza amri gani hususa, na kwa kusudi gani?

8 Yehova aliwapa Adamu na Hawa amri hususa ya kuijaza dunia na kuitunza. (Mwa. 1:28) Je, amri hiyo iliwanyima uhuru kwa njia fulani? La hasha! Amri hiyo ilitolewa ili wanadamu wapate fursa ya kushiriki katika kutimiza kusudi la Muumba wao, yaani, kuifanya dunia iwe paradiso ambapo wanadamu wakamilifu wangeweza kuishi milele. (Isa. 45:18) Leo, si kinyume na mapenzi ya Yehova kuchagua kubaki mseja au kufunga ndoa na kubaki bila watoto. Ingawa kuna changamoto nyingi zinazoletwa na kufunga ndoa na kulea watoto, watu wengi bado huamua kufanya hivyo. (1 Kor. 7:36-38) Kwa nini? Kwa sababu, katika hali za kawaida mambo hayo hufanya watu waridhike na kupata furaha. (Zab. 127:3) Ikiwa Adamu na Hawa wangetii wangeweza kufurahia ndoa yao na maisha pamoja na familia yao milele.

JINSI UHURU WA KWELI ULIVYOPOTEZWA

9. Kwa nini amri ya Mungu iliyo kwenye Mwanzo 2:17 haikuwa yenye kukandamiza, isiyo ya lazima, au iliyopita kiasi?

9 Yehova aliwapa Adamu na Hawa amri nyingine na akawaeleza waziwazi adhabu ambayo wangepata ikiwa wangeivunja. Aliwaambia hivi: “Kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwa. 2:17) Je, amri hiyo ilikuwa yenye kukandamiza, isiyo ya lazima, au iliyopita kiasi? Je, iliwanyima Adamu na Hawa uhuru wao? La hasha! Isitoshe, wasomi kadhaa wa Biblia wanasema kwamba hiyo ilikuwa amri yenye busara na iliyopatana na akili. Kwa mfano, msomi mmoja anaeleza hivi: “Amri ya Mungu inayopatikana kwenye [Mwanzo 2:16, 17] inafunua kwamba ni Mungu tu anayejua yaliyo mema . . . kwa wanadamu na ni Mungu tu anayejua mambo ambayo si mema . . . kwao. Ili wanadamu wafurahie mambo ‘mema’ ni lazima wamtegemee Mungu na kumtii. Wakikosa kutii, wataachwa wajiamulie wenyewe yaliyo mema . . . na yasiyo mema.” Huo ni mzigo mzito ambao wanadamu hawawezi kufanikiwa kuubeba kwa uwezo wao wenyewe.

Uamuzi wa Adamu na Hawa ulikuwa na matokeo mabaya sana! (Tazama fungu la 9 hadi 12)

10. Kwa nini hatupaswi kufikiri kwamba kuwa na uhuru wa kuchagua ni sawa na kuwa na haki ya kuamua lililo jema na lililo baya?

10 Leo, watu wengi wanaposoma kuhusu amri ambayo Yehova alimpa Adamu wanafikiri kwamba alinyimwa uhuru wa kufanya aliyotaka. Kwa kufikiri hivyo, wanashindwa kutambua tofauti iliyopo kati ya uhuru wa kuchagua jambo la kufanya na haki ya kuamua lililo jema na lililo baya. Adamu na Hawa walikuwa na uhuru wa kuchagua kumtii Mungu au kutomtii. Hata hivyo, ni Yehova pekee aliye na haki kamili ya kuamua lililo jema na lililo baya, jambo lililowakilishwa na “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” uliokuwa katika bustani ya Edeni. (Mwa. 2:9) Lazima tukiri kwamba si rahisi nyakati zote kujua matokeo ya mambo tunayochagua kufanya; wala hatuwezi kujua ikiwa matokeo ya mambo hayo yatakuwa mazuri nyakati zote. Hiyo ndiyo sababu mara nyingi tunaona watu wakifanya maamuzi kwa nia nzuri kabisa lakini mwishowe maamuzi waliyofanya yanasababisha wateseke na kukumbwa na misiba. (Met. 14:12) Naam, wanadamu wana mipaka kuhusiana na mambo wanayoweza kutimiza. Kupitia amri Yake, Yehova alikuwa akiwafundisha kwa upendo Adamu na Hawa jinsi ya kuwa na uhuru wa kweli. Kwa njia gani, na waliitikiaje?

11, 12. Kwa nini uamuzi wa Adamu na Hawa uliwaletea msiba? Toa mfano.

11 Kama tujuavyo, wazazi wetu wa kwanza walichagua kutotii. Hawa alishindwa kabisa kupinga kishawishi cha Shetani aliyemwahidi kwamba ‘macho yako yatafunguliwa nawe utakuwa kama Mungu, ukijua mema na mabaya.’ (Mwa. 3:5) Adamu na Hawa walipochagua kutomtii Mungu, je, walipata uhuru mwingi zaidi? Sivyo hata kidogo. Matokeo yalikuwa tofauti na kile ambacho Shetani alikuwa amewaahidi. Isitoshe, punde si punde walijionea kwamba kukataa mwongozo wa Yehova na kufanya walivyotaka kulisababisha wapatwe na matatizo makubwa. (Mwa. 3:16-19) Kwa nini? Kwa sababu Yehova hakuwapa wanadamu uhuru wa kujiamulia lililo jema na lililo baya.—Soma Methali 20:24 na maelezo ya chini; Yeremia 10:23.

12 Mfano wa rubani anayeendesha ndege unaweza kutusaidia kuelewa vizuri jambo hilo. Ili afike salama mahali anapotaka kwenda, kwa kawaida anapaswa kutumia njia iliyopangwa mapema ambayo ndege inapaswa kufuata. Vifaa vya kisasa vilivyo kwenye ndege humwongoza rubani na kumsaidia awasiliane na waongozaji wa ndege walio ardhini ambao humwelekeza ili afike mahali anapokusudia kwenda. Hata hivyo, rubani akichagua kupuuza mwongozo huo na kuamua kusafiri kwa kufuata njia nyingine ambayo yeye anapenda, matokeo yanaweza kuwa mabaya sana. Kama rubani huyo, Adamu na Hawa walijiamulia njia waliyotaka kufuata. Walikataa mwongozo ambao Mungu alikuwa amewapa. Ikawaje? Uamuzi huo uliwasababishia wao pamoja na watoto wao dhambi na kifo. (Rom. 5:12) Kwa kuwa walijiamulia waliyotaka kufanya, walipoteza uhuru wa kweli waliokuwa wamepewa.

JINSI YA KUPATA UHURU WA KWELI

13, 14. Tunaweza kupataje uhuru wa kweli?

13 Huenda watu wakafikiri kwamba kadiri walivyo na uhuru mwingi zaidi ndivyo maisha yao yatakavyokuwa mazuri zaidi, lakini ukweli wa mambo ni kwamba uhuru usio na mipaka ni upanga wenye makali pande mbili. Ni kweli kwamba uhuru huleta faida nyingi, hata hivyo, je, umewahi kuwazia jinsi ambavyo ulimwengu ungekuwa ikiwa hakungekuwa na vizuizi vyovyote? Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema hivi: “Sheria zilizopo katika jamii zote ni mfumo tata unaosawazisha aina mbalimbali za uhuru na vizuizi vilivyopo.” Neno “tata” linaeleza vizuri jinsi ilivyo vigumu kupata usawaziko huo. Ndio maana leo kuna sheria chungu nzima zilizotungwa na wanadamu, na vilevile wanasheria na mahakimu wengi ambao kazi yao ni kufafanua na kutekeleza sheria hizo.

14 Tofauti na hilo, Yesu Kristo alionyesha njia rahisi ya kupata uhuru wa kweli. Alisema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:31, 32) Yesu alionyesha kwamba ili tupate uhuru wa kweli ni lazima tutimize mambo mawili: Kwanza, tukubali kweli aliyofundisha, na pili, tuwe wanafunzi wake. Tutakuwa na uhuru wa kweli tukitimiza matakwa hayo. Lakini tutakuwa huru kutokana na nini? Yesu aliendelea kusema hivi: “Kila mtu anayetenda dhambi ni mtumwa wa dhambi. . . . Mwana akiwaweka ninyi huru, kwa kweli mtakuwa huru.”—Yoh. 8:34, 36.

15. Kwa nini uhuru ambao Yesu aliahidi unaweza kutufanya tuwe ‘huru kikweli’?

15 Ni wazi kwamba uhuru ambao Yesu aliwaahidi wanafunzi wake ni bora kuliko uhuru wa kijamii au wa kisiasa ambao watu wengi leo hutamani kupata. Yesu aliposema, “Mwana akiwaweka ninyi huru, kwa kweli mtakuwa huru,” alikuwa akizungumzia kuwa huru kutokana na utumwa na ukandamizaji mkubwa zaidi ambao wanadamu wamewahi kupitia, yaani, kuwa ‘watumwa wa dhambi.’ Dhambi haisababishi tu tufanye mambo mabaya lakini pia inaweza kutuzuia kutenda mambo ambayo tunajua ni sawa, au kutuzuia kutimiza mambo ambayo tunajua tunaweza kutimiza. Kwa msingi huo, sisi ni watumwa wa dhambi, na matokeo ya utumwa huo ni kukatishwa tamaa, maumivu, mateso, na mwishowe kifo. (Rom. 6:23) Mtume Paulo alikuwa na hisia hizo za maumivu na uchungu mwingi. (Soma Waroma 7:21-25.) Wakati ambapo minyororo ya dhambi itafunguliwa na kutupiliwa mbali, ndipo tutakapopata uhuru wa kweli ambao wazazi wetu wa kwanza walifurahia.

16. Ni nini kitakachotusaidia kuwa huru kikweli?

16 Yesu aliposema, “mkikaa katika neno langu,” alikuwa akionyesha kwamba kuna matakwa au mipaka iliyowekwa ambayo lazima mtu azingatie ili Yesu amweke huru. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tumejikana wenyewe na kuchagua kuishi ndani ya mipaka iliyowekwa kulingana na mafundisho ya Kristo kwa ajili ya wanafunzi wake. (Mt. 16:24) Kama Yesu alivyoahidi, tutakuwa na uhuru wa kweli tutakapopata manufaa kamili ya dhabihu ya fidia.

17. (a) Ni nini kitakachofanya tuwe na maisha yenye kuridhisha na yaliyo na kusudi? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Kujitiisha chini ya mafundisho ya Yesu tukiwa wanafunzi wake hufanya turidhike na kuwa na maisha yenye kusudi. Kufanya hivyo hutufungulia fursa ya kuwekwa huru kabisa kutokana na utumwa wa dhambi na kifo. (Soma Waroma 8:1, 2, 20, 21.) Makala inayofuata itazungumzia jinsi tunavyoweza kutumia kwa hekima uhuru tulio nao ili tumheshimu Yehova milele, Mungu anayetoa uhuru wa kweli.