Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana, Je, Mnatanguliza Malengo ya Kiroho Maishani?

Vijana, Je, Mnatanguliza Malengo ya Kiroho Maishani?

“Mkabidhi Yehova lolote unalofanya, na mipango yako itafanikiwa.”—MET. 16:3.

NYIMBO: 135, 144

1-3. (a) Ni changamoto gani inayowakabili vijana wote, na tunaweza kutumia mfano gani kuelezea hali yao? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Vijana Wakristo wanaweza kufanya nini ili wakabiliane kwa mafanikio na changamoto hiyo?

TUSEME kwamba unataka kusafiri kwenda mji wa mbali ili kuhudhuria tukio fulani muhimu. Ili ufike huko unahitaji kusafiri mwendo mrefu kwa basi. Ukiwa katika kituo cha basi unachanganyikiwa kuona wasafiri wengi na mabasi mengi. Jambo zuri ni kwamba una lengo hususa akilini, yaani, kupata basi linaloenda mahali unapotaka kwenda! Kwa kweli, ikiwa utapanda basi linaloenda mahali pengine, hutafika kule unakotaka kwenda.

2 Vijana leo, wanaweza kulinganishwa na abiria hao. Vijana wanakabili safari ndefu—safari ya maisha. Nyakati nyingine huenda wakalemewa na fursa na maamuzi yanayowakabili. Vijana, mnaweza kufanya mambo yawe rahisi kwa kujiwekea lengo hususa kuhusu mahali mnapotaka kufika maishani. Mnapaswa kuelekea upande gani?

3 Makala hii inajibu swali hilo kwa kuwatia moyo vijana wamtangulize Yehova na kufanya tamaa yao ya kumpendeza kuwa jambo kuu maishani mwao. Hilo linamaanisha kumhusisha Yehova katika nyanja zote za maisha, iwe ni elimu, kazi, majukumu ya kifamilia, na kadhalika. Pia, linamaanisha kujitahidi kufikia malengo ya kiroho. Vijana ambao lengo lao kuu maishani ni kumtumikia Yehova, wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawabariki na kuwasaidia wafanikiwe.—Soma Methali 16:3.

KWA NINI UJIWEKEE MALENGO YA KIROHO?

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Kujiwekea malengo ya kiroho ukiwa kijana ni jambo linalofaa sana. Kwa nini? Tutachunguza sababu tatu. Sababu mbili za kwanza zinatusaidia tuone kwamba mtu anapojitahidi kufikia malengo ya kiroho uhusiano wake na Yehova huimarika; sababu ya tatu inakazia faida za kujitahidi kufikia malengo ya kiroho mapema maishani.

5. Taja sababu ya msingi ya kujiwekea malengo ya kiroho.

5 Sababu ya msingi inayotufanya tujiwekee malengo ya kiroho maishani ni kwamba tunataka kumwonyesha Yehova kuwa tunathamini jinsi anavyotupenda na yote aliyotufanyia. Mtunga zaburi alisema hivi: “Ni vema kukushukuru, Ee Yehova . . . Kwa maana umenifanya nishangilie, Ee Yehova, kwa sababu ya matendo yako; kwa sababu ya kazi za mikono yako ninapaza sauti kwa shangwe.” (Zab. 92:1, 4) Kijana, fikiria mambo yote ambayo Yehova amekupa. Uhai wako, imani yako, Biblia, kutaniko, na tumaini zuri la wakati ujao. Kutanguliza mambo ya kiroho maishani ni njia ya kumwonyesha Mungu kwamba tunathamini baraka hizo, na tunapofanya hivyo tunazidi kumkaribia.

6. (a) Uhusiano wetu na Yehova utakuwaje tukijiwekea malengo ya kiroho? (b) Tunaweza kujiwekea malengo gani tukiwa tungali na umri mdogo?

6 Sababu ya pili ni kwamba mara tu unapoanza kujitahidi kufikia malengo ya kiroho, unaanza kujenga hazina ya matendo mema machoni pa Yehova. Hilo linakufanya umkaribie zaidi. Mtume Paulo alitoa ahadi hii: “Kwa maana Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Ebr. 6:10) Vijana, mnaweza kujiwekea malengo ya kiroho hata ikiwa umri wenu ni mdogo. Christine alikuwa na umri wa miaka kumi alipojiwekea lengo la kujisomea kwa ukawaida masimulizi ya maisha ya Mashahidi waaminifu. Akiwa na umri wa miaka 12, Toby alijiwekea lengo la kusoma Biblia nzima kabla ya kubatizwa. Maxim alikuwa na umri wa miaka 11 na mdogo wake wa kike Noemi alikuwa na umri wa miaka 10 walipobatizwa. Wote wawili walianza kujitahidi kufikia lengo la kuingia katika utumishi wa Betheli. Ili wasikengeuke kutoka kwenye lengo lao, walibandika fomu ya Betheli ukutani. Kwa nini wewe pia usifikirie ni malengo gani ambayo ungependa kujiwekea na kisha ujitahidi kuyafikia?—Soma Wafilipi 1:10, 11.

7, 8. (a) Kujiwekea malengo hutusaidiaje kufanya maamuzi mazuri? (b) Kwa nini kijana mmoja aliamua kutojiunga na chuo kikuu?

7 Sababu ya tatu inayotufanya tujiwekee malengo mapema maishani inahusiana na suala la kufanya maamuzi. Vijana wanahitaji kufanya maamuzi kuhusu elimu, kazi, na mambo mengine. Kufanya maamuzi ni kama kuchagua barabara sahihi ya kufuata unapofika kwenye njia panda. Maadamu unajua mahali unapotaka kwenda, haitakuwa vigumu kwako kuchagua barabara sahihi. Vivyo hivyo, ikiwa unajua malengo unayotaka kufikia, itakuwa rahisi zaidi kwako kufanya maamuzi mazuri. Methali 21:5 inasema hivi: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.” Kadiri unavyojitahidi kufanya mipango mapema kwa kujiwekea malengo mazuri maishani, ndivyo utakavyopata mafanikio haraka. Damaris alijionea ukweli wa jambo hilo alipohitaji kufanya uamuzi fulani muhimu akiwa kijana.

8 Damaris alikamilisha masomo yake ya sekondari akiwa na alama za juu. Alikuwa na fursa ya kukubali ufadhili aliopata wa kusomea sheria kwenye chuo kikuu, lakini alichagua kufanya kazi yenye mshahara mdogo katika benki. Kwa nini? Anaeleza hivi: “Tangu mwanzoni nilikuwa nimeamua kuwa painia. Hilo lilimaanisha kutafuta kazi ambayo ningefanya kwa saa chache. Ikiwa ningekuwa na shahada ya sheria ningeweza kupata kazi yenye mshahara mnono, lakini haingekuwa rahisi kwangu kupata kazi ambayo ningeweza kufanya kwa saa chache.” Tayari Damaris amekuwa akitumikia akiwa painia kwa miaka 20. Je, anahisi kwamba alijiwekea lengo linalofaa na kufanya uamuzi mzuri alipokuwa kijana? Anasema hivi: “Mimi hukutana na wanasheria wengi nikiwa kazini. Wanafanya kazi ambayo ningekuwa nikifanya iwapo ningekuwa nimesomea sheria. Hata hivyo, wengi wao hawafurahii kazi wanayofanya. Uamuzi wangu wa kuwa painia ulinisaidia kuepuka mikazo inayotokana na kufuatilia kazi zenye mshahara mnono, na kunipa fursa ya kumtumikia Yehova kwa shangwe kwa miaka mingi.”

9. Kwa nini vijana wetu wanastahili kupongezwa kutoka moyoni?

9 Maelfu ya vijana walio katika makutaniko mbalimbali kotekote duniani, wanastahili kupongezwa kutoka moyoni. Wameyakabidhi maisha yao mikononi mwa Yehova na wanatanguliza malengo ya kiroho. Vijana hao wanafurahia maisha kikamili na wakati huohuo wanaendelea kujifunza jinsi ya kufuata mwongozo wa Yehova katika nyanja zote za maisha yao, kama vile elimu, kazi, na familia. Sulemani aliandika hivi: “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote. . . . Katika njia zako zote mtambue yeye, naye atavinyoosha vijia vyako.” (Met. 3:5, 6) Vijana walio katika kutaniko la Kikristo ni wenye thamani machoni pa Yehova, naye anawapenda sana na huwapa ulinzi wake, mwongozo, na baraka zake.

JITAYARISHE VIZURI KUTOA USHAHIDI

10. (a) Kwa nini ni lazima tuipe kipaumbele kazi ya kuhubiri? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia tupate matokeo mazuri katika huduma yetu?

10 Kijana anayemtanguliza Yehova na kufanya tamaa yake ya kumpendeza kuwa jambo kuu maishani mwake, huipa huduma yake uangalifu wa pekee. Yesu Kristo alisisitiza kwamba “lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10) Kwa kuwa kazi ya kuhubiri inapaswa kukamilishwa haraka, tunapaswa kuipa kipaumbele. Je, unaweza kujiwekea lengo la kushiriki katika huduma mara nyingi zaidi? Je, unaweza kuwa painia? Lakini vipi ikiwa hufurahii kufanya kazi ya kuhubiri? Na ni nini kinachoweza kukusaidia upate matokeo mazuri katika huduma yako? Mambo haya mawili yatakusaidia: Jitayarishe vizuri, na usiache kamwe kuwaambia wengine mambo unayojua. Ukifanya mambo hayo, utastaajabu kuona jinsi shangwe yako katika kazi ya kuhubiri itakavyoongezeka.

Unajitayarishaje kwa ajili ya kutoa ushahidi? (Tazama fungu la 11 na 12)

11, 12. (a) Ni matayarisho gani ambayo vijana wanaweza kufanya ili kutoa ushahidi? (b) Kijana mmoja alitumiaje fursa aliyopata ili kutoa ushahidi shuleni?

11 Unaweza kuanza kwa kutafuta majibu ya maswali ambayo huenda wanafunzi wenzako wakauliza kama vile, “Je, unafikiri Mungu anajali tunapoteseka?” Tovuti yetu ya jw.org/sw ina makala zinazoweza kuwasaidia vijana kupata jibu la swali hilo. Tazama kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MATINEJA > MIONGOZO YA KUJIFUNZA > UKWELI KUMHUSU MUNGU (SEHEMU YA 1). Katika sehemu hiyo utapata mwongozo wa kujifunza wenye kichwa “Je, Mungu Anajali Tunapoteseka?” Mwongozo huo utakusaidia unapotafuta jibu la swali hilo. Kuna Maandiko unayoweza kutumia kuwaeleza wanafunzi wenzako mambo unayoamini kama vile andiko la Yakobo 1:13, Mwanzo 6:5, 6, na 1 Yohana 4:8. Unaweza kutumia miongozo hiyo kushughulikia swali moja baada ya lingine.—Soma 1 Petro 3:15.

12 Tumia fursa unazopata kuwatia moyo wanafunzi wenzako watembelee Tovuti yetu ya jw.org. Hivyo ndivyo kijana anayeitwa Luca alivyofanya. Walipokuwa wakizungumzia dini mbalimbali darasani, Luca aliona kwamba kitabu walichokuwa wakitumia kilikuwa na habari fulani zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Ingawa alikuwa na wasiwasi, alimwomba mwalimu ruhusa ili arekebishe maoni hayo, na mwalimu alikubali. Luca alieleza kuhusu imani yake na vilevile akaonyesha darasa lote Tovuti yetu. Mwalimu aliwaambia wanafunzi wote darasani wakatazame nyumbani kibonzo kwenye ubao chenye kichwa, Mshinde Mnyanyasaji Bila Kutumia Ngumi. Luca alifurahi sana kwamba alitumia vizuri fursa hiyo kutoa ushahidi.

13. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa tunapokabili hali ngumu?

13 Usife moyo hata ikiwa nyakati nyingine unakabili misukosuko katika safari yako. (2 Tim. 4:2) Hali ngumu zinapotokea, shikamana na malengo uliyojiwekea. Katharina alikuwa na umri wa miaka 17 alipojiwekea lengo la kuwahubiria watu wote aliofanya kazi nao. Mfanyakazi mmoja alimtukana mara kadhaa lakini hilo halikumfanya aache kuwahubiria wafanyakazi wenzake. Mwenendo wake mzuri licha ya hali ngumu aliyokuwa akipitia, ulimvutia mfanyakazi mwenzake aliyeitwa Hans. Hivyo, Hans alianza kusoma machapisho yetu, akajifunza Biblia, na kubatizwa. Katharina alikuwa amehamia eneo lingine na hivyo hakujua hayo yote. Wazia shangwe aliyokuwa nayo miaka 13 baadaye alipokuwa ameketi pamoja na familia yake kwenye Jumba la Ufalme na kumsikia mwenyekiti akimkaribisha Hans jukwaani. Alikuwa ametembelea kutaniko hilo ili kutoa hotuba! Lilikuwa jambo linalofaa sana kwamba Katharina alishikamana na lengo lake la kuwahubiria wafanyakazi wenzake!

USIKENGEUSHWE

14, 15. (a) Vijana wanapaswa kukumbuka nini wanaposhinikizwa na vijana wenzao? (b) Vijana wanaweza kufanya nini wanaposhinikizwa na vijana wenzao?

14 Kufikia hapa makala hii imekutia moyo kufikia uamuzi unaofaa wa kumtanguliza Yehova na kufanya tamaa yako ya kumpendeza kuwa jambo kuu maishani mwako. Hilo linamaanisha kutanguliza malengo ya kiroho maishani mwako. Huenda vijana wengine wa umri wako wanakazia tu kujifurahisha maishani, na inaelekea watakualika ujiunge nao. Wakati utafika utakapohitaji kuonyesha kwamba umeazimia kabisa kushikamana na malengo uliyojiwekea. Unaposhinikizwa na vijana wenzako, kumbuka kwamba hupaswi kuwaruhusu wakukengeushe kutoka kwenye malengo yako. Sasa fikiria tena ule mfano wa msafiri aliye katika kituo cha basi. Bila shaka hungepanda basi lolote lile eti kwa sababu tu abiria kwenye basi hilo wanaonekana kuwa wanafurahia maisha.

15 Kuna mambo mbalimbali yanayoweza kukusaidia kukabiliana na mkazo wa kushinikizwa na vijana wenzako. Jambo moja ni kuepuka hali zinazoweza kukuingiza katika kishawishi. (Met. 22:3) Jikumbushe madhara unayoweza kupata ikiwa utajiunga na wengine kufanya mambo yasiyofaa. (Gal. 6:7) Jambo lingine litakalokusaidia ni kutambua kwamba unahitaji ushauri. Sifa ya unyenyekevu itakusaidia kuwa tayari kukubali mapendekezo kutoka kwa wazazi wako na Wakristo wakomavu katika kutaniko lako.—Soma 1 Petro 5:5, 6.

16. Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha manufaa ya kuwa mnyenyekevu.

16 Sifa ya unyenyekevu ilimsaidia Christoph kukubali ushauri mzuri aliopewa. Muda mfupi baada ya kubatizwa alianza kufanya mazoezi kwa ukawaida katika kituo kimoja cha mazoezi. Vijana wengine katika kituo hicho walimshinikiza ajiunge na klabu yao ya michezo. Christoph alizungumza na mzee mmoja wa kutaniko kuhusu jambo hilo, naye akamwomba afikirie kuhusu hatari fulani zinazoweza kumpata ikiwa atafanya uamuzi wa kujiunga na klabu hiyo, kama vile hatari ya kuathiriwa na roho ya mashindano. Ingawa hivyo, Christoph aliamua kujiunga na klabu hiyo. Hata hivyo, baada ya muda fulani, alitambua kwamba mchezo huo ulikuwa wenye jeuri na hatari. Alizungumza tena na wazee kadhaa, na wote walimpa ushauri wa Kimaandiko. “Yehova alinipa washauri wazuri, nami nikamsikiliza ingawa ilichukua muda fulani kabla ya kutumia ushauri wao.” Je, una unyenyekevu wa kutosha kukubali ushauri unaopewa?

17, 18. (a) Yehova angependa vijana wawe na hali gani? (b) Baadhi ya watu wazima hujikuta katika hali gani inayosikitisha, na unawezaje kuepuka hali hiyo? Toa mfano.

17 “Shangilia, ewe kijana, wakati ungali kijana, na moyo wako ushangilie siku za ujana wako.” (Mhu. 11:9) Naam, ewe kijana, Yehova anataka uwe na shangwe moyoni. Makala hii imeonyesha njia moja ya kuwa na shangwe. Endelea kutanguliza malengo ya kiroho kwa kumhusisha Yehova katika mipango yako yote. Utakapofanya hivyo bila kukawia, upesi utajionea jinsi Yehova anavyokuongoza, anavyokulinda, na kukubariki. Tafakari mashauri yote yenye hekima yaliyo katika Neno la Mungu, nawe uzingatie moyoni ushauri huu: “Mkumbuke Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.”—Mhu. 12:1.

18 Hakuna yeyote anayeendelea kuwa kijana sikuzote. Vijana hukua haraka na kuwa watu wazima. Inasikitisha kwamba watu wengi wazima hujutia malengo mabaya waliyojiwekea walipokuwa vijana au hutamauka kwa kuwa hawakujiwekea malengo yoyote. Lakini vijana wanaotanguliza malengo ya kiroho watakuwa na furaha na kuridhika hata watakapokuwa watu wazima kwa sababu ya maamuzi waliyofanya. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Mirjana, ambaye alikuwa na kipawa kikubwa sana cha michezo. Alialikwa kushiriki katika Michezo ya Olimpiki ya Majira ya Baridi lakini badala yake akaamua kuingia katika utumishi wa wakati wote. Zaidi ya miaka 30 imepita na bado Mirjana yupo katika utumishi wa wakati wote pamoja na mume wake. Anaeleza hivi: “Umashuhuri, utukufu, mamlaka, na utajiri ni malengo yasiyodumu na duni. Kumtumikia Mungu na kujitahidi angalau kwa kadiri fulani kuwasaidia watu kiroho ni malengo yenye kuheshimika na yanayodumu.”

19. Taja manufaa ambayo mtu anaweza kupata ikiwa atatanguliza malengo ya kiroho mapema maishani.

19 Vijana walio kutanikoni wanastahili kupongezwa kutoka moyoni kwa jitihada wanazotia ili kupambana na changamoto mbalimbali na kwa azimio lao la kumtanguliza Yehova maishani mwao. Vijana hufaulu kupambana na changamoto hizo kwa kujitahidi kujiwekea malengo ya kiroho na kwa kuipa kipaumbele kazi ya kuhubiri. Zaidi ya hilo, wao huazimia kwamba hawatakengeushwa na chochote katika ulimwengu huu. Vijana, muwe na uhakika kwamba kazi yenu si ya bure. Ndugu na dada kutanikoni wako tayari kuwategemeza kwa upendo, na mnapojikabidhi mikononi mwa Yehova, mipango yenu maishani itafanikiwa.