Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanaume Mliowekwa Rasmi—Jifunzeni Kutoka kwa Timotheo

Wanaume Mliowekwa Rasmi—Jifunzeni Kutoka kwa Timotheo

MWAKA uliopita, maelfu ya wanaume duniani pote waliwekwa rasmi kuwa wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Ikiwa wewe ni mmoja wa ndugu hao wapendwa, bila shaka unafurahia pendeleo lako jipya la utumishi.

Hata hivyo, huenda una wasiwasi kidogo, na hilo linaeleweka. Jason, mzee wa kutaniko aliye kijana, anaeleza hivi: “Nilipowekwa rasmi, nilihisi kulemewa na majukumu yangu mapya.” Musa na Yeremia walihisi hawastahili walipopata migawo yao mipya kutoka kwa Yehova. (Kut. 4:10; Yer. 1:6) Ikiwa unahisi kama wao, unaweza kufanya nini ili kushinda hisia hizo na kuendelea kufanya maendeleo? Fikiria mfano wa mwanafunzi Mkristo Timotheo.—Mdo. 16:1-3.

IGA MFANO WA TIMOTHEO

Huenda Timotheo alikuwa mwishoni mwa miaka yake ya kubalehe au alikuwa na umri wa miaka 20 hivi Paulo alipomwalika ajiunge naye katika safari zake za umishonari. Kwa kuwa alikuwa kijana, huenda Timotheo alikosa ujasiri kwa kiasi fulani na huenda alisita kutimiza daraka lake jipya. (1 Tim. 4:11, 12; 2 Tim. 1:1, 2, 7) Hata hivyo, miaka kumi baadaye, Paulo aliliambia hivi kutaniko la Filipi: “Ninatumaini katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo kwenu upesi . . . Kwa maana sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama wake.”—Flp. 2:19, 20.

Ni nini kilichomfanya Timotheo awe mzee aliyeweka mfano unaostahili kuigwa? Fikiria mambo sita tunayoweza kujifunza kutoka kwake.

1. Aliwajali watu kikweli. Paulo aliwaambia hivi akina ndugu huko Filipi: “[Timotheo atayajali] kwa unyoofu mahangaiko yenu.” (Flp. 2:20) Naam, Timotheo aliwajali watu. Alihangaikia kikweli hali yao ya kiroho, naye alijitoa mwenyewe kwa ajili yao.

Epuka kuwa kama dereva wa basi ambaye anahangaikia sana kufika kwa wakati hivi kwamba hasimami kubeba abiria. William, mzee mwenye kuheshimika, ambaye ametumikia akiwa mzee kwa zaidi ya miaka 20, anawashauri hivi wazee wapya: “Wapende akina ndugu. Kazia fikira mahitaji yao kuliko kushughulikia tu majukumu uliyo nayo kutanikoni.”

2. Alitanguliza mambo ya kiroho. Paulo alipolinganisha kielelezo cha Timotheo na ndugu wengine, alisema hivi: “Wengine wote wanatafuta faida zao wenyewe, si za Yesu Kristo.” (Flp. 2:21) Paulo alikuwa Roma alipoandika barua yake. Alitambua kwamba akina ndugu huko Roma walijishughulisha sana na mambo yao ya kibinafsi. Kwa kadiri fulani, hawakujitahidi kufanya yote waliyoweza katika mambo ya kiroho. Lakini sivyo ilivyokuwa kwa Timotheo! Fursa ilipojitokeza ya kueneza habari njema, alikuwa na mtazamo kama wa Isaya, ambaye alisema: “Mimi hapa! Nitume mimi!”—Isa. 6:8.

Unawezaje kutimiza kwa usawaziko majukumu yako ya kibinafsi na ya kiroho? Kwanza, tambua mambo unayopaswa kutanguliza. Paulo alihimiza hivi: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” (Flp. 1:10) Tanguliza mambo ambayo ni ya muhimu machoni pa Mungu. Pili, rahisisha maisha yako. Epuka mambo yasiyo ya muhimu na yatakayokupotezea wakati na nguvu. Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Zikimbie tamaa za ujana, lakini fuatilia uadilifu, imani, upendo, amani.”—2 Tim. 2:22.

3. Alimtumikia Yehova kwa bidii. Paulo aliwakumbusha hivi Wafilipi: “Ninyi mnajua jinsi [Timotheo] alivyojithibitisha mwenyewe, kwamba kama mtoto na baba yake alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Flp. 2:22) Timotheo hakuwa mvivu. Alifanya kazi kwa bidii pamoja na Paulo, na jambo hilo liliimarisha sana uhusiano wao.

Leo, kuna kazi nyingi sana katika tengenezo la Mungu. Kazi hizo huturidhisha sana na zinaweza kufanya tuwe na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na ndugu na dada zetu. Hivyo, azimia sikuzote kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Kor. 15:58.

4. Alitumia mambo aliyojifunza. Paulo alimwandikia hivi Timotheo: “Wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, kusudi langu, imani yangu, subira yangu, upendo wangu, uvumilivu wangu.” (2 Tim. 3:10) Kwa kuwa Timotheo alitumia mambo aliyojifunza, alistahili mapendeleo makubwa hata zaidi.—1 Kor. 4:17.

Je, kuna ndugu ambaye ungependa kuiga mfano wake mzuri katika mambo ya kiroho? Ikiwa jibu ni la, kwa nini usizungumze na ndugu mmoja ambaye anaweza kukusaidia kiroho? Tom, ndugu ambaye ametumikia akiwa mzee kwa miaka mingi, anasema hivi: “Mzee mmoja mwenye uzoefu alipendezwa nami kibinafsi naye akaamua kuchukua jukumu la kunizoeza. Mara kwa mara nilimwomba ushauri nami nikautumia. Jambo hilo lilinisaidia haraka kupata ujasiri.”

5. Aliendelea kujizoeza. Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Endelea kujizoeza ukiwa na lengo la ujitoaji-kimungu.” (1 Tim. 4:7) Huenda mwanariadha akawa na kocha wake lakini anahitaji pia kujizoeza mwenyewe. Paulo alimwambia hivi Timotheo: “Endelea kujitahidi kusoma mbele ya watu, kuhimiza, na kufundisha. . . . Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yaonekane wazi kwa watu wote.”—1 Tim. 4:13-15.

Wewe pia unahitaji kuendelea kufanyia kazi ustadi wako. Usiruhusu hali yako ya kiroho ibaki palepale wala usiruhusu uelewaji wako kuhusu utaratibu wa kitengenezo upitwe na wakati. Pia, epuka kujiamini kupita kiasi—labda kwa kufikiri kwamba kwa kuwa una uzoefu mwingi unaweza kushughulikia hali yoyote ile bila kufanya utafiti kwa makini. Hivyo basi mwige Timotheo, kwa “[kujiangalia] daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.”—1 Tim. 4:16.

6. Alitegemea roho ya Yehova. Alipokuwa akizungumza kuhusu huduma ya Timotheo, Paulo alimkumbusha hivi: “Linda amana hii nzuri kupitia roho takatifu, inayokaa ndani yetu.” (2 Tim. 1:14) Ili afaulu kuilinda huduma yake, Timotheo alihitaji kutegemea roho ya Mungu.

Donald, ambaye amekuwa mzee wa kutaniko kwa makumi ya miaka, anaeleza hivi: “Wanaume waliowekwa rasmi wanapaswa kuthamini sana uhusiano wao na Mungu. Wale wanaofanya hivyo wataendelea kuimarika ‘kutoka nguvu hadi nguvu zaidi.’ Ikiwa watamwomba Mungu awape roho yake na kusitawisha sifa za tunda la roho hiyo, watakuwa baraka kubwa kwa ndugu zao.”—Zab. 84:7; 1 Pet. 4:11.

THAMINI PENDELEO LAKO

Inatia moyo sana kuwaona ndugu wengi wapya waliowekwa rasmi, kutia ndani wewe, wakifanya maendeleo ya kiroho. Jason, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, anasema hivi: “Katika kipindi chote ambacho nimetumikia nikiwa mzee, nimejifunza mambo mengi na ujasiri wangu umeongezeka. Sasa, ninafurahia sana mgawo wangu na ninauona kuwa pendeleo la pekee!”

Je, utaendelea kufanya maendeleo ya kiroho? Jiwekee lengo la kujifunza kutokana na kielelezo cha Timotheo. Hivyo, wewe pia utakuwa baraka kwa watu wa Mungu.