Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 15

Unayaonaje Mashamba?

Unayaonaje Mashamba?

“Inueni macho yenu mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.”​—YOH. 4:35.

WIMBO 64 Kuyashiriki Mavuno kwa Furaha

MUHTASARI *

1-2. Huenda Yesu alimaanisha nini aliposema maneno yaliyo kwenye Yohana 4:35, 36?

YESU alikuwa akisafiri kwenye eneo lenye mashamba, inaelekea yalikuwa mashamba ya shayiri ambayo bado haijakomaa. (Yoh. 4:3-6) Zao hilo lingekuwa tayari kwa ajili ya kuvunwa baada ya miezi minne hivi. Yesu alisema jambo ambalo halikuwa la kawaida: “Inueni macho yenu mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Soma Yohana 4:35, 36.) Alimaanisha nini?

2 Inaelekea Yesu alikuwa akirejelea kwa njia ya mfano kuhusu kuwavuna watu. Fikiria jambo lililokuwa limetoka kutendeka. Ingawa kwa kawaida Wayahudi hawakushirikiana na Wasamaria, Yesu alikuwa amemhubiria mwanamke Msamaria—na mwanamke huyo akamsikiliza! Isitoshe, Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu mashamba yaliyokuwa “meupe kwa ajili ya kuvunwa,” umati wa Wasamaria waliokuwa wamesikia kumhusu Yesu kutoka kwa mwanamke huyo, walikuwa njiani ili kuja kujifunza mengi zaidi kutoka kwa Yesu. (Yoh. 4:9, 39-42) Kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinasema hivi kuhusu simulizi hilo: “Shauku ya watu hao . . . ilionyesha kwamba walikuwa kama nafaka iliyo tayari kuvunwa.”

Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahisi kwamba mashamba yetu ni “meupe kwa ajili ya kuvunwa”? (Tazama fungu la 3)

3. Kuwaona watu kama Yesu alivyowaona, kutakusaidiaje kuwa mhubiri mzuri zaidi?

3 Vipi kuhusu watu unaowahubiria habari njema? Je, unawaona kama nafaka iliyo tayari kuvunwa? Ikiwa ndivyo, utafanya mambo haya matatu. Kwanza, utahubiri ukiwa na hisi ya uharaka zaidi. Kipindi cha mavuno ni kifupi; hatupaswi kupoteza muda. Pili, utafurahi unapoona watu wakikubali habari njema. Biblia inasema hivi: ‘Watu hushangilia wakati wa mavuno.’ (Isa. 9:3) Na tatu, utakuwa na mtazamo wa kwamba kila mtu anaweza kuwa mwanafunzi wa Kristo, hivyo utazungumza na kila mtu kwa njia inayoonyesha kwamba unazingatia mapendezi yao.

4. Tutajifunza nini kutoka kwa mtume Paulo katika makala hii?

4 Yesu hakufikiri kwamba Wasamaria hawawezi kubadilika, kama baadhi ya wafuasi wake walivyofikiri. Badala yake, aliona kwamba wanaweza kuwa wanafunzi wake. Sisi pia, tunapaswa kuwa na mtazamo wa kwamba watu katika eneo letu wanaweza kuwa wanafunzi wa Kristo. Mtume Paulo alituwekea mfano bora wa kuiga. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwake? Katika makala hii, tutazungumzia (1) jinsi Paulo alivyofahamu mambo ambayo wale aliowahubiria waliamini, (2) jinsi alivyotambua mapendezi yao, na (3)  jinsi alivyoona kwamba wanaweza kuwa wanafunzi wa Yesu.

WANAAMINI NINI?

5. Kwa nini Paulo angeweza kuwaelewa wasikilizaji wake katika sinagogi?

5 Paulo alihubiri mara kwa mara katika masinagogi ya Wayahudi. Kwa mfano, ‘kwa sabato tatu alijadiliana na Wayahudi akitumia Maandiko’ katika sinagogi moja huko Thesalonike. (Mdo. 17:1, 2) Inaelekea Paulo alijihisi huru akiwa katika sinagogi. Alilelewa na wazazi Wayahudi. (Mdo. 26:4, 5) Paulo aliwafahamu vizuri Wayahudi, hivyo angeweza kuwahubiria akiwa na uhakika.—Flp. 3:4, 5.

6. Watu waliokuwa kwenye soko la Athene walitofautianaje na wale ambao Paulo aliwahubiria kwenye sinagogi?

6 Baada ya watu waliomtesa Paulo kumlazimisha aondoke Thesalonike na kisha Beroya, aliwasili Athene. Kwa mara nyingine tena, “akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi na watu wengine waliomwabudu Mungu.” (Mdo. 17:17) Hata hivyo, alipokuwa akihubiri sokoni, Paulo alikutana na wasikilizaji tofauti. Miongoni mwa wasikilizaji wake kulikuwa na wanafalsafa na watu wengine wa mataifa ambao waliuona ujumbe wa Paulo kuwa ‘fundisho jipya.’ Walimwambia hivi: “Unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu.”—Mdo. 17:18-20.

7. Kulingana na Matendo 17:22, 23, Paulo alibadili jinsi gani njia yake ya kuhubiri?

7 Soma Matendo 17:22, 23. Paulo hakuwasilisha ujumbe wake kwa watu wa mataifa waliokuwa Athene kwa njia ileile aliyotumia alipozungumza na Wayahudi katika sinagogi. Inaelekea Paulo alijiuliza, ‘Watu hawa wa Athene wanaamini nini?’ Alichunguza kwa makini mambo yaliyomzunguka na kutambua desturi za kidini za watu. Kisha, Paulo alitafuta mambo ambayo wangekubaliana pamoja, yaliyopatana na ukweli wa Maandiko. Msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Akiwa Mkristo Myahudi, [Paulo] anatambua kwamba Wagiriki wapagani hawamwabudu Mungu wa ‘kweli’ wa Wayahudi na Wakristo, lakini anajaribu kuonyesha kwamba kihalisi Mungu anayemtangaza si mgeni kwa Waathene.” Hivyo, Paulo alikuwa tayari kubadili utangulizi wake. Aliwaambia Waathene kwamba ujumbe wake ulitoka kwa “Mungu Asiyejulikana” ambaye walikuwa wakijitahidi kumwabudu. Ingawa watu hao wa mataifa hawakuyafahamu Maandiko, Paulo hakukata tamaa. Badala yake, aliwaona kama nafaka iliyo tayari kuvunwa, na alibadili njia aliyotumia kuwahubiria habari njema.

Fuata mfano wa mtume Paulo kwa kuwa macho, kubadili utangulizi wako ili ufaane na hali, na kuwa na mtazamo mzuri kwamba watu wanaweza kuwa wanafunzi wa Kristo (Tazama fungu la 8, 12, na 18) *

8. (a) Unaweza kutambuaje imani ya kidini ya watu katika eneo lako? (b) Unaweza kumwambiaje mtu anayesema kwamba ana dini yake?

8 Uwe macho, kama Paulo. Tafuta ishara zinazoonyesha mambo ambayo watu katika eneo lako wanaamini. Mwenye nyumba amepambaje nyumba yake au gari lake? Je, jina lake, mavazi, mapambo, au hata maneno yake yanaonyesha yeye ni wa dini gani? Labda amekueleza moja kwa moja kwamba ana dini yake. Dada mmoja painia wa pekee anayeitwa Flutura husema hivi anapokutana na hali kama hiyo, “Lengo langu la kukutembelea si kukulazimisha uamini mambo ninayoamini, bali ili tuzungumzie jambo hili . . . ”

9. Ni mambo gani ambayo huenda mkakubaliana na mtu wa dini?

9 Unaweza kuzungumzia mambo gani na mtu wa dini? Jaribu kutafuta mambo mnayokubaliana. Huenda akawa anamwabudu Mungu mmoja, huenda anamtambua Yesu kuwa Mwokozi wa wanadamu, au huenda anaamini kwamba tunaishi katika nyakati zenye uovu ambazo zitakoma hivi karibuni. Kwa kutegemea mambo mnayokubaliana, wasilisha ujumbe wa Biblia kwa njia itakayomvutia.

10. Tunapaswa kujitahidi kufanya nini, na kwa nini?

10 Kumbuka kwamba huenda watu wasiamini kila kitu ambacho dini zao hufundisha. Hivyo, hata baada ya kutambua dini ya mtu, jitahidi kujua mambo ambayo yeye binafsi anaamini. David, painia wa pekee nchini Australia, anasema hivi: “Watu wengi leo wanachanganya falsafa na mambo ya kidini wanayoamini.” Donalta, dada kutoka Albania anasema, “Baadhi ya watu tunaokutana nao wanasema kwamba wao ni wafuasi wa dini fulani, lakini baadaye wanakiri kwamba kwa kweli hawaamini katika Mungu.” Ndugu mmoja mmishonari kutoka Argentina amejionea kwamba baadhi ya watu wanaosema kwamba wanaamini Utatu, kihalisi hawaamini kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni Mungu mmoja. Anasema hivi: “Kujua jambo hilo kunafanya iwe rahisi zaidi kupata mambo tunayokubaliana na mtu huyo.” Hivyo, jitahidi kujua mambo ambayo watu wanaamini hasa. Kisha, kama Paulo, unaweza kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.”—1 Kor. 9:19-23.

WANAPENDEZWA NA NINI?

11. Kama andiko la Matendo 14:14-17 linavyoonyesha, Paulo aliwasilishaje ujumbe wake kwa njia yenye kupendeza kwa watu walioishi Listra?

11 Soma Matendo 14:14-17. Paulo alitambua mambo yaliyowapendeza wasikilizaji wake, na kisha alibadili utangulizi wake ili uwafae. Kwa mfano, umati wa watu ambao alizungumza nao huko Listra ulikuwa na ujuzi mdogo kuhusu Maandiko au hawakuyafahamu hata kidogo. Hivyo, Paulo alitumia hoja ambazo wangezielewa. Alizungumza nao kuhusu mavuno ya chakula kingi na uwezo wa kufurahia maisha. Alitumia maneno na mifano ambayo wasikilizaji wake wangeweza kuelewa kwa urahisi.

12. Unaweza kutambuaje mambo yanayompendeza mtu na kubadili utangulizi wako ili ufaane na hali yake?

12 Tumia ufahamu kutambua mambo yanayowapendeza watu katika eneo lenu na ubadili utangulizi wako ili ufaane na hali zao. Unaweza kutambuaje mambo yanayompendeza mtu unapomkaribia yeye au nyumba yake? Kwa mara nyingine tena, uwe macho. Huenda anatunza bustani, anasoma kitabu, anarekebisha gari, au anafanya jambo fulani lingine. Ikiwa inafaa, je, unaweza kutumia jambo analofanya kuanzisha mazungumzo pamoja naye? (Yoh. 4:7) Hata mavazi ya mtu yanaweza kutueleza jambo fulani kumhusu—labda kututambulisha taifa lake, kazi yake, au timu ya michezo anayopenda. Ndugu anayeitwa Gustavo anasema hivi: “Nilianzisha mazungumzo na mwanamume mwenye umri wa miaka 19 aliyekuwa amevaa shati lenye picha ya mwimbaji fulani maarufu. Nilimuuliza kuhusu hilo, naye alinieleza kwa nini alimpenda mwimbaji huyo. Mazungumzo hayo yaliongoza kwenye funzo la Biblia, na sasa yeye ni ndugu yetu.”

13. Unaweza kuanzishaje funzo la Biblia kwa njia itakayowavutia watu unaozungumza nao?

13 Unapoanza kujifunza Biblia pamoja na mtu, ongoza funzo kwa njia yenye kuvutia; mwonyeshe jinsi funzo hilo litakavyomnufaisha. (Yoh. 4:13-15) Kwa mfano, dada anayeitwa Poppy, alikaribishwa kwenye nyumba ya mwanamke fulani aliyependezwa. Alipoona ukutani cheti kinachoonyesha kwamba mwanamke huyo ni profesa aliyesomea elimu, alikazia kwamba sisi pia tunawaelimisha watu kupitia programu ya kujifunza Biblia na mikutano yetu. Mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia, akahudhuria mkutano siku iliyofuata, na muda mfupi baadaye alihudhuria kusanyiko la mzunguko. Mwaka mmoja baadaye alibatizwa. Jiulize: ‘Watu ninaowarudia wanapendezwa na mambo gani? Je, ninaweza kuwaeleza kuhusu programu yetu ya kujifunza Biblia kwa njia itakayowavutia?’

14. Unaweza kuongozaje funzo la Biblia kwa njia itakayofaana na hali za kila mwanafunzi?

14 Baada ya kuanza kujifunza Biblia na mtu, jitayarishe kihususa kwa ajili ya kila kipindi cha funzo, ukizingatia malezi na mambo yanayompendeza mwanafunzi wako. Unapojitayarisha, chagua maandiko utakayosoma, video utakazoonyesha, na mifano utakayotumia ili kufafanua kweli za Biblia. Jiulize, ‘Ni nini hasa kitakachomvutia mwanafunzi wangu na kugusa moyo wake?’ (Met. 16:23) Nchini Albania, mwanamke aliyekuwa akijifunza na painia aliyeitwa Flora alisema hivi kwa uthabiti, “Siwezi kukubali fundisho la ufufuo.” Flora hakumlazimisha akubali fundisho hilo. Anaeleza hivi: “Nilihisi kwamba anahitaji kwanza kumjua Mungu anayeahidi ufufuo.” Kuanzia wakati huo na kuendelea, kila mara alipojifunza naye, Flora alikazia kuhusu upendo, hekima, na nguvu za Yehova. Baadaye, mwanafunzi wake aliamini fundisho la ufufuo kwa hiari. Sasa yeye ni Shahidi wa Yehova mwenye bidii.

WAONE KUWA WANAFUNZI WA KRISTO WA WAKATI UJAO

15. Kulingana na Matendo 17:16-18, ni tabia gani zilizokuwepo katika Ugiriki ya kale zilizomtaabisha Paulo, lakini kwa nini hakukata tamaa ya kuwasaidia Waathene?

15 Soma Matendo 17:16-18. Paulo hakukata tamaa ya kuwasaidia Waathene, hata ingawa jiji lao lilikuwa limejaa ibada ya sanamu, uasherati, na falsafa za kipagani; wala hakuruhusu matusi yao yamvunje moyo. Paulo mwenyewe alikuwa amebadilika na kuwa Mkristo, ingawa mwanzoni alikuwa “mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:13) Kama tu Yesu alivyoona kwamba Paulo anaweza kuwa mwanafunzi wake, ndivyo pia Paulo alivyoona kwamba Waathene wanaweza kuwa wanafunzi wa Kristo. Na alikuwa na msingi mzuri wa kuwa na uhakika huo.—Mdo. 9:13-15; 17:34.

16-17. Ni nini kinachoonyesha kwamba watu kutoka matabaka yote wanaweza kuwa wanafunzi wa Kristo? Toa mfano.

16 Katika karne ya kwanza, watu kutoka matabaka yote walikuja kuwa wanafunzi wa Yesu. Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi katika jiji la Kigiriki la Wakorintho, alisema kwamba wakati fulani baadhi ya ndugu na dada wa kutaniko hilo walikuwa wahalifu au waliishi maisha mapotovu yenye kushtua. Kisha aliongezea hivi: “Baadhi yenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi.” (1 Kor. 6:9-11) Je, ungeona kwamba watu hao wanaweza kubadilika na kuwa wanafunzi wa Kristo?

17 Leo watu wengi wako tayari kufanya mabadiliko yanayohitajika ili wawe wanafunzi wa Yesu. Kwa mfano nchini Australia, dada painia wa pekee anayeitwa Yukina alijifunza kwamba watu wa namna zote wanaweza kukubali ujumbe wa Biblia. Siku moja, alipokuwa kwenye ofisi ya wakala wa kuuza nyumba na viwanja, alimwona mwanamke mmoja kijana aliyekuwa amejichanja chale (tattoo) na kuvalia mavazi makubwa-makubwa. Yukina anasema hivi: “Nilisita kidogo, lakini nikaanza kuzungumza naye. Nikatambua kwamba alipendezwa sana na Biblia hivi kwamba baadhi ya chale zake zilikuwa mistari ya kitabu cha Zaburi!” Mwanamke huyo alianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano. *

18. Kwa nini hatupaswi kuwahukumu watu?

18 Je, Yesu aliona kwamba mashamba yalikuwa tayari kuvunwa kwa sababu alitarajia kwamba watu wengi wangekuwa wafuasi wake? Hapana. Maandiko yalikuwa yametabiri kwamba watu wachache wangemwamini. (Yoh. 12:37, 38) Na Yesu alikuwa na uwezo wa kimuujiza wa kusoma mioyo ya watu. (Mt. 9:4) Hata hivyo, aliwakazia uangalifu watu hao wachache ambao wangemwamini, na aliwahubiria watu wote kwa bidii. Ikiwa Yesu alifanya hivyo, je, sisi ambao hatuwezi kusoma mioyo hatupaswi kuepuka mwelekeo wa kumhukumu yeyote katika eneo letu? Tunapaswa kuwa na mtazamo mzuri kwamba watu wanaweza kuwa wanafunzi wa Kristo. Mmishonari anayeitwa Marc kutoka Burkina Faso, anaeleza hivi: “Kwa kawaida watu ninaodhani kwamba wanaweza kufanya maendeleo huacha kujifunza. Lakini watu ninaodhani kwamba hawatafanya maendeleo ndio wanaofanya vizuri zaidi. Hivyo, nimejifunza kwamba ni bora turuhusu roho ya Yehova ituongoze.”

19. Tunapaswa kuwaonaje watu katika eneo letu?

19 Tukitazama tu kijuu-juu kwa mara ya kwanza, huenda ikaonekana kwamba eneo letu halina watu wengi walio kama nafaka iliyo tayari kuvunwa. Lakini kumbuka mambo ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake. Mashamba ni meupe, yaani, yako tayari kuvunwa. Watu wanaweza kubadilika na kuwa wanafunzi wa Kristo. Yehova anawaona watu hao wanaoweza kuwa wanafunzi wa Kristo kuwa “vitu vyenye thamani.” (Hag. 2:7) Ikiwa tutawaona watu kama Yehova na Yesu wanavyowaona, tutajifunza kuhusu malezi yao na mambo wanayopenda. Hatutawaona kama wageni, bali kama watu wanaoweza kuwa ndugu na dada zetu.

WIMBO 57 Kuwahubiria Watu wa Namna Zote

^ fu. 5 Mtazamo wetu kuhusu eneo letu unaweza kuwa na matokeo gani inapohusu jinsi tunavyohubiri na kufundisha? Makala hii inazungumzia jinsi Yesu na mtume Paulo walivyowaona watu waliowahubiria na jinsi tunavyoweza kuwaiga kwa kuzingatia imani, mapendezi, na uwezekano wa watu tunaowahubiria kuwa watumishi wa Yehova.

^ fu. 17 Mfululizo wa “Biblia Inabadili Maisha” una mifano zaidi ya jinsi watu wanavyoweza kubadilika. Mfululizo huo ulikuwa ukichapishwa kwenye Mnara wa Mlinzi kufikia mwaka wa 2017. Sasa unapatikana kwenye tovuti ya jw.org®. Tazama kwenye KUTUHUSU > MASIMULIZI.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Wenzi fulani wa ndoa wanapohubiri nyumba kwa nyumba, wanaona (1) nyumba iliyotunzwa vizuri na kupambwa kwa maua; (2) nyumba iliyo na familia yenye watoto wadogo; (3) nyumba iliyo shaghalabaghala ndani na nje; na (4) nyumba yenye familia ya kidini. Ni nyumba ipi iliyo na mtu anayeweza kuwa mwanafunzi wa Kristo?