Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 18

“Kimbia Mbio Mpaka Mwisho”

“Kimbia Mbio Mpaka Mwisho”

“Nimekimbia mbio mpaka mwisho.”—2 TIM. 4:7.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

MUHTASARI *

1. Ni lazima sisi sote tufanye nini?

JE, UNGEKUBALI kushiriki katika mbio ambazo unajua kwamba ni ngumu, hasa ikiwa wewe ni mgonjwa au umechoka? Bila shaka hapana. Ingawa hivyo, mtume Paulo alisema kwamba Wakristo wote wa kweli wako katika shindano la mbio. (Ebr. 12:1) Na sisi sote, vijana kwa wazee, wenye nguvu au waliochoka, lazima tuvumilie mpaka mwisho ikiwa tunataka kupokea tuzo ambayo Yehova ameweka mbele yetu.—Mt. 24:13.

2. Kama inavyotajwa kwenye 2 Timotheo 4:7, 8, kwa nini Paulo alikuwa na uhuru wa kusema?

2 Paulo alikuwa na uhuru wa kusema kwa sababu alikuwa amefanikiwa ‘kukimbia mbio mpaka mwisho.’ (Soma 2 Timotheo 4:7, 8.) Lakini Paulo alikuwa akizungumzia mbio gani kihususa?

NI MBIO GANI HIZO?

3. Paulo alikuwa akizungumzia mbio gani?

3 Nyakati nyingine, Paulo alitumia mambo yaliyofanyika kwenye michezo huko Ugiriki ya kale kufundisha masomo muhimu. (1 Kor. 9:25-27; 2 Tim. 2:5) Katika pindi kadhaa, alilinganisha maisha ya Mkristo na shindano la mbio za miguu. (1 Kor. 9:24; Gal. 2:2; Flp. 2:16) Mtu huingia katika “mbio” hizo anapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. (1 Pet. 3:21) Anavuka mstari wa mwisho Yehova anapompa tuzo ya uzima wa milele.—Mt. 25:31-34, 46; 2 Tim. 4:8.

4. Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Kuna ulinganisho gani kati ya kukimbia mbio za masafa marefu na maisha ya Mkristo? Kuna mambo kadhaa yanayofanana. Acheni tuzungumzie mambo matatu. Kwanza, tunahitaji kukimbia kwenye njia sahihi; pili, ni lazima tukazie fikira mstari wa mwisho; na tatu, tunapaswa kushinda changamoto tunazokabili katika shindano letu la mbio.

KIMBIA KWENYE NJIA SAHIHI

Ni lazima sisi sote tufuate njia ya maisha ya Kikristo (Tazama fungu la 5 hadi 7) *

5. Ni lazima tufuate njia gani, na kwa nini?

5 Ili wakimbiaji wastahili kupata tuzo katika mbio halisi, ni lazima wakimbie wakifuata njia ambayo imewekwa na waandaaji wa shindano hilo. Vivyo hivyo, ikiwa tunataka kupata tuzo ya uzima wa milele ni lazima tufuate mwendo au njia ya maisha ya Kikristo, yaani, njia ya uzima. (Mdo. 20:24; 1 Pet. 2:21) Hata hivyo, Shetani na wale wanaofuata mfano wake wanataka tuchague jambo tofauti; wanataka ‘tuendelee kukimbia pamoja nao.’ (1 Pet. 4:4) Wanadhihaki njia ya maisha tuliyochagua kufuata na wanadai kwamba njia wanayoifuata ndiyo bora zaidi, yaani, inawafanya wawe huru. Lakini madai yao ni ya uwongo.—2 Pet. 2:19.

6. Kisa cha Brian kinakufundisha nini?

6 Watu wanaokimbia pamoja na watu walioathiriwa na ulimwengu wa Shetani, hutambua upesi kwamba njia waliyochagua haiwapi uhuru na badala yake inawafanya wawe watumwa. (Rom. 6:16) Fikiria kisa cha Brian. Wazazi wake walimtia moyo afuate njia ya maisha ya Kikristo. Lakini alipokuwa katika umri wa utineja, alitilia shaka ikiwa njia hiyo ingemletea furaha. Brian aliamua kukimbia pamoja na wale walioishi kulingana na viwango vya Shetani. Anasema hivi: “Pole kwa pole nikatambua kwamba uhuru niliotamani ungeniongoza katika utumwa wa uraibu. Muda si muda, nikaanza kutumia dawa za kulevya, kunywa pombe, na kuishi maisha mapotovu. Kwa miaka kadhaa, nilitumia dawa kali za kulevya na kuwa mraibu wa dawa hizo. . . . Nilianza kuuza dawa za kulevya ili kutegemeza maisha yangu.” Mwishowe, Brian aliamua kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Alibadili njia aliyokuwa akifuata na kubatizwa mwaka wa 2001. Amepata furaha ya kweli kwa sababu sasa anafuata njia ya maisha ya Kikristo. *

7. Kulingana na Mathayo 7:13, 14, kuna barabara ngapi zilizo mbele yetu?

7 Ni jambo la muhimu sana kwamba tuchague barabara iliyo sahihi! Shetani anataka sisi sote tuache kukimbia kwenye barabara yenye nafasi ndogo “inayoongoza kwenye uzima” na tuanze kuifuata barabara yenye nafasi kubwa ambayo watu wengi wanaifuata. Barabara hiyo inapendwa na watu wengi na ni rahisi kutembea humo. Lakini ‘inaongoza kwenye uharibifu.’ (Soma Mathayo 7:13, 14.) Ili tuendelee kubaki kwenye barabara iliyo sahihi bila kukengeuka, ni lazima tumtumaini Yehova na kumsikiliza.

ENDELEA KUKAZA FIKIRA NA UWE MWANGALIFU USIJIKWAE AU KUWAKWAZA WENGINE

Tunahitaji kuendelea kukaza fikira na kuepuka kuwakwaza wengine (Tazama fungu la 8 hadi 12) *

8. Mkimbiaji hufanya nini anapojikwaa?

8 Wakimbiaji katika shindano la mbio za masafa marefu hukaza macho yao kwenye barabara ili wasijikwae. Hata hivyo, bila kutarajia huenda mkimbiaji akajikwaa au kuangushwa na mkimbiaji mwingine au anaweza kujikwaa anapopita kwenye barabara yenye mashimo. Mkimbiaji anapoanguka, yeye huinuka na kuendelea kukimbia. Badala ya kukazia fikira kitu kilichosababisha ajikwae, jambo kuu ambalo mkimbiaji hukazia ni mstari wa mwisho na tuzo anayotazamia kupata.

9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunajikwaa?

9 Huenda tukajikwaa mara nyingi katika shindano letu la mbio kwa sababu ya mambo tunayosema au kutenda. Au huenda wakimbiaji wenzetu wakafanya makosa yanayotuumiza. Tunatarajia hali kama hizo. Sisi sote si wakamilifu, na sote tunakimbia katika barabara ileile yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima wa milele. Hivyo, huenda nyakati nyingine “tukagongana” na mkimbiaji mwenzetu. Paulo alikiri kwamba nyakati fulani huenda tukamfanya ndugu yetu awe na “sababu ya kulalamika” juu yetu. (Kol. 3:13) Lakini badala ya kukazia fikira mambo yaliyosababisha tujikwae, acheni tukazie fikira tuzo iliyo mbele yetu. Ikiwa tutajikwaa, acheni tuamue kuinuka tena na kuendelea kukimbia. Ikiwa tutakataa kuinuka kwa sababu ya hisia za uchungu na kinyongo, hatutavuka mstari wa mwisho na kupokea tuzo. Isitoshe, huenda tukawa kikwazo kwa wengine wanaojitahidi kukimbia katika barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima.

10. Tunaweza kuepukaje kuwa “kikwazo” kwa wengine?

10 Njia nyingine ya kuepuka kuwa “kikwazo” kwa wakimbiaji wenzetu ni kwa kuwa tayari kukubaliana na mapendezi ya wengine inapowezekana, badala ya kusisitiza mapendezi au haki zetu. (Rom. 14:13, 19-21; 1 Kor. 8:9, 13) Katika njia hiyo ya pekee, tunatofautiana na wakimbiaji katika mbio halisi. Wao hushindana na wakimbiaji wenzao, na kila mkimbiaji anang’ang’ania kushinda tuzo yake mwenyewe. Wakimbiaji hao wanafikiria tu kuhusu masilahi yao wenyewe. Hivyo huenda wakawasukuma wakimbiaji wengine ili wawe mbele ya kila mtu. Tofauti nao, sisi hatushindani na wakimbiaji wenzetu. (Gal. 5:26; 6:4) Lengo letu ni kuwasaidia wengi kadiri iwezekanavyo wavuke mstari wa mwisho pamoja nasi na kupata tuzo ya uzima. Hivyo, tunajitahidi kufuata shauri la Paulo lililoongozwa na roho takatifu kwamba ‘tuangalie, si faida zetu wenyewe, bali pia faida za wengine.’—Flp. 2:4.

11. Wakimbiaji hukazia nini, na kwa nini?

11 Mbali na kukaza macho yao kwenye barabara, wakimbiaji katika mbio halisi hukazia pia mstari wa mwisho. Hata kama hawauoni mstari huo, wanaweza kujiwazia wakiuvuka na kupata tuzo. Wanapata nguvu ya kuendelea kukimbia kwa kuendelea kufikiria kuhusu tuzo iliyo mbele yao.

12. Yehova ameahidi kutupatia nini?

12 Katika shindano la mbio tunalokimbia, Yehova amewahakikishia watu wake kwa fadhili kwamba atawapa thawabu ya uzima wa milele iwapo watakamilisha mbio hizo—iwe ni mbinguni au katika dunia paradiso. Maandiko yanatupatia picha ya jinsi thawabu hiyo itakavyokuwa ili tuweze kuwazia maisha yatakavyokuwa mazuri ajabu. Kadiri tunavyoendelea kuliona tumaini hilo likiwa halisi katika akili na mioyo yetu, ndivyo tutakavyoazimia kuendelea kuvumilia.

ENDELEA KUKIMBIA LICHA YA CHANGAMOTO

Tungependa kuendelea kukimbia mbio za uzima licha ya matatizo tunayokabili (Tazama fungu la 13 hadi 20) *

13. Tunapata msaada gani ambao wakimbiaji halisi hawapati?

13 Wakimbiaji katika mashindano huko Ugiriki walihitaji kushinda changamoto, kama vile kuhisi uchovu na maumivu. Lakini walihitaji hasa kutegemea mazoezi na nguvu zao wenyewe. Sisi ni kama wakimbiaji hao katika maana ya kwamba tunapata mazoezi ya jinsi ya kukimbia katika shindano letu. Lakini tuna msaada ambao wakimbiaji halisi hawana. Tunaweza kupata nguvu zisizo na kikomo kutoka kwa Yehova. Yehova anatuahidi kwamba ikiwa tutamtegemea, atatuzoeza na kututia nguvu!—1 Pet. 5:10.

14. Andiko la 2 Wakorintho 12:9, 10 linatusaidiaje kukabiliana na changamoto?

14 Paulo alilazimika kukabiliana na changamoto nyingi. Mbali na kutukanwa na kuteswa, nyakati nyingine Paulo alijihisi akiwa dhaifu na alihitaji kukabiliana na hali ambayo aliitaja kuwa “mwiba katika mwili.” (2 Kor. 12:7) Lakini badala ya kuona changamoto hizo kuwa sababu ya kukata tamaa, aliziona kuwa fursa ya kumtegemea Yehova. (Soma 2 Wakorintho 12:9, 10.) Kwa kuwa Paulo alisitawisha mtazamo huo, Yehova alimsaidia kukabiliana na matatizo yake yote.

15. Tutajionea nini ikiwa tutamwiga Paulo?

15 Huenda sisi pia tukatukanwa au kuteswa kwa sababu ya imani yetu. Pia, huenda tukalazimika kukabiliana na matatizo ya afya au uchovu. Lakini tukimwiga Paulo, changamoto hizo zote zinaweza kuwa fursa ya kujionea utegemezo wa Yehova wenye upendo.

16. Unaweza kufanya nini hata ikiwa una matatizo ya afya?

16 Je, wewe ni mgonjwa kitandani au unatumia kiti cha magurudumu? Je, miguu yako ni dhaifu au uwezo wako wa kuona umepungua? Ikiwa ndivyo, je, unaweza kukimbia pamoja na wale ambao ni vijana na wenye afya? Ndiyo, unaweza! Ndugu na dada wengi wenye umri mkubwa na wenye matatizo ya afya wanakimbia katika barabara ya uzima. Hawawezi kufanya hivyo kwa nguvu zao wenyewe. Badala yake, wanategemea nguvu kutoka kwa Yehova wanaposikiliza mikutano ya Kikristo kupitia simu au kupitia Intaneti. Pia, wanashiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi kwa kuwahubiria madaktari, wauguzi, na watu wa ukoo.

17. Yehova anahisije kuhusu wale walio na matatizo ya afya?

17 Usiruhusu kamwe matatizo yako ya afya yakufanye uvunjike moyo na kuamini kwamba wewe ni dhaifu na huwezi kukimbia kwenye barabara ya uzima. Yehova anakupenda kwa sababu ya imani uliyo nayo kwake na uvumilivu wako wa miaka mingi. Unahitaji msaada wake sasa kuliko wakati mwingine wowote, naye hatakuacha kamwe. (Zab. 9:10) Badala yake, atazidi kukukaribia hata zaidi. Dada mmoja mwenye matatizo ya afya alisema hivi: “Hali yangu ya afya inapozidi kuzorota, nimegundua kwamba fursa zangu za kushiriki kweli pamoja na wengine zinazidi kupungua. Lakini ninajua kwamba hata nikitimiza mambo madogo ninaufanya moyo wa Yehova ushangilie, na jambo hilo hunifanya niwe na furaha.” Unapohisi umevunjika moyo, kumbuka kwamba hauko peke yako. Tafakari kuhusu mfano wa mtume Paulo, na ukumbuke maneno haya yenye kutia moyo aliyosema: “Ninapendezwa na udhaifu, . . . kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.”—2 Kor. 12:10.

18. Baadhi ya ndugu na dada wanakabili changamoto gani?

18 Baadhi ya ndugu na dada wanaokimbia katika barabara ya uzima wanakabili changamoto nyingine. Wanakabiliana na hali za kibinafsi ambazo wengine hawawezi kuona au kuzielewa. Kwa mfano, wanakabiliana na ugonjwa wa kushuka moyo au kulemewa na wasiwasi mwingi. Kwa nini changamoto ambayo watumishi hao wapendwa wa Yehova wanakabili ni ngumu hata zaidi? Ni kwa sababu ikiwa mtu amevunjika mkono au anatumia kiti cha magurudumu, kila mtu anaweza kuona tatizo la mtu huyo na kuchochewa kumsaidia. Hata hivyo, wale wanaokabiliana na matatizo ya kihisia au ugonjwa wa akili huenda wasionyeshe dalili zozote zinazoonyesha kwamba wana tatizo fulani. Wanakabili maumivu halisi kama tu ya mtu aliyevunjika mguu au mkono, lakini huenda wasionyeshwe huruma kama wengine.

19. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Mefiboshethi?

19 Ikiwa una matatizo ya afya na unahisi kwamba wengine hawakuelewi, unaweza kutiwa moyo na mfano wa Mefiboshethi. (2 Sam. 4:4) Alikuwa na ulemavu, na Mfalme Daudi alimhukumu vibaya. Mefiboshethi hakuwa amejisababishia matatizo hayo. Hata hivyo, hakuruhusu hisia zozote zisizofaa zimlemee; alithamini mambo mazuri aliyopata maishani mwake. Alionyesha shukrani kwa fadhili ambazo Daudi alimwonyesha wakati uliopita. (2 Sam. 9:6-10) Hivyo, Daudi alipomhukumu vibaya, Mefiboshethi aliona mambo kwa njia pana zaidi. Hakuruhusu kosa la Daudi limfanye awe na uchungu moyoni. Na hakumlaumu Yehova kwa jambo ambalo Daudi alifanya. Mefiboshethi alikazia fikira mambo ambayo angeweza kufanya ili kumuunga mkono mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova. (2 Sam. 16:1-4; 19:24-30) Yehova aliruhusu mfano bora wa Mefiboshethi uandikwe katika Neno Lake ili utunufaishe.—Rom. 15:4.

20. Ugonjwa wa kuwa na wasiwasi mwingi huwaathirije baadhi ya watu, lakini wanaweza kuwa na uhakika gani?

20 Kwa sababu ya ugonjwa wa kuwa na wasiwasi mwingi sana, baadhi ya ndugu na dada huwa na hofu na mkazo mkubwa sana wanapochangamana na wengine katika maisha ya kila siku. Huenda wakaona kuwa jambo gumu kushirikiana na wengine katika sehemu zenye watu wengi, lakini wanaendelea kuhudhuria mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Ni changamoto kwao kuzungumza na watu wasiowajua, lakini bado wanazungumza na watu katika huduma ya shambani. Ikiwa unakabili hali kama hiyo, hauko peke yako. Watu wengi wanakabili hali kama yako. Kumbuka kwamba Yehova anapendezwa na jitihada zako za kumtumikia kwa nafsi yote. Kwa kuwa bado hujakata tamaa, hilo linathibitisha kwamba Yehova anakubariki na anakupatia nguvu unazohitaji. * (Flp. 4:6, 7; 1 Pet. 5:7) Ikiwa unamtumikia Yehova licha ya kuvumilia matatizo ya kimwili au ya kihisia, uwe na uhakika kwamba unampendeza Yehova.

21. Tutafanikiwa kufanya nini kwa msaada wa Yehova?

21 Tunashukuru kwamba kuna tofauti kati ya mbio halisi na mbio ambazo Paulo alizungumzia. Ni mtu mmoja tu aliyeshinda tuzo katika mbio halisi za nyakati za Biblia. Kinyume cha hilo, kila mtu anayevumilia kwa uaminifu katika mwendo au njia ya maisha ya Kikristo hupata tuzo ya uzima wa milele. (Yoh. 3:16) Katika mbio halisi, wakimbiaji wote walihitaji kuwa na afya nzuri ya kimwili, la sivyo, wasingeweza kushinda. Kwa upande mwingine, wengi wetu tuna matatizo ya afya, lakini bado tunaendelea kuvumilia. (2 Kor. 4:16) Kwa msaada wa Yehova, sisi sote tutaendelea kukimbia mbio mpaka mwisho!

WIMBO 144 Kaza Macho Kwenye Zawadi!

^ fu. 5 Leo, watumishi wengi wa Yehova huteseka kwa sababu ya umri kusonga, na wengine wengi wanakabiliana na magonjwa yenye kudhoofisha. Na nyakati nyingine sisi sote huchoka. Hivyo, huenda suala la kushiriki katika mbio likaonekana kuwa jambo gumu. Makala hii itazungumzia jinsi ambavyo sisi sote tunaweza kukimbia kwa uvumilivu na kushinda mbio za uzima ambazo mtume Paulo alizungumzia.

^ fu. 6 Tazama makala “Biblia Inabadili Maisha” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2013.

^ fu. 20 Kwa mapendekezo zaidi kuhusu jinsi ya kushughulika na ugonjwa wa kuwa na wasiwasi mwingi na pia masimulizi ya wale ambao wamefanikiwa kukabiliana na hali hiyo, tazama programu ya Mei 2019 kwenye jw.org®. Tafuta kwenye MAKTABA > JW BROADCASTING®.

^ fu. 63 MAELEZO YA PICHA: Kuwa na mengi ya kufanya katika huduma kunamsaidia ndugu huyu mwenye umri mkubwa aendelee kubaki katika njia sahihi ya maisha ya Kikristo.

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Huenda tukawakwaza wengine ikiwa tutasisitiza wanywe pombe nyingi zaidi au ikiwa tutashindwa kujidhibiti inapohusu kiasi cha pombe tunachokunywa.

^ fu. 67 MAELEZO YA PICHA: Hata akiwa kitandani hospitalini, ndugu huyu anaendelea kukimbia mbio za Kikristo kwa kuwahubiria wale wanaomtunza.