Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 16

Sikiliza, Jifunze, na Uonyeshe Huruma

Sikiliza, Jifunze, na Uonyeshe Huruma

“Acheni kuhukumu kwa kutazama sura ya nje tu, bali hukumuni kwa uadilifu.”—YOH. 7:24.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

MUHTASARI *

1. Biblia inafunua kweli gani yenye kufariji kumhusu Yehova?

JE, UNGEPENDA watu wakuhukumu kwa msingi wa rangi yako, jinsi uso wako ulivyo, au ukubwa wa mwili wako? Bila shaka, la. Hivyo, inafariji sana kwamba Yehova hatuhukumu kwa kutegemea mambo yanayoonekana kwa macho ya wanadamu! Kwa mfano, Samweli alipowatazama wana wa Yese, hakuona mambo ambayo Yehova aliona. Yehova alikuwa amemwambia Samweli kwamba mmoja wa wana wa Yese angekuwa mfalme wa Israeli. Lakini mwana yupi? Samweli alipomwona Eliabu, mwana wa kwanza wa Yese, alisema, “Hakika mtiwa-mafuta wa Yehova amesimama hapa mbele zake.” Eliabu alionekana kama mfalme. “Lakini Yehova akamwambia Samweli: ‘Usitazame sura yake wala urefu wake, kwa maana nimemkataa.’” Tunajifunza nini? Yehova aliendelea kusema hivi: “Mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.”—1 Sam. 16:1, 6, 7.

2. Kama inavyotajwa kwenye Yohana 7:24, kwa nini hatupaswi kumhukumu mtu kwa kutegemea sura yake ya nje? Toa mfano.

2 Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sisi sote tuna mwelekeo wa kuwahukumu wengine kwa kutegemea sura ya nje. (Soma Yohana 7:24.) Lakini tunaweza kujifunza mambo machache tu kumhusu mtu kwa kumtazama kwa macho. Kwa mfano, hata daktari mwenye uzoefu mkubwa hawezi kujua mambo mengi kumhusu mgonjwa kwa kumtazama tu. Ni lazima asikilize kwa makini ikiwa anataka kujua historia ya kitiba ya mgonjwa, hisia zake, na dalili zozote alizo nazo. Daktari anaweza kuagiza mgonjwa apigwe picha ya X-ray ili aone sehemu ya ndani ya mwili wa mgonjwa. Asipofanya hivyo, daktari anaweza kusema kimakosa kwamba ana ugonjwa fulani. Vivyo hivyo, hatuwezi kuwaelewa kikamili ndugu na dada zetu kwa kutazama tu sura yao ya nje. Ni lazima tujitahidi kuona zaidi ya kinachoonekana kwa macho, yaani, yule mtu wa ndani. Bila shaka, hatuwezi kusoma moyo, hivyo hatuwezi kamwe kuwaelewa vizuri wengine kama Yehova anavyowaelewa. Lakini tunaweza kufanya yote tuwezayo ili kumwiga Yehova. Jinsi gani?

3. Masimulizi ya Biblia katika makala hii yatatusaidiaje?

3 Yehova hushughulikaje na waabudu wake? Yeye huwasikiliza. Anaelewa malezi yao na mambo waliyopitia. Yeye huwaonyesha huruma. Tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na Yona, Eliya, Hagari, na Loti, acheni tuone jinsi tunavyoweza kumwiga Yehova tunaposhughulika na ndugu na dada zetu.

SIKILIZA KWA MAKINI

4. Kwa nini huenda tukawa na maoni yasiyofaa kumhusu Yona?

4 Kwa kuwa hatujui kila jambo kumhusu Yona, huenda tukamhukumu kimakosa kuwa mtu ambaye hakutegemeka, au hata aliyekosa ushikamanifu. Yehova alimpa amri moja kwa moja kwamba atangaze hukumu dhidi ya jiji la Ninawi. Lakini badala ya kutii, Yona alipanda meli iliyokuwa ikisafiri upande tofauti ili “amkimbie Yehova.” (Yon. 1:1-3) Je, ungempa Yona fursa nyingine ya kutimiza mgawo huo? Huenda hungefanya hivyo. Licha ya hilo, Yehova aliona kwamba Yona alistahili kupata fursa nyingine.—Yon. 3:1, 2.

5. Unajifunza nini kumhusu Yona kutokana na maneno yake kwenye Yona 2:1, 2, 9?

5 Yona alifunua jinsi alivyo kihalisi katika sala yake. (Soma Yona 2:1, 2, 9.) Sala hiyo, ambayo bila shaka ni kati ya sala nyingi alizotoa, inatusaidia tusimwone tu kuwa yule mtu ambaye alikimbia mgawo wake. Maneno yake yanaonyesha kwamba alikuwa mtu mnyenyekevu, mwenye shukrani, na aliyeazimia kumtii Yehova. Ndiyo maana haishangazi kwamba Yehova aliona zaidi ya kosa alilofanya, akajibu sala yake, na akaendelea kumtumia akiwa nabii!

Tukiwa na habari kamili, tunaweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi zaidi (Tazama fungu la 6) *

6. Kwa nini inafaa tujitahidi kuwasikiliza wengine kwa makini?

6 Ili kuwasikiliza wengine kwa makini, tunahitaji kuwa wanyenyekevu na wenye subira. Kuna manufaa ya kujitahidi kufanya hivyo kwa sababu ya mambo haya matatu. Kwanza, hatutakuwa wepesi wa kuwahukumu wengine kimakosa. Pili, tutatambua nia na hisia za ndugu yetu, na hilo litatusaidia tumwonyeshe hisia-mwenzi zaidi. Na tatu, huenda tukamsaidia ndugu yetu ajifunze jambo fulani kujihusu. Nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kwa mtu kuelewa hisia zake mpaka anapowaeleza wengine jinsi anavyohisi. (Met. 20:5) Mzee mmoja wa kutaniko huko Asia anakiri hivi: “Ninakumbuka nikifanya kosa la kuzungumza kabla ya kusikiliza. Nilimwambia dada mmoja kwamba alihitaji kuboresha maelezo anayotoa mikutanoni. Baadaye, nilitambua kwamba haikuwa rahisi kwake kusoma vizuri na alifanya jitihada nyingi sana ili kutoa maelezo.” Ni jambo la muhimu kwamba kila mzee wa kutaniko ‘asikie ukweli wa mambo’ kabla ya kutoa shauri!—Met. 18:13.

7. Unajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Eliya?

7 Baadhi ya ndugu na dada zetu huona kuwa vigumu kuzungumzia hisia zao kwa sababu ya mambo waliyopitia maishani, utamaduni, au utu wao. Tunaweza kufanya nini ili iwe rahisi kwao kufunua mambo yaliyo moyoni mwao? Kumbuka jinsi Yehova alivyoshughulika na Eliya alipokuwa akimkimbia Yezebeli. Siku nyingi zilipita kabla ya Eliya kumfunulia Baba yake wa mbinguni hisia zake kikamili. Yehova alimsikiliza kwa makini. Kisha alimtia moyo Eliya na kumpa kazi muhimu ya kufanya. (1 Fal. 19:1-18) Huenda ikachukua muda mrefu kabla ya ndugu na dada zetu kujihisi huru kuzungumza nasi kuhusu hisia zao. Lakini ikiwa tutaonyesha subira kama Yehova, hatimaye watatuamini na kutufunulia jinsi wanavyohisi. Hivyo, watakapokuwa tayari kutufunulia hisia zao, tunapaswa kuwasikiliza kwa makini.

WAFAHAMU VIZURI NDUGU NA DADA ZAKO

8. Kulingana na Mwanzo 16:7-13, Yehova alimsaidiaje Hagari?

8 Hagari, kijakazi wa Sarai, alitenda kipumbavu baada ya kuwa mke wa Abramu. Hagari alipata mimba kisha akaanza kumdharau Sarai, ambaye hakuwa na mtoto. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Sarai alimfukuza Hagari. (Mwa. 16:4-6) Kwa mtazamo wa wanadamu wasio wakamilifu, huenda ikaonekana kwamba Hagari alikuwa mwanamke mwenye kiburi aliyepata adhabu aliyostahili. Lakini Yehova aliona mengi zaidi. Alimtuma malaika amfuate. Malaika huyo alipompata, alimsaidia arekebishe mtazamo wake na akambariki. Hagari alitambua kwamba Yehova alikuwa akimtazama na alijua mambo yote kuhusu hali yake. Alichochewa kumwita Yehova, “Mungu anayeona, . . . yeye ambaye huniona.”—Soma Mwanzo 16:7-13.

9. Mungu alizingatia nini alipokuwa akishughulika na Hagari?

9 Yehova alitambua nini kumhusu Hagari? Alijua vizuri kabisa malezi yake na mambo yote aliyokuwa amepitia maishani mwake. (Met. 15:3) Hagari alikuwa Mmisri aliyeishi katika familia ya Kiebrania. Je, nyakati nyingine alijihisi akiwa mgeni au mtu asiyetakiwa? Je, aliikosa familia yake na nchi yake? Si yeye tu aliyekuwa mke wa Abramu. Kwa muda fulani, baadhi ya wanaume waaminifu walikuwa na zaidi ya mke mmoja. Lakini hilo halikuwa kusudi la awali la Mungu. (Mt. 19:4-6) Hivyo, haishangazi kwamba jambo hilo lilisababisha wivu na chuki katika familia. Ingawa Yehova hakuunga mkono kitendo cha Hagari kumdharau Sarai, tuna hakika kwamba alizingatia malezi ya Hagari na hali aliyopitia maishani aliposhughulika naye.

Wafahamu vizuri zaidi ndugu na dada zako (Tazama fungu la 10 hadi 12) *

10. Tunaweza kufanya nini ili tuwafahamu vizuri zaidi ndugu na dada zetu?

10 Tunaweza kumwiga Yehova kwa kujitahidi kuwaelewa ndugu na dada zetu. Jitahidi kuwafahamu vizuri zaidi ndugu na dada zako. Zungumza nao kabla na baada ya mikutano, shirikiana pamoja nao katika huduma, na ikiwezekana, waalike kwa ajili ya mlo. Unapofanya hivyo, huenda ukatambua kwamba kumbe dada uliyefikiri si mwenye urafiki kihalisi ni mwenye haya, ndugu uliyedhani anapenda vitu vya kimwili ni mkarimu, au familia ambayo ina kawaida ya kuchelewa mikutano inakabili upinzani. (Ayu. 6:29) Bila shaka, hatupaswi “kujiingiza katika mambo ya watu wengine.” (1 Tim. 5:13) Hata hivyo, ni vizuri kujua mambo fulani kuhusu ndugu na dada zetu na mambo waliyopitia maishani yanayowafanya wawe jinsi walivyo.

11. Kwa nini ni muhimu kwa wazee wa kutaniko kuwajua vizuri kondoo?

11 Kihususa, wazee wa kutaniko wanahitaji kujua malezi na hali ambazo ndugu na dada walio chini ya utunzaji wao wamepitia maishani. Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Artur, aliyetumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko. Yeye na mzee mwingine walimtembelea dada ambaye alionekana kuwa mwenye haya. Artur anaeleza hivi: “Tulitambua kwamba alifiwa na mume wake muda mfupi baada kufunga ndoa. Lakini licha ya changamoto nyingi, aliwasaidia binti zake wawili kuwa watumishi waaminifu wa Yehova. Hata hivyo, alikuwa ameanza kupoteza uwezo wake wa kuona, na alikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo. Licha ya hayo, aliendelea kumpenda sana Yehova na imani yake kwake bado ilikuwa imara. Tuligundua kwamba kulikuwa na mengi ambayo tungeweza kujifunza kutokana na mfano wake mzuri.” (Flp. 2:3) Mwangalizi huyo wa mzunguko alikuwa akimwiga Yehova. Yehova anawajua kondoo wake na maumivu wanayokabili. (Kut. 3:7) Wazee wanaowajua vizuri kondoo ndio wanaoweza kuwasaidia vizuri zaidi.

12. Dada anayeitwa Yip Yee alinufaikaje alipojitahidi kumfahamu vizuri zaidi dada fulani katika kutaniko lake?

12 Unapojua malezi ya Mkristo mwenzako ambaye ana tabia fulani zinazokuudhi, itakuwa rahisi zaidi kwako kumwonyesha hisia-mwenzi. Fikiria mfano ufuatao. Dada anayeitwa Yip Yee kutoka barani Asia anaeleza hivi: “Dada fulani katika kutaniko letu alizoea kuzungumza kwa sauti kubwa sana. Nilihisi kwamba hana adabu. Lakini niliposhirikiana naye kwenye huduma, nilitambua kwamba zamani alikuwa akiwasaidia wazazi wake kuuza samaki sokoni. Alihitaji kuzungumza kwa sauti kubwa ili kuwavutia wateja.” Yip Yee anaendelea kusema hivi: “Nilijifunza kwamba ili niwaelewe ndugu na dada zangu, ninahitaji kujua malezi yao.” Jitihada zinahitajika ili kuwafahamu vizuri zaidi ndugu zako. Ingawa hivyo, unapofuata ushauri wa Biblia wa kufungua kabisa moyo wako, unamwiga Yehova ambaye anawapenda “watu wa namna zote.”—1 Tim. 2:3, 4; 2 Kor. 6:11-13.

ONYESHA HURUMA

13. Kama andiko la Mwanzo 19:15, 16, linavyoonyesha, malaika walifanya nini Loti alipozidi kukawia, na kwa nini?

13 Loti hakutii upesi mwongozo wa Yehova katika kipindi kilichokuwa hatari sana maishani mwake. Malaika wawili walimtembelea Loti na kumwambia aondoke Sodoma pamoja na familia yake. Kwa nini? Walimwambia hivi: “Tutaliangamiza jiji hili.” (Mwa. 19:12, 13) Asubuhi iliyofuata, Loti na familia yake bado walikuwa nyumbani. Hivyo, malaika wakamwonya tena Loti. Lakini Loti ‘alizidi kukawia.’ Huenda tukamhukumu Loti kuwa mtu aliyepuuza maagizo ya Yehova, au asiye mtiifu. Hata hivyo, Yehova hakuchoka kumsaidia. “Kwa sababu Yehova alimhurumia,” malaika walimshika mkono yeye pamoja na familia yake na kumtoa nje ya jiji.—Soma Mwanzo 19:15, 16.

14. Huenda ni mambo gani yaliyomfanya Yehova amhurumie Loti?

14 Kuna sababu kadhaa ambazo huenda zilimfanya Yehova amhurumie Loti. Inawezekana Loti alisita kutoka nje ya nyumba yake kwa sababu aliwaogopa watu waliokuwa nje ya jiji. Kulikuwa na hatari nyingine pia. Inaelekea Loti alikuwa amepata habari kuhusu wafalme wawili waliokuwa wameanguka ndani ya mashimo ya lami katika bonde lililokuwa karibu. (Mwa. 14:8-12) Akiwa mume na baba pia, lazima Loti alikuwa na wasiwasi kuhusu familia yake. Isitoshe, alikuwa tajiri, hivyo huenda alikuwa na nyumba nzuri katika jiji la Sodoma. (Mwa. 13:5, 6) Bila shaka, hakuna sababu yoyote kati ya hizo iliyopaswa kumfanya Loti ashindwe kutii upesi maagizo ya Yehova. Hata hivyo, Yehova aliona zaidi ya kosa ambalo Loti alifanya, na alimwona kuwa ‘mtu mwadilifu.’—2 Pet. 2:7, 8.

Ikiwa tutawasikiliza ndugu zetu, tutaweza kuelewa jinsi tunavyoweza kuwaonyesha huruma (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Badala ya kumhukumu mtu kwa sababu ya mambo anayofanya, tunapaswa kufanya nini?

15 Badala ya kumhukumu mtu kwa sababu ya mambo anayofanya, jitahidi kadiri uwezavyo kuelewa hisia zake. Veronica, dada kutoka Ulaya, alijitahidi kufanya hivyo. Anaeleza hivi: “Kuna dada mmoja ambaye sikuzote alikuwa na tabia ya kununa-nuna. Alizoea kujitenga na wengine. Nyakati nyingine niliogopa kumfikia. Lakini nikajiambia, ‘Ikiwa ningekuwa katika hali yake, ningehitaji rafiki.’ Hivyo, niliamua kumuuliza jinsi alivyohisi. Naye akaanza kunifungulia moyo wake! Sasa ninaelewa mengi zaidi kumhusu.”

16. Kwa nini tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie kusitawisha sifa ya hisia-mwenzi?

16 Yehova pekee ndiye anayetuelewa kikamili. (Met. 15:11) Hivyo, mwombe akusaidie uwaone wengine kama anavyowaona na akusaidie kuelewa jinsi unavyoweza kuwaonyesha huruma. Sala ilimsaidia dada anayeitwa Anzhela kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi zaidi. Kulikuwa na dada katika kutaniko lake ambaye haikuwa rahisi kushughulika naye. Anzhela anakiri hivi: “Ingekuwa rahisi kuangukia mtego wa kumchambua dada huyo na kuepuka kushirikiana naye. Lakini nilimwomba Yehova anisaidie kumwonyesha dada huyo hisia-mwenzi.” Je, Yehova alijibu sala ya Anzhela? Anasema hivi: “Tulienda kuhubiri pamoja na baada ya hapo tulizungumza kwa saa nyingi. Nilimsikiliza kwa huruma. Sasa ninampenda zaidi, na nimeazimia kumsaidia.”

17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Hatupaswi kubagua ni ndugu au dada yupi anayestahili tumhurumie kwa wororo na yupi asiyestahili. Kama Yona, Eliya, Hagari, na Loti, ndugu na dada hao wote hukabili matatizo. Katika visa fulani, wao wenyewe ndio waliojisababishia matatizo. Ukweli wa mambo ni kwamba wakati fulani sisi sote tumewahi kujisababishia wenyewe matatizo. Hivyo, ni jambo linalofaa kabisa kwamba Yehova anatusihi tuonyeshane hisia-mwenzi. (1 Pet. 3:8) Tunapomtii Yehova, tunachangia umoja katika familia yetu ya pekee ya ulimwenguni pote yenye watu tofauti-tofauti. Hivyo tunaposhughulika na ndugu na dada zetu, acheni tuazimie kuwasikiliza, kujifunza kuwahusu, na kuwaonyesha huruma.

WIMBO 87 Njooni! Mburudishwe

^ fu. 5 Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tuna mwelekeo wa kuwahukumu watu na kutilia shaka nia yao. Kwa upande mwingine, Yehova “huona ndani ya moyo.” (1 Sam. 16:7) Katika makala hii tutachunguza jinsi Yehova alivyomsaidia kwa upendo Yona, Eliya, Hagari, na Loti. Pia, itatusaidia tuone jinsi tunavyoweza kumwiga Yehova tunaposhughulika na ndugu na dada zetu.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa anaudhika kwa sababu ndugu kijana amechelewa mikutano, lakini baadaye anatambua kwamba alichelewa kwa sababu alipatwa na aksidenti ya gari.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Ingawa mwanzoni mwangalizi wa kikundi cha utumishi alidhani kwamba dada huyu alipenda kujitenga na hakuwa mwenye urafiki, baadaye alitambua kwamba dada huyo alikuwa mwenye haya na hajihisi huru anapokuwa na watu asiowafahamu vizuri.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Dada alipojitahidi kumfahamu vizuri zaidi dada mwingine, alitambua kwamba dada huyo hakuwa na tabia ya kununa-nuna au asiyejali kama alivyokuwa akidhani awali walipokutana kwa mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme.