Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 15

Tunaweza Kujifunza Nini Kutokana na Miujiza ya Yesu?

Tunaweza Kujifunza Nini Kutokana na Miujiza ya Yesu?

“Akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya.”—MDO. 10:38.

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

MUHTASARI a

1. Eleza jinsi hali ilivyokuwa Yesu alipofanya muujiza wake wa kwanza.

 WAZIA jinsi hali ilivyokuwa mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K. mwanzoni mwa huduma ya Yesu. Yesu na Maria, mama yake, na baadhi ya wanafunzi wake wanaalikwa katika karamu ya ndoa huko Kana, kijiji kilicho upande wa kaskazini wa Nazareti, mji wa nyumbani wa Yesu. Maria ni rafiki ya familia hiyo na inaonekana anasaidia kuwatunza wageni. Lakini wakati wa karamu hiyo, tatizo linatokea ambalo linaweza kuaibisha familia hiyo na wenzi hao wapya—divai inakwisha. b Labda wageni ni wengi kuliko walivyotazamia. Maria anaenda upesi kwa mwanaye na kusema: “Hawana divai.” (Yoh. 2:1-3) Yesu anafanya nini? Anafanya jambo la kustaajabisha—anabadili maji kimuujiza kuwa “divai nzuri.”—Yoh. 2:9, 10.

2-3. (a) Yesu alitumiaje uwezo wake wa kufanya miujiza? (b) Tunawezaje kunufaika kwa kuchunguza miujiza ya Yesu?

2 Baadaye, Yesu alifanya miujiza mingi wakati wa huduma yake. c Alitumia uwezo wake wa kufanya miujiza kuwasaidia makumi ya maelfu ya watu. Kwa mfano, miujiza yake miwili tu—kuwalisha wanaume 5,000 na baadaye wanaume 4,000—huenda ilihusisha jumla ya watu zaidi ya 27,000 ikiwa tutatia ndani wanawake na watoto waliokuwepo. (Mt. 14:15-21; 15:32-38) Katika pindi hizo mbili, Yesu aliwaponya pia watu wengi waliokuwa wagonjwa. (Mt. 14:14; 15:30, 31) Wazia jinsi umati wa watu ulivyoshangaa Yesu alipowaponya na kuwalisha kimuujiza!

3 Leo, tunaweza kujifunza mengi kutokana na miujiza ya Yesu. Katika makala hii, tutachunguza baadhi ya masomo yanayoimarisha imani ambayo tunaweza kujifunza kutokana na miujiza hiyo. Kisha tutachunguza jinsi tunavyoweza kuiga sifa ya unyenyekevu na huruma ambayo Yesu alionyesha alipokuwa akifanya miujiza hiyo.

MASOMO KUMHUSU YEHOVA NA YESU

4. Miujiza ya Yesu inatufundisha masomo yanayoimarisha imani kumhusu nani?

4 Miujiza ya Yesu inatufundisha masomo yanayojenga imani kumhusu yeye na pia Baba yake, kwa sababu Yehova ndiye aliyekuwa Chanzo halisi cha miujiza hiyo. Andiko la Matendo 10:38 linasema hivi: “Mungu [alimtia Yesu] mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi, kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.” Pia, kumbuka kwamba katika mambo yote ambayo Yesu alisema na kufanya—kutia ndani miujiza aliyofanya—alionyesha kikamili njia ya kufikiri na hisia za Baba yake. (Yoh. 14:9) Fikiria masomo matatu tunayoweza kujifunza kutokana na miujiza ya Yesu.

5. Ni nini kilichomchochea Yesu kufanya miujiza? (Mathayo 20:30-34)

5 Kwanza, Yesu na Baba yake wanatupenda sana. Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha jinsi alivyowapenda sana watu kwa kutumia uwezo wake kufanya miujiza ili kuwasaidia wale waliokuwa wakiteseka. Pindi moja, wanaume wawili waliokuwa vipofu walimlilia wakiomba msaada. (Soma Mathayo 20:30-34.) Ona kwamba Yesu ‘aliwasikitikia’ na akawaponya. Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “akawasikitikia” kinarejelea huruma nyingi ambayo mtu anahisi ndani kabisa mwilini. Huruma hiyo nyingi, ambayo ni wonyesho wa upendo, ilimchochea pia Yesu kuwalisha wenye njaa na kumponya mtu mwenye ukoma. (Mt. 15:32; Marko 1:41) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova, Mungu mwenye “huruma nyororo,” na Mwana wake wanatupenda sana na wanaumia tunapoteseka. (Luka 1:78; 1 Pet. 5:7) Bila shaka, wanatamani sana kuondoa matatizo yanayowapata wanadamu!

6. Mungu amempa Yesu uwezo wa kufanya nini?

6 Pili, Mungu amempa Yesu nguvu za kutatua matatizo yote ya wanadamu. Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwamba ana nguvu za kutatua matatizo yote ambayo hatuwezi kusuluhisha. Kwa mfano, ana uwezo wa kutuweka huru kutoka kwa chanzo cha matatizo ya wanadamu, yaani, dhambi tuliyorithi na matokeo yake, ugonjwa na kifo. (Mt. 9:1-6; Rom. 5:12, 18, 19) Miujiza aliyofanya inathibitisha kwamba anaweza kuponya “kila aina ya ugonjwa” na hata kuwafufua wafu. (Mt. 4:23; Yoh. 11:43, 44) Pia, ana nguvu za kudhibiti dhoruba kali ya upepo na kuwashinda roho waovu. (Marko 4:37-39; Luka 8:2) Tunafarijika kujua kwamba Yehova amempa Mwana wake nguvu hizo!

7-8. (a) Miujiza ya Yesu inatuhakikishia jambo gani? (b) Ni miujiza gani ambayo unatarajia katika ulimwengu mpya unaokuja?

7 Tatu, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba baraka za wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu zitatimia. Miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa mwanadamu duniani, inatufundisha mambo atakayofanya kwa kiwango kikubwa zaidi akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu ulio mbinguni. Fikiria mambo tutakayofurahia hivi karibuni chini ya utawala wa Kristo. Tutafurahia afya kamilifu, kwa sababu ataondoa magonjwa yote na ulemavu ambao umewasumbua wanadamu. (Isa. 33:24; 35:5, 6; Ufu. 21:3, 4) Hatutakuwa na njaa kamwe au kuteseka kwa sababu ya misiba ya asili. (Isa. 25:6; Marko 4:41) Tutakuwa na shangwe kubwa ya kuwakaribisha wapendwa wetu kutoka katika “makaburi ya ukumbusho.” (Yoh. 5:28, 29) Ni muujiza gani ambao wewe unatarajia hasa katika ulimwengu mpya unaokuja?

8 Alipokuwa akifanya miujiza, Yesu alionyesha unyenyekevu na huruma nyingi—sifa ambazo tunahitaji kuiga. Acheni tuchunguze mifano miwili, tukianza na simulizi la karamu ya ndoa huko Kana.

SOMO KUHUSU UNYENYEKEVU

9. Yesu alifanya nini kwenye karamu ya ndoa? (Yohana 2:6-10)

9 Soma Yohana 2:6-10. Divai ilipokwisha katika karamu ya ndoa, je, Yesu alilazimika kufanya chochote? Hapana. Hakuna unabii uliotabiri kwamba Masihi angetokeza divai kimuujiza. Lakini wazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa vinywaji vingeisha katika harusi yako mwenyewe. Inaelekea kwamba Yesu aliihurumia familia hiyo, hasa bwana na bibi harusi, na hakutaka waaibike. Basi kama ilivyotajwa mwanzoni, alifanya muujiza. Alibadili maji—kiasi cha lita 390 hivi—kuwa divai bora. Labda alitokeza kiasi kikubwa hivyo ili divai ambayo ingebaki itumike wakati ujao au hata iuzwe ili kuwasaidia wenzi hao wapya kifedha. Bila shaka, wenzi hao wapya wa ndoa walithamini sana tendo hilo!

Mwige Yesu kwa kuepuka kujigamba kuhusu mambo unayotimiza (Tazama fungu la 10 na 11) e

10. Ni baadhi ya mambo gani muhimu yaliyo kwenye simulizi la Yohana sura ya 2? (Tazama pia picha.)

10 Fikiria baadhi ya mambo muhimu yaliyoandikwa katika simulizi la Yohana sura ya 2. Je, ulitambua kwamba Yesu mwenyewe hakujaza maji kwenye ile mitungi? Badala ya kujielekezea fikira yeye mwenyewe, aliwaambia watumishi wajaze mitungi hiyo. (Mstari wa 6, 7) Na baada ya kugeuza maji kuwa divai, Yesu mwenyewe hakumpelekea divai hiyo msimamizi wa karamu. Badala yake, aliwaambia watumishi wafanye hivyo. (Mstari wa 8) Bila shaka, Yesu hakuchukua kikombe cha divai na kukiinua mbele ya wageni, na kujigamba, ‘Onjeni divai ambayo nimetengeneza!’

11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu?

11 Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai? Tunajifunza somo kuhusu unyenyekevu. Yesu hakujigamba kuhusu muujiza huo; kwa kweli, hakujigamba kamwe kuhusu mambo aliyotimiza. Kinyume chake, kwa unyenyekevu, tena na tena alimpa sifa na utukufu Baba yake. (Yoh. 5:19, 30; 8:28) Ikiwa tutamwiga Yesu kwa kuwa wanyenyekevu, hatutajigamba kuhusu mambo tunayotimiza. Hata tutimize jambo gani kwenye utumishi wa Yehova, acheni tujigambe si kujihusu sisi wenyewe, bali kumhusu Mungu mwenye kustaajabisha ambaye tuna pendeleo la kumtumikia. (Yer. 9:23, 24) Acheni tumpe sifa anazostahili. Isitoshe, hatuwezi kamwe kutimiza jambo lolote zuri bila msaada wa Yehova.—1 Kor. 1:26-31.

12. Ni kwa njia gani nyingine tunaweza kuiga unyenyekevu wa Yesu? Toa mfano.

12 Fikiria njia nyingine ambayo tunaweza kuiga unyenyekevu wa Yesu. Fikiria hali ifuatayo: Mzee wa kutaniko anatumia muda mwingi kumsaidia mtumishi wa huduma kijana kutayarisha hotuba yake ya kwanza ya watu wote. Matokeo ni kwamba ndugu huyo kijana anatoa hotuba yenye kutia moyo na watu wanafurahi kutanikoni. Baada ya mkutano, mtu fulani anamwendea mzee huyo na kumwambia: ‘Ndugu ametoa hotuba nzuri sana, sivyo?’ Je, yule mzee anahitaji kusema: ‘Ndiyo, lakini nilitumia muda mwingi sana kumsaidia’? Au je, kwa unyenyekevu atasema: ‘Ndiyo, ametoa hotuba nzuri. Amenifurahisha sana’? Tunapokuwa wanyenyekevu, hatujitafutii sifa kwa mambo mazuri tunayowafanyia wengine. Tunaridhika kujua kwamba Yehova anaona na kuthamini mambo tunayofanya. (Linganisha Mathayo 6:2-4; Ebr. 13:16) Kwa kweli, tunamfurahisha Yehova tunapomwiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu.—1 Pet. 5:6.

SOMO KUHUSU HURUMA

13. Yesu aliona nini karibu na jiji la Naini, na alifanya nini kuhusu jambo hilo? (Luka 7:11-15)

13 Soma Luka 7:11-15. Fikiria jambo lililotokea pindi fulani katika huduma ya Yesu. Alikuwa amesafiri kwenda Naini, jiji la Galilaya ambalo halikuwa mbali kutoka Shunemu, ambako nabii Elisha alikuwa amemfufua mwana wa mwanamke fulani miaka 900 hivi mapema. (2 Fal. 4:32-37) Yesu alipokuwa akikaribia lango la jiji, aliona msafara wa mazishi ukitoka jijini. Lilikuwa tukio lenye kuhuzunisha—mjane fulani alikuwa amefiwa na mwana wake wa pekee. Lakini mama huyo aliyekuwa akiomboleza hakuwa peke yake; umati mkubwa kutoka jijini ulikuwa pamoja naye. Yesu aliusimamisha msafara huo na akamfanyia jambo lenye kustaajabisha mama huyo aliyekuwa akiomboleza—alimfufua mwana wake! Huo ni muujiza wa kwanza wa Yesu wa ufufuo, kati ya miujiza mitatu ya ufufuo ambayo inatajwa kihususa katika vitabu vya Injili.

Mwige Yesu kwa kuchukua hatua ya kwanza ili kuwaonyesha huruma wale wanaoomboleza (Tazama fungu la 14 hadi 16)

14. Ni baadhi ya mambo gani muhimu yaliyoandikwa kwenye Luka sura ya 7? (Tazama pia picha.)

14 Fikiria baadhi ya mambo muhimu yaliyo kwenye simulizi la Luka sura ya 7. Je, ulitambua kwamba Yesu ‘alimwona’ yule mama aliyekuwa akiomboleza kisha “akamsikitikia”? (Mstari wa 13) Basi, jambo aliloona—labda mwanamke huyo alipokuwa akilia mbele ya mwili wa mwana wake—lilifanya moyo wa Yesu ujae huruma nyingi kumwelekea. Yesu hakuwa tu na hisia za kumsikitikia yule mama; bali pia alimwonyesha huruma. Alizungumza naye, bila shaka kwa sauti yenye kufariji, na kumwambia: “Acha kulia.” Kisha akachukua hatua na kufanya jambo fulani. Alimfufua mwana huyo na “akamkabidhi kwa mama yake.”—Mstari wa 14, 15.

15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu?

15 Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kumfufua mwana wa mjane? Tunajifunza somo la kuwaonyesha huruma wale wanaoomboleza. Bila shaka, hatuwezi kuwafufua wafu kama Yesu alivyofanya. Lakini kama Yesu, tunaweza kusitawisha huruma kuwaelekea wale wanaoomboleza kwa kuwa macho. Tunaweza kuchukua hatua ya kwanza kuonyesha huruma kwa kusema na kufanya mambo tunayoweza ili kuwasaidia na kuwafariji. d (Met. 17:17; 2 Kor. 1:3, 4; 1 Pet. 3:8) Hata maneno rahisi na matendo madogo ya fadhili yanaweza kuwafariji sana.

16. Kama igizo lililo kwenye picha linavyoonyesha, unajifunza nini kutokana na kisa cha mama ambaye alikuwa amefiwa na binti yake hivi karibuni?

16 Fikiria jambo hili lililoonwa. Miaka kadhaa iliyopita, walipokuwa wakiimba wimbo katika mkutano wa kutaniko, dada mmoja alimwona mama aliyekuwa akilia hapo karibu. Wimbo huo ulitaja tumaini la ufufuo, na muda mfupi uliopita mama huyo alikuwa amempoteza binti yake mdogo katika kifo. Kwa kuwa alijua jambo hilo, yule dada alienda mara moja na kumkumbatia mama huyo, na wakaimba wimbo huo pamoja. Mama huyo alisema hivi: “Nilihisi upendo mwingi kuwaelekea ndugu na dada.” Alishukuru sana kwamba alikuwa amehudhuria mkutano. Alisema hivi: “Hapo ndipo tunapopokea msaada, katika Jumba la Ufalme.” Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anatambua na kuthamini hata mambo madogo tunayofanya ili kuwaonyesha huruma wale wanaoomboleza, “waliopondeka roho.”—Zab. 34:18.

MRADI WA KUJIFUNZA WENYE KUTHAWABISHA

17. Tumejifunza nini katika makala hii?

17 Masimulizi ya vitabu vya Injili kuhusu miujiza ya Yesu yanaweza kuwa mradi wa kujifunza wenye kuthawabisha. Yanatufundisha kwamba Yehova na Yesu wanatupenda sana, Yesu ana nguvu za kutatua matatizo ya wanadamu, na kwamba tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika ahadi za baraka za Ufalme ambazo zitatimizwa hivi karibuni. Tunapochunguza masimulizi hayo, tunaweza kutafakari kuhusu njia ambazo tunaweza kuiga sifa za Yesu. Kwa nini usipange kufanya mradi wa kujifunza kibinafsi au kipindi cha Ibada ya Familia kinachokazia miujiza mingine ya Yesu? Tambua masomo unayoweza kujifunza, kisha uzungumze na wengine kuhusu mambo uliyojifunza. Kwa kweli, mtakuwa na mazungumzo mengi yenye kujenga sana!—Rom. 1:11, 12.

18. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

18 Karibu na mwisho wa huduma yake, Yesu alifanya muujiza wake wa tatu wa ufufuo uliorekodiwa. Lakini muujiza huo ulikuwa tofauti—alimfufua rafiki yake mpendwa, na alifanya hivyo katika hali zisizo za kawaida. Tunaweza kujifunza masomo gani kutokana na masimulizi ya kitabu cha Injili kuhusu muujiza huo? Na tunawezaje kuimarisha imani yetu katika tumaini la ufufuo? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.

WIMBO 20 Ulimtoa Mwana Wako Mpendwa

a Alituliza dhoruba kali ya upepo, aliwaponya wagonjwa, na akawafufua wafu. Inasisimua sana kusoma kuhusu miujiza ambayo Yesu alifanya! Masimulizi hayo yameandikwa katika Biblia, si ili kutuburudisha, bali kutufundisha. Tunapoyachunguza, tunajifunza masomo yanayotuimarisha imani kumhusu Yehova na Yesu na tunatambua sifa za kiroho ambazo tunahitaji kusitawisha.

b Msomi fulani wa Biblia anaeleza hivi: “Huko Mashariki, ukaribishaji wageni ulionwa kuwa jukumu takatifu na yule aliyewakaribisha wageni alipaswa kuhakikisha kwamba aliwaandalia maandalizi mengi kuliko walivyohitaji. Ukaribishaji wageni wa kweli, hasa kwenye karamu ya ndoa, ulimaanisha kuandaa chakula na vinywaji kwa wingi kuliko wageni walivyohitaji.”

c Vitabu vya Injili vinataja zaidi ya miujiza 30 ya Yesu. Kwa kuongezea, wakati mwingine baadhi ya miujiza inajumlishwa pamoja. Pindi moja, “jiji lote” lilikuja kwa Yesu naye “akawaponya watu wengi waliokuwa na magonjwa.”—Marko 1:32-34.

d Ili kupata mapendekezo kuhusu mambo unayoweza kusema au kufanya ili kuwafariji wale wanaoomboleza, ona makala “Wafariji Waliofiwa Kama Yesu Alivyofanya” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2010.

e MAELEZO YA PICHA: Yesu akiwa amesimama kando, bwana na bibi harusi na wageni wao wanafurahia divai nzuri.