Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Yesu alinukuu maneno ya Daudi yanayopatikana kwenye Zaburi 22:1 kabla tu ya kifo chake?

Miongoni mwa maneno ya mwisho ambayo Yesu alisema kabla ya kifo chake ni yale yanayopatikana kwenye Mathayo 27:46: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” Kwa kusema maneno hayo, Yesu alitimiza maneno ya mtunga-zaburi Daudi yanayopatikana kwenye Zaburi 22:1. (Marko 15:34) Lingekuwa kosa kufikia mkataa kwamba Yesu alinukuu maneno hayo kwa sababu alikuwa amevunjika moyo au kwa sababu wakati huo alikosa imani. Yesu alielewa kikamili kwa nini alihitaji kufa, naye alikuwa tayari kufanya hivyo. (Mt. 16:21; 20:28) Pia, alijua kwamba wakati wa kifo chake, Yehova angehitaji kuondoa ‘ukuta wowote wa ulinzi’ kumzunguka. (Ayu. 1:10) Hivyo, Yehova aliruhusu Yesu athibitishe bila kuacha shaka yoyote kwamba angeendelea kuwa mwaminifu haidhuru angepitia hali ngumu kadiri gani wakati wa kifo chake.—Marko 14:35, 36.

Hivyo, kwa nini Yesu alisema maneno ya zaburi hiyo? Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika kabisa kuhusu jambo hilo, acheni tuchunguze baadhi ya sababu ambazo huenda zilimfanya aseme maneno hayo. *

Kwa kusema maneno hayo, je, Yesu alikuwa akikazia kwamba Yehova hangeingilia kati kifo chake? Yesu alihitaji kulipia fidia bila kusaidiwa na Yehova. Alikuwa mwanadamu halisi na alihitaji kufa ili “aonje kifo kwa ajili ya kila mtu.”—Ebr. 2:9.

Aliponukuu maneno machache kutoka kwenye zaburi hiyo, je, Yesu alikuwa akiwasaidia wengine wakazie uangalifu zaburi hiyo yote? Katika siku hizo ilikuwa kawaida kwa Wayahudi kukariri zaburi nyingi. Waliposikia mstari mmoja wa zaburi, kwa kawaida wangeanza kufikiria kuhusu zaburi nzima. Ikiwa hilo ndilo lililokuwa akilini mwa Yesu, basi angeweza kuwasaidia wafuasi wake wengi waliokuwa Wayahudi wakumbuke unabii mwingi unaopatikana katika zaburi hiyo kuhusu matukio ya kabla na baada ya kifo chake. (Zab. 22:7, 8, 15, 16, 18, 24) Pia, mwishoni mwa zaburi hiyo, ushindi wa ufalme wa Yehova unafafanuliwa kuwa unaenea hadi kwenye miisho ya dunia.—Zab. 22:27-31.

Kwa kunukuu maneno hayo ya Daudi, je, Yesu alikuwa akikazia kwamba hana hatia? Kabla ya Yesu kuuawa, alihitaji kuvumilia kesi isiyo halali dhidi yake, iliyofanya apatikane na hatia ya kukufuru. (Mt. 26:65, 66) Kesi ilifanywa haraka, usiku sana, na haikufuata hata kidogo matakwa ya kisheria. (Mt. 26:59; Marko 14:56-59) Kwa kunukuu maneno hayo kama swali lisilohitaji jibu, huenda Yesu alikuwa akiwasaidia wengine wakazie uangalifu ukweli wa kwamba hakuwa amefanya jambo lolote lililofanya astahili adhabu ya aina hiyo.

Je, Yesu alikuwa pia akiwakumbusha wengine kwamba hata ingawa Daudi, mwandikaji wa zaburi hiyo aliteseka, hilo halikumaanisha kwamba alikuwa amepoteza kibali cha Yehova? Swali ambalo Daudi aliuliza halikumaanisha kwamba alikosa imani. Baada ya kuuliza swali hilo, Daudi aliendelea kuonyesha uhakika wake katika nguvu za Yehova za kuokoa na Yehova aliendelea kumbariki. (Zab. 22:23, 24, 27) Vivyo hivyo, hata ingawa Yesu, “Mwana wa Daudi” alikuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, hilo halikumaanisha kwamba Yesu hakuwa na kibali cha Yehova.—Mt. 21:9.

Je, Yesu alikuwa akionyesha huzuni kubwa sana kwa kuwa Yehova alihitaji kuondoa ulinzi Wake ili aweze kuthibitisha kikamili utimilifu wake? Mwanzoni, Yehova hakukusudia Mwana wake ateseke na kufa. Ilikuwa lazima afanye hivyo baada tu ya Adamu na Hawa kuasi. Yesu hakuwa amefanya kosa lolote, lakini alihitaji kuteseka na kufa ili kujibu masuala ambayo Shetani alizusha, na kuandaa bei ya fidia ambayo ilikuwa inahitajika ili kurudisha kile ambacho mwanadamu alipoteza. (Marko 8:31; 1 Pet. 2:21-24) Hilo lingeweza kutimizwa ikiwa tu, kwa mara ya kwanza katika maisha ya Yesu, Yehova angeondoa ulinzi wake kwa muda mfupi.

Je, Yesu alikuwa akijaribu kuwasaidia wafuasi wake wakazie fikira sababu iliyomfanya Yehova aruhusu Mwana wake afe kwa njia hiyo? * Yesu alijua kwamba kufa kwa njia hiyo, kama mhalifu kwenye mti wa mateso, kungefanya wengi wajikwae. (1 Kor. 1:23) Ikiwa wafuasi wake wangekazia fikira sababu halisi ya kifo chake, wangeelewa umuhimu wa kifo hicho. (Gal. 3:13, 14) Hivyo, wangemwona kuwa Mwokozi, na si mhalifu.

Haidhuru Yesu alikuwa na sababu gani ya kunukuu maneno hayo, alitambua kwamba mambo aliyokuwa akipitia yalikuwa sehemu ya mapenzi ya Yehova kwake. Muda mfupi baada ya kunukuu zaburi hiyo, Yesu alisema: “Imetimizwa!” (Yoh. 19:30; Luka 22:37) Naam, kuondolewa ulinzi wa Yehova kwa muda mfupi, kulimruhusu Yesu atimize kikamili mambo yote aliyokuwa ametumwa kufanya duniani. Pia, kulimwezesha atimize mambo yote yaliyoandikwa kumhusu “katika Sheria ya Musa, Manabii, na Zaburi.”—Luka 24:44.

^ fu. 2 Tazama pia fungu la 9 na 10 katika makala yenye kichwa “Mambo Tunayojifunza Kutokana na Maneno ya Mwisho ya Yesu” katika toleo hili.

^ fu. 4 Wakati wa huduma yake, nyakati nyingine Yesu alizungumza au kuuliza maswali ambayo kihalisi hayakuwa yakifunua alivyokuwa akihisi. Alifanya hivyo ili kuwapa fursa wafuasi wake waeleze maoni yao.—Marko 7:24-27; Yoh. 6:1-5; tazama Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 15, 2010, ukurasa 4-5.